Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 6/15 kur. 5-7
  • Wapendwa Wako Waliokufa—Je! Utawaona Tena?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wapendwa Wako Waliokufa—Je! Utawaona Tena?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Nani Wanaofufuliwa Kwenda Mbinguni?
  • Ufufuo Kwenye Uhai Duniani
  • Ufufuo wa Wengi
  • Inakuwaje kwa Wapendwa Wetu Waliokufa?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Maisha Mapya kwa Wazazi Wetu wa Kale Waliokufa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Wakati Watu Waliokufa Watakapoishi Tena!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ufufuo—wa Nani, na Wapi?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 6/15 kur. 5-7

Wapendwa Wako Waliokufa—Je! Utawaona Tena?

JOHN alikuwa mwenye miaka tisa tu mamake alipokufa. Baadaye, yeye alikumbuka yale yaliyotokea kwenye mochari: “Nilimchorea picha na kuandika maneno machache juu yayo nikimwomba atungojee sisi sote mbinguni. Nilimpa baba picha hiyo ili aitie ndani ya jeneza alimokuwa mama, na hata ingawa alikuwa amekufa, mimi hupenda kufikiri kwamba alipata ujumbe huo wa mwisho kutoka kwangu.”—How It Feels When a Parent Dies, cha Jill Krementz.

Hakuna shaka kwamba John alimpenda sana mamake. Baada ya kusimulia sifa zake nzuri, yeye alisema hivi: “Labda ni vile tu sitaki kukumbuka yale mambo mabaya, lakini siwezi kufikiri juu ya chochote kibaya kumhusu. Yeye alikuwa mwanamke mrembo zaidi niliyepata kuona maishani mwangu mwote.”

Kama John, wengi wana kumbukumbu wanazopenda juu ya wapendwa wao waliokufa nao hukiri uhitaji wa kihisiamoyo wa kuwaona tena. Edith, ambaye mwanae wa miaka 26 alikufa kwa kansa, alisema hivi: “Nahitaji kuamini kwamba mwanangu aendelea kuishi mahali fulani, lakini sipajui. Je! nitamwona tena? Sijui lakini natumaini nitamwona.”

Hakika, Muumba wa mwanadamu mwenye upendo anafahamu juu ya tamaa hiyo ya wanadamu iliyo ya kawaida. Hiyo ndiyo sababu yeye ameahidi kwamba wakati utakuja ambapo mamilioni wataungana tena pamoja na wapendwa wao waliokufa. Neno la Mungu lina marejezo mengi juu ya ahadi hiyo ya ufufuo wa wafu unaokuja.—Isaya 26:19; Danieli 12:2, 13; Hosea 13:14; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:12, 13.

Ni Nani Wanaofufuliwa Kwenda Mbinguni?

Ebu tufikirie tumaini la John kwamba mamake mpendwa amngojea mbinguni. Waenda-kanisa wengi wana tumaini au itikadi hiyo. Katika kujaribu kuunga mkono maoni hayo, makasisi na baadhi ya wafanyakazi wa huduma za jamii hutumia vibaya maandiko ya Biblia.

Kwa kielelezo, mtaalamu mmoja wa kusaidia waliofiwa, Dakt. Elisabeth Kübler-Ross, alisema hivi katika kitabu chake On Children and Death: “Kufa humaanisha tu kwamba twatupilia mbali mwili wetu kama vile tunavyoweza kutupilia mbali koti zee lililochakaa, au kutoka kwenye chumba kimoja na kuingia kingine. Katika Mhubiri, 12:7, twasoma hivi: ‘Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.’ Yesu alisema hivi: ‘Naenda kuwaandalia mahali ili nilipo mimi nanyi mwepo.’ Na kwa yule mwivi juu ya msalaba alisema: ‘Leo wewe utakuwa pamoja nami katika paradiso.’”

Je! maandiko yaliyo juu kwa kweli yamaanisha kwamba wapendwa wetu waliokufa wako hai sasa na watungojea mbinguni? Ebu tuchunguze hayo maandiko kwa uangalifu zaidi, tukianza na Mhubiri 12:7. Kwa wazi, yule mwanamume mwenye hekima aliyeandika maneno hayo hakukusudia kupinga yale aliyokuwa tayari amesema katika kitabu icho hicho cha Biblia: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Yeye alikuwa akizungumza juu ya kifo cha wanadamu kwa ujumla. Je! ni jambo la akili kuamini kwamba wote wasioamini kuwako kwa Mungu kwa dhati na wahalifu-sugu humrudia Mungu wanapokufa? La. Kwa kweli, hilo haliwezi kusemwa juu ya yeyote kati yetu, hata iwe twajiona wenyewe kuwa wema au wabaya. Kwa kuwa hakuna yeyote kati yetu ambaye amekuwa pamoja na Mungu mbinguni, inaweza kusemwaje kwamba twamrudia yeye?

Basi, mwandikaji wa Biblia alimaanisha nini kwa kusema kwamba baada ya kifo, ‘roho humrudia Mungu wa kweli’? Katika kutumia neno la Kiebrania linalotafsiriwa “roho,” yeye hakuwa akirejezea kitu cha kipekee kinachotofautisha binadamu mmoja na mwingine. Badala ya hivyo, kwenye Mhubiri 3:19, mwandikaji uyo huyo wa Biblia aliyepuliziwa aeleza kwamba mwanadamu na wanyama “wote wanayo pumzi [roho, NW] moja.” Kwa wazi alimaanisha kwamba “roho” ni kani ya uhai katika chembe zinazofanyiza miili ya kimwili ya wanadamu na wanyama. Sisi hatukupokea roho hiyo moja kwa moja kutoka kwa Mungu. Ilipitishwa kwetu na wazazi wetu wa kibinadamu tulipotungwa mimba na baadaye kuzaliwa. Isitoshe, roho hiyo haisafiri kihalisi kupitia angani na kumrudia Mungu baada ya kifo. Maneno, ‘roho humrudia Mungu wa kweli,’ ni usemi wa mfano kumaanisha kwamba mataraja ya uhai ya wakati ujao ya mtu aliyekufa sasa yamtegemea Mungu. Ni juu yake kuamua ni nani atakayekumbuka na hatimaye amfufue. Ona mwenyewe jinsi Biblia inavyoonyesha hilo waziwazi kwenye Zaburi 104:29, 30.

Yehova Mungu amekusudia kwamba idadi ndogo ya wafuasi waaminifu wa Kristo, wanaojumlika kuwa 144,000 pekee, watafufuliwa kwenye uhai wa kimbingu wakiwa wana wa Mungu wa kiroho. (Ufunuo 14:1, 3) Hao wafanyiza serikali ya kimbingu pamoja na Kristo kwa ajili ya kubarikiwa kwa wanadamu duniani.

Mitume waaminifu wa Yesu ndio waliokuwa wa kwanza kujua juu ya hilo, akiwaambia hivi: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.” (Yohana 14:2, 3) Mitume hao na Wakristo wengine wa mapema walikufa na ikawabidi kungojea wakiwa hawana ufahamu katika kifo hadi kuja kwa Yesu ili awathawabishe kwa ufufuo wa kimbingu. Hiyo ndiyo sababu twasoma kwamba Mkristo mfia-imani wa kwanza, Stefano, “alilala usingizi katika kifo.”—Matendo 7:60, NW; 1 Wathesalonike 4:13.

Ufufuo Kwenye Uhai Duniani

Lakini vipi juu ya ahadi ya Yesu kwa yule mhalifu aliyekufa kando yake? Kama vile Wayahudi wengi wa wakati huo, mtu huyo aliamini kwamba Mungu angemtuma Mesiya ambaye angesimamisha ufalme na kurudisha amani na usalama kwa taifa la Wayahudi duniani. (Linganisha 1 Wafalme 4:20-25 na Luka 19:11; 24:21 na Matendo 1:6.) Zaidi ya hiyo, mtenda-maovu huyo alidhihirisha imani kwamba Yesu alikuwa Yule aliyechaguliwa na Mungu kuwa Mfalme. Lakini, katika pindi hiyo, kifo cha Yesu kilichokaribia akiwa mwanadamu aliyehukumiwa adhabu kilifanya hilo lionekane kuwa haliwezekani. Hiyo ndiyo sababu Yesu alimhakikishia yule mhalifu kwa kutanguliza ahadi Yake kwa maneno haya: “Kweli mimi nakuambia wewe leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43, NW.

