Kuutetea Ukweli Katika Ulimwengu Unaomkana Mungu
“Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli.”—YOHANA 17:17.
1. (a) Ni wakati gani na jinsi gani ukweli ulipata kuwa suala la kubishaniwa? (b) Ni ukweli gani mpya ulio bora sana uliotajwa katika Edeni?
UKWELI ni suala lililobishaniwa muda mrefu! Suala hilo, ambalo ni la zamani kama historia ya wanadamu, lilitokezwa kule nyuma katika Edeni, wakati Nyoka wa kwanza alipotilia shaka ukweli wa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Waliposhawishwa, wazazi wetu wa kwanza walichagua kuwa na mawazo ya kujitegemea na kufuata njia yao wenyewe ya kichoyo. Hawakuwa watetea ukweli wenye kushika ukamilifu. Lakini hapo Mungu alijulisha ukweli ulio bora kati ya kweli zote mpya, kwamba “uzao” wa Ufalme ungezaliwa uvunje kazi za Ibilisi.—Mwanzo 3:1-6, 14, 15.
2. (a) Ukweli ulishambuliwaje katika ulimwengu ulioitangulia Gharika? (b) Kwa sababu gani Noa na jamaa yake walipata upendeleo wa Yehova?
2 Sasa ukweli ulikuwa ukishambuliwa. Yule Mdanganyi mkuu alitafuta kuungwa mkono na wana wengine wa kiroho wa Mungu waliokuwa waasi ili aiharibu dunia. Kizazi kisichofuata adili kabla ya Gharika kilijishughulisha sana kufanya mambo kivyao hata kikashindwa kutii onyo lililotolewa na Noa. Kiliangamia. Lakini Noa na jamaa yake waliokoka kwa sababu ya ukamilifu wao usio na lawama. Wateteaji hao wa ukweli walipotoka katika safina ya hifadhi, wazo lao la kwanza lilikuwa kutoa dhabihu za shukrani—“harufu ya kupumzisha” Yehova—Mwanzo 6:4-12; 8:18-21; Luka 17:26, 25 2 Petro 2:5, NW.
Hasara Iliyoletwa na Uwongo
3. Babuloni Mkuu ni nini, nayo ilianzaje?
3 Hata hivyo, Nyoka huyo wa zamani, Ibilisi, aliendelea na jitihada zake za kuyatia matope maji ya ukweli. Bila shaka ilikuwa chini ya mwelekezo wa Kishetani kwamba Babuloni wa kale ukajengwa. ‘Mafumbo ya Babuloni’ yakawa ndiyo msingi wa milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, inayosimuliwa katika Ufunuo 17:5 (NW) kuwa,’“Babuloni Mkuu, mama ya makahaba na ya vitu vyenye kuchukiza vya dunia.” Maelfu ya visehemu vyake, vyenye mafundisho ya kimadhehebu yenye kupingana, vimeendelea kuwapo mpaka leo hii vikiwa mkusanyo mkubwa wa makosa ya kidini.—Mwanzo 10:8-10; Yeremia 51:6.
4. Yesu aliteteaje ukweli, na matokeo yalikuwa nini?
4 Yesu Kristo alipokuwa duniani, aliutetea ukweli kwa ujasiri. Akisema na wanafiki wa kidini wa siku zake, yeye alisema: “Ninyi mnatoka kwa baba yenu Ibilisi . . . Yeye hakusimama katika ule ukweli, kwa sababu ukweli haumo ndani yake.” Zaidi ya hayo, Yesu, aliye “uzao” wa ahadi uliotabiriwa, alikazia umaana wa ukweli alipomwambia Pontio Pilato hivi: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mfalme. Kwa ajili ya hili mimi nimekuja kuingia ndani ya ulimwengu, kwamba nipaswe kutoa ushuhuda kwa ule ukweli.” Yesu aliutoa uhai wake wa kibinadamu kwa kuutetea ukweli—ukweli wa Ufalme.—Yohana 8:44; 18:37, NW; Mwanzo 3:2-5.
5, 6. (a) Shetani aliendeleaje kupiga vita dhidi ya ukweli? (b) Ni uchafuzi gani uliotokea, na ni mambo gani ya uwongo yaliyotokana nao? (c) Kwa sababu gani tutake kuwa wateteaji wenye bidii wa ukweli?
