Wapiga-Mbiu ya Ufalme Waripoti
Mungu Hana Upendeleo
ZAIDI ya miaka 1,900 iliyopita, mtume Petro alimtolea ushahidi ofisa wa jeshi aitwaye Kornelio, akisema hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Kornelio alidhihirisha hofu ya Mungu na upendo wa uadilifu. Yeye alikubali ule ushahidi uliotolewa na Petro akawa Mkristo.
Kanuni iyo hiyo ni ya kweli leo—Mungu hana upendeleo. Twaona hilo kutokana na ono fulani kutoka Ujerumani. Ripoti hiyo yasema hivi:
“Katika eneo la kutaniko letu, kuna makao makubwa ya askari-jeshi Warusi. Katika 1989, muda mfupi baada ya Ukuta wa Berlin kuanguka, wazee waliuliza ikiwa yeyote kati ya wahubiri alijua lugha ya Kirusi. Baadhi yetu tulijua, nasi tukaanza kufanyia kazi eneo hilo, jambo ambalo limethibitika kuwa shangwe halisi. Lifuatalo ni mojayapo maono mengi.
“Nilikuwa pamoja na mhubiri asiyebatizwa (ambaye amebatizwa sasa) tulipokuwa tukiongea na kamanda wa jeshi. Kamanda huyo alisikiliza yale tuliyosema kisha akatualika tuseme na askari-jeshi wake. Alisema kwamba ni lazima wasikie juu ya Mungu na Biblia pia, kwa hiyo tulifanya mpango wa kurudi.
“Tulimuuliza dada fulani asemaye Kirusi kwa ufasaha aambatane nasi akiwa mkalimali wetu. Katika chumba cha kukutania cha makao ya askari-jeshi, tuliweka meza yenye fasihi tukaweza kusema na askari-jeshi 68 na kujibu maswali yao. Baadaye wao walikubali kwa furaha vitabu 35 na karibu magazeti 100. Tulipoondoka chumba hicho, tuliona vikundi vidogo vikizungumzia fasihi hizo.
“Tulifanya mpango wa kurudi Julai 4, 1992. Tulipowasili saa 4:50 ya asubuhi, na mlinzi wa makao ya askari-jeshi alituambia kwamba askari-jeshi walikuwa wakitutazamia. Meja mmoja alitupeleka kwenye chumba cha kukutania, na tulipata kwamba mwanamke fulani, aliyekuwa amepokea hivi karibuni fasihi kutoka kwetu kwa ajili ya maktaba, alikuwa ametangaza kuja kwetu kwa kuweka mabango katika makao ya askari-jeshi. Ndugu watatu walitoa hotuba fupi juu ya kazi yetu ya ulimwenguni pote wakaonyesha ni kwa nini twaweza kuwa na uhakika katika Biblia. Kisha tuliruhusu maswali kutoka kwa wasikilizaji, tukitoa majibu kutoka kwa Biblia. Miongoni mwa maswali hayo kulikuwa hili, Ni nini msimamo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu utumishi wa kijeshi, na kuna wowote wao walio askari-jeshi? Hilo lilimpa yule mhubiri asiyebatizwa aliyekuwa ameandamana nami fursa ya kueleza juu ya kazi-maisha yake ya miaka 25 katika jeshi la Ujerumani Mashariki, miaka ya mwisho-mwisho akiwa kapteni wa jeshi la wanahewa. Yeye alisimulia jinsi alivyopata kujifunza juu ya Mungu na Biblia na sasa alitaka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Askari-jeshi walivutiwa na yale waliyosikia. Katika muda wa dakika saba fasihi yote ilikuwa mikononi mwa askari-jeshi, na wengi wakataka Biblia. Kwenye duka la vitabu, tuliweza kupata Biblia saba za Kirusi, ambazo walithamini kupokea. Ilikuwa shangwe ya kweli kuwapa watu hao wenye njaa ya kiroho habari ya Biblia, na twatumaini kwamba watatenda kulingana nayo.”
Kwa kweli, Mungu hana upendeleo. Kupitia Neno lake yeye huwavutia watu wenye mioyo ya kufuatia haki wawe ni nani na pawe ni wapi wapatikanapo. Yeye huwakaribisha wajifunze kutoka kwake na Mwana wake, Yesu Kristo, na wengi kutoka kwenye aina za maisha mbalimbali wanafanya hivyo.—Yohana 17:3.y