Mageuzi na Wewe
WAKATI wa karne ya 19, The Origin of Species kilisadikisha halaiki za watu kwamba mwanadamu alikuwa ameokoka bila ya mwingilio wa kimungu na angeendelea kufanya hivyo. Kwa kushangazwa na maendeleo ya kisayansi, wengi walihisi kwamba Mungu hakuhitajiwa kamwe na kwamba sayansi ingeweza kuokoa jamii ya kibinadamu. Kile kitabu Age of Progress kilionyesha kwamba karne ya 19 “ilikuwa imehamasishwa na usadikisho kwamba jitihada za kibinadamu zikitumiwa kwa akili zingeweza kubadili ulimwengu.”
Hata hivyo, kuelekea mwisho wa karne hiyo, hata Charles Darwin alisitasita katika mtazamo wake chanya. Kulingana na mwanahistoria mmoja, Darwin alihofia kwamba nadharia ya mageuzi “ilikuwa imemwua Mungu na kwamba matokeo ya wakati ujao kwa wanadamu yalikuwa si hakika.” Alfred Russel Wallace, mchanga aliyeishi wakati mmoja na Darwin, akumbuka hivi: “Wakati wa mazungumzo yangu ya mwisho na Darwin [muda mfupi kabla ya kifo cha Darwin] yeye alionyesha mwono wenye utusitusi kuhusu wakati ujao wa wanadamu.”
Jitihada za Kibinadamu Zimetokeza Nini?
Historia ya karne ya 20 tangu wakati huo imefunua kwamba utusitusi mwingi bado ulikuwa mbele. Maendeleo ya kitekinolojia tangu wakati wa Darwin yalifunika tu ule uliothibitika kuwa muhula wenye giza kupita yote, na wenye ujeuri katika historia yote ya binadamu. Twaishi miongoni mwa kile mwanahistoria H. G. Wells alifafanua kuwa “upotovu wa kimaadili halisi.”
Tangu Wells atoe taarifa hiyo (yapata miaka 75 iliyopita), ulimwengu umeendelea kupatwa na upotovu zaidi wa kimaadili. Hakuna chochote ambacho wanasayansi, wanauchumi, mashirika ya kijamii, serikali za kibinadamu, ama dini za ulimwengu zimejaribu kimetibu hali au hata kusimamisha hilo wimbi. Hali zaendelea kuharibika.
Hivyo basi, kwa uhalisi ni lazima iulizwe hivi: Jitihada za kibinadamu zimetokeza nini? Je, sayansi na tekinolojia zimetokeza ulimwengu ulio bora? “Tunapofungua magazeti ya habari ya kila siku na kutazama yale yanayoendelea,” akasema mwanabiolojia Ruth Hubbard, “hayo matatizo si ya kisayansi. Ni matatizo ya mpangilio wa kijamii, ya mambo yaliyovuka mipaka, ya watu wakifuatia faida na kupuuza mahitaji ya kibinadamu.” Hubbard aliongezea hivi: “Kwa kweli sifikiri kwamba katika kugawanywa kwa rasilimali kwa usawa, kama sayansi kwaweza kusuluhisha yoyote ama mengi ya matatizo yanayosumbua watu walio wengi katika ulimwengu.”
Kwa kweli, kuna faida gani mwanadamu kuweza kusafiri hadi mwezini lakini kutoweza kusuluhisha matatizo ya msingi ya familia ya kibinadamu? Je, ubuni wenye kuongezeka wa silaha zenye kuharibu, kama vile bomu ya atomu, umemaliza vita na ujeuri wa kikabila? Je, matimizo ya kisayansi yamepunguza kwa kutokeza uhalifu, mvunjiko wa familia, maradhi yapitishwayo kingono, ukosefu wa adili, uzaaji wa kiharamu, ufisadi katika vyeo vya juu, umaskini, njaa, kukosa makao, utumizi mbaya wa dawa, uchafuzi? La, kinyume, sayansi imefanyiza baadhi ya mambo haya kuwa mabaya zaidi. Kwa kumwacha Mungu na kumbadilisha na mageuzi na sayansi, familia ya binadamu haijasaidia hali yayo bali imeiumiza.
Si ajabu, wengi wanafikiria upya kuhusu hiyo nadharia ya kwamba mwanadamu aligeuka kutokana na viumbe vifananavyo na nyani, kinyume na kuwapo kwa Mungu aliyeumba binadamu wa kwanza. Uchunguzi wa Gallup katika Marekani ulifunua kwamba ni asilimia 9 tu ya Wamarekani iliyoshikilia ile itikadi ya kwamba mwanadamu aligeuka bila mwingilio wowote wa kimungu; asilimia 47 walikubali lile wazo la kwamba Mungu aliumba mwanadamu katika hali yake ya sasa.
Kile Biblia Ilitabiri
Ingawa The Origin of Species ilitabiri kwamba mwanadamu angesonga mbele kuelekea ukamilifu, Biblia ilitabiri kwamba ulimwengu ungekumbwa na masaibu ya kimaadili. (Mathayo 24:3-12; 2 Timotheo 3:1-5) Biblia pia ilitabiri kwamba masaibu haya yangefikia upeo, ambapo baada ya hapo urithi wa wanadamu waaminifu ungekuwa paradiso, isiyo na matatizo yote ya leo.—Zaburi 37:10, 11, 29; Isaya 11:6-9; 35:1-7; Ufunuo 21:4, 5.
Tumaini hili limefanya wengi kuchunguza Biblia wakiwa na upendezi mkubwa. Je, ingeweza kuwa kwamba kusudi la uhai ni zaidi ya mng’ang’ano ili kuishi? Je, ingeweza kuwa Biblia ina ufunguo si wa wakati uliopita wa mwanadamu tu bali pia wa wakati ujao, kutia ndani wakati wako ujao? Ingekuwa yenye kufaa kwako sana kuchunguza kile Biblia hufunza kwa kweli kuhusu Mungu na makusudi yake kwa ajili ya dunia hii na watu wayo. Ikiwa ungependa habari zaidi, Mashahidi wa Yehova wangefurahia kukusaidia.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Mamilioni wamesaidiwa kuchunguza upya uthibitisho wa Mungu kuhusu uumbaji, wakitumia kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?a Kufikia leo, nakala zipatazo milioni 30 zimechapwa katika lugha 27. Pia, gazeti la Amkeni! laendelea kuchapa habari kuhusu kile hakika za sayansi ya kweli huonyesha kuhusiana na nadharia ya mageuzi.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Kinyume na nadharia ya mageuzi, Biblia ilitabiri masaibu ya kimaadili ya leo na suluhisho layo—paradiso isiyo na masumbufu
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Picha ya U.S. Coast Guard
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Mtoto anayeteseka kwa njaa: Picha ya WHO na P. Almasy
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Kulia: Picha ya U.S National Archives