5 Uwongo unaambatana na uvunjaji wa sheria. Kwa hiyo haishangazi kwamba Shetani, akiendelea na vita yake dhidi ya ukweli, alitokeza jamii ya makasisi wenye kuasi imani, inayosimuliwa katika 2 Wathesalonike 2:3 kuwa “mtu wa kuasi.” Baada ya mitume wa Yesu Kristo kufa, waasi-imani hao walijiinua juu ya makabwela wa kidini na kuchafua mafundisho safi ya Kikristo kwa kuyaingiza “mafumbo” ya Kibabuloni na falsafa ya Kigiriki, yenye kutokeza ikiwa ni nadharia ya Plato kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa.
6 “Uwongo huo umekuwa msingi wa uwongo mwingine mwingi, kama vile kusema ‘watu wote wema huenda mbinguni,’ ‘watu wasio wazuri sana huenda kwenye purgatori,’ na ‘wabaya wanachomwa milele katika moto wa mateso.’ Kwa kuwa kuna mafundisho mengi sana yenye makosa katika milki ya dini ya Kibabuloni, tunaweza kuwa wenye furaha kama nini kwamba Yesu aliahidi hivi: “Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli. Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru”! Inatupasa tutake kuwa wateteaji wenye bidii wa ukweli unaotoa uhuru!—Yohana 8:31, 32.
Kuangulia Uwongo Mkubwa
7. (a) Mradi wa Shetani ni nini, naye anajaribuje kuutimiza? (b) Ni fundisho gani la uwongo lililotokea wazi katika karne ya 19?
7 Lakini, Ibilisi anafanya kila jambo aupinge ukweli. Anakasirika sana mtu ye yote akiliamini neno la Mungu la ukweli, Biblia Takatifu. Mradi wake ni ‘kupofusha akili za wasioamini, ili wasijue habari njema tukufu juu ya Kristo.’ Ibilisi amelenga kuusingizia ukweli, si kwa kumfanya tu “mtu wa kuasi” ajaribu kuingiza mafundisho ya uwongo wa kidini katika Biblia bali pia kwa kudai kwamba Biblia inategemea hadithi za uwongo na mapokeo. Kwa hiyo, wakati wa karne ya 19, Nyoka huyo wa zamani aliangua fundisho jingine la uwongo na udanganyifu. Limeitwa nadharia ya mageuzi.—2 Wakorintho 4:4, NW.
8. Nadharia ya Darwin inasema nini?
8 Mwaka 1859, “wakati wa mwisho” unaotajwa na Biblia ulipokaribia, Charles Darwin alichapisha katika Kiingereza kitabu chake chenye kichwa “Kuhusu Chanzo cha Aina za Viumbe Kupitia Uchaguzi wa Asili, au Kuhifadhiwa kwa Jamii Zilizopendelewa Katika Mng’ang’ano wa Kuishi.” (Danieli 12:4) Darwin alitokeza nadharia ya kwamba vitu vilivyo hai havikuumbwa bali viligeuka kutoka namna za awali za uhai kupitia “uchaguzi wa asili uliotokezwa na mng’ang’ano wa kuishi.” Mwishowe, mtu akageuka kutokana na nyani fulani. Darwin alidai ati ilitokea hivyo kwa kutegemea “kusalimika kwa vilivyo bora na vyenye uwezo zaidi.”
9. (a) Ni kweli gani za Biblia zilizofundishwa na Yesu ambazo zingekuwa hazina maana kama mageuzi yangekuwa jambo la kweli? (b) Ile dhana tupu ya “kusalimika kwa vilivyo bora na vyenye uwezo zaidi” imeleteaje wanadamu madhara makubwa?