Tafsiri za Biblia zinazotia alama ya koma kabla ya neno “leo” hutatanisha watu wanaotaka kuelewa maneno ya Yesu. Yesu hakuenda kwenye paradiso yoyote siku iyo hiyo. Badala ya hivyo, yeye alilala bila ufahamu katika kifo kwa siku tatu hadi Mungu alipomfufua. Hata baada ya ufufuo na kupaa mbinguni kwa Yesu, ilimbidi angoje kwenye mkono wa kulia wa Baba yake hadi wakati ulipowadia atawale akiwa Mfalme juu ya wanadamu. (Waebrania 10:12, 13) Karibuni, utawala wa Ufalme wa Yesu utaletea wanadamu faraja na kugeuza dunia nzima kuwa paradiso. (Luka 21:10, 11, 25-31) Halafu atatimiza ahadi yake kwa mhalifu huyo kwa kumfufua kwenye uhai duniani. Na Yesu atakuwa na mtu huyo katika maana ya kwamba Yeye atasaidia katika mahitaji yote ya mtu huyo, kutia ndani uhitaji wa kubadilisha mtindo-maisha wake upatane na sheria zenye uadilifu za Mungu.

Ufufuo wa Wengi

Kama ilivyo kuhusu mhalifu huyo mwenye kutubu, ufufuo wa wanadamu walio wengi utatukia hapa duniani. Hilo lapatana na kusudi la Mungu katika kuumba mwanadamu. Mwanamume na mwanamke wa kwanza waliwekwa katika bustani ya paradiso na kuambiwa waitiishe dunia. Kama wangaliendelea kuwa watiifu kwa Mungu, wao wasingalikuwa wazee na kufa kamwe. Katika wakati uliowekwa na Mungu, dunia nzima ingalitiishwa, ifanywe kuwa paradiso ya duniani pote na Adamu pamoja na wazao wake wakamilifu.—Mwanzo 1:28; 2:8, 9.

Hata hivyo, kwa sababu Adamu na Hawa walifanya dhambi kimakusudi, walileta kifo juu yao wenyewe na wazao wao wa wakati ujao. (Mwanzo 2:16, 17; 3:17-19) Hiyo ndiyo sababu Biblia husema hivi: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Warumi 5:12.

Kumekuwako binadamu mmoja tu aliyezaliwa bila dhambi ya kurithiwa. Huyo alikuwa Mwana wa Mungu aliye mkamilifu, Yesu Kristo, ambaye uhai wake ulihamishwa kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi, Mariamu. Yesu aliendelea kuwa bila dhambi na hakustahili kuuawa. Kwa hiyo, kifo chake kina thamani ya kufidia kwa ajili ya “dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29; Mathayo 20:28) Hiyo ndiyo sababu Yesu angeweza kusema: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi [atakuja kwenye uhai, NW].”—Yohana 11:25.

Hivyo, naam, unaweza kutazamia kuungana tena na wapendwa wako waliokufa, lakini hilo lataka kwamba udhihirishe imani katika Yesu akiwa Mfidiaji wako na kumtii akiwa Mfalme aliyewekwa wa Mungu. Karibuni Ufalme wa Mungu utaondolea mbali ubaya wote kutoka dunia hii. Wanadamu wote wanaokataa kunyenyekea utawala wao wataharibiwa. Hata hivyo, raia wa Ufalme wa Mungu wataokoka na kujishughulisha katika kazi ya kugeuza dunia hii kuwa paradiso.—Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 21:3-5.

Ndipo wakati wenye kusisimua utawadia ili ufufuo uanze. Je! wewe utakuwapo ili uwakaribishe wafu warudipo? Yote yanategemea yale unayofanya sasa. Baraka nzuri ajabu zawangojea wote wanaojitiisha sasa chini ya utawala wa Ufalme wa Yehova kupitia Mwanae, Yesu Kristo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki