Kukabiliana na Tatizo la Kutamani Nyumbani Katika Utumishi wa Mungu
YESU KRISTO aliamuru wafuasi wake hivi: “Enendeni . . . mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi.” (Mathayo 28:19) Kwa Wakristo wengi, kutimiza agizo hilo kumemaanisha kukubali hali ngumu wakiwa mbali na nyumbani. Waangalizi wasafirio, wake zao, na wengine huacha mambo mengi nyuma kwa sababu ya utumishi wa Mungu. Kutamani nyumbani kwaweza kuwa tatizo kubwa kwa Mashahidi wa Yehova wote hao.
Kutamani nyumbani hutukia wakati makumbukumbu yanapofanya fikira zako ziwazie usalama na upendo wa nyakati nzuri zilizopita. Hiyo yaweza kutokeza hisiamoyo nyingi sana hivi kwamba uhisi umeshuka moyo na kushindwa kuendelea. Kwa kweli, baada ya wao kuuza mali zao na kufunga safari ya gharama kubwa kwenda nchi ya kigeni, wengine wameacha mipango yao na kurudi nyumbani. Kutamani nyumbani kuliwashinda nguvu.
Mashambulizi hayo ya hisiamoyo huwa yanatukia mara nyingi punde tu baada ya kuhama, lakini kwa wengine, hayo huendelea kwa muda wa maisha yao yote. Baada ya kuwa mbali kwa zaidi ya miaka 20, Yakobo alikuwa ‘akitamani sana nyumba ya babake.’ (Mwanzo 31:30) Ni nani wanaoweza kutazamia kuwa na tatizo la kutamani nyumbani? Ni nini kinacholianzisha? Mtu aweza kukabilianaje na hisia hizo?
Ni Nini Kinachoanzisha Huzuni Hiyo?
Kutamani nyumbani kwaweza kumwathiri yeyote. Amytis, binti wa mfalme wa Umedi aitwaye Astyages, yaonekana alikuwa na kila sababu ya kuwa mwenye furaha: utajiri mwingi, ufanisi, makao mazuri. Lakini, alitamani sana milima ya Umedi hivi kwamba mume wake, Mfalme Nebukadneza, alimjengea bustani za Babiloni zinazoning’inia ili kujaribu kumfariji.
Kutamani nyumbani kwaweza hasa kuwa tatizo kubwa wakati maisha yaonekanapo kuwa magumu zaidi ya vile yalivyokuwa kabla ya mtu kuhama. Watu wa Yuda walipokuwa wahamishwa, wao waliomboleza hivi: “Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, tukalia tulipoikumbuka Sayuni. Tuuimbeje wimbo wa BWANA katika nchi ya ugeni?”—Zaburi 137:1, 4.
Mambo mengi yaweza kuanzisha huzuni ya kutamani nyumbani. Terri, aliyekuwa ameondoka Kanada, asema hivi: “Siku moja picha ya familia ilianguka kutoka katika kitabu kimoja. Nilipoichukua, kwa ghafula nililemewa na kule kutamani sana nyumbani, nami nikalia.” Chris, aliyehama kutoka Uingereza kwenda kwenye nchi iliyo maskini zaidi, akiri hivi: “Kule kutambua tu mfuatano wa sauti ya wimbo wa kale au harufu ya chakula nikijuacho kungeweza kunifanya nitamani mambo niliyoacha nyuma.”—Linganisha Hesabu 11:5.
Mara nyingi uhusiano wa karibu wa familia huleta tatizo hilo. Roseli, Mbrazili anayeishi sasa katika nchi jirani, asema hivi: “Nahuzunika nipatapo habari mbaya kutoka nyumbani na siwezi kuwapo ili kusaidia. Nyakati nyingine inakuwa vibaya zaidi nikosapo kupata habari yoyote na kuanza kuwazia mambo mbalimbali.” Janice alihama kutoka Amerika Kaskazini kwenda kwenye mji mdogo katika tropiki za Amazon. Yeye asema: “Mimi hutamani nyumbani nisikiapo habari njema kutoka nyumbani. Nasikia jinsi wao wanavyofurahia ushirika mzuri pamoja, nami natamani ningekuwa pamoja nao.”