9 Nadharia hiyo inakanusha kwa ukaidi masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji na kuanguka kwa mwanadamu katika dhambi. Inaelekea kufanya dhabihu ya ukombozi ya Yesu na mafundisho ya Biblia juu ya Ufalme, ufufuo, uzima wa milele, na dunia-paradiso yakose maana. Zaidi ya hayo, nadharia ya mageuzi, kama ni ya kweli, ingewaondolea wanadamu hali ya kulaumiwa na Muumba juu ya mwenendo mbaya.a Kwa kulipendekeza wazo la “kusalimika kwa vilivyo bora na vyenye uwezo zaidi” tu, bila shaka nadharia hiyo iliweka msingi wa kusitawi kwa siasa za Marksi, za Nazi, za Ufashisti na nyinginezo.b Wateteaji wa mageuzi ni lazima walibebe lawama kubwa kwa kutokeza sehemu kubwa ya kule kumkana Mungu na kuteseka ambako kumo ulimwenguni leo.—Zaburi 14:1-4.
Wateteaji wa Uwongo
10. Kwa habari ya Darwin, ni kwa njia gani makasisi walionekana kuwa wateteaji wa uwongo?
10 Je! makasisi wa wakati wa Darwin walipinga nadharia hiyo yenye kumvunjia Mungu heshima? Kwa kushangaza, profesa mmoja wa Chuo Kikuu cha Kembriji anaandika hivi: “Hapo kwanza upinzani mwingi kwa nadharia ya Darwin ulitoka kwa wanasayansi kwa sababu ya kukosa ushuhuda, wala haukutoka kwa walimu wa dini kwa sababu ya kukosa uthibitisho wa maandiko.” Mtaalamu mwingine mwenye elimu anaongeza hivi: “Wataalamu maarufu wa Kikristo katika Uingereza na Amerika, isipokuwa wachache, walikubaliana upesi sana na nadharia ya Darwin na mageuzi.” Mwaka 1882, Darwin hata alizikwa kati ya wafalme katika Makao ya Watawa ya Westminster, kwa mpango wa pekee uliofanywa pamoja na kasisi wa Anglikana wa makao hayo ya watawa!—Linganisha Matendo 20:30; 2 Timotheo 4:3.
11. Makasisi wamesema maneno gani juu ya nadharia ya Darwin inayoonyesha hakuna Mungu?
11 Sasa nadharia ya Darwin inayoonyesha hakuna Mungu inakubaliwa kuwa ‘ukweli wa Injili’ na wengi wa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Askofu mkuu wa York, ambaye ndiye kasisi mwenye cheo cha pili kwa ukubwa katika Kanisa la Uingereza, anaiona nadharia ya mageuzi ya kibayolojia (uhai) kuwa imethibitika sana hivi kwamba hiyo ndiyo “msingi wa pekee wa bayolojia ya kisasa.” Hivi majuzi, kwenye mkutano mmoja wa Vatikani, wanachuo 12 wenye kuwakilisha baraza kuu zaidi la kisayansi la Kanisa Katoliki walisema: “Tumesadikishwa kwamba ushuhuda mwingi sana unafanya uhalisi wa wazo la mageuzi ya mtu na nyani wengine lisiweze kukanushwa.” Nacho kitabu New Catholic Encyclopedia kinaongeza hivi: “Mageuzi ya ujumla, hata ya mwili wa mtu yaelekea ndiyo maelezo ya kisayansi yanayoonyesha vizuri zaidi mianzo [ya vitu vilivyo hai].” Lakini kweli ni ya kisayansi? Je, mageuzi yanaungwa mkono na uthibitisho wa kisayansi unaotegemeka? Uzima wako unategemea kuujua ukweli wa jambo hili.—Yohana 14:6; 16:13; 17:17.
12. Kwa sababu gani ni lazima tuseme kwamba nadharia ya uumbaji haipatani na Maandiko tena haiaminiki?
12 Hivi majuzi, dini fulani zinazochukua mambo yote kwa uhalisi zimeitokeza nadharia ya uumbaji ili kulijibu wazo la mageuzi. Lakini kwa kufanya hivyo, zinatokeza dai ambalo si la kimaandiko na lisiloaminika. Dai hilo ni kwamba mbingu, dunia, na kila kitu duniani kiliumbwa na Mungu katika siku zenye saa 24 kila moja—ndiyo, kwa saa halisi 144 tu! Fundisho hilo limewafanya wengi waidhihaki Biblia. Lakini je, nyakati zote “siku” katika Biblia maana yake ni muda wa saa 24? Andiko la Mwanzo 2:4 linasema juu ya “siku ambayo Yehova Mungu alifanya dunia na mbingu.” (NW) Siku hiyo moja inatia ndani “siku” zote sita za uumbaji zinazotajwa katika Mwanzo sura ya kwanza. Kulingana na matumizi ya Biblia, “siku” moja ni kipindi fulani cha wakati uliopimwa. “Siku” moja kwa Yehova inaweza kuwa miaka elfu moja, au maelfu kadha ya miaka—kama zilivyokuwa “siku” za uumbaji. Kwa hiyo, kuhusu jambo hili, masimulizi ya Biblia yanasadikika na kupatana na sayansi ya kweli.—2 Petro 3:8.
Mwanzo wa Uhai
13. (a) Wateteaji wa mageuzi wanauelezaje mwanzo wa uhai? (b) Kwa sababu gani ni ujinga kusema kwamba chembe iliyo hai ilijiumba yenyewe kwa aksidenti?
13 Wateteaji wa mageuzi wanaelezaje mwanzo wenyewe wa uhai? Wanasema kwamba mabilioni fulani ya miaka iliyopita bahari yenye kuizunguka dunia huenda ikawa ilikuwa “mchuzi wenye mabaki ya vitu-vitu,” ingawa bado vilikuwa bila uhai. Halafu, wanaeleza, ‘molekyuli yenye kutokeza ilifanyizwa na aksidenti isiyoelekea sana kutukia.’ Kwa muujiza, molekyuli hiyo ikajigawanya ifanyize molekyuli nyingine zilizojiunganisha zifanyize chembe iliyo hai. Hii ni ndoto, au nini? Mwandikaji aliyetoa maelezo hayo alisema hivi katika utangulizi wa kitabu chake: “Kitabu hiki chapasa kusomwa kama kwamba ni hadithi ya sayansi ya kubuniwa tu.” Ndiyo, hadithi tu ya kubuniwa, lakini si sayansi hata kidogo! Gazeti National Geographic limesema kuhusu maagizo yaliyoamrishwa (DNA) katika chembe moja ndogo kwamba “kama yangeandikwa, yangejaa vitabu elfu moja vya kurasa 600.” Ni ujinga ulioje kusema kwamba chembe iliyo hai ilijiumba yenyewe kwa aksidenti katika mchuzi fulani wa kale na kale!
14. Ni fundisho gani la msingi ambalo ni lazima sisi tulio wateteaji wa ukweli tuliunge mkono?
14 Maelezo yenye kusadikika zaidi, na yaliyo rahisi kuelewa, ni yale yanayotolewa na mwandikaji wa Biblia, Daudi, aliyeandika hivi katika Zaburi 36, mistari 5 na 9: “Ee [Yehova],. .. kwako Wewe iko chemchemi ya uzima.” Sisi tulio wateteaji wa ukweli ni lazima tuliunge mkono fundisho hilo la msingi la Biblia.—Ona pia Zaburi 100:3; Isaya 42:5, 8.
Mageuzi ya Hatua kwa Hatua—au Uumbaji wa Moja kwa Moja?
15. (a) Kwa habari ya kutokea kwa namna za uhai, masalio ya vitu vilivyokuwa hai yanaonyeshaje mageuzi ni uwongo? (b) Ukweli ulio hakika unatajwaje kwenye Mwanzo 1:25?
15 Lakini, je, haiwezi ikawa kwamba, baada ya uhai kuwapo, aina mbalimbali za vitu vilivyo hai huenda vikawa viligeuka hatua kwa hatua vikawa aina nyingine? Kama ingetokea hivyo, sehemu za vitu vilivyokuwa hai ambazo zilisalia ndani ya ardhi zingeonyesha hivyo. Lakini, je, zinaonyesha hivyo? Ebu fikiria kile kinachoitwa kipindi cha Kambria. Hapo masalio ya vikundi vikubwa-vikubwa visivyokuwa na mifupa ya uti wa mgongo yanaonyeshwa kwa mara ya kwanza yakiwa pamoja katika “mlipuko” wa vitu vilivyo hai. Ikiwa vikundi-vikundi hivyo vinavyotofautiana sana vililipuka vyote pamoja vikawa hai wakati mmoja, ingaliwezekanaje kuwa kimoja kikageuka kutokana na kingine? Darwin mwenyewe aliungama hivi waziwazi: “Ikiwa aina-aina nyingi . . . zimeanza kweli kweli kuwa hai kwa wakati mmoja, uhakika huo ungeiangamiza nadharia ya mageuzi.” Iangamie kweli kweli!—1 Wakorintho 3:19, 20.
16. (a) Kwa habari ya kutokea kwa namna za uhai, masalio yanatoaje uwongo kwa mageuzi? (b) Ukweli katika Mwanzo 1:25 unaelezwaje?
16 Masalio ya vitu vilivyokuwa hai yanaonyesha kwamba namna tofauti za uhai wa hali ya juu sana zilitokea kwa ghafula zikiwa zimekamilika kabisa. Ni kama profesa mmoja wa sayansi ya asili alivyoeleza: “Nyangumi, popo, farasi, jamii ya nyani, ndovu, sungura, kindi, n.k., wote wanatofautiana kabisa sasa sawa na vile walivyotofautiana mara ya kwanza. Hakuna dalili yo yote ya kuonyesha kwamba walikuwa na mzazi mmoja, achilia mbali kuwa na uhusiano na mtambaazi ye yote, anayedhaniwa kuwa ndiye babu yao.” Je! kuna masalio yo yote ya twiga wenye shingo zilizo theluthi mbili au robo tatu ya urefu ule wa kawaida? La, hakuna. Ukweli wa jambo hilo ni kama ulivyotajwa katika Mwanzo 1:25: “Mungu akafanya mnyama wa mwitu kwa jinsi zake, na mnyama wa kufugwa kwa jinsi zake. Mungu akaona ya kuwa ni vyema.” Ndiyo, vyema sana!
17. Ni uzuri na ubuni gani unaoonekana kati ya vitu vilivyo hai vyenye namna namna, na ni nani peke yake angeweza kuwa ndiye aliyevianzisha?
17 Pia fikiria utofautiano wenye kusisimua unaoonekana kati ya vitu vilivyo hai hapa duniani! Je! waridi, kipepeo, ndege-mvumaji, tausi, na maelfu mengine ya vitu vilivyo hai vilipata kwa bahati tu uzuri wavyo unaotofautiana, katika mng’ang’ano wa kusalimika kwa vilivyo bora na vyenye uwezo zaidi? Au hivyo ni ubuni wa ustadi wa Mungu mwenye upendo anayetaka wanadamu wafurahie kazi zake? Tunapoona uzuri wa vitu vingi vizuri ajabu ambavyo Mungu wetu ameleta duniani, hakika ni lazima tuitikie kwa mshangao hivi: “Kazi zako ni nyingi kama nini, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa mazao yako.”—Zaburi 104:24, NW.
18. Kwa sababu gani wewe ungesema kwamba Mungu peke yake ndiye angeweza kuwa alibuni mnyama platipo?
18 Nyakati zote ubuni unataka mbuni. Na kuna ubuni wenye kustaajabisha katika vitu vilivyo hai. Fikiria mnyama mmoja anayeitwa platipo, anayeishi katika Australia. Ukubwa wake ni kama wa sungura, ana manyoya kama ya fisimaji, ana mdomo kama wa bata, vikwaru kama vya jogoo, na vidole vyenye utando na kucha. Anataga mayai kama mtambaazi, ananyonyesha watoto wake kama wanyama wanyonyeshao. Anazoea kuishi katika nchi kavu au chini ya maji. Sasa mnyama huyo platipo aligeuka kutokana na kitu gani? Kwa kuwa anajitokeza usiku tu, mnyama huyo angeweza kuitwa jinamizi la wanamageuzi. Mtaalamu wa elimu-viumbe (mbayolojia) wa Chuo Kikuu cha Harvard anamsimulia kuwa “kiumbe aliyebuniwa vizuri ajabu kwa ajili ya namna fulani ya pekee na isiyo ya kawaida, ya maisha.” Naye Mbuni huyo wa ajabu ni nani? Hakuna mwingine ila yule Mungu anayesema: “Kila hayawani [au mnyama-mwitu] ni wangu.”—Zaburi 50:10,
19. (a) Ndege-mwimbaji aliye mdogo sana anafanya tendo gani la ajabu? (b) Anaweza kufanya hivyo Kwa njia gani?
19 Zaidi ya hilo, namna gani silika iliyoingizwa ndani ya vitu vingi vilivyo hai? Kwa mfano, kuna ndege-mwimbaji aliye mdogo sana, ambaye uzito wake ni gramu 21. Anajua jinsi ya kuchagua majira yanayofaa ya vuli aruke kutoka Alaska mpaka New England (sehemu ya Amerika Kaskazini). Akiwa huko ananona kwa kula chakula kizuri kisha anangojea upepo wa baridi. Halafu anaondoka, akiruka juu mwinuko wa kufikia meta 6,100 au zaidi ili aupate mkondo mkubwa wa upepo unaoelekea Afrika, mpaka anaposhikwa na pepo zenye nguvu zinazovuma na kumrusha mpaka makao yake katika Amerika ya Kusini. Ujuzi wote wa kisilika wa ndege-mwimbaji umeamrishwa katika ubongo unaolingana na punje ya mbaazi kwa ukubwa. Je! mwenye kuamini mageuzi anaweza kueleza jinsi silika hiyo ilivyotokea? Wapi. Lakini Biblia inaonyesha kwamba Yehova ndiye mwenye hekima yote “aliyezifanya mbingu na nchi, bahari na vitu vyote vilivyomo,” kutia na viumbe wale ambao wana “hekima kisilika.”—Zaburi 146:5, 6, UV Mithali 30:24-28, NW.
Je! Wewe Unaonyesha Shukrani?
20. (a) Ni nini ambacho bila shaka ndilo elezo la maajabu yanayotuzunguka? (b) Fadhili za upendo za Muumba wetu zinaonyeshwaje kutuelekea sisi? (c) Inatupasa tuitikieje sisi tulio wateteaji wa ukweli?
20 Ukweli ni huu: Katika mbingu na dunia inayotuzunguka kuna vitu vingi sana vinavyovutia, vinavyofaa, na vyenye kutia woga wa mshangao, hivi kwamba jawabu la pekee juu ya jinsi vilivyotokea ni kwamba viliumbwa na Mbuni mwenye nguvu zote aliye na upendo! Jinsi hisia zetu tulizopewa na Mungu zinavyofanana vizuri ajabu na mazingira yetu ya asili, chini ya hali za kawaida zenye afya, ili kufanya maisha yafurahike! Machweo ya jua tunayoona, maua yenye kunukia vizuri tunayonusa, matunda matamu tunayoonja, upepo mtulivu wenye kuburudisha tunaohisi, muziki wa misitu tunaosikia—vitu hivyo vinaonyesha fadhili za upendo za Muumba na Mungu wetu kwa njia iliyoje! (Zaburi 136:1-6, 25, 26) Inatupasa tutake kuonyesha shukrani zetu kwa bidii nyingi kama nini kwa kuutetea ukweli katika ulimwengu huu unaomkana Mungu! Naam, “neno [la Mungu] ndiyo kweli”!
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha ukweli wa Biblia kama ulivyofundishwa na Yesu Kristo katika Ufunuo 4:11; Mathayo 19:4; Luka 24:46, 47; Mathayo 20:28; 6:10; Yohana 5:28, 29; 17:3; Luka 23:43.
b Karl Marx alisema: “Kitabu cha Darwin ni cha maana sana nacho kinanisaidia kupata msingi wa pambano la kitabaka ambalo limekuwako katika historia.”
Katika Kuutetea Ukweli, Wewe Ungejibuje?
◻ Ukweli ulipataje kuwa suala la kubishaniwa?
◻ Ukweli wa Biblia unafunuaje makosa ya Kibabuloni?
◻ Ni maelezo gani tu yanayoweza kutolewa juu ya mahali zilikotoka aina za uhai?
◻ Ubuni ulio katika vitu vilivyo hai unatuambia nini?
◻ Tunaweza kumshukuruje Muumba wetu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Yesu aliwaambia wazi wapinzani wa ukweli, “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi”
[Picha katika ukurasa wa 12]
Charles Darwin—mteteaji wa nadharia ya nyani-mtu
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kanisa la Uingereza lilimhifadhi Darwin katika Makao ya Watawa ya Westminster
[Picha Credit Line katika ukurasa wa 15]
U.S. Fish & Wildlife Service
[Picha katika ukurasa wa 15]