Je! Umeipata Dini ya Kweli?
“Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii.” —YAKOBO 1:27.
1, 2. (a) Kulingana na maoni ya watu wengi, ni nini kinachoamua kama dini yao ni ya kweli? (b) Ni nini kipaswacho kufikiriwa kwa uzito katika kuhukumu dini?
SISI tunaishi katika enzi ambayo watu wengi wameridhika kuipa dini sehemu ndogo ya maisha yao. Huenda wakahudhuria mahubiri kadhaa ya kidini, lakini ni wachache wanaofanya hivyo kwa ukawaida. Wengi hawaoni kwamba dini nyingine zote ni bandia na kwamba yao ni ya kweli. Wao huona tu kwamba dini yao inawafaa.
2 Kwa sababu hiyo, je, swali, Umepata dini ya kweli? lamaanisha tu kama, Umepata dini unayopenda? Ni nini kinachoamua kile unachopenda? Familia yako? Washiriki wako? Hisia zako? Umefikiria kwa uzito kadiri gani maoni ya Mungu juu ya jambo hilo?
Twaweza Kujuaje Maoni ya Mungu?
3. (a) Ili tujue maoni ya Mungu, ni lazima tuweze kupata nini? (b) Twapaswa kuuliza maswali gani kuhusiana na sababu sisi binafsi tunaamini kwamba Biblia inatoka kwa Mungu?
3 Ili tupate kujua yale ambayo Mungu mwenyewe hufikiri, basi lazima kuwe na ufunuo fulani kutoka kwake. Biblia ndicho kitabu cha kale zaidi kinachodai kuwa kimepuliziwa na Mungu. (2 Timotheo 3:16, 17) Lakini, je, yaweza kusemwa kwa ukweli kwamba kitabu hicho, tofauti na vingine vyote, kina ujumbe wa Mungu kwa jamii yote ya kibinadamu? Wewe ungejibuje swali hilo, na kwa nini? Je! ni kwa sababu ya mtazamo wa washiriki wako? Je! umepata kujichunguzia uthibitisho wewe mwenyewe? Kwa nini usifanye hivyo sasa, kwa kutumia mathibitisho manne?
4. Kwa habari ya kupatikana, nini kionyeshacho kwamba Biblia, badala ya kitabu kingine fulani, inatoka kwa Mungu?
4 Kupatikana: Ujumbe utokao kwa Mungu kwelikweli na ambao ni wa familia nzima ya kibinadamu wapaswa kupatikana kwa wote. Je! hiyo ni kweli kuhusiana na Biblia? Fikiria hili: Biblia nzima au sehemu yayo, inachapishwa sasa katika zaidi ya lugha 2,000. Kulingana na American Bible Society, karibu mwongo mmoja uliopita lugha ambazo Biblia ilichapishwa ziliifanya ipatikane kwa asilimia 98 ya wakazi wa ulimwengu. Kama ilivyoonyeshwa na kitabu Guinness Book of World Records, Biblia haina kifani ikiwa “kitabu kilichogawanywa zaidi ulimwenguni.” Ndilo jambo tungetazamia kuhusiana na ujumbe kutoka kwa Mungu ambao wapaswa kufikia watu wa rangi na mataifa na vikundi vyote vya lugha. (Linganisha Ufunuo 14:6.) Hakuna kitabu kingine ulimwenguni kilicho na rekodi ifikiayo hiyo hata kidogo.
5. Kwa nini msingi wa kihistoria wa Biblia ni jambo la maana?
5 Historia: Uchunguzi wenye uangalifu wa masimulizi ya Biblia hufunua njia nyingine ambayo Biblia ni tofauti na vitabu vingine vinavyodai kuwa vitakatifu. Biblia ina mambo ya hakika ya kihistoria, si hekaya zisizoweza kuthibitishwa. Irwin Linton, ambaye akiwa wakili alizoea kuchanganua mambo yaliyohitajiwa kuwa ithibati mahakamani, aliandika hivi: “Ingawa vitabu vya hadithi za kimahaba, hekaya na ushuhuda bandia huwa zenye uangalifu kuweka matukio yaliyosimuliwa katika mahali palipo mbali sana na katika wakati usio dhahiri, . . . Biblia hutupa sisi tarehe na mahali pa mambo yaliyosimuliwa kwa usahihi kabisa.” (Kupata vielelezo, ona 1 Wafalme 14:25; Isaya 36:1; Luka 3:1, 2.) Kwa watu wanaogeukia dini ili kupata kweli wala si kuepuka uhalisi wa hali, hilo ni jambo la maana kufikiria.
6. (a) Biblia kwa kweli humsaidiaje mtu na matatizo ya maisha? (b) Biblia humsaidia mtu kwa njia zipi tatu akabiliane na magumu halisi?
6 Yenye Kutumika: Wale wachunguzao Biblia kwa uzito hung’amua upesi kwamba amri na kanuni zayo hazikusudiwi kuwaumiza. Badala ya hivyo, hizo huonyesha njia ya maisha iletayo manufaa kwa wale washikamanao nazo kwa ukaribu. (Isaya 48:17, 18) Faraja inayowatolea wale wanaosononeka si ya kijuujuu tu, yenye msingi wa falsafa zisizo na maana. Badala ya hivyo, faraja hiyo husaidia watu wakabiliane na magumu halisi ya maisha. Kwa jinsi gani? Kwa njia hizi tatu: (1) kwa kutoa shauri lifaalo kuhusu jinsi ya kushughulikia magumu, (2) kwa kueleza jinsi ya kupokea ule utegemezo wenye upendo ambao Mungu hutolea watumishi wake sasa, na (3) kwa kufunua ule wakati ujao mzuri ajabu ambao Mungu amewawekea wale wanaomtumikia, akiwapa sababu nzuri za kuwa na uhakika katika ahadi zake.
7. (a) Kwa kutumia maandiko yaliyotajwa katika kielezi-chini, eleza jibu la Biblia kwa mojapo masuala makuu yanayohangaisha watu leo. (b) Onyesha jinsi shauri la Biblia hutulinda sisi au kutusaidia tukabiliane na hali zenye mkazo?
7 Ingawa mara nyingi shauri la Biblia halipendwi sana miongoni mwa wale wanaokataa kabisa mamlaka na ambao hufuatia maisha ya kula raha, wengi wamekuja kung’amua kwamba maisha ya aina hiyo hayakuwaletea furaha ya kweli. (Wagalatia 6:7, 8) Biblia hutoa majibu ya moja kwa moja kwa maswali juu ya utoaji wa mimba, talaka, na ugoni-jinsia moja. Shauri layo ni ulinzi dhidi ya matumizi mabaya ya madawa na kileo na dhidi ya kupatwa na UKIMWI kupitia damu iliyoambukizwa au uholela wa kingono. Hutuonyesha jinsi ya kuwa na familia zenye furaha. Huandaa maswali ambayo huwezesha mtu akabiliane na hali za maisha zenye kusononesha sana, kutia na kukataliwa na washiriki wa familia wa karibu, ugonjwa wenye kuleta msiba, na kifo cha mpendwa. Hutusaidia tutambue mambo tupaswayo kutanguliza ili maisha zetu zijawe na maana badala ya majuto.a
8, 9. (a) Ni unabii upi unaokuvutia wewe binafsi ikiwa ithibati ya kupuliziwa kwa Biblia? (b) Unabii mwingi wa Biblia huthibitisha nini kuhusu chanzo chao?
8 Unabii: Biblia haina kifani ikiwa kitabu cha unabii, kitabu kisemacho juu ya yale yatakayotukia katika wakati ujao, na hufanya hivyo kwa kutaja hata mambo madogo-madogo. Ilitabiri juu ya uharibifu wa Tiro ya kale, anguko la Babiloni, kujengwa upya kwa Yerusalemu, kuinuka na kuanguka kwa wafalme wa Midiani na Uajemi na Ugiriki, na matukio mengi katika maisha ya Yesu Kristo. Ilitabiri pia mambo madogo-madogo juu ya hali za ulimwengu ambazo zimetokea katika karne hii, nayo hueleza maana yazo. Huonyesha jinsi matatizo yanayowashinda watawala wa kibinadamu yatakavyosuluhishwa, nayo humtambulisha yule Mtawala atakayeletea jamii ya kibinadamu amani ya kudumu na usalama wa kweli.b—Isaya 9:6, 7; 11:1-5, 9; 53:4-6.
9 Kwa njia ya maana, Biblia huonyesha kuwa uwezo wa kutabiri wakati ujao kwa usahihi ni mtihani wa Uungu. (Isaya 41:1–46:13) Yule awezaye kufanya hivyo au awezaye kuwapulizia wengine wafanye hivyo si sanamu tu isiyo na uhai. Yeye si binadamu mchaji tu. Yeye ndiye Mungu wa kweli, na kitabu kilicho na unabii huo ni Neno lake.—1 Wathesalonike 2:13.
Je! Wote Watumiao Biblia Ni wa Dini ya Kweli
10, 11. Kama ilivyoonyeshwa na Yesu, ingawa huenda kasisi fulani akatumia Biblia, ni nini huenda ikafanya dini anayounga mkono isifae?
10 Je! inafaa—na la maana zaidi, je, ni jambo la Kimaandiko—basi kukata maneno kwamba vikundi vyote vya kidini vinavyodai kuitumia Biblia vinafundisha dini ya kweli? Je! kila mtu achukuaye au anukuuye Biblia anazoea dini ya kweli?
11 Ingawa makasisi wengi wana Biblia, wao hutumia dini ikiwa njia ya kujitukuza wenyewe. Wao huchanganya kweli safi za Biblia pamoja na mapokeo na falsafa za kibinadamu. Je! ibada yao inakubalika kwa Mungu? Yesu alitumia ifaavyo lile julisho la Mungu kupitia Isaya, kuwahusu viongozi wa kidini katika Yerusalemu la karne ya kwanza, akisema hivi: “Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mathayo 15:8, 9; 23:5-10) Kwa wazi, dini ya namna hiyo si dini ya kweli.
12, 13. (a) Mwenendo wa washiriki wa kanisa waweza kusaidiaje mtu aamue kama dini yao ni ya kweil? (b) Mungu ataonaje ibada yetu tukichagua washiriki ambao yeye hukataa kabisa? (2 Mambo ya Nyakati 19:2)
12 Namna gani ikiwa matunda yanayotokezwa na mafundisho ya dini fulani, kama yadhihirishwavyo katika maisha ya washiriki wao walio na msimamo mzuri, ni mabaya? Katika Mahubiri ya Mlimani yake, Yesu alionya hivi: “Jihadharini na manabii wa uongo . . . Mtawatambua kwa matunda yao. . . . Kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya.” (Mathayo 7:15-17) Ni kweli kwamba huenda watu mmoja-mmoja wakafanya mabaya na kuhitaji kusahihishwa. Lakini hali ni tofauti wakati washiriki wa kanisa, kutia na makasisi, wanapojiingiza katika uasherati na uzinzi, kupigana, ulevi, pupa, uwongo, uwasiliani-roho, ibada ya sanamu—yoyote ya mambo hayo au hayo yote—hata hivyo nidhamu haitolewi, na wale wanaoendelea katika mwendo huo hawaondoshwi kutanikoni. Biblia husema kwa wazi kwamba wale wazoeao mambo ya jinsi hiyo wapaswa waondoshwe kutanikoni; hawatakuwa na mahali katika Ufalme wa Mungu. (Wagalatia 5:19-21) Ibada yao haimpendezi Mungu, wala ibada yetu haitampendeza Mungu ikiwa tunachagua watu wanaokataa kabisa kuwa washiriki wetu.—1 Wakorintho 5:11-13; 6:9, 10; Ufunuo 21:8.
13 Ni wazi kwamba si vikundi vyote vinavyodai kutumia Biblia ambavyo huzoea dini ya kweli ambayo hiyo hufafanua. Basi, Biblia huonyesha nini kuwa alama za kutambulisha dini ya kweli?
Alama Zinazotambulisha Dini ya Kweli
14. (a) Mafundisho yote ya dini ya kweli yanategemea nini? (b) Mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo kuhusu Mungu na nafsi yana matokeo gani katika mtihani huo?
14 Mafundisho yayo yanategemea kwa uthabiti Maandiko yaliyopuliziwa. “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao na kwa kuwaongoza.” (2 Timotheo 3:16) Lakini ni wapi ambapo Biblia Takatifu inasema juu ya Utatu wa Jumuiya ya Wakristo? Na ni wapi ambapo Biblia hufundisha, kama vile makasisi hufundisha, kwamba wanadamu wana nafsi iokokayo kifo cha mwili wenye nyama? Je! umepata kumuuliza kasisi akuonyeshe mafundisho hayo katika Biblia yako? The New Encyclopædia Britannica yasema hivi: “Wala neno Utatu wala fundisho hilo la kidini lililo dhahiri halionekani katika Agano Jipya.” (1992, Micropædia, Buku 11, ukurasa 928) Na New Catholic Encyclopedia yakiri hivi: “Miongoni mwa Mababa wa Kimitume, kulikuwa hakuna jambo lolote lenye kukaribia hata kwa mbali kuwaza huko wala oni hilo.” (1967, Buku 14, ukurasa 299) Kwa habari ya wazo la Jumuiya ya Wakristo juu ya nafsi itenganayo na mwili wakati wa kifo, wasomi wa kanisa wakiri kwamba wao waliazima wazo hilo kutoka kwa falsafa ya Kigiriki. Hata hivyo, dini ya kweli haipuuzi kweli ya Biblia ili kutumia falsafa za kibinadamu.—Mwanzo 2:7; Kumbukumbu la Torati 6:4; Ezekieli 18:4; Yohana 14:28.
15. (a) Biblia hutambulishaje Yule pekee apaswaye kuabudiwa? (b) Waabudu wa kweli huhisije juu ya kumkaribia Yehova?
15 Dini ya kweli huunga mkono ibada ya yule Mungu mmoja wa kweli, Yehova. (Kumbukumbu la Torati 4:35; Yohana 17:3) Yesu Kristo alisema hivi kwa uthabiti, akifasiri Kumbukumbu la Torati 5:9: “Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye pekee.” (Mathayo 4:10) Kwa kupatana na hayo, Yesu alijulisha jina la Babake kwa wanafunzi wake. (Yohana 17:26) Je! dini yako imekufundisha umwabudu Yehova? Je! umepata kumjua yule Mtu atambulishwaye na jina hilo—makusudi yake, utendaji wake, sifa zake—hivi kwamba wahisi kuwa waweza kumkaribia kwa uhakika? Ikiwa dini yako ni ya kweli, jibu ni ndiyo.—Luka 10:22; 1 Yohana 5:14.
16. Imani katika Kristo humaanisha nini kwa wale wanaoshiriki kwa bidii katika dini ya kweli?
16 Sehemu ya maana ya ibada inayompendeza Mungu ni imani katika Mwana wake, Yesu Kristo. (Yohana 3:36; Matendo 4:12) Hiyo haimaanishi tu kuamini kwamba yeye aliishi au kwamba alikuwa mtu mwenye kutokeza. Yatia ndani uthamini wa yale ambayo Biblia hufundisha kuhusu thamani ya dhabihu ya uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Yesu na utambuzi wa cheo chake leo akiwa Mfalme wa kimbingu. (Zaburi 2:6-8; Yohana 3:16; Ufunuo 12:10) Ikiwa unashiriki pamoja na wale wazoeao dini ya kweli, wewe wajua kwamba wao hujitahidi kwa kudhamiria kumtii Yesu katika maisha ya kila siku, kuiga kielelezo chake, na kushiriki kibinafsi na kwa bidii katika kazi aliyogawia wanafunzi wake. (Mathayo 28:19, 20; Yohana 15:14; 1 Petro 2:21) Ikiwa hiyo si kweli kwa habari ya wale unaoabudu pamoja nao, wewe wahitaji kuangalia kwingineko.
17. Kwa nini waabudu wa kweli huwa waangalifu kuendelea bila kutiwa waa na ulimwengu, na hilo latia ndani nini?
17 Ibada ya kweli si yenye waa kwa kujishughulisha katika siasa na mapigano ya kilimwengu. (Yakobo 1:27) Kwa nini? Kwa sababu Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si wa [sehemu ya, NW] ulimwengu, kama mimi nisivyo wa [sehemu ya, NW] ulimwengu.” (Yohana 17:16) Yesu hakujiingiza katika siasa, na aliwakataza wafuasi wake wasitumie silaha za kimwili. (Mathayo 26:52) Wale watiao maanani yale ambayo Neno la Mungu husema ‘hawajifunzi vita tena kamwe.’ (Isaya 2:2-4) Ikiwa dini yoyote ambayo wewe washiriki nayo hata kwa jina tu haifaani na ufafanuzi huo, wakati umefika wa kuacha kushirikiana nayo.—Yakobo 4:4; Ufunuo 18:4, 5.
18. (a) Yohana 13:35 hutambulisha nini kuwa sifa yenye kutokeza ya dini ya kweli? (b) Ungeweza kumsaidiaje mtu aamue ni kikundi kipi kifuatacho Yohana 13:35?
18 Dini ya kweli hufundisha na kuzoea upendo usio na ubinafsi. (Yohana 13:35; 1 Yohana 3:10-12) Upendo huo hauzungumziwi tu katika mahubiri. Huo kwa kweli huunganisha watu wa jamii zote, vikundi vyote vya kiuchumi, lugha zote, mataifa yote, katika udugu wa kweli. (Ufunuo 7:9, 10) Huo huwaweka kando Wakristo wa kweli mbali na ulimwengu unaowazunguka. Hudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, na pia mikusanyiko yao mikubwa zaidi, ikiwa hujafanya hivyo bado. Watazame wanapofanya kazi pamoja wakijenga mojapo Majumba ya Ufalme yao. Ona jinsi wanavyotendea wazee-wazee (kutia na wajane) na vijana pia (kutia na wale walio na mzazi mmoja tu au wasio na wowote). (Yakobo 1:27) Linganisha yale unayoona na yale ambayo umeona katika dini nyingine yoyote. Kisha ujiulize mwenyewe, ‘Ni nani azoeaye dini ya kweli?’
19. (a) Dini ya kweli hutetea nini kuwa ndilo suluhisho kwa matatizo ya jamii ya kibinadamu? (b) Washiriki wa kile kikundi kinachoshikamana na dini ya kweli wanapaswa wawe wanafanya nini?
19 Dini ya kweli hutetea Ufalme wa Mungu kuwa ndilo suluhisho la kudumu kwa matatizo ya jamii ya kibinadamu. (Danieli 2:44; 7:13, 14; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:4, 5) Je! makanisa yoyote ya Jumuiya ya Wakristo hufanya hivyo? Ni lini mara ya mwisho uliposikia kasisi fulani akieleza juu ya Ufalme wa Mungu na yale ambayo Maandiko huonyesha itatimiza? Je! lile tengenezo unaloshirikiana nalo hukutia moyo uongee na wengine juu ya Ufalme wa Mungu, na ikiwa ndivyo, je, washiriki wote kwa ujumla hushiriki katika kufanya hivyo? Yesu alitoa ushahidi wa jinsi hiyo; wanafunzi wake wa mapema walifanya hivyo. Wewe pia waweza kuwa na pendeleo la kushiriki katika utendaji huo. Ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo.—Mathayo 24:14.
20. Zaidi ya kutambulisha dini ya kweli, ni lazima tufanye nini?
20 Ingawa kuna maelfu ya dini, Biblia hutusaidia tuondoe mvurugo upesi ili tutambulishe ile ya kweli. Lakini twahitaji kufanya mengi zaidi ya kuitambulisha. Ni muhimu tuizoee. Kile kinachotiwa ndani kitazungumziwa kwa urefu zaidi katika makala yetu inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Utoaji wa mimba: Matendo 17:28; Zaburi 139:1, 16; Kutoka 21:22, 23. Talaka: Mathayo 19:8, 9; Warumi 7:2, 3. Ugoni-jinsia-moja: Warumi 1:24-27; 1 Wakorintho 6:9-11. Matumizi mabaya ya madawa na kileo: 2 Wakorintho 7:1; Luka 10:25-27; Mithali 23:20, 21; Wagalatia 5:19-21. Damu na Uholela: Matendo 15:28, 29; Mithali 5:15-23; Yeremia 5:7-9. Familia: Waefeso 5:22–6:4; Wakolosai 3:18-21. Kukataliwa: Zaburi 27:10; Malaki 2:13-16; Warumi 8:35-39. Ugonjwa: Ufunuo 21:4, 5; 22:1, 2; Tito 1:2; Zaburi 23:1-4. Kifo: Isaya 25:8; Matendo 24:15. Mambo ya kutangulizwa: Mathayo 6:19-34; Luka 12:16-21; 1 Timotheo 6:6-12.
b Ili kupata mifano ya unabii huo na utimizo wao, ona vitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kurasa 117-61; na Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kurasa 42-4, 325-32, 297-303. Vyote viwili vimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Ungejibuje?
◻ Ni maoni ya nani yaliyo ya maana zaidi, katika kutambulisha dini ya kweli?
◻ Ni mathibitisho gani manne yanayoonyesha Biblia kuwa Neno la Mungu?
◻ Kwa nini si dini zote zinazotumia Biblia ambazo hukubalika kwa Mungu?
◻ Ni nini alama sita zinazotambulisha ile dini moja ya kweli?
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Mashahidi wa Yehova . . .
◆ Hutegemeza mafundisho yao yote juu ya Biblia.
◆ Humwabudu yule Mungu mmoja wa kweli, Yehova.
◆ Huishi kupatana na imani yao katika Yesu Kristo.
◆ Hawashiriki katika siasa na mapigano ya kilimwengu.
◆ Hujitahidi kudhihirisha upendo usio na ubinafsi katika maisha ya kila siku.
◆ Hutetea Ufalme wa Mungu kuwa suluhisho la kudumu kwa matatizo ya wanadamu.
[Picha katika ukurasa wa 9]
BIBLIA—nini kionyeshacho kwamba ina ujumbe wa Mungu kwa jamii yote ya kibinadamu?