Sayansi, Dini, na Jitihada ya Kutafuta Kweli
“Jambo la kwamba dini nyingi za bandia zimeenea sana . . . lilikuwa na uvutano fulani juu yangu.”—Charles Darwin
KATIKA kipindi cha mapema cha karne ya 19, sayansi na dini zilikuwa na uhusiano wa karibu sana. “Hata katika maandishi ya kisayansi,” chasema kitabu Darwin: Before and After, “waandikaji hawakusita kusema na Mungu kwa njia ambayo kwa wazi ilikuwa ya kawaida na yenye unyoofu.”
Kitabu cha Darwin cha Origin of Species kilichangia badiliko hilo. Sayansi na mageuzi zilikuja kufanyiza mkataba ulioacha dini—na Mungu—nje. “Kwa mawazo ya kimageuzi,” asema Bwana Julian Huxley, “hakuna tena uhitaji wa kuwa na muumba fulani wa kimungu wala hata haifai.”
Leo nadharia ya mageuzi hudaiwa kuwa msingi muhimu wa sayansi. Sababu kubwa ya uhusiano huo yatajwa na mwanafizikia Fred Hoyle: “Wanayasansi wasiotaka kubadili maoni yao ya kale wanahangaikia zaidi kuzuia maoni shupavu ya kidini ya wakati uliopita badala ya kutazamia kweli.” Ni mambo gani yapitayo kiasi yaliyofanya dini ichukiwe sana na sayansi?
Dini Yaupa Uumbaji Sifa Mbaya
Katika jaribio lililokusudiwa kuunga mkono Biblia, ‘wale wanaounga mkono nadharia ya kwamba ulimwengu uliumbwa kwa muda mfupi’—ambao mara nyingi huungana na Waprotestanti wenye ushupavu—wamesisitiza kwamba dunia na ulimwengu wote mzima umekuwapo kwa miaka ipungukayo 10,000. Ono hilo lenye kupita kiasi limefanya wajiolojia, wastadi wa anga, na wanafizikia wadhihaki fundisho hilo kwa sababu linapingana na mambo waliyogundua.
Lakini kweli Biblia inasema nini? “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” (Mwanzo 1:1) Wakati uliohusika hautajwi wazi. “Siku ya kwanza” ya uumbaji hata haitajwi mpaka Mwanzo 1:3-5, New World Translation. Tayari “mbingu na dunia” zilikuwa zimekuwapo “siku” hii ya kwanza ilipoanza. Kwa hiyo, je, yawezekana kwamba mbingu na dunia zimekuwapo kwa mabilioni ya miaka, kama wanasayansi wanavyodai? Huenda ikawa. Biblia haitaji wakati uliohusika.
Jambo jingine lenye kupita kiasi kuhusu dini ni jinsi wengine wanavyofasiri zile “siku” sita za uumbaji. Baadhi ya watu shupavu husisitiza kwamba hizo ni siku halisi, kufanya uumbaji wa dunia uwe muda wa saa 144 tu. Jambo hilo hutokeza shaka kwa wanasayansi, kwa kuwa wao wahisi kwamba dai hilo linapingana na mambo hakika ya kisayansi.
Hata hivyo, ni fasiri ya watu wenye ushupavu juu ya Biblia—bali si Biblia yenyewe—ndiyo inayopingana na sayansi. Biblia haisemi kwamba kila “siku” ya uumbaji ilikuwa muda wa saa 24; kwa kweli, inatia ndani “siku” hizo zote katika “siku ile BWANA Mungu alipoziumba mbingu na nchi,” ikionyesha kwamba si “siku” zote za Biblia zilikuwa za muda wa saa 24 tu. (Mwanzo 2:4) Huenda baadhi ya siku hizo zilikuwa za muda wa maelfu ya miaka.a
Kwa hiyo, wazo la uumbaji limepata sifa mbaya kutokana na wafuasi wa nadharia ya kwamba ulimwengu uliumbwa kwa muda mfupi tu na watu wenye ushupavu. Mafundisho yao juu ya muda ambao ulimwengu wote mzima umekuwapo na urefu wa “siku” za uumbaji hayapatani na sayansi inayotoa sababu nzuri wala hayapatani na Biblia. Hata hivyo, kuna mambo mengine yapitayo kiasi ambayo yamefanya dini idharauliwe na wanasayansi.
Matumizi Mabaya ya Uwezo
Kupitia historia yote, dini imesababisha ukosefu mwingi wa haki. Kwa kielelezo, katika Enzi za Kati, fundisho la uumbaji liligeuzwa ili liunge mkono kanisa katika kutegemeza autokrasi (mamlaka kamili ya mtu mmoja) ya Ulaya. Lilimaanisha kuwa wanadamu walipangiwa hali zao, wawe matajiri au maskini, na amri ya kimungu. Kitabu The Intelligent Universe chaeleza hivi: “Wana wachanga wa matajiri waliambiwa kwamba ulikuwa ‘mpango wa Mungu’ kwao kupokea sehemu kidogo tu ya mali ya familia zao au kutopokea kitu chochote, na mfanyakazi alihimizwa nyakati zote aridhike na ‘hali ambayo Mungu alimpangia.’”
Si ajabu kwamba wengi wanahofu kurudia “mambo ya kidini yapitayo kiasi katika wakati uliopita”! Badala ya kujaza mahitaji ya kiroho ya mwanadamu, mara nyingi dini bandia imeyatumia mahitaji hayo vibaya. (Ezekieli 34:2) Maelezo katika makala ya mhariri katika gazeti India Today yasema hivi: “Kwa kufikiria rekodi ambayo dini imeweka kwa miaka ambayo imepita, ni ajabu kwamba imedumisha ustahili wowote. . . . Katika jina la Muumba Mkuu Zaidi ya Wote, . . . wanadamu wamefanya ukatili mbaya zaidi dhidi ya wanadamu wenzao.”
Rekodi mbaya sana ya dini bandia ilikuwa na uvutano mwingi juu ya kufikiri kwa Darwin. “Polepole niliacha kuamini Ukristo kuwa ufunuo wa kimungu,” yeye aliandika. “Sababu ya kwamba dini nyingi zilizo bandia zimeenea sehemu kubwa za dunia kwa kasi sana ilikuwa na uvutano juu yangu.”
Ushindi wa Dini ya Kweli
Unafiki wa kidini si jambo jipya katika ulimwengu huu. Yesu aliwaambia watawala wa kidini wa siku yake wenye kutaka makuu: “Mwaonekana kuwa watu wazuri kwa nje—lakini ndani yenu mmejaa unafiki na uovu.”—Mathayo 23:28, Phillips.
Hata hivyo, Ukristo wa kweli “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, NW) Wafuasi wake hawashiriki katika dini na siasa zenye ufisadi; wala hawapotoshwi na falsafa zinazokana kuwapo kwa Muumba. “Hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu,” akaandika mtume Paulo.—1 Wakorintho 3:19.
Lakini, hilo halimaanishi kwamba Wakristo wa kweli ni wajinga kuhusu mambo ya kisayansi. Badala ya hivyo, wafuasi wa dini ya kweli hustaajabia sayansi. ‘Inua macho yako juu, ukaone,’ nabii wa kale Isaya aliambiwa. “Ni nani aliyeziumba hizi?” (Isaya 40:26) Vivyo hivyo, ili kumwelewa Muumba kwa njia bora zaidi, Ayubu aliombwa achunguze maajabu ya asili na ulimwengu wote mzima.—Ayubu, sura za 38-41.
Naam, wale waaminio Muumba huuona uumbaji kwa staha yenye kicho. (Zaburi 139:14) Na zaidi, wao hutumaini asemayo Muumba, Yehova Mungu, juu ya tumaini ajabu la wakati ujao. (Ufunuo 21:1-4) Kupitia funzo la Biblia, mamilioni wanajifunza kwamba wala chanzo cha binadamu wala wakati wake ujao hautegemei nasibu tu. Yehova alikuwa na kusudi fulani alipomfanya mwanadamu, na kusudi hilo litatimizwa—liwe baraka kwa wanadamu wote watiifu. Twakuomba ujichunguzie suala hilo mwenyewe.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Amkeni!, Novemba 8, 1982, kurasa 6-9, Kiingereza, na Insight on the Scriptures, Buku 1, ukurasa 545, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Kwa habari zaidi juu ya nadharia ya uumbaji wa ulimwengu kwa muda mfupi tu na jinsi inavyopingana na sayansi na Biblia, ona matoleo ya Amkeni! ya Kiingereza ya Machi 8, 1983, kurasa 12-15, na Machi 22, 1983, kurasa 12-15.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
JE! HAWAUJUI UTHIBITISHO?
“HATA Mashahidi wa Yehova wamejifunza biolojia sana,” akaandika wakili Norman Macbeth katika kitabu chake cha 1971 Darwin Retried—An Appeal to Reason. Aliposoma makala moja ya Amkeni! katika suala la mageuzi, Macbeth asema: “Nilishangaa kuona kwamba ilikuwa na uchambuzi fulani wenye akili kwa fundisho la Darwin.” Akiona utafiti mwingi sana na manukuu yapatanayo na akili kutoka kwa watu wenye ujuzi kuhusu suala hilo, mtungaji huyo wa vitabu alimalizia hivi: “Si sawa tena kwa Simpson kusema: ‘. . . wale wasioamini [mageuzi], karibu kila mmoja wao, kwa wazi hawaujui uthibitisho wa kisayansi.’”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wakati ujao wa binadamu hautegemei nasibu inayotukia yenyewe