Sayansi Isemapo Unasikilizaje?
MARADHI mapya na vilevile yale ya zamani yanayoibuka tena yanatokeza ugumu kwa sayansi. Watu wakitamani sana kuponywa husikiliza kwa makini wakati sayansi isemapo. Kuhofu kufa hufanya wengi wawe na hamu ya kujaribu dawa yenye matokeo iliyovumbuliwa karibuni, na mara nyingi matokeo ya muda mrefu baadaye hayafikiriwi.
Katika visa vingi sayansi imesaidia watu wengi wenye kuteseka wafurahie hali bora ya maisha. Zenye kutokeza ni njia za upasuaji ambazo huondoa utiaji-damu mishipani, ambao ni hatari. Sayansi na tekinolojia zimempa mwanadamu nguvu ya kufanya mambo yaonekanayo kuwa magumu kuwazia. Zile zilizokuwa hadithi zenye kubuniwa za sayansi wakati mmoja sasa ni uhalisi wa kila siku. Na bado, si sayansi yote inasukumwa na mahitaji ya kukata tumaini ya jamii ya binadamu.
Ni Nani Asemaye?
Sayansi nyingi huchochewa na faida za kimwili na hutegemezwa na mashirika yenye nguvu, kama ilivyotajwa mapema. Kwa hiyo, kabla ya kufikia mikataa au kusisimuliwa na ugunduzi mpya wa sayansi, jiulize, ‘Kwa kweli ni nani asemaye?’ Jifunze kutambua mambo fulani yaliyofichika. Si jambo la siri kwamba vyombo vya habari husitawi juu ya kuripoti mambo yenye kushtua. Waandishi fulani wa habari watafanya jambo lolote liwezekanalo ili kuuza magazeti yao ya habari. Na hata majarida fulani yenye kustahikiwa huruhusu kiwango fulani cha mambo yenye kushtua nyakati fulani.
Mara nyingi hutukia kwamba sayansi na vyombo vya habari huwa na uhusiano wa upendo na chuki. Vyombo vya habari vinaweza kufanya sayansi isifike, lakini, kwa upande mwingine, “mara nyingi wanasayansi hujaribu kudhibiti uenezaji wa habari kwa kukataa mahojiano isipokuwa kama wanaweza kupitia na kusahihisha nakala kabla ya kuchapishwa. Kwa kuogopa kudhibitiwa na wanasayansi walio na haki za kisheria, kwa kawaida maripota husitasita kuwaonyesha wanasayansi makala zao, ijapokuwa mara nyingi huthibitisha usahihi wa habari pamoja nao.” Ndivyo aandikavyo Dorothy Nelkin, katika kitabu chake Selling Science.
Kisha ataja vielelezo ili kuthibitisha hoja yake: “Habari za magazeti kuhusu maendeleo mapya ya sayansi huelekea kufanya watu waliokata tumaini wawe na matumaini makuu. . . . Wagonjwa huja kwenye ofisi za madaktari wao wakiwa na nakala ya karibuni [ya gazeti linalopendwa] na kudai tiba hiyo ya karibuni zaidi.” Kisha, kuna kile kielelezo, kilichonukuliwa na Dorothy Nelkin, cha ripota aliyemwuliza mwenyekiti wa Kamati Maalumu ya Kimataifa Inayoshughulikia Afya na Kazi Ulimwenguni “kama alifikiria waganga wanaweza kutoa matibabu kwa matokeo katika Afrika.” Alijibu kwamba “labda wangeweza kwa sababu wanastahiwa sana na watu.” Lakini namna gani kichwa cha habari katika siku iliyofuata? Kilisema: “Mtaalamu wa U.M. Ametoa Wito Kuwe na Waganga Wengi Zaidi”!
Kwa kusikitisha, yaonekana kuwa mwelekeo wa kisasa ni kwamba watu wengi zaidi na zaidi hutegemea magazeti ya habari na magazeti kuwaarifu juu ya sayansi ya kisasa, asema Nelkin. Na kwa wengi, ambao hawako tayari au labda hawana uwezo sana wa kusoma, televisheni huwa chanzo kikuu cha habari.
Kudumisha Maoni Yaliyosawazika Juu ya Sayansi
Japo ushindi wa sayansi unaonufaisha jamii ya binadamu, lazima tukumbuke kwamba wanasayansi ni wanadamu tu. Wanaweza kushawishiwa na kuwa wafisadi. Nia zao si njema sikuzote. Kwa kweli, sayansi ina mahali pake panapoifaa katika jamii, lakini si nuru isiyoweza kukosea katika ulimwengu unaozidi kupatwa na giza.
Jarida Speculations in Science and Technology laonelea: “Historia ya sayansi huonyesha kwamba hata viongozi wa sayansi . . . waonekane kuwa wenye fahari namna gani, bado wanaweza kukosea.” Kwa hakika, wengine wao wanaweza kukosea hata zaidi.
Kwa ajili ya sababu zilizotolewa katika makala hizi, lingekuwa jambo lisilo la hekima kwa Wakristo kujihusisha katika ubishi wa kisayansi au kuendeleza nadharia za sayansi zisizothibitishwa. Kwa kielelezo, huenda wengine wakajawa na hofu ya usumakuumeme. Kisha, wakiwa na makusudi mazuri kabisa, wanaweza kuanza kuwatia moyo wengine watupilie mbali majoko yao ya microwave, blanketi za umeme, na vitu vinavyofanana na hivyo. Bila shaka, kila mtu ana uhuru wa kujiamulia, bila kuchambuliwa na wengine. Lakini wale wanaochagua jambo tofauti wanapaswa kutarajia kuwa na uhuru uo huo. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuepuka kueneza mambo yenye kushtua. Kama madai mengi yasiyo ya kawaida ni ya kweli au si ya kweli ni jambo ambalo lingali halijathibitishwa. Ikiwa baadhi ya madai haya hatimaye yanathibitishwa kuwa hayana msingi au hata yana makosa, basi wale wanaopigania madai kama hayo hawaonekani wapumbavu tu bali huenda wakawa wamesababisha madhara kwa wengine bila kukusudia.
Uhitaji wa Kuwa na Busara
Mkristo apaswa kuitikia jinsi gani kwa ripoti za sayansi zenye kushtua katika vyombo vya habari? Kwanza, chunguza mwelekeo. Nia ya makala hiyo au taarifa hiyo ni nini? La pili, soma makala nzima. Kichwa cha habari chenye kushtua huenda kisipatane na habari zilizo katika makala yenyewe. La tatu, na la maana zaidi, pima kwa makini rekodi ya wale wanaosema hayo. Je, wao husema kweli? Je, wana mambo fulani yaliyofichika?—Waroma 3:4.
Inaweza kusemwa kuwa ikiwa wanasayansi wanatiliwa shaka na wengine, wao wamechangia jambo hilo. Ustahilifu wa wanasayansi wengine wakiwa watafuta-ukweli wasiopendelea upande wowote umeharibiwa sifa sana. Sayansi imefungua mambo mengi yenye kusisimua juu ya ujuzi wa ulimwengu wetu na ulimwengu wote mzima. Hata hivyo, utabiri fulani juu ya ulimwengu mpya ulio bora wenye msingi wa sayansi hutokeza hofu na hangaiko badala ya tumaini.
Wataalamu fulani wanavumisha maonyo yenye kuogopesha kuhusu misiba iwezayo kutokea wakati ujao. Mshindi wa Tuzo la Amani la Nobeli ambaye ni mwanafizikia Mwingereza Joseph Rotblat alieleza mahangaiko yake namna hii: “Wasiwasi wangu ni kwamba maendeleo mengine katika sayansi yanaweza kutokeza njia nyingine za kuangamiza watu kwa wingi, labda ziwe zikipatikana kwa urahisi zaidi kuliko hata silaha za nyuklia. Ubadilishaji wa jeni ni eneo liwezalo kutumiwa kwa kuangamiza watu kwa wingi, kwa sababu ya maendeleo haya yenye kuogofya ambayo yanatukia katika ubadilishaji wa jeni.” Profesa Ben Selinger wa Chuo Kikuu cha Kitaifa cha Australia alisema juu ya tatizo analoweza kuona kimbele: “Kwa maoni yangu, tatizo linalofuata linaweza kutokea katika eneo la ubadilishaji wa jeni, lakini sijui ni namna gani, au jinsi gani, au lini.”
Kwa upande mwingine, Biblia, Neno la Mungu, ni ‘mwanga wa njia yetu’ ulio hakika na wenye kutegemeka kwa wakati ujao wenye amani, afya njema, na muungano wa ulimwengu, katika dunia iliyosafishwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Zaburi 119:105; Ufunuo 11:18; 21:1-4.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
“Ukuu Wenye Kuenea wa Ngano”
Katika miaka ya majuzi wanasayansi fulani wamezusha shaka nzito kuhusu uwezo wa kudumu kwa nadharia ya mageuzi kama ilivyoelezwa na Charles Darwin. Jambo hilo ni kweli hasa kuhusu wanabiolojia wa molekuli.
Katika kitabu chake Evolution: A Theory in Crisis, Michael Denton, ambaye ni mtafiti wa biolojia, aliandika: “Kuinuliwa kwa nadharia ya Darwin ili kuwa kweli iliyojishuhudia yenyewe kumekuwa na matokeo ya kwamba matatizo yaleyale na upingamizi uleule ambao Darwin alitetea sana katika Origin hayaonekani kabisa. Matatizo mazito kama vile ukosefu wa miunganisho kati ya wanyama au ugumu wa kuona aina za uhai zilizo katikati ya mageuzi ni kama hazizungumziwi kamwe na uumbaji wa hata uhai wenye utata zaidi unapuuzwa kuwa tu uteuzi asilia bila hata shaka yoyote.”
Yeye aendelea kusema: “Ukuu wenye kuenea wa ngano hiyo umetokeza madanganyo yaliyoenea ya kwamba nadharia ya mageuzi ilithibitishwa miaka mia moja iliyopita . . . Huo ni uwongo mtupu.”—Ukurasa wa 77.
“Ikiwa inaweza kuthibitishwa kwamba kuna kiungo chochote tata ambacho hakiwezekani kufanyizwa kwa marekebisho madogo-madogo ya mfululizo, nadharia yangu ingeambulia patupu kabisa.”—Origin of Species, Charles Darwin, ukurasa wa 154.
“Kadiri mifumo ya kibiolojia ya mfumo-tendeano ambayo haiwezi kufafanuliwa iongezekapo,a tuna uhakika kwamba kanuni zinazoshindwa za Darwin hazikubaliki kamwe na sayansi.” (Darwin’s Black Box—The Biochemical Challenge to Evolution, Michael J. Behe, ukurasa wa 39-40) Yaani, ugunduzi wa majuzi katika uwanja wa biolojia ya molekuli wazusha shaka nzito kuhusu nadharia ya Darwin.
“Matokeo ya jitihada nyingi za kuchunguza chembe—kuchunguza uhai kwa kiwango cha molekuli—ni kilio kikubwa kilicho kikali kisemacho ‘ubuni!’ Matokeo hayatatanishi na ni yenye umaana sana hivi kwamba ni lazima yaorodheshwe kuwa mojawapo ya matimizo makubwa zaidi katika historia ya sayansi. Uvumbuzi huo unafikia mavumbuzi ya Newton na Einstein, Lavoisier na Schrödinger, Pasteur, na Darwin. Kutambua huo ubuni wenye akili wa uhai ni muhimu kama vile kutambua kwamba dunia huzunguka jua.”—Darwin’s Black Box, ukurasa wa 232-233.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mazungumzo marefu juu ya mageuzi na biolojia ya molekuli, ona Amkeni!, Mei 8, 1997, ukurasa wa 3-17, lililochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wakristo huepuka kwa hekima ubishi juu ya uwezekano wa kuwepo kwa uhai katika sayari nyinginezo au matokeo yanayodhaniwa ya usumakuumeme
[Hisani]
Picha ya NASA/JPL
Picha ya NASA/JPL