Wapiga-Mbiu ya Ufalme Waripoti
“Uthibitisho wa Roho ya Ushirikiano”
KARIBU na ncha ya sehemu ya kusini zaidi mwa Hispania kuna jiwe kubwa sana la chokaa linaloitwa Jiwe la Gibraltar. Kwa mamia ya miaka, jiwe hili limekuwa shahidi-mkimya kwa mizozo ya kisiasa na mabishano kati ya mataifa. Tofauti na hivyo, Jiwe la Gibraltar hivi majuzi lilikuwa mandhari ya nyuma kwa wonyesho wa ushirikiano na muungano usioonekana kwa urahisi ulimwenguni leo.
Kilometa tatu tu kutoka kwenye Jiwe hilo kuna mji wa La Línea, Hispania. Kujengwa kwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova huko kulileta pamoja mamia ya wafanyakazi wenye kujitolea waliokuwa na hamu ya kuchangia wakati wao na nishati zao. Walipojitahidi kujenga mahali panapofaa pa kumwabudu Muumba, Yehova Mungu, hata mandhari ya nyuma yenye fahari nyingi ya Jiwe la Gibraltar ikafifia ikilinganishwa na kazi iliyokuwa itimizwe.
Wapiga-mbiu ya Ufalme katika sehemu hiyo ya ulimwengu waleta ripoti hii ifuatayo:
“Wafanyakazi wa kujitolea 900 wenye idili walifanya kazi usiku na mchana, wakianza kazi Ijumaa alasiri, Septemba 24, 1993. Kufikia saa moja ya Jumapili jioni, ishara mpya inayotambulisha jengo hilo kuwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ilikuwa imesimamishwa, na jengo hilo lenye kuvutia lilikuwa linatumiwa kwa mkutano walo wa kwanza wa watu wote.
“Mashahidi wengi kutoka Gibraltar iliyoko karibu nasi walivuka mpaka kuja kusaidia ndugu zao Wahispania. ‘Migawanyiko ya kisiasa haiharibu roho ya udugu wetu wa kimataifa,’ mmoja wa wafanyakazi wa kujitolea aliye mzaliwa wa Gibraltar akaeleza. Yeye aliongezea hivi: ‘Miaka kadhaa iliyopita, marafiki kutoka La Línea walikuja kutusaidia kujenga Jumba la Ufalme letu katika Gibraltar, kwa hiyo sasa twafurahi kuwaonyesha fadhili vilevile.’
“Ili kuongezea jitihada nyingi za makutaniko hayo mawili ya Mashahidi wa Yehova na mamia ya wasaidizi stadi kutoka eneo la Andalusia, jiji la La Línea liliamua kutoa upaji wa ploti ya ardhi iliyohitajika. ‘Kidesturi, mamlaka za huko za Hispania nyakati zote zimekuwa zikiyapa makanisa ya Katoliki ardhi ya kujengea,’ akaeleza meya wa La Línea wakati alipozuru mahali pa ujenzi. ‘Mbona tusifanye vivyo hivyo kwa mashirika mengine ya kidini? Nimevutiwa sana na ukosefu wa ubinafsi wa wafanyakazi wa kujitolea, na nahisi wanastahili utegemezo wetu. Twahitaji roho kama hii zaidi katika ulimwengu wa leo uliogawanyika.’
“Alirejezea Jumba la Ufalme kuwa ‘uthibitisho wa roho ya ushirikiano.’ Kwa kweli, jambo lililovutia zaidi halikuwa ubuni wa ujenzi huo wala ukubwa wa jengo hilo. Badala ya hivyo, jambo lililovutia wengi katika jumuiya hiyo lilikuwa kwamba jumba hilo lote lilijengwa na wafanyakazi wenye kujitolea nalo likajengwa kwa muda wa saa 48 pekee!”
Ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova katika La Línea na maeneo yalo ya ujirani wanathibitika kuwa waaminifu kupatana na maneno ya Wagalatia 6:10. Hapo mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”y