Si kule kuacha tu watu kunakofanya mtu atamani nyumbani. Linda aeleza hivi: “Ningefadhaika niliposhindwa kujua mahali pa kununua vitu nilivyohitaji. Sikujua bei au jinsi ya kubadilishana vitu. Kuwa na gari kulikuwa gharama kubwa sana, na sikuzote nilikuwa nikisukumwa-sukumwa niking’ang’ana kupanda magari ya umma yaliyosongamana. Hayo yalinifanya nitamani nyumbani.” Akisema juu ya pengo la kitamaduni na kiuchumi, Janet asema: “Ni umaskini ndio ulionihuzunisha. Sikuwa nimepata kuona watu wakiomba mkate, au familia kubwa zikiishi katika chumba kimoja bila maji ya mfereji. . . . Mambo kama hayo yalinihuzunisha sana hivi kwamba nilihisi nisingeweza kukaa huko muda mrefu zaidi.”
Kukabiliana na Hisia Zako
Hatupaswi kuona aibu kwa sababu ya kuwa na hisiamoyo zenye nguvu kwa watu tuwapendao au kuelekea mazingira tuliyojua tulipokuwa tukikua. Yehova Mungu alitupa hisiamoyo ili tufurahie uhusiano mchangamfu wa kibinafsi. Waangalizi Wakristo wa kutaniko la Efeso walikuwa wanaume waliokomaa kihisiamoyo. Lakini ni nini kilichotukia ziara ya mtume Paulo ilipokaribia kwisha? “Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu”! (Matendo 20:37) Bila shaka, tukio hilo halikuwa la kutamani nyumbani. Lakini, ni jambo la kufikiria. Ni jambo la kawaida kuwa na hisia, lakini hatupaswi kuziacha zitudhibiti. Basi, wewe waweza kukabilianaje kwa mafanikio na hali ya kutamani nyumbani?
Kujifunza kusema lugha ya wenyeji ni ufunguo wa kuhisi kama uko nyumbani. Hisia za kutamani nyumbani zaweza kuongezeka uwasiliano unapozuiwa kwa sababu yakubidi kushughulika na lugha ya kigeni. Kwa hiyo, ikiwezekana, jifunze kusoma na kusema lugha ya eneo hilo kabla hujahamia huko. Au sivyo, kaza akili juu ya masomo ya lugha wakati wa majuma machache ya kwanza baada ya wewe kuwasili. Huo ndio wakati ambao una msukumo mkubwa zaidi na hivyo mataraja mazuri zaidi ya kujifunza lugha. Ukitumia majuma hayo hasa ili kujifunza lugha, upesi utakuwa ukifurahia mazungumzo, na hilo laweza kusaidia kuondoa hisia za kutamani nyumbani.
Fanya marafiki wapya upesi iwezekanavyo, kwani hilo litakusaidia ujisikie kama uko nyumbani. Kutaniko la Mashahidi wa Yehova ndipo mahali bora kabisa pa kufanyiza marafiki halisi. Chukua hatua ya kwanza na upendezwe na wengine. Jitahidi kujua malezi yao, familia zao, matatizo yao, na mapendezi yao. Alika waamini wenzako nyumbani mwako. Nawe utaona kwamba wengine watapendezwa nawe.
Miongoni mwa watu wa Mungu, urafiki waweza kuwa wa karibu kama vile uhusiano wa familia. Yesu alisema hivi: “Mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.” (Marko 3:35) Kristo pia aliwahakikishia wafuasi wake hivi: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Tukiwa na udugu wa kiroho mzuri kama huo, sisi hatuko peke yetu, hata katika nchi mpya.
Kudumisha urafiki na wale walio mbali nyumbani kwaweza kukusaidia pia kukabiliana na hali ya kutamani nyumbani. Huenda ukashangaa kupata kwamba kwa vile sasa umehama, uwasiliano kwa barua ni wenye maana hasa, kwa kuwa yaelekea utafikiria zaidi maneno yako. Kutakuwa na mambo ya kusisimua utakayosema. Janet, aliyetajwa mapema, adokeza hivi: “Kupiga simu mbali ni ghali, lakini kupeleka kwa posta kaseti iliyorekodiwa ni rahisi kwa kulinganisha. Kuzungumzia mashine huwa jambo geni mwanzoni. Lakini, ukizungumza na mtu huku maikrofoni ikiwa kati yenu, ni jambo rahisi na lenye kupendeza.” Huenda ukaomba upokee mrekodio wa kaseti pia.
