Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 6/1 kur. 19-23
  • Walituwekea Sisi Kielelezo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Walituwekea Sisi Kielelezo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Kweli za Biblia
  • Kupainia Katika Australia
  • Kualikwa Kwenye Shamba la Kigeni
  • Ndoa, Marufuku, na Vita
  • Maisha Katika Kambi za Mateso
  • Uhuru na Kuungana Tena Kwenye Kutokeza
  • Kurudi Australia
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Washindi Wajapokabiliwa na Kifo
    Amkeni!—1993
  • Yehova Alithibitika Kuwa Pamoja Nami
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 6/1 kur. 19-23

Walituwekea Sisi Kielelezo

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA CRAIG ZANKER

Kwa miaka minane mke wangu, Gayle, na mimi tumekuwa mapainia, wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Kwa miaka sita iliyopita, tumekuwa tukitumikia miongoni mwa wakazi Waaborigini katika maeneo ya mashambani ya Australia. Tunafuata tu kielelezo chema ambacho wazazi wangu na babu na nyanya yangu walituwekea.

ACHENI niwaambie hasa juu ya babu na nyanya yangu. Sikuzote tumewaita kwa shauku Opa na Oma, maneno ya Kiholanzi yaliyo sawasawa na babu na nyanya. Babu yangu, Charles Harris angali akitumikia kwa bidii katika Melbourne, ambako ameishi karibu miaka 50.

Kujifunza Kweli za Biblia

Opa alizaliwa katika mji mdogo wa Tasmania, jimbo la kisiwa cha Australia. Katika 1924, alipokuwa na miaka 14, babake alinunua kutoka mnada fulani sanduku la hazina la baharia. Hilo lilithibitika kuwa sanduku la hazina halisi, kwa kusema kiroho, kwani lilikuwa na vitabu kadhaa vilivyoandikwa na msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society, Charles Taze Russell.

Yaonekana babake Opa hakupendezwa hasa na vitabu hivyo, lakini Opa alianza kuvisoma na mara iyo hiyo akatambua kwamba vilikuwa na kweli muhimu za Biblia. Kwa hiyo akaanza kutafuta Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, wawakilishi wa watangazaji wa vitabu hivyo ambao sasa huitwa Mashahidi wa Yehova. Yeye alitaka kusema nao ili aweze kupokea maelezo zaidi juu ya kweli za Biblia alizokuwa akijifunza.

Baada ya kuuliza sana yeye alipata wanawake watatu wazee-wazee waliokuwa wenye bidii katika kuwafundisha wengine. Wao walimwathiri sana Charles aliyekuwa mchanga. Hatimaye, katika 1930, alijiweka wakfu kwa Yehova Mungu akabatizwa majini. Alijiuzulu kazi yake akiwa mchinja-nyama kisha akasafiri kuelekea kaskazini hadi Sydney, alikopokea mgawo akiwa mwevanjeli wa wakati wote.

Kupainia Katika Australia

Katika miaka michache iliyofuata, maeneo ambayo Charles alihubiri yalitia ndani pwani ya Sydney na viunga vya Bondi pamoja na maeneo ya mashambani katika jimbo la New South Wales. Kisha akapewa mgawo kwenda Perth, Australia Magharibi, maelfu ya kilometa kwenye ule upande mwingine wa kontinenti hiyo. Kwa muda wa miezi sita alitoa ushahidi katika eneo la biashara la Perth, kisha, akiwa pamoja na mapainia wengine wawili, alipewa mgawo kwenda kwenye yale maeneo makubwa yenye wakazi wachache ya Australia kaskazini-magharibi.

Mgawo wa kuhubiri wa hao watatu—Arthur Willis, George Rollsten, na Charles—ulikuwa wenye ukubwa wa mara nne zaidi ya ule wa Italia! Wakazi walikuwa wachache, eneo lilikuwa jangwa, na joto lilikuwa jingi sana. Nyakati nyingine ilikuwa lazima kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa 500 kati ya mashamba ya kufugia ng’ombe, yaliyoitwa vituo vya ng’ombe. Gari walilotumia lilikuwa zee sana, hata kwa viwango vya 1930 (wakati wa ule mshuko mkubwa wa kiuchumi), lakini walikuwa na imani yenye nguvu na walikuwa wamepiga moyo konde.

Zile barabara nyembamba, zenye mashimo-mashimo zilipitwa-pitwa sana na ngamia, na hapa na hapa yale mavumbi laini (yaitwayo mavumbi ya fahali) yalificha vigutu vya miti vyenye hatari. Si ajabu kwamba springi za gari zilivunjika mara nyingi. Akseli ya nyuma ilivunjika katika pindi mbili, na tairi zilikatika mara nyingi. Mara nyingi mapainia walitengeneza matabaka kwa kutumia tairi nzee-nzee na kuyakaza kwa parafujo (bolti) za paa kwenye sehemu ya ndani ya tairi zilizokuwako ili waweze kuendelea na safari yao.

Nilipokuwa kijana tu, nilimuuliza Opa ni nini kilichowatia moyo waendelee wakiwa chini ya hali ngumu jinsi hiyo. Yeye alieleza kwamba katika hali hiyo ya kutengwa na watu wengine kulikuwa na ukaribu na Yehova. Hali iliyokuwa ugumu wa kimwili nyakati nyingine, ilikuwa baraka ya kiroho.

Bila ishara yoyote ya kuhisi ukubwa au kujiona kuwa mwadilifu, Opa alionyesha mshangao kwamba watu wengi sana huonekana wakihangaikia sana vitu vya kimwili. “Uhai,” yeye akanikumbusha, “wafaa zaidi ukiwa na vitu vichache vya kimwili. Ikiwa Yesu alikuwa tayari kulala akiwa nje ilipohitajika, kwa hiyo twapaswa kufurahi kufanya vivyo hivyo ikiwa mgawo wetu wataka hivyo.” (Mathayo 8:19, 20) Na kwa kweli, yeye na waandamani wake walifanya hivyo.

Kualikwa Kwenye Shamba la Kigeni

Katika 1935, Opa alipokea mgawo mpya wa kuhubiri—kuwatolea ushahidi wakaa-visiwani wa Pasifiki Kusini. Akiwa na mabaharia sita wengine, yeye aliabiri akiwa ndani ya meli ya Watch Tower Society yenye urefu wa meta 16 iitwayo Lightbearer.

Siku moja, walipokuwa katika Bahari ya Coral kaskazini mwa Australia, injini ya pili ya Lightbearer iliharibika. Hakukuwa na upepo wowote kabisa, kwa hiyo hawakuweza kuabiri kilometa nyingine kutoka bara. Ingawa kulikuwa na hatari ya kuvunjikiwa meli kwenye ile Miamba Mikubwa ya Kizingiti, Opa alivutiwa sana na ule utulivu wenye kupendeza. “Bahari ilikuwa kama ziwa dogo la maji,” yeye aliandika hivi katika kitabu chake cha maandishi ya kila siku. “Sitasahau kamwe kutua kwa jua kila jioni kwenye ile bahari yenye utulivu. Mwono ulikuwa mzuri sana hivi kwamba umeandikwa akilini mwangu sikuzote.”

Kwa furaha, kabla yao kupeperuka hadi kizingitini, upepo ulirudi, nao waliabiri kwa usalama kwa kutumia tanga hadi Bandari ya Moresby, Papua New Guinea, ambako injini yao ilirekebishwa. Kutoka Bandari ya Moresby wao waliabiri hadi Kisiwa cha Thursday kisha hadi Java, kisiwa kikubwa cha Indonesia. Opa alisitawisha upendo wenye kina kuelekea nchi hiyo ambayo imesimuliwa kuwa “mkufu wa lulu wenye kuenea upana wa ikweta.” Wakati huo, Indonesia ilikuwa koloni ya Uholanzi, kwa hiyo Opa alijifunza Kiholanzi na Kiindonesia pia. Hata hivyo, fasihi alizotoa katika utendaji wake wa kuhubiri, zilikuwa katika lugha tano: Kiholanzi, Kiindonesia, Kichina, Kiingereza, na Kiarabu.

Opa alikuwa na mafanikio sana katika kuangusha fasihi za Biblia. Wakati mmoja Clem Deschamp, aliyesimamia depo ya Watch Tower katika Batavia (sasa Djakarta), aliitwa mbele ya ofisa fulani Mholanzi aliyekuwa akichunguza kwa ukaribu kazi yetu ya kuhubiri. “Mna watu wangapi wanaofanya kazi huko Java Mashariki?” Ofisa huyo akauliza.

“Mmoja tu,” akajibu Ndugu Deschamp.

“Je! watazamia niamini hivyo?” Ofisa huyo akasema kwa ukali. “Ni lazima iwe mna jeshi kubwa sana la wafanya kazi huko, kulingana na kiasi cha fasihi kinachogawanywa kila mahali!”

Opa ahisi kwamba hiyo ilikuwa mojapo sifa alizopewa zenye kuridhisha zaidi maishani mwake. Lakini kwa hakika alistahili sifa hiyo, kwa kuwa ilikuwa kawaida kwake kuangusha vipande vya fasihi kati ya 1,500 na 3,000 kila mwezi.

Ndoa, Marufuku, na Vita

Katika Desemba 1938, Opa alimwoa mwanamke mchanga Mwindonesia aliyeitwa Wilhelmina, aliyekuja kuwa nyanya yangu. Oma, au nyanya, alikuwa mwenye fadhili, mwanana, mwenye bidii ya kazi, na mpole. Najua hivyo, kwani wakati wa utoto wangu yeye alikuwa rafiki yangu wa karibu zaidi.

Baada ya ndoa yao Opa na Oma waliendelea na utumishi wao wa painia wakiwa pamoja. Kufikia wakati huo, wale mabaharia wengine wa Lightbearer walikuwa wametawanyika hadi sehemu nyingine za ulimwengu au walikuwa wamerudi nyumbani. Lakini Opa alikuwa amefanya Indonesia kuwa nyumbani kwake, naye alikuwa ameazimia kubaki huko.

Vita ya Ulimwengu 2 ilipokaribia, serikali ya Uholanzi iliyokuwa ikitawala Indonesia, na kutenda chini ya mbano wa makasisi, ikaanza kuwekea vizuizi utendaji mbalimbali wa Mashahidi wa Yehova, hatimaye ikipiga kazi yetu marufuku. Kwa hiyo kuhubiri kulifanywa kwa ugumu, kwa kutumia Biblia pekee. Katika karibu kila mji ambao Opa na Oma walizuru, walipelekwa kwa nguvu mbele ya maofisa na kuhojiwa. Walitendwa kama wahalifu. Muda mfupi baada ya kupigwa marufuku, ndugu-mkwe wa Oma alifungwa gerezani kwa ajili ya msimamo wake wa kutokuwamo kwa Kikristo. Yeye alikufa katika gereza fulani la Uholanzi.

Opa na Oma waliishi katika lori lenye makao yaliyojengwa na kushikanishwa nalo. Kwa kutumia gari hilo lenye nyumba, walihubiri kotekote katika Java. Katika 1940, kukiwa na tisho la kushambuliwa na jeshi la Wajapani, wao walibarikiwa na binti, aliyekuja kuwa mama yangu. Walimwita mtoto huyo Victory, baada ya kichwa cha ile hotuba iliyotolewa miaka miwili mapema zaidi na yule aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, wa wakati huo, J. F. Rutherford. Waliendelea kufanya upainia muda wote wa wakati wa kuzaliwa kwa mtoto huyo.

Mapema katika 1942, Opa, Oma, na Victory walikuwa katika meli ya Uholanzi iliyokuwa ikirudi kutoka Borneo wakati waliposikia fyatuo la bunduki lenye sauti kubwa kutoka kwa meli ya vita ya Japani. Taa zote zilizima, na watu wakalia kwa sauti. Kwa njia hiyo vita iliingia maishani mwa familia yangu. Ingawa walifika bandari kwa usalama, Japani ilishambulia Java siku chache tu baadaye, na ofisa fulani Mholanzi akawaambia askari-jeshi Wajapani mahali pa kuwapata Opa na Oma.

Wajapani walipowapata, walinyang’anya mali zao zote, hata kutia na vidude vya kuchezea vya Victory mdogo, kisha wakapelekwa hadi kambi mbili mbalimbali za mateso. Victory aliruhusiwa kukaa na Oma, na Opa hakuwaona kwa miaka mitatu na nusu iliyofuata.

Maisha Katika Kambi za Mateso

Wakati wa kifungo chake, Opa alihamishwa kutoka mji mmoja hadi mwingine—kutoka Surabaja hadi Ngawi, hadi Bandung, na hatimaye hadi Tjimahi. Kuhamishwa-hamishwa huko kwa daima kulikuwa ili kuzuia jaribu lolote la kufanya mpango wa kuponyoka. Wafungwa walikuwa Waholanzi hasa, kukiwa na Waingereza wachache na Waaustralia kadhaa. Alipokuwa katika kambi hizo, Opa alijifunza kazi ya kunyoa nywele, ustadi ambao yeye hutumia bado mara kwa mara. Kitabu pekee alichoruhusiwa kuweka kilikuwa Biblia yake—ya tafsiri ya King James Version.

Wakati uo huo, Oma na Victory walikuwa pia wakihamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine. Katika kambi hizo wanawake waliambiwa na mkuu wa kambi watumikie nje katika “utumishi wa kijamii.” Hata hivyo, kwa sababu fulani, Oma hakuchaguliwa kamwe. Baadaye alipata kujua kwamba wanawake hao walipelekwa watumikie wakiwa malaya wa askari-jeshi Wajapani.

Kwa kuwa askari-jeshi Wajapani hawakupendelea watoto wa kike, sikuzote Oma alikuwa akimvalisha Victory kama mvulana na kumnyoa nywele zake. Jina Victory (Ushindi) lilisababisha tatizo kubwa wakati mkuu wa kambi alipotaka kujua maana ya jina hilo—Ushindi wa Jeshi la Ufalme wa Kijapani au Ushindi wa Waamerika?

“Ushindi wa Ufalme wa Mungu juu ya serikali zote za kidunia!” nyanya yangu akajibu kwa fahari.

Ikiwa adhabu ya kukataa kusema, “Ushindi wa Jeshi la Ufalme wa Kijapani,” Oma na binti yake mwenye miaka mitano walilazimishwa wasimame wima kabisa kwa muda wa saa nane chini ya jua la kitropiki lenye kuunguza. Bila kivuli, bila maji, bila kuketi, bila kuinama mbele. Lakini kwa msaada wa Yehova waliokoka jaribu hilo mbaya sana.

Mwaka mmoja baada ya kifungo cha Oma, mkuu wa kambi alimwambia kwamba mume wake alikuwa amekufa! Kwa huzuni aliweka picha ya Opa chini ya sanduku lake lililokuwa limebonyezwabonyezwa na kuendelea, ijapokuwa huzuni yake.

Maisha ya kambi ya gereza yalikuwa magumu. Posho ya kila siku ya kila mtu ilikuwa kikombe kimoja cha wanga wa muhogo kwa kiamsha-kinywa, gramu 190 za mkate uliofanyizwa kutoka sago kwa mlo wa mchana, na kwa mlo wa jioni, kikombe kimoja cha wali uliopikwa katika mchuzi wa mboga wenye umajimaji. Kwa sababu ya posho ndogo jinsi hiyo, utapiamlo ulikuwa jambo la kawaida, na wale waliougua ugonjwa wa kuhara damu walikufa kila siku.

Wakati wa kifungo cha Opa, yeye alipatwa na ugonjwa wa pelagra na edema ya kilishe (ugonjwa unaotokana na njaa). Oma alikaribia kufa pia, kwa kuwa mara nyingi alimpa Victory chakula chake ili kumzuia msichana huyo mdogo asife njaa. Ukatili na njaa ilikuwako daima. Waliweza kuokoka kwa kuendelea kuwa karibu na Mungu wao, Yehova.

Nakumbuka vema mojapo semi ambazo Opa alipenda sana: “Uhuru ni kuwa katika upatano na Yule Mungu, Yehova.” Hivyo, Opa alijiona mwenyewe kuwa huru kwa maana halisi hata alipokuwa akivumilia kifungo kigumu. Upendo ambao yeye na Oma walikuwa nao kuelekea Yehova kwa hakika uliwasaidia ‘wavumilie mambo yote.’ (1 Wakorintho 13:7) Uhusiano huo wa karibu na Mungu ndilo jambo ambalo Gayle na mimi hujaribu kudumisha sasa.

Uhuru na Kuungana Tena Kwenye Kutokeza

Hatimaye, Vita ya Ulimwengu 2 iliisha katika 1945. Muda mfupi baada ya Japani kujisalimisha, Opa alikuwa akisafirishwa kwa gari-moshi. Njiani kutoka Djakarta hadi Bandung, gari-moshi lilisimamishwa na askari-jeshi Waindonesia. Ingawa uhasama dhidi ya Wajapani ulikuwa umekoma, Waindonesia walikuwa wakipigania uhuru kutoka kwa Waholanzi. Opa alishangaa sana kuondolewa kwenye gari-moshi kwa ghafula hivi kwamba alisahau kusema Kiingereza na badala ya hivyo akasema Kiholanzi. Kwa Waindonesia, Kiholanzi ilikuwa lugha ya adui, na adui alipaswa auawe.

Kwa furaha, wanajeshi walipokuwa wakimtafuta Opa, walipata leseni yake ya uendeshaji-gari ya Australia, ambayo alikuwa amesahau kabisa. Kwa furaha, Waindonesia hawakuwa wakipigana vita na Australia. Hadi leo, Opa huona kupatikana kwa leseni hiyo iliyotambulisha uraia wake wa Australia kuwa kujiingiza kwa Mungu katika jambo hilo, kwani katika hatua iyo iyo muda wa saa kadhaa zilizopita, askari-jeshi hao waliwaua Waholanzi 12 waliokuwa wakipitia hapo wakiwa katika gari-moshi hilo.

Muda mfupi baada ya tukio hilo, Oma na Victory walikuwa wakingojea kusafiri kutoka katika mikoa iliyokumbwa na vita. Walipokuwa wameketi kando ya barabara, mstari mrefu sana wa malori yaliyokuwa yakibeba askari-jeshi na raia ulipitia. Kwa ghafula, kwa sababu isiyojulikana kwa wazi, mstari huo ulitua. Ilitukia kwamba Oma aliangalia ndani ya sehemu ya nyuma ya lori fulani lililokuwa karibu zaidi, na kwa mshangao wake, aliona gofu la mtu akiwa ameketi humo aliyemtambua mara iyo hiyo. Alikuwa mume wake! Hakuna maneno ambayo yangeweza kueleza hisiamoyo za kuungana kwao tena.

Kurudi Australia

Babu aliporudi Australia pamoja na familia yake katika 1946, baada ya kuishi Indonesia kwa muda wa miaka 11, maisha hayakuwa rahisi kwao. Walirudi wakiwa wakimbizi wa vita—wakiwa maskini, wenye utapiamlo, na kushukiwa na watu wengi wa hapo. Oma na Victory walilazimika kustahimili ubaguzi wa rangi dhidi ya wahamiaji kutoka Asia. Opa alilazimika kufanya kazi kwa bidii sana na kwa muda wa saa nyingi ili atunze familia yake na kuiandalia makao. Yajapokuwa magumu hayo, walivumilia na kuokoka wakiwa na hali yao ya kiroho.

Sasa, muda wa zaidi ya miaka 48, Opa huishi Melbourne, ambako yeye bado hushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Yeye ameona Victory na watoto wake wakiikubali kweli, wakiweka wakfu maisha zao kwa Yehova, kisha kila mmoja wao akiingia utumishi wa painia wa wakati wote.

Des Zanker, aliyekuja kuwa baba yangu, na Victory walibatizwa katika miaka ya mapema ya 1950, na Des akaja kuwa mshiriki wa familia ya Betheli ya Australia katika 1958. Baada ya yeye kumwoa Victory, aliyekuwa akitumikia akiwa painia wa pekee, wao walipainia kwa muda fulani kisha wakaalikwa kufanya huduma ya kusafiri. Kisha nikazaliwa, nao wakalazimika kuacha kazi ya kusafiri ili kunilea. Hata hivyo, baada ya miaka 27, baba angali anapainia.

Mapema katika 1990, Oma alikufa bila kusumbuka akiwa nyumbani, katika nyumba iyo hiyo ambamo mama yangu alilelewa. Mimi pia nililelewa katika nyumba iyo hiyo ya Melbourne, na ndivyo ilivyo na ndugu na dada yangu. Imekuwa baraka kwa familia yetu kushiriki nyumba pamoja. Nyakati nyingine tulikuwa tumesongamana, lakini siwezi kukumbuka tukihangaikia hilo hata kidogo. Hata wakati wa ile miaka minne ya kwanza ya ndoa yetu, mke wangu, Gayle, aliishi katika makao hayo yaliyosongamana na alifurahia kuishi humo. Hatimaye tulipoondoka kwenda kwenye mgawo wetu mpya, nililia machozi. Nilikuwa nimepokea utegemezo na upendo mwingi sana katika nyumba hiyo.

Lakini sasa, Gayle nami tuna sababu ya kuwa na shangwe nyingi, kwani tunaweza kufanya yale wazazi wangu na wazazi wao kabla yao waliyofanya. Tulipoondoka nyumbani, tulipata faraja katika sababu ya kuondoka, ambayo ilikuwa ni kufanya mapenzi ya Yehova katika utumishi wa wakati wote. Tunajitahidi sana kufuata kile kielelezo chema cha watangulizi wetu waaminifu, waliopata faraja iliyo sawa na hiyo walipofanya kazi katika migawo migumu, hata katika umaskini wenye kupita kiasi, na hata walipofungwa katika kambi za mateso za Kijapani kwa muda wa miaka kadhaa.—2 Wakorintho 1:3, 4.

Sikuzote Opa amepata faraja kutokana na maneno haya yaliyopuliziwa ya Mfalme Daudi kwa Yehova: “Fadhili [fadhili-upendo, NW] zako ni njema kuliko uhai.” (Zaburi 63:3) Sikuzote babu yangu ametamani sana kufurahia fadhili-upendo hizo milele. Familia nzima inatamani kuzishiriki pamoja naye.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Oma na Opa Harris

[Picha katika ukurasa wa 23]

Craig Zanker (nyuma), pamoja na mke wake, wazazi wake, na ndugu na dada zake wachanga zaidi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki