Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 8/11 kur. 4-6
  • Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2011
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Unaweza Kuvuka na Kuingia Makedonia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la kigeni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Njia za Kupanua Huduma Yako
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Je, Nikaishi Ng’ambo?
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2011
km 8/11 kur. 4-6

Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?

1. Ni nini kilichowafanya Paulo na waandamani wake waende Makedonia?

1 Karibu mwaka wa 49 W.K., mtume Paulo aliondoka Antiokia ya Siria ili kuanza safari yake ya pili ya umishonari. Alikusudia kutembelea Efeso na majiji mengine katika Asia Ndogo. Hata hivyo, kupitia mwongozo wa roho takatifu, alipata mwaliko wa ‘kuvuka aingie Makedonia.’ Paulo na waandamani wake waliukubali mwaliko huo kwa furaha, na wakawa na pendeleo la kuanzisha kutaniko la kwanza katika eneo hilo. (Mdo. 16:9, 10; 17:1, 2, 4) Leo, maeneo fulani ya shamba la ulimwenguni pote yana uhitaji mkubwa wa wafanyakazi wa mavuno. (Mt. 9:37, 38) Je, unaweza kusaidia?

2. Kwa nini wahubiri wengine hawajafikiria kuhamia nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote?

2 Labda ungependa kuwa mmishonari kama Paulo lakini hujafikiria kwa uzito kuhamia nchi ya kigeni. Kwa mfano, huenda huwezi kuhudhuria Shule ya Gileadi kwa sababu ya umri wako au wewe ni dada mseja au una watoto wadogo. Yawezekana hujafikiria kuhamia nchi ya kigeni kwa sababu una wasiwasi kwamba utalazimika kujifunza lugha nyingine. Au, labda wewe ni mhamiaji kwa sababu za kiuchumi na hivyo unasita kuhama. Hata hivyo, baada ya kufikiria jambo hilo kwa uzito na kusali, huenda ukaona kwamba unaweza kuhamia nchi ya kigeni au katika eneo lenye uhitaji ambalo halijagawiwa yeyote.

3. Kwa nini si lazima mtu awe na mazoezi ya umishonari ili ahubiri kwa mafanikio katika nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote?

3 Je, Kuwa na Mazoezi ya Umishonari ni Takwa? Ni nini kilichofanya Paulo na waandamani wake wafanikiwe? Walimtegemea Yehova na roho takatifu yake. (2 Kor. 3:1-5) Hivyo basi, hata kama hali zako hazikuruhusu kupata mazoezi ya kipekee, bado unaweza kuhubiri kwa mafanikio katika nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote. Pia, kumbuka kwamba unaendelea kupokea mazoezi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Ukihamia nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote, utajionea mwenyewe jinsi utumishi wa umishonari ulivyo, na utapata uzoefu utakaokusaidia baadaye ikiwa utafikia mradi wako wa kuhudhuria Shule ya Gileadi au nyingine kama hiyo.

4. Kwa nini wahubiri wenye umri mkubwa hawapaswi kukata kauli kwamba hawawezi kwenda kuhubiri katika nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote?

4 Wahubiri Wenye Umri Mkubwa: Wahubiri wenye umri mkubwa ambao ni wakomavu kiroho, na walio na afya nzuri wanaweza kusaidia sana katika nchi au maeneo yenye uhitaji. Je, umestaafu? Kwa kuwa gharama ya maisha iko chini katika nchi zinazoendelea au maeneo ya mashambani ikilinganishwa na nchi walimozaliwa, wahubiri wengine wanaohamia huko wanaweza kuishi vizuri na kukimu mahitaji yao hata kama wana malipo kidogo ya uzeeni.

5. Simulia kisa cha ndugu aliyestaafu ambaye alihamia nchi ya kigeni.

5 Ndugu mmoja aliyestaafu, kutoka nchi inayotumia lugha ya Kiingereza, ambaye ni painia na mzee wa kutaniko, alihamia eneo la Kusini-mashariki mwa Asia lenye watalii wengi ili kusaidia kikundi cha Kiingereza kilicho na wahubiri tisa. Kikundi hicho kiliwahubiria wageni 30,000 walioishi katika eneo hilo. Baada ya miaka miwili, watu 50 walikuwa wakihudhuria mikutano. Ndugu huyo aliandika hivi: “Kuhamia hapa kumeniletea baraka nzuri ajabu ambazo sijawahi kupata. Hata hazihesabiki!”

6. Simulia kisa cha dada mseja ambaye alihamia nchi yenye uhitaji mkubwa.

6 Dada Waseja: Yehova anawatumia akina dada kwa njia kubwa ili kusambaza habari njema katika nchi au maeneo yenye uhitaji mkubwa. (Zab. 68:11) Dada mmoja mseja mwenye umri mdogo alikuwa na mradi wa kuongeza utumishi wake katika nchi ya kigeni, lakini wazazi wake walikuwa na wasiwasi kuhusu usalama wake. Hivyo, alichagua nchi ambayo haikuwa na mizozo ya kisiasa wala matatizo ya kiuchumi, akaandikia ofisi ya tawi, na akapokea habari hususa zilizomsaidia sana. Katika kipindi cha miaka sita aliyoishi huko, alifurahia baraka nyingi. Anasema: “Nyumbani, sikuwa na nafasi nyingi za kuanzisha mafunzo ya Biblia. Lakini, kutumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa kumeniwezesha kuongoza mafunzo mengi na kuboresha uwezo wangu wa kufundisha.”

7. Simulia kisa cha familia ambayo ilihamia nchi ya kigeni.

7 Familia: Ikiwa una watoto, je, hilo linamaanisha kwamba haiwezekani kuhamia nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote ili kueneza habari njema? Familia moja yenye watoto wawili, mmoja mwenye umri wa miaka minane na mwingine miaka kumi, waliamua kujaribu. Mama anaandika hivi kuhusu jambo hilo: “Tunafurahi sana kwamba tuliweza kuwalea watoto wetu hapa, kwa kuwa walishirikiana na mapainia wa pekee na wamishonari. Maisha yetu yameboreka kwa sababu ya kutumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa.”

8. Je, inawezekana kutumika katika nchi ya kigeni au katika eneo ambalo halijagawiwa yeyote bila kujifunza lugha nyingine? Eleza.

8 Wasiwasi kwa Sababu ya Lugha: Je, kufikiri kwamba utalazimika kujifunza lugha ya kigeni kunakuzuia kuhamia nchi au eneo lingine? Yaelekea kwamba lugha yako inazungumzwa pia katika nchi au maeneo yaliyo na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Mume na mke fulani wanaozungumza Kiingereza walihamia nchi inayotumia lugha ya Kihispania lakini yenye wahamiaji wengi wanaozungumza Kiingereza. Baada ya kupokea habari kutoka ofisi ya tawi kuhusu makutaniko kadhaa ya Kiingereza ambayo yalikuwa na uhitaji, walichagua kutaniko moja na wakalitembelea mara mbili. Walirudi nyumbani, wakapunguza gharama zao za kila mwezi, na wakawa wakihifadhi pesa kwa mwaka mmoja. Walipokuwa tayari kuhama, akina ndugu wa eneo walimokuwa wakihamia waliwasaidia kupata nyumba ambayo wangeweza kugharimia.

9, 10. Wahubiri ambao ni wahamiaji wanaweza kufikiria kuhusu nini, na kwa nini?

9 Wahamiaji: Je, wewe ni mhamiaji, na labda ulihama kabla ya kujifunza kweli? Huenda kukawa na uhitaji wa wafanyakazi wa mavuno katika nchi ulimozaliwa. Unaweza kufikiria kurudi ili kusaidia? Yaelekea utapata kazi na mahali pa kuishi kwa urahisi zaidi kuliko mtu anayetoka nchi ya kigeni. Huenda pia tayari unaijua lugha inayotumiwa katika nchi ulimozaliwa. Kwa kuongezea, unapowahubiria watu, huenda wakawa tayari zaidi kukusikiliza kuliko vile wangemsikiliza mtu ambaye wanamwona kuwa mgeni.

10 Mwanamume mmoja kutoka Albania alienda Italia akiwa mkimbizi ambako alipata kazi nzuri na akawa akituma pesa nyumbani. Baada ya kujifunza kweli, alianza kufunza Kialbania kikundi cha mapainia wa pekee kutoka Italia, ambao walikuwa wanahamia Albania ili kuhubiri katika eneo lenye uhitaji mkubwa. Ndugu huyo aandika: “Walikuwa wakielekea eneo nililotoka. Ijapokuwa hawakujua lugha inayozungumzwa huko, walikuwa na hamu kubwa ya kwenda huko. Mimi ni mwenyeji wa Albania. Ninafanya nini Italia?” Ndugu huyo aliamua kurudi Albania ili kusaidia kueneza habari njema. Anasema: “Je, ninajuta kuacha kazi na pesa nchini Italia? Sijuti kamwe! Nilipata kazi bora Albania. Kwangu mimi, kazi bora na inayoleta shangwe ya kudumu ni kazi ya kumtumikia Yehova kwa vyote ulivyo navyo!”

11, 12. Wale ambao wanafikiria kuhamia nchi nyingine au eneo ambalo halijagawiwa yeyote wanapaswa kufanya nini?

11 Jinsi ya Kufanya Hivyo: Kabla ya kwenda Makedonia, Paulo na waandamani wake walitaka kuelekea magharibi, lakini kwa kuwa “walikatazwa na roho takatifu,”waligeuka na kuelekea kaskazini. (Mdo. 16:6) Walipokaribia Bithinia, Yesu aliwazuia kuingia humo. (Mdo. 16:7) Yehova, kupitia Yesu, anaendelea kuisimamia kazi ya kuhubiri. (Mt. 28:20) Hivyo basi, ikiwa unafikiria kuhusu kuhamia nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote, tafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala.—Luka 14:28-30; Yak. 1:5; ona sanduku “Jinsi ya Kujua Kama Nchi au Eneo Ambalo Halijagawiwa Yeyote Unalofikiria Kuhamia Lina Uhitaji.”

12 Waombe wazee na wahubiri wengine wakomavu wakueleze kwa unyoofu kama unaweza kufaulu katika utumishi huo. (Met. 11:14; 15:22) Soma habari zilizochapishwa kuhusu kutumika katika nchi ya kigeni, na pia ufanye utafiti kuhusu nchi au eneo ambalo ungependa kuhamia. Je, unaweza kutembea huko kwanza, labda kwa siku chache tu? Ikiwa unafikiria kwa uzito kuhusu kuhamia nchi au eneo lingine, unaweza kuiandikia ofisi ya tawi ya nchi hiyo ili upate habari zaidi ukitumia anwani iliyo katika Kitabu cha Mwaka cha karibuni. Hata hivyo, badala ya kuituma barua yako moja kwa moja kwa ofisi ya tawi, wapatie wazee wa kutaniko lako, ambao wataongeza maelezo yao kabla ya kuituma.—Ona Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 111-112.

13. Ofisi ya tawi itakusaidia katika njia gani, lakini wewe una jukumu gani?

13 Ofisi ya tawi itakutumia habari muhimu kuhusu nchi au eneo ili kukusaidia kufanya maamuzi, lakini haitakupa barua za ufadhili, vyeti vya ukaaji, viza, au msaada wowote unaohusiana na uhamiaji wala kukutafutia makao. Hiyo ni mipango ya kibinafsi ambayo ni lazima uchunguze na kuishughulikia wewe mwenyewe kabla ya kuhama. Isitoshe, ni jukumu lako kuwasiliana na ofisi za ubalozi ili kupata habari kuhusu matakwa ya kupata viza na vibali vya kazi. Wahubiri wanaotaka kuhama wanapaswa kuwa na uwezo wa kushughulikia mahitaji yao ya kibinafsi, na matakwa ya kisheria.—Gal. 6:5.

14. Unapaswa kuchukua tahadhari gani unapohamia eneo ambalo kazi yetu iko chini ya vizuizi?

14 Nchi Ambazo Kazi Yetu Iko Chini ya Vizuizi: Katika nchi nyingine, ndugu na dada hulazimika kujihadhari sana kuhusiana na ibada. (Mt. 10:16) Wahubiri wanaotembelea au kuhamia huko wanaweza kuvutia uangalifu kwa kazi yetu hata bila kukusudia na hivyo kuhatarisha usalama wa ndugu wenyeji. Ikiwa unafikiria kuhamia nchi kama hiyo, tafadhali ijulishe ofisi ya tawi ya nchi yako kupitia baraza la wazee la kutaniko lenu kabla ya kufanya mipango zaidi.

15. Watu ambao hawawezi kuhama kwa sababu ya hali nyingine mbalimbali wanaweza kupanuaje huduma yao katika eneo la kwao?

15 Ikiwa Hali Hazikuruhusu Kabisa Kuhama: Ikiwa huwezi kuhamia nchi nyingine au eneo lingine, usife moyo. Labda umefunguliwa ‘mlango mwingine mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.’ (1 Kor. 16:8, 9) Huenda mwangalizi wa mzunguko wako akajua uhitaji uliopo katika eneo lenu. Labda unaweza kusaidia katika kutaniko au kikundi cha lugha ya kigeni kilicho karibu nawe. Au unaweza kupanua huduma yako katika kutaniko unaloshirikiana nalo sasa. Hata iwe hali zako ni zipi, jambo la maana zaidi ni kwamba unashiriki ibada kwa moyo wote.—Kol. 3:23.

16. Tunapaswa kuwatendeaje wale wanaotaka kuhamia nchi au eneo lingine?

16 Unamfahamu Mkristo yeyote mkomavu ambaye ana mradi wa kutumika katika nchi ya kigeni au eneo ambalo halijagawiwa yeyote? Basi mtegemeze na umtie moyo! Kufikia wakati ambapo Paulo aliondoka Antiokia ya Siria, jiji hilo lilikuwa la tatu kwa ukubwa katika Milki ya Roma (baada ya Roma na Aleksandria). Kwa kuwa eneo lilikuwa kubwa, yaelekea kutaniko la Antiokia lilihitaji msaada wa Paulo na kina ndugu wa huko wangemkosa sana ikiwa angeondoka. Hata hivyo, Biblia haionyeshi kwamba ndugu hao walimvunja Paulo moyo asiende. Inaonekana kwamba hawakufikiria tu eneo lao, bali walikumbuka kuwa “shamba ni ulimwengu.”—Mt. 13:38.

17. Ni sababu gani zinazotuchochea tufikirie kuhusu ‘kuvuka tuingie Makedonia’?

17 Paulo na waandamani wake walibarikiwa sana kwa kukubali mwaliko wa kwenda Makedonia. Walipokuwa katika jiji la Filipi, walimpata Lidia, na “Yehova akafungua wazi moyo wake asikilize kwa makini mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo.” (Mdo. 16:14) Wazia shangwe ambayo Paulo na wamishonari wenzake walipata wakati Lidia na nyumba yake yote walipobatizwa! Katika nchi nyingi, kuna watu wanyoofu kama Lidia ambao bado hawajahubiriwa ujumbe wa Ufalme. Ikiwa ‘utavuka uingie Makedonia,’ unaweza kuwa na shangwe ya kupata watu kama hao na kuwasaidia.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Jinsi ya Kujua Kama Nchi au Eneo Ambalo Halijagawiwa Yeyote Unalofikiria Kuhamia Lina Uhitaji

• Ona Kitabu cha Mwaka cha karibuni. Angalia hasa takwimu ya nchi hiyo inayolinganisha idadi ya watu na ile ya wahubiri au uwasiliane na ofisi ya tawi ili kupata habari kuhusu eneo ambalo halijagawiwa yeyote.

• Tumia Fahirisi ili kupata makala na mambo yaliyoonwa yanayohusiana na nchi hiyo.

• Zungumza na wahubiri ambao wametembelea au kuishi katika nchi au eneo hilo.

• Ikiwa unafikiria kuhamia nchi au eneo ambamo utaweza kuhubiri katika lugha yako, wasiliana na ofisi ya tawi au kutaniko lililo karibu na eneo hilo ili kujua idadi ya watu wanaozungumza lugha hiyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki