Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 10/15 kur. 23-27
  • Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la kigeni?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la kigeni?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vichocheo Vifaavyo Vyahitajiwa
  • Hesabu Gharama
  • Ugumu Mkubwa Zaidi
  • Namna Gani Tamaa ya Kurudi Nyumbani?
  • Namna Gani Watoto?
  • Baraka za Kuhama
  • Namna Gani Wewe?
  • Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2011
  • Walijitoa Wenyewe kwa Hiari Nchini Ekuado
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Je, Unaweza Kuvuka na Kuingia Makedonia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Njia za Kupanua Huduma Yako
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 10/15 kur. 23-27

Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la kigeni?

“NIMETAMANI sikuzote kufanya kazi ya umishonari. Nikiwa mseja, nilitumikia katika jimbo la Texas, Marekani, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri. Mke wangu alijiunga nami huko baada ya ndoa yetu. Binti yetu alipozaliwa, niliwaza, ‘Huo ndio mwisho wa miradi yangu ya kufanya kazi ya umishonari.’ Lakini Yehova hufanya miradi itimie, hasa ikiwa yahusiana na mapenzi yake.”—Jesse, ambaye wakati huu anatumikia huko Ekuado pamoja na mke wake na watoto watatu.

“Sikujua kamwe kwamba ningeweza kutumikia katika nchi ya kigeni bila kupata mazoezi katika shule ya mishonari ya Gileadi. Nilisisimka sana nilipomwona mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia akitoa hotuba au akihubiri, nami nilimshukuru Yehova kwa kunipa fursa hii.”—Karen, mwanamke mseja ambaye amepainia kwa miaka minane huko Amerika ya Kusini.

“Baada ya kuhubiri wakati wote kwa miaka 13 nchini Marekani, mimi na mke wangu tuliona kwamba tulihitaji kichocheo kipya. Tuna furaha zaidi kuliko wakati mwingine wowote; kwa kweli haya ni maisha yenye kupendeza.”—Tom, anayepainia pamoja na mke wake Linda, katika eneo la Amazon.

Maneno hayo yenye uthamini ni ya watu ambao hali zao ziliwazuia kupata mazoezi ya umishonari kwenye Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Hata hivyo, wamepata furaha na magumu ya kutumikia katika maeneo ya kigeni. Iliwezekanaje? Je, unaweza kufanya utumishi huo?

Vichocheo Vifaavyo Vyahitajiwa

Mengi zaidi ya roho ya kujasiria tu yahitajiwa ili kufanikiwa katika eneo la kigeni. Wale ambao wamestahimili wamefaulu kwa sababu wamechochewa na mambo yafaayo. Kama mtume Paulo, wao hujiona kuwa wadeni kwa Mungu na pia kwa wanadamu. (Waroma 1:14) Wangeweza kutimiza amri ya Mungu ya kuhubiri kwa kushiriki katika huduma katika eneo la kwao. (Mathayo 24:14) Lakini walijiona kuwa na deni na kulazimika kwenda kuwasaidia wale ambao ni nadra wapate fursa ya kusikia habari njema.

Mara nyingi kichocheo kingine ni tamaa ya kuhubiri katika eneo lenye matokeo zaidi—nacho chafaa. Ni nani kati yetu ambaye hangekaribia mahali ambapo amwona mvuvi mwingine anafanikiwa sana kupata samaki wengi? Vivyo hivyo, ripoti zenye kutia moyo za maongezeko makubwa sana katika nchi nyingine zimewatia wengi moyo waende pale palipo na “wingi mkubwa wa samaki.”—Luka 5:4-10.

Hesabu Gharama

Nchi nyingi haziruhusu wajitoleaji wa kidini wanaotoka nchi za kigeni wafanye kazi ya kimwili. Hivyo, wale wanaotaka kutumikia katika nchi ya kigeni ni lazima kwa kawaida wawe wanajitegemea kifedha. Tatizo hilo la kiuchumi limetatuliwaje? Watu kadhaa wameuza au kupangisha nyumba zao ili kupata fedha zinazohitajika. Wengine wameuza biashara zao. Wengine wakaweka akiba ili kufikia mradi wao. Huku wengine watumikia katika nchi ya kigeni kwa mwaka mmoja au miwili na kurudi katika nchi zao kufanya kazi na kukusanya fedha, kisha hurudi katika nchi hizo kutumikia tena.

Ni jambo la hakika kwamba mtu hunufaika zaidi akiwa katika nchi inayositawi kwa sababu gharama ya maisha kwa kawaida ni ya chini zaidi kuliko ilivyo katika nchi iliyositawi zaidi. Hilo limewawezesha wengine waishi vizuri wakitegemea malipo ya kiasi ya uzeeni. Bila shaka, gharama za mtu zitategemea sanasana kiwango cha maisha anachochagua. Hata katika nchi zinazositawi, makazi yenye kuridhisha sana yanaweza kupatikana lakini kwa gharama ya juu zaidi.

Bila shaka, ni lazima uhesabu gharama kabla ya kuhama. Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika kuliko tu kuhesabu gharama za kiuchumi. Labda maelezo ya wengine ambao wametumikia katika Amerika ya Kusini yaweza kutusaidia.

Ugumu Mkubwa Zaidi

“Ilikuwa vigumu sana kwangu kujifunza Kihispania,” akumbuka Markku, kutoka Finland. “Nilidhania kwamba kwa kuwa sikujua lugha hiyo, ingenichukua muda kabla ya kutumikia nikiwa mtumishi wa huduma. Nilishangaa kama nini nilipoombwa niongoze funzo la kitabu baada ya miezi miwili tu! Bila shaka, kulikuwa na nyakati nyingi zenye kuaibisha. Hasa nilikuwa na shida ya kutamka majina. Siku moja nilimwita Ndugu Sancho ‘Ndugu Chancho (nguruwe),’ na sitasahau nilipomwita Dada Salamea ‘Malasea (mwovu).’ Inapendeza kwamba ndugu na dada walikuwa wenye subira sana.” Hatimaye, Markku alitumikia katika nchi hiyo akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miaka minane pamoja na mke wake, Celine.

Chris, mke wa Jesse aliyenukuliwa mwanzoni, asimulia: “Ninakumbuka wakati mwangalizi wa mzunguko alipotuzuru mara ya kwanza, baada ya sisi kuwa hapa kwa miezi mitatu tu. Ningeweza kuona kwamba ndugu huyo alikuwa anatumia vielezi na alikuwa akisema jambo fulani zuri ili kujaribu kutugusa moyo, lakini singeweza kumwelewa. Nilianza kulia humohumo ndani ya jumba. Sikuwa natoa machozi kimyakimya; nilikuwa ninalia kwikwi. Baada ya mkutano, nilijaribu kumweleza mwangalizi huyo wa mzunguko kwa nini nilifanya hivyo. Alikuwa mwenye fadhili sana, akaniambia kile ambacho kila mtu alikuwa akiniambia, ‘Ten paciencia, hermana’ (‘Uwe na subira, dada’). Miaka miwili au mitatu baadaye, tulikutana tena na kuzungumza kwa dakika 45, tukifurahi kwamba tungeweza kuwasiliana.”

“Kujifunza ni muhimu,” asema ndugu mwingine. “Kadiri tujitahidivyo zaidi kujifunza lugha, ndivyo tuboreshavyo zaidi ustadi wetu wa kuwasiliana.”

Wote hukubali kwamba jitihada hizo hunufaisha sana. Unyenyekevu, subira, na uvumilivu unasitawishwa mtu anapojitahidi kujifunza lugha mpya. Mtu anakuwa na fursa kubwa ya kuhubiria wengine habari njema. Kwa mfano, kujifunza Kihispania humwezesha mtu awasiliane katika lugha inayotumiwa na zaidi ya watu milioni 400 ulimwenguni. Wengi waliolazimika kurudi katika nchi zao bado wameweza kutumia ustadi wao wa lugha ili kusaidia watu ambao lugha yao ya kwanza ni Kihispania.

Namna Gani Tamaa ya Kurudi Nyumbani?

“Tulipokuja Ekuado mara ya kwanza mwaka wa 1989,” akumbuka Deborah, ambaye alitumikia pamoja na mume wake, Gary, katika eneo la Amazon, “nilikuwa nikitamani sana kurudi nyumbani. Nilijifunza kuwategemea zaidi ndugu na dada kutanikoni. Wakawa kama familia yangu.”

Karen, aliyetajwa mwanzoni, asema: “Mimi nilipambana na tamaa ya kurudi nyumbani kwa kushiriki katika huduma kila siku. Nikifanya hivyo, sikuwa nikiwazia nyumbani. Pia mimi nilikumbuka kwamba nyumbani wazazi wangu walijivunia kazi yangu katika eneo la kigeni. Wakati wote Mama alinitia moyo kwa maneno haya: ‘Yehova aweza kukutunza vyema zaidi ya vile niwezavyo.’”

Makiko, kutoka Japani, aongeza kusema hivi kwa ucheshi: “Baada kushiriki katika huduma ya shambani siku nzima, mimi huwa nimechoka sana. Hivyo, ninaporudi nyumbani na kuanza kutamani kurudi nyumbani, kwa kawaida mimi hushikwa na usingizi. Hivyo, hisia hiyo haidumu kwa muda mrefu.”

Namna Gani Watoto?

Watoto wanapohusika, lazima mahitaji yao yazingatiwe, kama vile elimu. Kuhusu jambo hilo wengine wamechagua kuwaelimisha watoto wao nyumbani ilhali wengine wamewapeleka katika shule za kule walikohamia.

Al alihamia Amerika Kusini akiwa na mke wake, watoto wawili, na mama yake. Yeye asema: “Tuligundua kwamba kuwapeleka watoto shuleni kuliwasaidia kujifunza lugha haraka sana. Walizungumza kwa ufasaha sana baada ya muda wa miezi mitatu.” Kwa upande mwingine, wavulana wawili matineja wa Mike na Carrie huelimishwa kwa barua kupitia shule moja inayotambuliwa rasmi. Wazazi hao wanasema: “Tuligundua kwamba haikufaa watoto hao wasome pekee yao tu. Ilitubidi tujiunge na mtaala huo na kuhakikisha kwamba wavulana hao hawakuachwa nyuma katika mtaala waliopangiwa.”

David na Janita, kutoka Australia, wanatoa maoni yao kuhusu wavulana wao wawili. “Tulitaka wavulana wetu wajionee jinsi watu wengine wanavyoishi. Ni rahisi kudhania kwamba maisha ambayo tumezoea tangu utotoni ni ya kawaida tu, lakini ukweli ni kwamba wale wanaoishi vile tunavyoishi ni wachache. Wameona pia jinsi kanuni za kitheokrasi zinavyofanya kazi ulimwenguni kote, hata iwe ni nchi gani au utamaduni gani.”

“Nilikuwa na umri wa miaka minne tu familia yetu ilipohama Uingereza mwaka wa 1969,” Ken akumbuka. “Ingawa nilisikitika kwamba hatukuishi katika nyumba ya matope iliyoezekwa kwa nyasi, kama nilivyotazamia, nafikiri kwamba nilipata malezi mazuri zaidi ambayo kijana aweza kupata. Sikuzote niliwahurumia watoto wengine ambao hawakupata fursa kama hiyo! Kwa sababu nilikuwa na ushirika mzuri pamoja na wamishonari na mapainia wa pekee, nilianza kufanya upainia-msaidizi nikiwa na umri wa miaka tisa.” Sasa Ken ni mwangalizi asafiriye.

“Kwa kweli Ekuado sasa ndiyo nyumbani,” akubali Gabriella, bintiye Jesse. “Ninafurahi sana kwamba wazazi wangu waliamua kuja hapa.”

Kwa upande mwingine, kuna watoto ambao hawakuweza kuzoeleana na hali kwa sababu mbalimbali, na familia zao zimelazimika kurudi katika nchi zao. Hiyo ndiyo sababu ni jambo la hekima kutembelea nchi ya kigeni kabla ya kuhamia huko. Kwa njia hiyo maamuzi yanaweza kufanywa kwa kutegemea yale ambayo mtu amejionea.

Baraka za Kuhama

Kwa kweli, kuna magumu mengi na dhabihu nyingi zinazohusika katika kuhamia eneo la kigeni. Je, kuhama kumewanufaisha wale waliohama? Acheni wao watuambie.

Jesse: “Miaka kumi ambayo tumekaa katika jiji la Ambato, tumeona idadi ya makutaniko ikikua kutoka makutaniko 2 hadi 11. Tumekuwa na pendeleo la kusaidia kuanzisha makutaniko matano kati ya hayo, na tumeshiriki katika kazi ya kujenga Majumba ya Ufalme mawili. Tumefurahia pia kusaidia wanafunzi wawili hivi wa Biblia kila mwaka wafikie ubatizo. Najutia kitu kimoja tu—kwamba sikuja hapa miaka kumi awali.”

