Unaweza Kumpata Ndugu Yako
“Nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.”—MATHAYO 18:15.
1, 2. Yesu alitoa shauri gani lenye kutumika kuhusu kushughulikia makosa?
KUKIWA kumebaki muda unaopungua mwaka mmoja wa huduma yake, Yesu alifundisha wanafunzi wake masomo muhimu. Unaweza kuyasoma katika Mathayo sura ya 18. Mojawapo ya masomo hayo lilikuwa ni umuhimu wa kuwa wanyenyekevu kama watoto. Kisha akakazia kwamba ni lazima tuepuke kukwaza ‘mmoja wa wadogo hao’ na kwamba tunapaswa kujaribu kuwapata ‘wadogo hao’ ili kwamba wasiangamie. Kisha Yesu akaongezea shauri lenye kutumika na lenye manufaa sana juu ya namna ya kutatua matatizo kati ya Wakristo.
2 Huenda unakumbuka maneno yake: “Ndugu yako akifanya dhambi, nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako. Lakini ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja nawe mmoja au wawili zaidi, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila jambo lipate kuthibitishwa. Ikiwa yeye hawasikilizi wao, liambie kutaniko. Ikiwa hasikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” (Mathayo 18:15-17) Tunapaswa kutumia shauri hilo wakati gani, na tunapaswa kuwa na mtazamo upi tunapofanya hivyo?
3. Kwa ujumla twapaswa kuwa na mtazamo gani juu ya makosa ya wengine?
3 Makala iliyotangulia ilikazia kwamba kwa kuwa sisi sote hatujakamilika na tuna mwelekeo wa kufanya makosa, tunahitaji kujitahidi kuwa wenye kusamehe. Hasa wakati ambapo tumeumizwa na jambo ambalo Mkristo mwenzetu alisema au kutenda. (1 Petro 4:8) Mara nyingi ni bora kuliachilia tu kosa hilo—kusamehe na kusahau. Tunaweza kuona kusamehe kuwa kuchangia amani katika kutaniko la Kikristo. (Zaburi 133:1; Mithali 19:11) Lakini, huenda kuna pindi ambapo huenda ukahisi kwamba ni lazima usuluhishe jambo fulani na ndugu au dada yako ambaye alikuumiza. Katika hali kama hiyo, maneno ya Yesu yaliyo juu yaandaa mwongozo.
4. Kwa ujumla, tunaweza kutumiaje andiko la Mathayo 18:15 kuhusu makosa ya wengine?
4 Yesu alishauri kwamba “ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake.” Hilo ni jambo la hekima. Tafsiri nyingine za Kijerumani zasema, uwasilishe kosa lake “mbele ya macho manne,” yaani macho yako na macho yake. Unapowasilisha tatizo kwa fadhili na kwa faragha, mara nyingi ni rahisi kutatuliwa. Ndugu ambaye alitenda au kusema jambo lenye kuudhi au lisilo la fadhili huenda akakiri mara moja kosa hilo ukiwa peke yako. Iwapo wengine wanasikiliza, asili ya wanadamu wasiokamilika huenda ikamfanya awe na mwelekeo wa kukana kuwa alitenda kosa au ajaribu kujitetea juu ya tendo lake. Lakini ukiwasilisha suala hilo “mbele ya macho manne,” unaweza kupata kwamba tatizo lilikuwa kutoelewana wala si dhambi au kosa la kimakusudi. Nyote mnapogundua kwamba kumbe ni kutoelewana, mnaweza kulisuluhisha, bila kuachilia jambo dogo liwe kubwa na kuharibu uhusiano wenu. Basi kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 18:15 inaweza kutumiwa hata kusuluhisha makosa madogo-madogo katika maisha ya kila siku.
Alimaanisha Nini?
5, 6. Kulingana na muktadha, andiko la Mathayo 18:15 linarejezea dhambi za aina gani, na ni nini kinachoonyesha jambo hilo?
5 Shauri la Yesu hasa lilihusu mambo mazito zaidi. Yesu alisema: “Ndugu yako akifanya dhambi.” Kwa ujumla, “dhambi” inaweza kuwa kosa lolote au kasoro yoyote. (Ayubu 2:10; Mithali 21:4; Yakobo 4:17) Lakini, muktadha wadokeza kwamba ni lazima Yesu alimaanisha dhambi nzito. Ilikuwa nzito kiasi cha kwamba ingeweza kufanya mkosaji aonwe “kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Maneno hayo yadokeza nini?
6 Wanafunzi wa Yesu waliosikia maneno hayo walijua kwamba Wayahudi wenzao hawakuwa na shughuli na watu wasio Wayahudi. (Yohana 4:9; 18:28; Matendo 10:28) Nao bila shaka waliwaepuka wakusanya-kodi, wanaume Wayahudi ambao waligeuka wakawa wanawadhulumu watu. Basi andiko la Mathayo 18:15-17 lilikuwa likirejezea hasa dhambi nzito, si kuumizwa au makosa madogo-madogo ya kibinafsi ambayo unaweza kusamehe tu na kusahau.—Mathayo 18:21, 22.a
7, 8. (a) Ni dhambi za aina gani zinazohitaji kushughulikiwa na wazee? (b) Ni dhambi za aina gani zingeweza kusuluhishwa kati ya Wakristo wawili, kwa kupatana na Mathayo 18:15-17?
7 Katika Sheria, dhambi nyingine hazikuhitaji msamaha tu wa mtu aliyekosewa. Kukufuru, uasi, ibada ya sanamu, na dhambi za kingono za uasherati, uzinzi, na ugoni wa jinsia moja zilipasa kuripotiwa kwa wazee (au makuhani) wazishughulikie. Na ndivyo ilivyo katika kutaniko la Kikristo. (Mambo ya Walawi 5:1; 20:10-13; Hesabu 5:30; 35:12; Kumbukumbu la Torati 17:9; 19:16-19; Mithali 29:24) Lakini, ona kwamba aina za dhambi ambazo Yesu alirejezea zingeweza kusuluhishwa kati ya watu wawili. Kwa mfano: Kwa sababu ya hasira au wivu, mtu amchongea mwenzake. Mkristo achukua kandarasi ya kufanya kazi fulani akitumia vifaa fulani hususa na kumaliza kazi hiyo kufikia tarehe fulani. Mkristo mwingine akubali kwamba atalipa deni kufikia tarehe fulani. Mtu aahidi kwamba mwajiri wake akimzoeza kazi, hatashindana naye (hata kama anabadili kazi) wala hatajaribu kuchukua wateja wa mwajiri wake kwa muda fulani au katika eneo fulani.b Ikiwa ndugu hawezi kutimiza ahadi yake na haonyeshi toba kwa makosa kama hayo, kwa hakika hilo lingekuwa jambo zito. (Ufunuo 21:8) Lakini makosa kama hayo yanaweza kusuluhishwa kati ya watu hao wawili wanaohusika.
8 Hata hivyo, wewe ungetatuaje jambo hilo? Mara nyingi maneno ya Yesu yameonwa kuwa yenye hatua tatu. Ebu tuchunguze kila hatua. Badala ya kuziona kama sheria kali zisizobadilikana, jaribu kupata maana ya maneno ya Yesu, bila kusahau lengo lako lenye upendo.
Jitahidi Kumpata Ndugu Yako
9. Tunapaswa kuzingatia nini tutumiapo Mathayo 18:15?
9 Yesu alianza kwa kusema: “Ndugu yako akifanya dhambi, nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.” Kwa wazi, hii si hatua inayotegemea mambo ya kushuku tu. Unapaswa kuwa na uthibitisho au habari hususa uwezayo kutumia ili kusaidia ndugu yako aone kwamba alikosea na anahitaji kunyosha mambo. Ni vizuri kuchukua hatua haraka iwezekanavyo, bila kuachilia jambo hilo likue au mtazamo wake uzidi kuwa mbaya. Na usisahau kwamba kufikiria sana jambo hilo kwaweza kukuumiza pia. Na kwa kuwa mazungumzo yatakuwa kati yenu mkiwa wawili tu, epuka kuzungumza na wengine kabla ya kuongea naye ili uonewe huruma au ili ujionyeshe kuwa bora. (Mithali 12:25; 17:9) Kwa nini? Kwa sababu ya lengo lako.
10. Ni nini kitakachotusaidia tumpate ndugu yetu?
10 Lengo lako lapasa kuwa kumpata ndugu yako, wala si kumwadhibu, kumshushia heshima, au kumwumiza. Ikiwa kweli ametenda kosa, uhusiano wake na Yehova umo hatarini. Kwa kweli unataka abaki akiwa ndugu yako wa Kikristo. Uwezekano wa kufanikiwa utaongezeka ikiwa unabaki mtulivu, ukiepuka maneno makali au hali ya kushtaki-shtaki katika mazungumzo yenu ya faragha. Katika kikao hicho chenye upendo, kumbuka kwamba nyote wawili ni wanadamu wenye dhambi ambao hawajakamilika. (Waroma 3:23, 24) Atambuapo kwamba hujapiga porojo kumhusu na kwamba kwa kweli unataka kusaidia, huenda mkapata suluhisho haraka. Mfikio huo wa wazi na wenye fadhili hasa utakuwa njia ya hekima inapotokea kwamba kumbe nyote wawili mlikosea kwa kadiri fulani au kwamba tatizo kubwa lilikuwa ni kutoelewana.—Mithali 25:9, 10; 26:20; Yakobo 3:5, 6.
11. Hata kama mkosaji hatusikilizi tunaweza kufanya nini?
11 Ukimsaidia aone kwamba kosa lilifanyika na kwamba ni kosa zito, huenda akasukumwa kutubu. Lakini, kwa kweli kiburi chaweza kutatiza. (Mithali 16:18; 17:19) Kwa hiyo hata kama mwanzoni hakubali kosa alilofanya na kutubu, unaweza kungoja kidogo kabla ya kufuatilia jambo hilo tena. Yesu hakusema ‘nenda mara moja tu ufunue wazi kosa lake.’ Kwa sababu hiyo ni dhambi ambayo mnaweza kusuluhisha, fikiria kumwendea tena kwa roho ya Wagalatia 6:1 na “mbele ya macho manne.” Huenda ukafaulu. (Linganisha Yuda 22, 23.) Lakini, namna gani ikiwa una hakika kwamba dhambi imefanywa, naye amekataa kukubali?
Kupata Msaada wa Watu Wakomavu
12, 13. (a) Yesu alitaja hatua gani ya pili ya kushughulikia makosa? (b) Kuna tahadhari zipi zifaazo unapochukua hatua hiyo?
12 Je, ungependa wengine wakuachilie kwa urahisi tu ikiwa una hatia ya kutenda kosa zito? La. Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba baada ya hatua ya kwanza, usiache kujaribu kumpata ndugu yako, ili kumfanya aendelee kuwa na umoja pamoja nawe na wengine katika kumwabudu Mungu ifaavyo. Yesu alitaja hatua ya pili: “Ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja nawe mmoja au wawili zaidi, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila jambo lipate kuthibitishwa.”
13 Alisema chukua “mmoja au wawili zaidi.” Yeye hakusema kwamba baada ya kuchukua hatua ya kwanza, uko huru kuongea na wengine juu ya tatizo hilo, kuongea na mwangalizi asafiriye, au kuandikia akina ndugu juu ya tatizo hilo. Hata kama una hakika kabisa kwamba kosa hilo lilifanyika, bado halijathibitishwa kabisa. Haitafaa kueneza habari za uwongo ambazo zingeweza kugeuka kuwa uchongezi kwa upande wako. (Mithali 16:28; 18:8) Lakini Yesu alisema uchukue mmoja au wawili zaidi. Kwa nini? Nao wanaweza kuwa nani?
14. Twaweza kuchukua nani katika hatua ya pili?
14 Unajaribu kumpata ndugu yako kwa kumsadikisha kwamba amefanya dhambi na kwa kumfanya atubu ili awe na amani pamoja nawe na pamoja na Mungu. Ili kutimiza jambo hilo, ingekuwa afadhali kama huyo “mmoja au wawili” walishuhudia kosa likifanywa. Labda walikuwapo kosa lilipofanywa, au wana habari yenye msingi mzuri juu ya jambo lililofanywa (au halikufanywa) katika suala la kibiashara. Ikiwa hakuna mashahidi kama hao, wale unaowachukua huenda wakawa wenye ujuzi wa suala linalozungumziwa na basi wanaweza kuthibitisha kama jambo lililotendeka kwa kweli ni kosa. Isitoshe, ikihitajiwa baadaye, wao wanaweza kuwa mashahidi wa jambo lililosemwa, wakithibitisha mambo yaliyosemwa na jitihada iliyofanywa. (Hesabu 35:30; Kumbukumbu la Torati 17:6) Basi hao si watu wasiohusika tu, waamuzi; lakini, kuwapo kwao ni kusaidia kumpata ndugu yako na ndugu yao.
15. Kwa nini wazee Wakristo wanaweza kusaidia ikiwa ni lazima tuchukue hatua ya pili?
15 Usifikiri kwamba wale unaowachukua ni lazima wawe wazee kutanikoni. Lakini, wanaume wakomavu ambao ni wazee wanaweza kuchangia kwa sababu ya sifa zao za kiroho. Wazee kama hao ni “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:1, 2) Wao wana ujuzi wa kusababu na akina ndugu na dada na kuwarekebisha. Na mkosaji ana sababu nzuri ya kuonyesha uhakika katika “zawadi zikiwa wanadamu.” c (Waefeso 4:8, 11, 12) Kuzungumzia mambo mbele ya watu wakomavu kama hao na kusali pamoja nao kwaweza kuleta mazingira mapya na kutatua suala lililoonekana kama haliwezi kutatuliwa.—Linganisha Yakobo 5:14, 15.
Jitihada ya Mwisho ya Kumpata Ndugu Yako
16. Yesu alitaja hatua gani ya tatu?
16 Hatua ya pili ikishindwa kusuluhisha suala hilo, bila shaka waangalizi wa kutaniko wanahusika katika hatua ya tatu. “Ikiwa yeye hawasikilizi wao [yule mmoja au wale wawili], liambie kutaniko. Ikiwa hasikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Hilo lahusisha nini?
17, 18. (a) Ni kielelezo gani kinachotusaidia kuelewa kinachomaanishwa na ‘kuliambia kutaniko’? (b) Tunatumiaje hatua hii leo?
17 Mwelekezo huo haumaanishi kuleta dhambi hiyo au kosa hilo kwenye mkutano wa kawaida au kwenye mkutano wa pekee wa kutaniko lote. Twaweza kujua utaratibu ufaao kutokana na Neno la Mungu. Ona jinsi mambo yalivyopasa kufanywa katika Israeli la kale kuhusu uasi, ulafi, na ulevi: “Mtu akiwa na mwana mkaidi, mshupavu, asiyetii sauti ya baba yake, wala sauti ya mama yake, nao wajapomwadhibu hawasikizi, ndipo babaye na mamaye na wamkamate, na kumpeleka kwa wazee wa mji wake, katika lango la mahali pake; wawaambie wazee wa mji wake, Huyu mwana wetu ni mkaidi, mshupavu, hasikizi sauti yetu; ni mwasherati, tena ni mlevi. Waume wote wa mji wake na wamtupie mawe.”—Kumbukumbu la Torati 21:18-21, italiki ni zetu.
18 Dhambi za mtu huyo hazikusikilizwa na kuamuliwa na taifa lote wala na kabila lake lote. Badala yake, “wazee” waliotambuliwa walishughulikia dhambi hiyo wakiwa wawakilishi wa kutaniko. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 19:16, 17 kuhusu kesi iliyoshughulikiwa na ‘makuhani na waamuzi waliokuwapo siku hizo.’) Leo vilevile, inapokuwa lazima kuchukua hatua ya tatu, wazee, wanaowakilisha kutaniko, hushughulikia jambo hilo. Wana lengo lilelile, la kumpata ndugu Mkristo ikiwezekana. Wao huonyesha hilo kwa kuwa wasiopendelea, bila kuhukumu kesi kimbele au kubagua.
19. Wazee wanaochaguliwa kusikiliza kesi hiyo watajitahidi kufanya nini?
19 Wao watajitahidi kupima mambo na kusikiliza mashahidi wanaohitajiwa ili kuthibitisha kama kweli dhambi imefanywa (au inaendelea kufanywa). Wanataka kulinda kutaniko dhidi ya ufisadi na kuzuia roho ya ulimwengu. (1 Wakorintho 2:12; 5:7) Kwa kupatana na sifa zao za Kimaandiko, wao watajitahidi “kuhimiza kwa bidii kwa fundisho lililo lenye afya na pia kukaripia wale ambao hupinganisha.” (Tito 1:9) Tunatumaini kwamba mkosaji hatakuwa kama Waisraeli ambao nabii wa Yehova aliandika hivi kuwahusu: “Nilipoita hamkuitika; niliponena, hamkusikia; bali mlitenda yaliyo mabaya machoni pangu, mlichagua mambo nisiyoyafurahia.”—Isaya 65:12.
20. Yesu alisema ni lazima nini litendeke ikiwa mtenda-dhambi anakataa kusikiliza na kutubu?
20 Hata hivyo, katika visa vichache, mtenda-dhambi huonyesha mtazamo uleule. Ikiwa ndivyo ilivyo, mwelekezo wa Yesu ni wazi: “Mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Bwana hakupendekeza tuwe wakatili au kuwa na lengo lolote la kuumiza. Hata hivyo, hakuna utatanishi wowote kuhusu mwelekezo wa mtume Paulo wa kutenga watenda-dhambi wasiotubu kutoka kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Hata hatua hiyo huenda hatimaye ikatimiza lengo la kumpata mtenda-dhambi.
21. Kunabaki uwezekano gani kwa mtu ambaye ametengwa na kutaniko?
21 Tunaweza kuona uwezekano wa kumpata tena kutokana na mfano wa Yesu wa mwana mpotevu. Kama ilivyoonyeshwa, baada ya kukaa kwa muda fulani mbali na ushirika wenye upendo katika nyumba ya babake, mtenda-dhambi huyo ‘alirudiwa na fahamu zake.’ (Luka 15:11-18) Paulo alimtajia Timotheo kwamba wakosaji wengine wangetubu hatimaye na “kurudiwa na fahamu zao nzuri kutoka katika mtego wa Ibilisi.” (2 Timotheo 2:24-26) Twatumaini kwamba watu wanaotenda dhambi bila kutubu na ambao ni lazima watengwe na kutaniko watahisi wamepoteza kitu—kibali cha Mungu na vilevile ushirika mchangamfu na mawasiliano na Wakristo waaminifu-washikamanifu—na kurudiwa na fahamu zao.
22. Bado tunawezaje kumpata ndugu yetu?
22 Yesu hakuwaona watu wa mataifa na wakusanya-kodi kuwa watu wasioweza kukombolewa. Mmojawapo wa wakusanya-kodi, Mathayo Lawi, alitubu, ‘akamfuata Yesu’ kwa moyo mweupe na hata akachaguliwa kuwa mtume. (Marko 2:15; Luka 15:1) Basi, leo mtenda-dhambi ‘asiposikiliza hata kutaniko’ na kutengwa, tunaweza kungoja na kuona ikiwa, baada ya muda fulani, atatubu na kunyosha njia zake. Anapofanya hivyo na kuwa mshiriki wa kutaniko tena, basi tutafurahi kwamba tumempata tena ndugu yetu katika ushirika wa ibada ya kweli.
[Maelezo ya Chini]
a Kitabu Cyclopedia cha McClintock na Strong chasema: “Wakusanya-kodi wa Agano Jipya walionwa kuwa wahaini na waasi-imani, waliochafuliwa kwa kuchangamana sana na wapagani, na walio tayari kutumiwa na waonezi. Wao walionwa kuwa sehemu ya watenda-dhambi . . . Wakiwa wametengwa, watu wenye heshima waliwaepuka, na rafiki zao au waandamani wao wa pekee walikuwa watu ambao pia walikuwa wametengwa.”
b Masuala ya kibiashara au ya kifedha yanayohusisha kadiri fulani ya udanganyi, upunjaji, au ujanja yanaweza kutiwa miongoni mwa dhambi ambayo Yesu alimaanisha. Hilo ladokezwa na jambo la kwamba baada ya kutoa mwelekezo uliorekodiwa kwenye Mathayo 18:15-17, Yesu alitoa kielezi cha watumwa (waajiriwa) ambao walikuwa na deni, wakashindwa kulipa.
c Msomi mmoja wa Biblia alieleza: “Nyakati nyingine hutukia kwamba mkosaji atakuwa tayari zaidi kupokea shauri la wawili au watatu (hasa ikiwa ni watu wenye kuheshimika) kuliko la mtu mmoja, hasa ikiwa huyo ni mtu ambaye amepata kutofautiana naye kwa maoni wakati mwingine.”
Je, Wakumbuka?
◻ Andiko la Mathayo 18:15-17 lahusu hasa dhambi ya aina gani?
◻ Tukumbuke nini ikiwa ni lazima tuchukue hatua ya kwanza?
◻ Ni nani wanaoweza kusaidia ikiwa ni lazima tuchukue hatua ya pili?
◻ Ni nani wanaohusika katika kuchukua hatua ya tatu, na bado twawezaje kumpata ndugu yetu?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wayahudi waliwaepuka wakusanya-kodi. Mathayo alirekebisha mwenendo wake, akamfuata Yesu
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mara nyingi twaweza kusuluhisha jambo “mbele ya macho manne”