Jitihada Yao ya Kutafuta Dini ya Kweli
TANGU utoto watu fulani wametafuta majibu yenye kuridhisha kwa maswali yao juu ya uhai. Wakiwa wachanga, huenda wakawa walihudhuria mahubiri ya kidini. Lakini wengi wao walipata kwamba wala majibu yanayotolewa wala desturi za kanisa kwa kweli hazijawasaidia kukabiliana na matatizo ya maisha.
Huenda wakasema kwamba wangali ni washiriki wa dini ya wazazi wao, ingawa wao huhudhuria mahubiri ya kidini mara chache. Kulingana na askofu fulani wa Church of England, imani yao ni ndogo sana. Wao wameweka dini kando. Wengine, wakiwa wamechukizwa na unafiki wanaoona katika washiriki wa dini, wameikataa dini kabisa. Hata hivyo, maswali yao juu ya maisha huendelea.
Kinachowasababisha Wengi Watilie Shaka Sana
Watu walio wengi wajua kwamba makanisa yana mashirika ya kuwasaidia wale wasio na makao, ya kugawa chakula kwa wale wenye uhitaji, na ya kudhamini sherehe za kitamaduni. Lakini karibu kila siku wao pia husikia habari za jeuri na umwagaji wa damu wenye msingi wa dini si miongoni mwa wale wasio Wakristo pekee bali pia miongoni mwa wale ambao hudai kuwa Wakristo. Je! itushangaze ikiwa wao hutilia shaka kama vile vikundi vinavyohusika katika jeuri vinazoea dini ya kweli?
Watu wengi wenye malezi ya kidini walikuwa wakifikiri kwamba makao ya mayatima yaliyodhaminiwa na makanisa yalikuwa jambo zuri. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni, wamechukizwa huku mapadri katika sehemu moja baada ya nyingine wameshtakiwa kuwatenda vibaya kingono wale watoto ambao wamekabidhiwa kuwatunza. Mwanzoni watu walifikiri kwamba ni mapadri wachache tu waliopaswa kulaumiwa. Sasa baadhi ya watu hao hujiuliza kama kuna jambo fulani lililo baya katika kanisa lenyewe.
Watu wachache, kama vile Eugenia, walikuwa wamehusika sana na dini yao wakati mmoja. Kama vile kijana fulani wa kike katika Argentina, yeye alikuwa miongoni mwa wale waliokuwa wakihiji ili kuabudu Bikira wa Itatí. Kwa muda wa miaka 14 yeye aliishi katika makao ya watawa wa kike akiwa mtawa wa kike. Kisha akaondoka ili kuwa sehemu ya kikundi cha mchanganyiko wa dini na siasa cha kimataifa kilichotetea badiliko kubwa, la mara moja, katika sehemu za jamii za watu zinazohusu jamii na fedha kwa njia ya mapinduzi. Likiwa tokeo la yale aliyoona na kupatwa nayo, yeye alipoteza imani na uhakika katika Mungu. Kwa kweli yeye hakuwa akitafuta dini ambayo angeweza kuamini. Kile alichotaka ni njia ya kuletea haki wale waliokuwa maskini—ndiyo, na rafiki ambaye yeye angeweza kutumaini.
Wengine huangalia yale yanayoendelea katika makanisa na wameepuka makanisa. Mtu fulani asiyeamini kuwako kwa Mungu ambaye maoni yake yalichapishwa 1991 katika gazeti Sputnik alisema hivi kwa unyofu: “Siwezi kuona tofauti yoyote kubwa kati ya sifa za ngano za upagani na za Kikristo.” Kikiwa kielelezo, yeye alisimulia mwandamano fulani ambamo mapadri wakiwa wamevikwa mavazi marefu yaliyotarizwa kwa uzi wa dhahabu, walitembea polepole kupitia barabara za Moscow, wakiwa wamebeba sanduku la jiwe lenye maiti aliyehifadhiwa kwa madawa. Huo ulikuwa mwili wa “Mkristo wa dini ya Orthodoksi aliyeonwa kuwa mtakatifu” uliokuwa ukihamishwa kutoka jumba la kuhifadhia mambo ya kale hadi kwenye kanisa fulani, na jambo hilo lilimkumbusha mwandikaji kuhusu makuhani na maiti waliohifadhiwa katika Misri. Alikumbuka pia, kwamba ingawa wale waliokuwa wakishiriki katika ule mwandamano huko Moscow waliamini katika “Utatu wa Kikristo,” Wamisri walikuwa pia wameabudu utatu wa miungu—Osirisi, Isisi, and Horasi.
Mwandikaji uyo huyo alirejezea wazo la Kikristo la upendo—“Mungu ni upendo,” na “mpende jirani wako”—kuwa halikufanana na jambo lolote katika Misri ya kipagani. Lakini alionelea hivi: “Upendo wa kidugu umekosa kushinda katika ulimwengu, hata katika ile sehemu yao ijiitayo ulimwengu wa Kikristo.” Na akafuatisha hilo na maelezo juu ya matunda mabaya kutokana na kule kusisitiza kwa kanisa kushiriki katika mambo ya Serikali. Yale aliyoyaona hayakumsukuma ahisi kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalitoa kile alichokuwa akitafuta.
Tofauti na hilo, wengine wamepata majibu yenye kuridhisha lakini si katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo.
Alijifunza Kweli Kuhusu Wafu
Magdalena, ambaye sasa ni wa umri wa miaka 37, huishi Bulgaria. Baada ya baba-mkwe wake kufa katika 1991, alikuwa amekata tamaa sana. Mara kwa mara alijiuliza, ‘Wafu huenda wapi? Baba-mkwe wangu yu wapi?’ Alienda kanisani, naye alisali mbele ya kisanamu akiwa nyumbani, hata hivyo hakupata majibu.
Kisha siku moja jirani alimpigia simu akimwalika nyumbani kwake. Kijana mmoja aliyekuwa akijifunza na Mashahidi wa Yehova alikuwa akimtembelea jirani huyo. Mwanamke huyo alisikiliza kijana huyo aliposema juu ya Ufalme wa Mungu na kusudi Lake la kufanya dunia iwe paradiso ambako watu wangeweza kuishi milele kwa furaha. Kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kilikuwa mezani. Kwa kukitumia, kijana huyo alielekeza uangalifu wa mwanamke huyo kwenye andiko la Biblia katika Mhubiri 9:5, lisemalo hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa.” Jioni hiyo mwanamke huyo alisoma mengi zaidi. Alijifunza kwamba wafu hawakwenda kwenye uhai mwingine mbinguni au katika helo; hawafahamu lolote, kana kwamba wamelala usingizi fofofo. Kwa furaha yeye alikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo. Baada ya mkutano yeye alikubali funzo la Biblia la kawaida. Akiwa ameona njia ambayo sala zilitolewa kwa Yehova kwenye mkutano, yeye pia alianza kusali kwa Yehova kumwomba msaada katika kushinda udhaifu uliokuwa mgumu sana kuacha. Sala yake ilipojibiwa, yeye alijua kwamba alikuwa amepata dini ya kweli.
Walipata Maisha Yenye Maana
André alikuwa amekua katika nyumba ya waumini thabiti wa Katoliki katika Ubelgiji na alikuwa ametumikia akiwa msaidizi wa padri wa hapo. Hata hivyo, wakati huo, yeye aliona mambo yaliyodhoofisha staha yake kuelekea kanisa. Likiwa tokeo, yeye alikuwa Mkatoliki kwa jina pekee.
Kwa muda wa miaka 15 alikuwa amecheza soka ya malipo. Katika pindi moja timu yake ilicheza mchezo katika Italia, walialikwa wakutane na papa. Ziara hiyo haikuwa yenye kujenga kiroho hata kidogo, na utajiri wa kilimwengu uliomzunguka papa ulimwudhi André. Shaka zake juu ya kanisa ziliongezeka. Maisha yake ya faragha hayakuwa na furaha kwa sababu ya ndoa mbili zilizovunjika. Hali ya ulimwengu ilimfadhaisha. Katika 1989 yeye aliandika hivi katika kitabu chake cha maandishi ya kila siku: ‘Ni nini maana ya mambo haya mapumbavu yanayoendelea kotekote kutuzunguka?’ Yeye hakupata majibu kutoka kwa dini yake.
Katika 1990, André alipokuwa akifanya kazi akiwa kocha wa soka katika Iceland, Iiris, ambaye ni mishonari wa Mashahidi wa Yehova, alimtembelea. André alikubali fasihi akamwalika mishonari huyo arudi. Yeye alirudi akiwa na mume wake, Kjell. Hatimaye walipoweza kuketi na kuongea pamoja na André, ilikuwa wazi kwamba yeye alipendezwa sana na kupata uelewevu wa Biblia. Mke wake, Ásta, alipendezwa vilevile. Katikati ya mchana, André alikuwa na muda wa saa tatu kati ya pindi zake za kufanya ukocha, na waliamua kutumia wakati huo kwa ajili ya funzo la Biblia. “Mimi huhisi kuburudishwa zaidi kwa kujifunza Biblia kuliko kupumzika tu,” yeye akasema. Hatua kwa hatua Biblia ilijibu maswali yao. Polepole imani yao katika Yehova na Ufalme wake ikakua. Ahadi tukufu za ulimwengu mpya wenye amani, ulimwengu usio na “mambo haya mapumbavu yanayoendelea,” ikawa halisi kwao. Sasa André na Ásta pia wanashiriki imani yao mpya pamoja na wengine.
Magdalena, André, na Ásta huhisi uhakika kwamba hatimaye walipata dini ya kweli. Eugenia pia, baada ya kujaribu kusuluhisha matatizo ya ulimwengu kupitia njia za kisiasa, hatimaye alipata miongoni mwa Mashahidi wa Yehova dini iliyoonekana kuwa ya kweli kwake. Lakini ni nini hasa linaloamua kama dini fulani ni ya kweli? Tafadhali ona habari ifuatayo.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Funzo la Biblia la kawaida pamoja na Mashahidi wa Yehova linasaidia watu zaidi ya milioni tano katika jitihada yao ya kutafuta majibu yenye kuridhisha