Linda: “Sisi hutiwa moyo sana na jinsi watu wanavyothamini habari njema na jitihada zetu. Kwa mfano, katika mji mmoja mdogo ulio msituni, mwanafunzi wa Biblia aitwaye Alfonso aling’amua jinsi ambavyo ingenufaisha kutoa hotuba katika eneo lake. Alikuwa ametoka tu kuhamia nyumba yake ya mbao aliyokuwa amejenga karibuni, ambayo ilikuwa mojawapo ya nyumba chache sana za aina hiyo kijijini humo. Akiamua kwamba nyumba yake ndiyo pekee mjini iliyostahili kwa Yehova, alirudi kwenye nyumba yake ya nyasi na kuitoa hiyo nyumba mpya itumiwe na akina ndugu kama Jumba la Ufalme.”

Jim: “Wakati tunaotumia tukizungumza na watu katika huduma ni mara kumi zaidi ya wakati tunaotumia huko Marekani. Kwa kuongezea, maisha hapa ni matulivu. Bila shaka, tuna wakati mwingi wa kujifunza na kushiriki katika utumishi wa shambani.”

Sandra: “Kuona jinsi kweli ya Biblia iwezavyo kugeuza watu wawe wema zaidi kwaniridhisha sana. Wakati mmoja nilijifunza Biblia na Amada mwenye umri wa miaka 69, ambaye alikuwa na duka dogo la vyakula. Alikuwa na mazoea ya kuongeza vipimo viwili vya maji kwa kila vipimo kumi vya maziwa. Pia aliwapunja wateja wake zaidi kwa kuwauzia maziwa hayo yaliyoongezewa maji kwa kutumia kipimo kilichopunguzwa. Lakini baada ya kujifunza habari zinazozungumziwa katika kichwa kidogo ‘Ufuatiaji-Haki Huleta Furaha’ katika sura ya 13 ya Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, Amada aliacha mazoea hayo mabaya. Ilikuwa furaha iliyoje kumwona akibatizwa wakati fulani baadaye!”

Karen: “Hapa ndipo mahali pekee ambapo imenibidi kumtegemea Yehova zaidi na kutumiwa naye zaidi. Urafiki wangu na Yehova umeongezeka zaidi na kuwa thabiti zaidi.”

Namna Gani Wewe?

Kwa miaka ambayo imepita maelfu ya Mashahidi wamehama kwenda kutumikia katika nchi za kigeni. Baadhi yao hukaa kwa mwaka mmoja au miwili, wengine hukaa kwa wakati usio dhahiri. Wao hutumia uzoefu wao, ukomavu wao wa kiroho, na fedha zao, wakiwa na mradi wa kuendeleza masilahi ya Ufalme katika maeneo ya kigeni. Wameweza kutumikia katika maeneo ambako wahubiri wa Ufalme wa huko hawangeweza kutumikia kwa sababu ya uhaba wa kazi ya kimwili. Wengi wamenunua magari yenye kuendeshwa kwa magurudumu yote manne ili kuhubiri katika maeneo ambayo vinginevyo hayafikiki. Wengine, kwa kupendelea zaidi maisha ya mjini, wameimarisha makutaniko makubwa yenye wazee wachache. Hata hivyo, wote husisitiza kwamba wamepata baraka nyingi za kiroho kuliko zile ambazo wao wametoa.

Je, unaweza kushiriki pendeleo la kutumikia katika eneo la kigeni? Ikiwa hali zako zakuruhusu, kwa nini usichunguze uwezekano wa kuchukua hatua hiyo? Hatua ya kwanza muhimu ni kuandikia ofisi ya tawi ya Sosaiti katika nchi ambayo unafikiria kwenda kutumikia. Habari hususa utakayopata itakusaidia kuamua kama unaweza kufanikiwa. Kwa kuongezea, madokezo mengi yawezayo kutumika yaweza kupatikana katika makala “Toka Katika Bara Lako na Kutoka kwa Watu wa Ukoo Wako,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1988. Kwa kuwa na mpango mzuri na baraka za Yehova, labda unaweza kupata furaha ya kutumikia katika eneo la kigeni.

[Picha katika ukurasa wa 24]

TOM NA LINDA WAKIWA KATIKA NJIA ISIYOTUMIWA SANA, WAKIENDA KWA WAHINDI WA SHUAR

[Picha katika ukurasa wa 25]

WENGI HUTUMIKIA KATIKA QUITO, JIJI KUU LA EKUADO

[Picha katika ukurasa wa 25]

MAKIKO AKIHUBIRI KATIKA MILIMA YA ANDES

[Picha katika ukurasa wa 26]

FAMILIA YA HILBIG IMEKUWA IKITUMIKIA KATIKA EKUADO KWA MIAKA MITANO ILIYOPITA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki