Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 6/1 kur. 20-24
  • Yehova Alithibitika Kuwa Pamoja Nami

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Alithibitika Kuwa Pamoja Nami
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupainia Uholanzi
  • Mapendeleo Zaidi
  • Chini ya Utawala wa Nazi
  • Magereza na Kambi za Mateso
  • Utendaji wa Baada ya Vita
  • Hakuna Kitu Kilicho Bora Kuliko Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kumngojea Yehova kwa Subira Tangu Ujana Wangu na Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 6/1 kur. 20-24

Yehova Alithibitika Kuwa Pamoja Nami

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MAX HENNING

Ilikuwa katika 1933, Adolf Hitler alikuwa tu amepata mamlaka Ujerumani. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova 500 hivi katika eneo la Berlin hawakutikiswa. Vijana wengi wakawa mapainia, au wahudumu wa wakati wote, na wengine hata walikubali migawo katika nchi nyingine za Ulaya. Rafiki yangu Werner Flatten nami tulizoea kuulizana hivi: “Mbona twasita-sita, tukipoteza wakati wetu? Mbona tusiende kupainia?”

SIKU nane baada ya kuzaliwa katika 1909, nilikuja kuwa chini ya utunzi wa wazazi walezi. Katika 1918 familia yetu ilikuwa na majonzi wakati dada yangu mchanga wa malezi alipokufa ghafula. Muda mfupi baadaye Wanafunzi wa Biblia, kama walivyoitwa Mashahidi wa Yehova, wakaja mlangoni petu, nayo mioyo ya wazazi wangu walezi ikafunguka kabisa ili kuzipokea kweli za Biblia. Wao pia walinifundisha kuthamini mambo ya kiroho.

Nilijishughulisha katika masomo ya kilimwengu nikawa fundibomba. Lakini la maana hata zaidi, nilichukua msimamo wangu kiroho. Werner nami tulianza kupainia katika Mei 5, 1933. Tuliendesha baiskeli hadi mji uliokuwa kilometa 100 hivi kutoka Berlin, ambapo tulikaa na kuhubiri kwa majuma mawili. Kisha tulirudi Berlin kushughulikia mambo ya lazima. Baadaye tulirudi katika eneo letu kwa majuma mengine mawili.

Tuliomba kutumikia katika nchi nyingine, na katika Desemba 1933 tulipokea mgawo wa kwenda ile iliyokuwa Yugoslavia wakati huo. Hata hivyo, kabla ya kuondoka, mgawo wetu ulibadilishwa kuwa Utrecht katika Uholanzi. Muda mfupi baadaye nikabatizwa. Siku hizo ubatizo haukukaziwa sana; huduma ndiyo iliyokuwa jambo la maana. Kumtegemea Yehova sasa kukawa jambo la kawaida katika maisha yangu. Nilipata faraja nyingi katika maneno ya mtunga-zaburi wa Biblia: “Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu.”—Zaburi 54:4.

Kupainia Uholanzi

Muda mfupi baada ya kufika Uholanzi, tulipewa mgawo mpya hadi jiji la Rotterdam. Baba na mmoja wa wana katika familia tuliyoishi nayo walikuwa mapainia pia. Miezi michache baadaye, nyumba kubwa katika Leersum, mji uliokuwa karibu na Utrecht, ilinunuliwa iwe makao ya mapainia, Werner nami tukahamia huko.

Tulipokuwa tukiishi katika makao hayo ya mapainia, tulisafiri kwa baiskeli hadi maeneo ya karibu na kutumia gari lililoweza kubeba watu saba kwenda maeneo ya mbali zaidi. Wakati huo, kulikuwa na Mashahidi mia moja tu Uholanzi yote. Leo, miaka 60 baadaye, eneo tulilohubiri tukiwa katika makao hayo ya mapainia lina watangazaji zaidi ya 4,000 katika makutaniko 50 hivi!

Tulifanya kazi kwa bidii, hata kufikia muda wa saa 14 katika huduma kila siku, na hilo lilifanya tudumu tukiwa na furaha. Lengo kuu lilikuwa kuangusha vichapo vingi iwezekanavyo. Kwa kawaida tuliachia wenye kupendezwa vijitabu zaidi ya mia moja kwa siku. Kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia bado hakukuwa sehemu ya kazi yetu ya kawaida.

Siku moja mwenzangu nami tulikuwa tukihubiri katika mji wa Vreeswijk. Alipokuwa akimtolea ushahidi mtu mmoja kwenye lango la ngome ya kijeshi, nilitumia wakati huo kusoma Biblia yangu. Ilikuwa imepigwa mistari mingi myekundu na ya buluu. Baadaye seremala mmoja aliyekuwa akifanya kazi katika paa iliyokuwa karibu akamwonya huyo mtu kwenye lango kwamba huenda nilikuwa jasusi wa aina fulani. Likiwa tokeo, siku iyo hiyo nilikamatwa nilipokuwa nikimtolea ushahidi mwenye duka, na Biblia yangu ikachukuliwa.

Nilipelekwa mahakamani. Huko ilidaiwa kwamba ile mistari katika Biblia yangu ilikuwa jitihada ya kuichora ile ngome. Nilitangazwa kuwa na hatia, naye hakimu akanihukumu miaka miwili gerezani. Hata hivyo, kesi ilikatwa rufani, nami nikaachiliwa. Jinsi nilivyokuwa na furaha kuwa huru, lakini nilikuwa na furaha hata zaidi wakati Biblia yangu pamoja na maandishi yayo yote iliporudishwa!

Wakati wa kiangazi cha 1936, Richard Brauning, mmoja wa mapainia katika yale makao, pamoja nami tulihubiri kaskazini mwa hiyo nchi wakati wa kiangazi. Mwezi wa kwanza, tulitumia muda wa saa 240 katika huduma tukaangusha kiasi kikubwa cha fasihi. Tuliishi katika hema na kushughulikia mahitaji yetu yote, tukifua nguo zetu, kupika, na kadhalika.

Baadaye nilihamishwa hadi ile mashua iitwayo Lightbearer, iliyokuja kujulikana sana kaskazini mwa Uholanzi. Mapainia watano waliishi katika mashua hiyo, na wakiwa katika mashua hiyo waliweza kufika maeneo mengi ya mbali.

Mapendeleo Zaidi

Katika 1938, nilipewa mgawo wa kuwa mtumishi wa kanda, jinsi waangalizi wa mzunguko wa Mashahidi wa Yehova walivyoitwa. Hivyo nikaiacha Lightbearer na kuanza kutembelea makutaniko na Mashahidi waliokuwa mbali katika mikoa mitatu ya kusini.

Baiskeli ilikuwa usafiri wetu wa pekee. Mara nyingi ilichukua siku nzima kusafiri kutoka kutaniko moja hadi lingine au kikundi kimoja cha wenye kupendezwa hadi kingine. Baadhi ya majiji niliyotembelea lilikuwa Breda, ambapo naishi sasa. Wakati huo, Breda halikuwa na kutaniko lolote ila wenzi wawili wazee waliokuwa Mashahidi.

Nilipokuwa nikitumikia akina ndugu katika Limburg, nilialikwa kujibu maswali mengi yaliyokuwa yameulizwa na mfanyakazi katika mgodi aitwaye Johan Pieper. Alichukua msimamo thabiti kwa ajili ya kweli ya Biblia naye akawa mhubiri mwenye moyo mkuu. Miaka minne baadaye alifungwa katika kambi ya mateso, ambapo alikaa miaka mitatu na nusu. Baada ya kuachiliwa alianza kuhubiri tena kwa bidii, na leo yeye angali mzee mwaminifu. Kutaniko hilo dogo la Mashahidi 12 katika Limburg sasa limekua kufikia makutaniko 17 yakiwa na watangazaji 1,550!

