Sababu kwa Nini Wapaswa Kuhudhuria
UTAPOKEA siku nne zenye kuthawabisha za maagizo ya kiroho kwenye “Kufundisha Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya, utakaofanywa kiangazi hiki katika majiji kotekote ulimwenguni. Katika United States pekee, mikusanyiko hiyo zaidi ya 150 itafanywa wakati wa Juni, Julai, na Agosti. Kwa kawaida, programu hiyo itaanza Alhamisi saa 7:20 za alasiri na kumalizika Jumapili saa 10:15 za alasiri. Jambo kuu kwenye mikusanyiko mingine litakuwa ripoti za wamishonari, ambao wamesaidiwa kurudi nyumbani kwao kwa ajili ya pindi hiyo yenye furaha.
Iwe wewe ni mzee au ni kijana—mume, mke, baba, mama, tineja, au mtoto—utapokea kufundisha kunakotolewa katika njia ya wazi, yenye kuvutia ambayo itakunufaisha. Kwa kielelezo, wengi leo huuliza, Kusudi la maisha ni nini? Ijumaa asubuhi, utafurahia kusikiza swali hilo likizungumziwa na utapendezwa na yale utakayopokea ili kuwasaidia wengine waelewe habari hiyo.
Ijumaa alasiri programu itakazia sehemu “Kufanya Ndoa Iwe Muungano wa Kudumu,” “Fanya Bidii Kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako” na “Wazazi—Watoto Wenu Wanahitaji Uangalifu wa Pekee.” Mara tu baada ya hizo, uangalifu wa pekee utakazwa juu ya matatizo ambayo vijana hukabili na jinsi wanavyoweza kuyashughulikia. Wanapaswa kutiwa moyo na drama ya kisasa yenye kichwa Vijana Wamkumbukao Muumba Wao Sasa.
Jumamosi programu itakazia unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho na hasa maneno yake: “Mara, baada ya dhiki ya siku zile, jua litatiwa giza.” (Mathayo 24:29) Utataka kusikia mazungumzo kuhusu wakati ambapo dhiki hiyo inapotukia. Programu ya Jumamosi itapitia pia rekodi ya Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa na kuonyesha yale ambayo wametimiza.
Jumapili drama nyingine yenye kichwa Usidanganyike Wala Kumdhihaki Mungu, itaonyesha ugumu unaokabili uaminifu-maadili wa Kikristo wa mtu kwa sababu ya vidio na muziki wa leo unaopendwa sana. Hotuba ya watu wote wakati wa alasiri itakazia kichwa kikuu “Kufundisha Kunakosaidia kwa Nyakati Zetu Zenye Hatari.” Programu hiyo itamalizia kwa onyo hili la upole “Endeleeni Kushika Sana Kufundisha Kimungu.”
Kwa hakika, utanufaika kwa kuwapo siku zote nne! Umealikwa kwa uchangamfu kuhudhuria. Ili kujua mahali pa mkusanyiko palipo karibu zaidi na nyumbani kwako, wasiliana na Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu au andikia I.B.S.A., Box 47788, Nairobi, Kenya, au tumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa 2.