Hakuna Kitu Kilicho Bora Kuliko Kweli
Kama Ilivyosimuliwa na G. N. Van Der Bijl
Juni 1941, nilipelekwa kwa Shirika la Gestapo na kupelekwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen karibu na Berlin, Ujerumani. Niliendelea kukaa huko, nikiwa mfungwa namba 38190, hadi wakati wa ule msafara wa kifo wenye sifa mbaya katika Aprili 1945. Lakini kabla sijaeleza matukio hayo, acheni kwanza nieleze jinsi nilivyopata kuwa mfungwa.
NILIZALIWA Rotterdam, Uholanzi, muda mfupi baada ya kuanza kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mwaka wa 1914. Baba alifanyia kazi shirika la reli, na nyumba yetu ndogo ilikuwa karibu na njia ya reli. Kuelekea mwisho wa vita mwaka wa 1918, niliona magarimoshi mengi yaliyoitwa kwa kawaida magarimoshi ya matatizo yakipita kwa mngurumo. Bila shaka yalijawa na askari-jeshi waliojeruhiwa ambao walikuwa wakipelekwa nyumbani kutoka katika ule muungano wa majeshi.
Nilipokuwa na umri wa miaka 12, niliacha shule ili nipate kazi. Miaka minane baadaye niliajiriwa kuwa mhudumu katika meli ya abiria, na kwa miaka minne iliyofuata, nilisafiri kati ya Uholanzi na Marekani.
Tulipotia nanga katika bandari ya New York katika kiangazi cha mwaka wa 1939, vita nyingine ya ulimwengu ilikuwa ikitisha kuzuka. Kwa hiyo mtu fulani alipoingia katika meli yetu na kunipatia kitabu Government, ambacho kilizungumza juu ya serikali adilifu, nilikikubali kwa mteremo. Niliporudi Rotterdam, nilianza kutafuta kazi barani, kwa kuwa maisha baharini hayakuonekana kuwa salama tena. Septemba 1, Ujerumani ilivamia Poland na mataifa yakatumbukizwa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili.
Kujifunza Kweli ya Biblia
Asubuhi moja Jumapili katika Machi 1940, nilikuwa nikimtembelea ndugu yangu aliyeoa, wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipopiga kengele ya mlango. Nilimwambia kwamba tayari nilikuwa na kile kitabu Government nami nikamwuliza juu ya mbinguni na ni nani huenda huko. Nilipokea jibu lililo wazi sana na lenye kupatana na akili hivi kwamba nikajiambia, ‘Hii ndiyo kweli.’ Nilimweleza mahali nilipokaa na kumwalika anitembelee nyumbani kwangu.
Baada ya ziara tatu tu, ambazo katika hizo tulikuwa na mazungumzo yenye kina juu ya Biblia, nilianza kuandamana na huyo Shahidi katika kazi ya kuhubiri nyumba hadi nyumba. Tulipofika katika eneo, alinionyesha mahali pa kuanzia, nami nilikuwa peke yangu. Hivyo ndivyo wapya wengi walivyozoezwa kazi ya kuhubiri siku hizo. Nilishauriwa kwamba, ili nisionekane barabarani, sikuzote nilipaswa kuwa ushorobani nilipotoa fasihi. Tahadhari ilihitajiwa katika siku za mapema za hiyo vita.
Majuma matatu baadaye, Mei 10, 1940, jeshi la Ujerumani lilishambulia Uholanzi, na Mei 29, balozi wa Reich, Seyss-Inquart akatangaza kwamba tengenezo la Mashahidi wa Yehova lilikuwa limepigwa marufuku. Tulikutana katika vikundi vidogo tu, na tulikuwa wenye tahadhari katika kuweka mahali petu pa kukutania pakiwa siri. Ziara za waangalizi wasafirio zilikuwa zenye kututia moyo hasa.
Nilikuwa mvutaji-sigareti sana, na nilipompa sigareti Shahidi aliyejifunza nami na kugundua kwamba havuti sigareti, nilisema: “Siwezi kamwe kuacha kuvuta sigareti!” Hata hivyo, muda mfupi baadaye, nilipokuwa nikitembea barabarani, nilifikiri hivi, ‘Ikiwa nitakuwa Shahidi, nataka kuwa Shahidi halisi.’ Kwa hiyo sikuvuta sigareti tena kamwe.
Kuchukua Msimamo kwa Ajili ya Kweli
Juni 1940, muda unaopungua miezi mitatu tangu nilipokutana na Shahidi mlangoni pa ndugu yangu, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova na kubatizwa. Miezi michache baadaye, katika Oktoba 1940, niliingia katika huduma ya wakati wote nikiwa painia. Wakati huo, nilipewa lililoitwa koti la painia. Lilikuwa na mifuko mingi ya vitabu na vijitabu, nalo lingeweza kuvaliwa ndani ya koti.
Karibu tangu mwanzo wa kumiliki kwa Ujerumani, Mashahidi wa Yehova walisakwa kwa utaratibu na kukamatwa. Asubuhi moja katika Februari 1941, nilikuwa katika huduma ya shambani pamoja na Mashahidi wengine wachache. Walipokuwa wakiwatembelea watu upande mmoja wa bloku ya nyumba, nilihubiri kuzunguka upande ule mwingine wa hiyo bloku ili nikutane nao. Baada ya muda, nilienda kuona ni nini kilichokuwa kikiwachelewesha, nikakutana na mwanamume aliyeuliza, “Je, wewe pia una vyovyote vya vitabu vidogo hivi?”
“Ndiyo,” nikajibu. Ndipo akanikamata na kunipeleka katika kituo cha polisi. Niliwekwa rumande kwa karibu majuma manne. Wengi wa maofisa walikuwa wenye urafiki. Maadamu mtu hakupelekwa kwa Shirika la Gestapo, angeweza kupata kuachiliwa kwake kwa kutia sahihi tu julisho lililoandikwa la kwamba hangegawanya tena fasihi ya Biblia. Nilipotakwa nitie sahihi julisho hilo, nilijibu hivi: “Hata ikiwa mngenipa gulden milioni moja au mbili, bado singetia sahihi.”
Baada ya kuendelea kuwa rumande kwa muda mrefu zaidi, nilipelekwa kwa Shirika la Gestapo. Kisha nikapelekwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, Ujerumani.
Maisha Katika Sachsenhausen
Nilipofika katika Juni 1941, tayari kulikuwako Mashahidi wapatao 150—wengi wao wakiwa Wajerumani—katika Sachsenhausen. Sisi wafungwa wapya tulipelekwa katika sehemu ya hiyo kambi iliyoitwa Upweke. Huko ndugu zetu Wakristo walituengaenga, wakatutayarisha kwa ajili ya yale ambayo tungetarajia. Juma moja baadaye shehena nyingine ya Mashahidi kutoka Uholanzi ilifika. Mwanzoni tulipewa mgawo wa kusimama mahali pamoja mbele ya kambi ya jeshi tangu saa moja kamili asubuhi hadi saa 12 kamili jioni. Nyakati nyingine wafungwa walipaswa kufanya hivyo kila siku kwa juma moja au zaidi.
Kujapokuwa kutendwa kwa dhuluma, ndugu waling’amua uhitaji wa hima wa kuendelea kuwa na utaratibu na kutwaa lishe ya kiroho. Kila siku mtu fulani alipewa mgawo wa kutayarisha mawazo fulani juu ya andiko la Biblia. Baadaye, katika uwanja wa kukusanyikia, Mashahidi mmoja-mmoja walimfikia huyo na kusikiliza aliyokuwa ametayarisha. Kwa njia moja au nyingine, fasihi ziliingizwa kisiri kwa ukawaida katika kambi, nasi kwa hakika tulikutana kila Jumapili, tukajifunza fasihi hizo za Biblia pamoja.
Kwa njia fulani nakala ya kitabu Children, kilichokuwa kimetolewa kwenye mkusanyiko wa St. Louis, Marekani katika kiangazi cha 1941, kiliingizwa kisiri katika Sachsenhausen. Ili kupunguza hatari ya hicho kitabu kugunduliwa na kuharibiwa, tulikibomoa, na hivyo visehemu vikasambazwa miongoni mwa akina ndugu ili kwamba kila mtu angeweza kuwa na zamu ya kukisoma.
Baada ya muda, wasimamizi wa kambi waligundua juu ya mikutano tuliyokuwa tukifanya. Kwa hiyo Mashahidi wakatengwa katika kambi tofauti-tofauti. Hilo lilitutolea fursa bora ya kuhubiria wafungwa wengine, na tokeo likawa kwamba, Wapoland, Waukrainia, na watu wengine wengi waliikubali kweli.
Wanachama wa Nazi walionyesha waziwazi nia yao ya kuvunja uaminifu-maadili au kuua Bibelforscher, kama walivyoitwa Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, mkazo tuliowekewa ulikuwa mkali. Tuliambiwa kwamba tungeweza kuwekwa huru ikiwa tungetia sahihi julisho linalokana imani yetu. Ndugu fulani wakaanza kusababu hivi, “Nikiwa huru, naweza kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.” Ingawa wachache walitia sahihi, wengi wa ndugu zetu walibaki waaminifu kujapokuwa kunyimwa mahitaji ya maisha, kudhulumiwa, na kutendwa vibaya. Baadhi yao waliokana imani hawakusikiwa tena kamwe. Ingawa hivyo, kwa kufurahisha baadaye wengine walirudia tena hali yao na wangali Mashahidi watendaji.
Tulilazimishwa kwa ukawaida kutazama wafungwa walipokuwa wakiadhibiwa vikali kimwili, kama vile kuchapwa viboko 25 kwa fimbo. Pindi moja, tulilazimishwa kutazama kuuawa kwa kunyongwa kwa wanaume wanne. Mambo hayo yaliyoonwa humwathiri sana mtu. Ndugu mmoja, mrefu, mwenye umbo zuri aliyeishi katika kambi niliyoishi, aliniambia hivi: “Kabla sijaja hapa, singeweza kuona damu bila ya kupoteza fahamu papo hapo. Lakini sasa nimepata kuwa sugu.” Hata hivyo, ingawa huenda ikawa tulipata kuwa sugu, hatukupata kuwa watu wasio na hisia. Lazima niseme, sikuwa kamwe na nia ya kuwadhuru au kuwachukia waliotunyanyasa.
Baada ya kufanya kazi na kommando (kundi la wafanyakazi) kwa muda fulani, nililazwa hospitalini nikiwa na homa kali. Daktari Mnorway mwenye fadhili na mwuguzi Mchekoslovakia walinisaidia, na labda fadhili zao ziliokoa uhai wangu.
Msafara wa Kifo
Kufikia Aprili 1945, ilikuwa wazi kwamba Ujerumani ilikuwa ikishindwa vitani. Majeshi ya muungano ya magharibi yalikuwa yakisonga upesi kutoka magharibi, nao Wasovieti, kutoka mashariki. Ilikuwa vigumu kwa Wanachama wa Nazi kuua kikatili mamia ya maelfu ya watu waliokuwa katika kambi za mateso na kuitupa miili yao mnamo siku chache bila kuacha alama zozote ambazo zingefanya wapatikane. Kwa hiyo waliamua kuwaua wagonjwa na kuwahamisha wafungwa waliosalia hadi bandari zilizokuwa karibu zaidi. Huko walipanga kuwapandisha katika meli na kuzizamisha hizo meli baharini.
Msafara huo wa wafungwa wapatao 26,000 kutoka Sachsenhausen ulianza usiku wa Aprili 20. Kabla hatujaondoka kambini, ndugu zetu wagonjwa waliokolewa kutoka katika zahanati. Mkokoteni ulipatikana ambamo wangeweza kusafirishiwa. Wote pamoja, tulikuwa watu 230 kutoka nchi sita tofauti. Miongoni mwa wagonjwa mlikuwa Ndugu Arthur Winkler, aliyekuwa amechangia sana upanuzi wa kazi katika Uholanzi. Sisi Mashahidi tulikuwa wa mwisho katika huo msafara, nasi tuliendelea kutiana moyo mmoja na mwenzake ili tuendelee kwenda.
Kwanza kabisa, tulipiga mwendo kwa saa 36 bila kupumzika. Nilipokuwa nikitembea, kwa hakika nililala usingizi kutokana na taabu tupu na uchovu. Lakini kubaki nyuma au kupumzika hakukuwezekana kwa sababu mtu alikuwa akihatarisha kupigwa risasi na walinzi. Usiku tulilala uwanjani au vichakani. Chakula kilikuwa kidogo sana au hakikuwako. Maumivu ya njaa yalipopata kuwa yasiyovumilika, nililamba dawa ya meno ambayo Shirika la Msalaba Mwekundu la Sweden lilikuwa limetupatia.
Kufikia wakati mmoja, kwa sababu walinzi Wajerumani walichanganyikiwa wasijue yalipokuwa majeshi ya Urusi na ya Marekani, tulipiga kambi msituni kwa siku nne. Hilo lilikuwa jambo lenye mafaa kwa sababu, tokeo lilikuwa kwamba, hatukufika Ghuba ya Lübeck kwa wakati ufaao ili tuingie meli ambazo zilipaswa kutupeleka katika kaburi letu la maji mengi. Hatimaye, baada ya siku 12 na kupiga mwendo kwa zaidi ya kilometa 200, tulifika Msitu wa Crivitz. Huo haukuwa mbali kutoka Schwerin, jiji lipatalo kilometa 50 kutoka Lübeck.
Wasovieti walikuwa kuumeni mwetu, na Wamarekani, kushotoni. Kutokana na milio ya bunduki kubwakubwa na kufyatuliwa kwa risasi kusikokoma, tulijua kwamba tulikuwa karibu na mistari ya mbele ya vita. Walinzi Wajerumani wakapatwa na hofu ya ghafula; baadhi yao wakakimbia, na wengine wakabadili yunifomu zao za kijeshi na kuvaa mavao ya gereza waliyokuwa wamewavua wafu, wakitumainia kutotambuliwa. Katikati ya mvurugo huo, sisi Mashahidi tulikusanyika ili kuomba tupate mwongozo.
Ndugu waliosimamia waliamua kwamba tuondoke saa za mapema siku iliyofuata na tuelekee upande wa mistari ya vita ya majeshi ya Marekani. Hata ingawa, karibu nusu ya wafungwa waliokuwa wameanza msafara wa kifo walikuwa wamekufa au kuuawa njiani, Mashahidi wote walibaki hai.
Nilipata lifti kutoka kwa maofisa fulani wa kijeshi Wakanada hadi jiji la Nijmegen, ambapo dada yangu alikuwa akiishi. Lakini nilipofika hapo, nilipata kwamba alikuwa amehama. Hivyo nikaanza kutembea kuelekea Rotterdam. Kwa uzuri, njiani nilipewa lifti katika gari la mtu binafsi ambalo lilinipeleka moja kwa moja hadi mwisho wa safari yangu.
Kweli Imekuwa Maisha Yangu
Siku ileile niliyofika Rotterdam, nilitoa tena ombi la kazi ya painia. Majuma matatu baadaye nilikuwa katika mgawo wangu katika jiji la Zutphen, ambako nilitumikia kwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu kilichofuata. Wakati huo, nilipata tena kadiri fulani ya nguvu zangu za kimwili. Kisha nikawekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko, kama vile wahudumu wasafirio waitwavyo. Miezi michache baadaye, nilialikwa katika Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower katika South Lansing, New York. Baada ya kuhitimu kutoka darasa la 12 la shule hiyo katika Februari 1949, nilipewa mgawo wa kwenda Ubelgiji.
Nimetumikia nyanja mbalimbali za huduma katika Ubelgiji, kutia na karibu miaka minane kwenye ofisi ya tawi na miongo kadhaa ya miaka katika kazi ya kusafiri nikiwa mwangalizi wa mzunguko na mwangalizi wa wilaya. Mwaka wa 1958, nilimwoa Justine, aliyepata kuwa mwandamani wangu wa kusafiri. Sasa, miaka ianzapo kunilemea, ningali na shangwe ya kuweza kutumikia katika njia ndogo nikiwa mwangalizi asafiriye wa badala.
Nikumbukapo huduma yangu, kwa kweli naweza kusema: “Hakuna kitu kilicho bora kuliko kweli.” Bila shaka, haijawa rahisi sikuzote. Nimegundua uhitaji wa kujifunza kutokana na makosa na kasoro zangu. Kwa hiyo nizungumzapo na vijana, mara nyingi mimi huwaambia hivi: “Ninyi pia mtafanya makosa na labda hata mfanye ukiukaji mzito, lakini msiseme uwongo juu ya huo. Zungumzeni jambo hilo na wazazi wenu au na mzee mmoja, kisha mfanye marekebisho yahitajiwayo.”
Katika miaka yangu karibu 50 katika huduma ya wakati wote Ubelgiji, nimependelewa kuona watu fulani ambao wakati mmoja niliwajua wakiwa watoto, wakitumikia wakiwa wazee na waangalizi wa mzunguko. Na nimeona wale wapiga-mbiu wa Ufalme wapatao 1,700 nchini wakiongezeka kupita 27,000.
Nauliza hivi, “Je, kungeweza kuwa njia iliyobarikiwa zaidi ya kuishi kuliko kumtumikia Yehova?” Haikuwapo kamwe, haipo sasa, wala haitapata kuwapo kamwe. Nasali kwamba Yehova aendelee kuongoza na kubariki mke wangu nami ili tuweze kuendelea kumtumikia milele.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nikiwa na mke wangu muda mfupi baada ya ndoa yetu mwaka wa 1958