Chini ya Utawala wa Nazi

Katika Mei 1940 Nazi walishambulia Uholanzi. Nilipokea mgawo wa kwenda ofisi ya Watch Tower Society katika Amsterdam. Tulilazimika kuendelea na kazi yetu kwa uangalifu mkubwa, jambo ambalo lilifanya tuthamini mithali ya Biblia: “Mwandamani wa kweli . . . ni ndugu ambaye amezaliwa kwa wakati wa taabu.” (Mithali 17:17, NW) Kile kifungo chenye kupendeza cha umoja uliokuwapo wakati huo wa shida kilikuwa na matokeo makubwa katika ukuzi wangu wa kiroho, kulinitayarisha kwa ajili ya nyakati ngumu hata zaidi zilizokuwa mbele.

Mgawo wangu ulikuwa kusimamia kazi ya kupeleka fasihi kwenye makutaniko, ambao kwa kawaida ulifanywa na matarishi. Nyakati zote Gestapo walikuwa wakitafuta wanaume wa kufanya kazi ya kulazimishwa huko Ujerumani, hivyo tukatumia dada Wakristo wakiwa matarishi. Hatimaye Wilhelmina Bakker, aliyeitwa Nonnie kila wakati, alitumwa kwetu kutoka kwa The Hague, nami nikampeleka mahali ambapo mwangalizi wa ofisi ya tawi, Arthur Winkler, alikuwa akijificha. Ili kujaribu iwezekanavyo kutotambuliwa kwa urahisi, nilijivalia kama mkulima Mholanzi, hata nilivaa viatu vya mbao na vitu vinginevyo ambavyo mkulima angeweza kuvaa, nikamsindikiza Nonnie kwa gari-reli. Baadaye nilikuja kujua kwamba alikuwa na wakati mgumu sana akijaribu kujizuia asicheke, kwa kuwa alihisi kuwa ilikuwa rahisi sana kunitambua.

Katika Oktoba 21, 1941, mahali pa kuweka fasihi na makaratasi katika Amsterdam palifichuliwa kwa Nazi. Wakati wa uvamizi wa Gestapo, Winkler na Nonnie walikamatwa. Walipowekwa gerezani, waliwasikia kwa mbali polisi wawili wa Gestapo wakizungumza jinsi walivyokuwa wakimfuata “mtu mdogo mwenye nywele nyeusi-nyeusi” aliyewapotelea barabarani iliyokuwa na watu wengi. Ilikuwa wazi kwamba walikuwa wakizungumza juu yangu, hivyo Winkler alifaulu kuwafikishia akina ndugu habari. Mara moja, nilihamishwa hadi The Hague.

Wakati huohuo Nonnie aliachiliwa, akarudi The Hague kupainia. Huko nilikutana naye tena. Lakini wakati mtumishi wa kutaniko katika Rotterdam alipokamatwa, nilitumwa kuchukua mahali pake. Baadaye mtumishi wa Kutaniko la Gouda alikamatwa, nami nikahamishwa huko ili kuchukua mahali pake. Hatimaye, katika Machi 29, 1943, nilikamatwa. Nilipokuwa nikichunguza hali ya akiba yetu ya fasihi ya Biblia, nilikumbwa ghafula na uvamizi wa Gestapo.

Zaidi ya fasihi za Biblia zilizokuwa mezani, pia kulikuwako orodha ya majina ya ndugu na dada Wakristo, ingawa majina hayo yalikuwa katika njia ya mficho. Nikiwa na maumivu makali ya moyoni nilisali kwamba Yehova aniandalie njia ili niwalinde wale ambao bado walikuwa huru kuhubiri. Bila ya kugunduliwa, nilifaulu kuuweka mkono wangu uliokuwa umekunjuliwa juu ya hiyo orodha ya majina na kuikunja-kunja mkononi mwangu. Kisha nikaomba ruhusa ya kwenda choo, ambapo niliichana-chana ile orodha na kuipiga maji.

Nilipokuwa katika pindi ngumu kama hiyo, nilijifunza kupata nguvu kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake siku zilizopita na kutokana na ahadi za ukombozi. Huu ni mojawapo uhakikisho uliopuliziwa ambao sikuzote nimeukumbuka: “Kama si BWANA aliyekuwa pamoja nasi, wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, hasira yao ilipowaka juu yetu.”—Zaburi 124:2, 3.

Magereza na Kambi za Mateso

Nilipelekwa katika gereza la Rotterdam, ambapo nilishukuru kwa kuwa na Biblia yangu. Pia nilikuwa na kitabu Salvation, visehemu vya kitabu Children, na wakati wa kutosha kusoma fasihi zote hizo. Baada ya miezi sita nikawa mgonjwa sana na ikawa lazima niende hospitali. Kabla ya kuondoka gerezani, nilificha hizo fasihi chini ya godoro langu. Baadaye nikapata habari kwamba Shahidi mwingine, Piet Broertjes, alihamishiwa seli yangu naye akazigundua. Hivyo hizo fasihi zilikuwa zikitumiwa kuwatia nguvu wengine zaidi katika imani.

Nilipopona nilihamishwa hadi gereza moja katika The Hague. Nikiwa huko nilikutana na Leo C. van der Tas, mwanafunzi wa sheria aliyekuwa gerezani kwa sababu ya kupinga umilikaji wa Nazi. Hakuwa amepata kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova, nami nikawa na fursa ya kumtolea ushahidi. Nyakati nyingine aliniamsha usiku wa manane na kuuliza maswali. Hakuweza kuficha uvutio wake kwa Mashahidi, hasa baada ya kujua kwamba tungeweza kuachiliwa ikiwa tungetia sahihi hati ya kuikana imani yetu. Baada ya vita, Leo akawa wakili na alitetea kisheria kesi nyingi za Watch Tower Society zilizohusisha uhuru wa ibada.

Katika Aprili 29, 1944, nilipandishwa katika gari la moshi kwa safari ya kwenda Ujerumani ya siku 18 yenye kuumiza sana. Katika Mei 18 nilifungwa katika kambi ya mateso ya Buchenwald. Hadi tulipowekwa huru na majeshi ya Muungano karibu mwaka mmoja baadaye, maisha yalikuwa mabaya isivyoweza kuelezeka. Maelfu ya watu walikufa, wengi tukiwaona kwa macho yetu. Kwa kuwa nilikataa kufanya kazi katika kiwanda cha karibu kilichokuwa kikitengeneza vifaa vya vita, niliwekwa kufanya kazi katika mabomba ya maji machafu.

Siku moja hicho kiwanda kililipuliwa kwa bomu. Wengi walikimbilia majengo ya wanajeshi ili kupata usalama, huku wengine wakikimbilia misituni. Mabomu yaliyokosa lengo yaliyapiga majengo ya wanajeshi, na mabomu ya moto yakaichoma misitu. Lilikuwa ono baya sana! Wengi walichomeka wakiwa hai! Nilikuwa nimepata mahali salama pa kujificha, nao moto ulipopungua, nikirudi kambini nilipita miili mingi sana ya wafu.

Watu wengi leo wanajua juu ya mambo ya kuogofya ya lile Teketezo la Umati la Nazi. Namshukuru Yehova kwa kuwa aliutia nguvu uwezo wangu wa kufikiri, hivi kwamba mambo ya kuogofya niliyojionea hayajakuwa yakisumbua akili yangu kwa miaka hiyo yote. Nifikiripo juu ya kipindi changu gerezani, hisia yangu kuu ni ile ya shangwe ya kudumisha uaminifu-maadili kwa Yehova katika kulitukuza jina lake.—Zaburi 124:6-8.

Utendaji wa Baada ya Vita

Baada ya kuwekwa huru na kurudi Amsterdam, nilienda moja kwa moja hadi ofisi ya tawi nipate mgawo. Nilitamani sana kujulishwa yote yaliyokuwa yametendeka wakati ambapo sikuwapo. Tayari Nonnie alikuwa akifanya kazi huko. Wakati wa mwaka wa mwisho wa vita, alikuwa ametumikia akiwa tarishi akipeleka fasihi za Biblia makutanikoni. Hakukamatwa tena, ingawa alikuwa ameponyoka chupuchupu mara nyingi.

Nilipainia kwa muda mfupi nilipokuwa Haarlem, lakini katika 1946, niliombwa kwenda ofisi ya tawi Amsterdam kufanya kazi katika Idara ya Upakizi. Kuelekea mwisho wa 1948, Nonnie nami tulioana, tukaondoka ofisi ya tawi tukapainie pamoja. Mgawo wetu wa upainia ulikuwa Assen. Miaka 12 mapema Richard Brauning nami tulikuwa tumekaa huko wakati wa kiangazi, tukiishi katika hema na kuhubiri. Nilipata habari kwamba Richard alikuwa amepigwa risasi na kuuawa akiwa njiani kuelekea kambi ya mateso.

Ni wazi kwamba muda niliokuwa gerezani ulikuwa umedhuru afya yangu. Miaka sita baada ya kuachiliwa kutoka Buchenwald, ugonjwa ulinilaza kitandani kwa miezi minne. Miaka kadhaa baadaye, katika 1957, niliugua kifua kikuu kwa mwaka mmoja. Mwili wangu ulikuwa umeishiwa nguvu, lakini roho yangu ya upainia bado ilikuwa na nguvu. Nilipokuwa mgonjwa, nilitumia kila fursa ili kuhubiri. Nahisi kwamba roho hii ya upainia ilikuwa jambo la maana kwa kutoruhusu magonjwa yangu yanigeuze kuwa mgonjwa mzembe. Nonnie nami tumeazimia kushikamana na huduma ya wakati wote kwa muda wote ambao afya yetu itaruhusu.

Baada ya kupona, tulipewa mgawo wa kwenda jiji la Breda. Ilikuwa miaka 21 tangu nilipotembelea hilo jiji nikiwa mtumishi wa kanda. Tulipofika katika 1959, kulikuwa na kutaniko dogo la Mashahidi 34. Leo, miaka 37 baadaye, kumekuwa na ongezeko kufikia makutaniko sita yakiwa na Mashahidi zaidi ya 500, wanaokutanika katika Majumba ya Ufalme matatu! Katika mikutano na makusanyiko yetu, sisi huona wengi ambao walipata ujuzi wa kweli ya Biblia kwa sababu ya jitihada zetu fulani. Mara nyingi sisi huhisi kama alivyohisi mtume Yohana alipoandika: “Sina furaha iliyo kuu kuliko hii, kusikia ya kwamba watoto wangu wanakwenda katika kweli.”—3 Yohana 4.

Sasa tumezeeka. Nina miaka 86 na Nonnie ana miaka 78, lakini lazima niseme kwamba upainia ni kazi iletayo afya. Tangu niwe Breda, nimeshinda mengi ya matatizo ya afya niliyopata nilipokuwa nimefungwa. Pia nimefurahia miaka mingi yenye matokeo katika utumishi wa Yehova.

Kutazama nyuma na kuona miaka mingi ya utumishi wenye matokeo ni chanzo cha shangwe kwetu. Sala yetu ya kila siku ni kwamba Yehova atatupa roho na nguvu za kuendelea katika utumishi wake kwa kadiri tutakavyoishi. Tukiwa na uhakika twajieleza kwa kutumia maneno ya mtunga-zaburi: “Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu.”—Zaburi 54:4.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tukiwa tumesimama kando ya hema lililotumiwa tulipokuwa tukipainia katika miaka ya 1930

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mashua iliyotumiwa kufikia maeneo ya mbali

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kuhojiwa kwenye programu ya mkusanyiko katika 1957

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na mke wangu leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki