“Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya Umekaribia
Siku tatu za kuthawabisha zenye maagizo ya Biblia zakungoja kwenye “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Katika Afrika Mashariki na nchi nyinginezo, mikusanyiko 15 imeratibiwa. Kwa hiyo utaweza kuhudhuria mmoja ulio wa karibu kadiri fulani na mahali uishipo.
Mkusanyiko utaanza na muziki saa 4:20 asubuhi ya Ijumaa, na programu itakwisha siku hiyo karibu na saa 11 alasiri. Jumamosi na Jumapili, vipindi vitaanza saa 3:30 asubuhi, navyo vitamalizika karibu na saa 11 alasiri ya Jumamosi na saa 10:15 alasiri Jumapili.
Hotuba ya msingi asubuhi ya Ijumaa, zaidi ya kuonyesha hofu ya kimungu ni nini, itatambulisha pia manufaa zayo kwa wale wasitawishao hofu hiyo. Programu nzima ya mkusanyiko itakazia manufaa hizo.
Wakati wa mfululizo wa muda wa saa moja wenye hotuba na maonyesho alasiri ya Ijumaa, utasikia jinsi hofu ya kimungu iwezavyo kutia nguvu ndoa na maisha ya familia, na vilevile jinsi iwezavyo kuwasaidia wachanga wabaki thabiti katika uaminifu-mshikamanifu wao kwa Mungu. Vipindi vya Ijumaa vitamalizia kwa utoaji wa kuchangamsha moyo “Faraja kwa Waliofiwa.” Utathamini msaada wenye kutumika wenye kuandaliwa wakati wa hotuba hiyo ili kuwategemeza wale ambao wamepoteza wapendwa katika kifo.
Programu ya Jumamosi itaonyesha jinsi hofu ya kimungu iwezavyo kuimarisha ushikamano wetu kwa mwelekezo wa Yehova kuhusu kutaniko na huduma yetu. Ile hotuba “Kikundi cha Watu Wasioachwa Kabisa na Yehova” itaeleza jinsi ahadi ya Mungu ya kutowaacha kabisa watu wake ipasavyo kuwaathiri katika ulimwengu wa leo. Baadaye alasiri hiyo, katika ile hotuba “Soma Neno la Mungu, Biblia Takatifu, Kila Siku,” wajumbe watapokea madokezo yenye kutumika ya kusoma na kujifunza Biblia. Programu ya Jumamosi itamalizia kwa hotuba juu ya kile kichwa chenye kuamsha upendezi “Siku ya Yehova Yenye Kupulizia Hofu Imekaribia.”
Sehemu moja ya programu ya Jumapili ni ile hotuba “Kutakuwa na Ufufuo wa Waadilifu.” Katika hotuba itakayofuata, “Waokolewa Wakiwa Hai Kupitia Dhiki Kubwa,” elezo litaandaliwa juu ya ahadi nzuri ajabu ya Yesu kuhusu wale ambao hawatakufa kamwe hata kidogo.—Yohana 11:26.
Kipindi cha asubuhi ya Jumapili kitamalizika kwa ile drama ya dakika 40 ya kuchochea mawazo yenye kichwa Machaguo Unayokabili. Wasikilizaji watarudishwa siku ya Yoshua na kuona azimio lake imara la kumtumikia Yehova. Watashuhudia pia ule mtihani wenye moto siku za Eliya, na masomo yatachotwa kutokana na matukio yote mawili haya ambayo yatasaidia wajumbe waonyeshe hofu ya kimungu leo.
Jambo kuu la mkusanyiko alasiri ya Jumapili litakuwa ile hotuba ya watu wote, “Kwa Nini Umhofu Mungu wa Kweli Sasa.” Hakika utanufaika kwa kuwapo siku zote tatu! Wewe waalikwa kwa ukunjufu uhudhurie. Ili upate mahali palipo karibu zaidi na nyumbani kwako, wasilisha habari kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu, au uandikie wachapishaji wa gazeti hili.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
T. Rosenthal/SUPERSTOCK