Shirley, aliyehama Marekani kwenda Amerika ya Latini miaka 25 iliyopita, asema hivi: “Sikuzote mimi huandika juu ya maono yenye kujenga badala ya matatizo. Hilo huwatia moyo wengine waendelee kuniandikia.” Hata hivyo, uwe mwangalifu. Kuandika barua nyingi mno kwaweza kukuzuia usifanye marafiki wapya. Del, aliyehama Kanada kwenda nchi nyingine, asema hivi: “Epuka kubaki nyumbani na kuota juu ya mambo unayokosa. Badala ya hivyo, toka nje na ufurahie eneo lako jipya.”
Fahamu desturi, historia, ucheshi, na mahali pa upendezi na uzuri pa nchi hiyo mpya. Hilo litakusaidia uondoe fikira kwenye mambo yasiyofaa. Na ukikusudia kukaa mahali ulipohamia, ni vema zaidi usizuru nchi yako upesi mno au mara nyingi mno. Huchukua wakati kufanyiza marafiki wapya na kuzoea mazingira mapya. Ziara za muda mrefu kule nyumbani huzuia jambo hilo. Baada ya kutulia, waweza kufurahia kwenda nyumbani kuzuru—na kisha kurudi. Kwa wakati huu, jishughulishe upate kupenda makao yako mapya.
Endelea Kutazamia Mbele
Yehova alitupa dunia nzima kuwa makao yetu. (Zaburi 115:16) Ukiwa na roho yenye shangwe ya Kikristo, maisha yaweza kufurahisha katika nchi yoyote. Ukihama ili kuendeleza masilahi ya Ufalme na kuhubiri habari njema katika nchi nyingine au kwingineko katika nchi yako, fanya hivyo ukiwa na matazamio mazuri. Tazamia mbele kufanyiza marafiki wapya, kujifunza juu ya desturi tofauti, kufanya wanafunzi, au kufanya mambo yenye kuthawabisha katika utumishi wa Mungu.
Yehova Mungu ni Rafiki mmoja ambaye sikuzote atakuwa nawe, hata uwe wapi. (Zaburi 94:14; 145:14, 18) Kwa hiyo kaa karibu naye kwa sala. (Warumi 12:12) Hilo litakusaidia uzingatie akilini kusudi lako maishani ukiwa mtumishi wa Mungu. Abrahamu na Sara walizingatia kusudi lao akilini walipoacha makao yao yenye starehe katika jiji la Uru. Kwa kutii amri ya Yehova, waliacha marafiki na watu wa ukoo. (Matendo 7:2-4) Kama wangeliendelea kukumbuka na kutamani kule walikoacha, wangelikuwa na fursa ya kurudi. Lakini wao walikuwa wakifikilia mahali bora zaidi—hatimaye uhai katika dunia-paradiso chini ya Ufalme wa kimbingu wa Mungu.—Waebrania 11:15, 16.
Kuhubiri katika mashamba ya kigeni au mahali ambapo uhitaji wa wapiga-mbiu ya Ufalme ni mkubwa zaidi katika nchi yako kwaweza kuwa kugumu. Lakini kazi hiyo pia ni yenye matokeo na yenye kuthawabisha sana. (Yohana 15:8) Na iwapo mawazo yasiyofaa yakulemea kwa muda, hayo yaweza kushindwa kwa kuendelea kuzingatia mradi wako akilini na kutazamia mbele. Dada mmoja mishonari aliye mseja alisema: “Huzuni inaponilemea, mimi hujaribu kufikiria ulimwengu mpya na jinsi wanadamu wote watakavyokuwa familia moja.” Mawazo mazuri kama hayo yaweza kukusaidia kudumisha shangwe yako na usishindwe na hali ya kutamani nyumbani.
[Picha katika ukurasa wa 29]
Kutamani nyumbani hakuhitaji kuingilia huduma ya Kikristo