Athari za Nadharia ya Mageuzi
MAPEMA katika karne ya 19, dini na sayansi zilifurahia uhusiano wenye amani ya kiasi. Miaka miwili tu kabla ya kuchapishwa kwa The Origin of Species, mwanabiolojia na profesa wa Chuo Kikuu cha Harvard Louis Agassiz aliandika kwamba ulimwengu wa viumbe-hai huonyesha “makusudio, hekima, ukuu” na kwamba kusudi kuu la usitawi wa asili lilikuwa kuchanganua “mawazo ya Muumba wa Ulimwengu Mzima.”
Maoni ya Agassiz yalikuwa ya kawaida. Watu wengi waliiona sayansi na dini kuwa kitu kimoja. Mavumbuzi ya sayansi mara nyingi yalionekana kuwa uthibitisho wa Muumba Mtukufu. Lakini ufa ambao haukuwa bayana ulikuwa ukisitawi kati ya dini na sayansi.
Kushuku Kwatia Mizizi
Principles of Geology vya Charles Lyell, juzuu la kwanza ambalo lilitokea katika 1830, lilitokeza mashaka juu ya masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji. Lyell alidai kwamba uumbaji haungeweza kuwa ulitukia kwa siku sita halisi. Mwanafizikia Fred Hoyle aliandika hivi: “Vitabu vya Lyell vilikuwa na daraka kubwa la kusadikisha ulimwengu kwa ujumla kwamba Biblia ingeweza kuwa na makosa, kwa kiwango fulani vilisadikisha, wazo ambalo halikuwaziwa kamwe.”a
Hivyo msingi uliwekwa kwa ajili ya kushuku. Katika akili za wengi, sayansi na Biblia hazingeweza kupatanishwa kamwe. Walipokabiliwa na uchaguzi, wengi walichagua sayansi. “Vitabu vya Lyell vilikuwa vimetokeza mashaka juu ya sura za kwanza za Testamenti ya Kale,” Fred Hoyle akaandika, “nacho kitabu cha Darwin kilikuwa pale kuchukua mahali pavyo.”
The Origin of Species kilikuja kwa wakati wake kwa wale ambao hawakutaka kukubali Biblia kuwa Neno la Mungu. Usahibu ulikuwa tayari umesitawi kati ya mwanadamu na sayansi. Umma iliyokuwa imeshawishiwa na sayansi ilihisi kuvutiwa na ahadi na matimizo ya sayansi. Kama mchumba mwenye mali, sayansi ilimpa mwanadamu zawadi mpya kwa wingi—darubini, hadubini, na injini ya kutumia mvuke na baadaye, umeme, simu, na magari. Tekinolojia tayari ilikuwa imetokeza vuvumko la kiviwanda ambalo liliandalia watu wa kawaida faida za kimwili chungu zima.
Kinyume na hilo, dini ilionekana kuwa kizuizi cha maendeleo. Wengine walihisi kwamba ilifungia watu katika uduni, wasiweze kwenda sambamba na maendeleo ya haraka ya kisayansi. Waatheisti walianza kutangaza maoni yao kwa uthabiti na ujasiri zaidi. Kwa kweli, kama Richard Dawkins alivyoandika, “Darwin alifanya iwezekane kwa watu kuwa waatheisti wenye akili wenye kuridhika.” Sayansi ilikuwa inakuja kuwa tumaini jipya la wokovu la mwanadamu.
Mwanzoni, viongozi wa kidini walipinga nadharia ya mageuzi. Lakini kadiri miongo ilivyopita, makasisi kwa ujumla walikubali maoni yaliyokuwa maarufu, wakikubali mwigizo wa mageuzi na uumbaji. Kichwa kikuu cha New York Times la 1938 kilitangaza hivi: “Ripoti ya Kanisa la Uingereza Yakubali Maoni ya Kimageuzi ya Uumbaji.” Hiyo ripoti, ya tume iliyokuwa chini ya Askofu Mkuu wa York, ilitaarifu hivi: “Hakuna kukataa nadharia ya mageuzi kuwezako kutolewa kutokana na masimulizi mawili ya uumbaji katika Mwanzo 1 na 2, kwa sababu imekubaliwa kwa ujumla miongoni mwa Wakristo walioelimika kwamba masimulizi haya ni ya kihekaya kwa msingi na kwamba thamani yayo kwetu ni ya kimfano badala ya kihistoria.” Tume ya askofu mkuu ilimalizia hivi: “Unaweza kufikiri utakavyo na bado uwe Mkristo.”
Kwa wengi, majaribio kama hayo ya kupatanisha Biblia pamoja na mageuzi yalipunguza tu ustahiki wa kusadikisha wa Biblia. Hilo lilitokeza uenezi mkubwa wa kushuku Biblia, na jambo hili bado lipo leo, hata miongoni mwa viongozi fulani wa kidini. Kielelezo ni maelezo ya askofu wa Episkopali katika Kanada aliyedai kwamba Biblia iliandikwa katika muhula wa kabla ya sayansi na kwamba ilidhihirika kuwa yenye kupendelea na kutofahamu mambo. Yeye alisema kwamba Biblia ina “makosa ya kihistoria” na “utiaji-chumvi wenye kupita kiasi” kuhusu kuzaliwa kwa Yesu na kufufuka.
Hivyo, wengi kutia ndani washiriki wa makasisi, wamekuwa wepesi sana kuikosoa Biblia. Lakini je, kushuku huko kumeongoza wapi? Ni tumaini jipi la badala ambalo limetolewa? Kukiwa na kudhoofika kwa imani kuelekea Biblia, wengine wameendea falsafa na siasa.
Athari juu ya Falsafa na Siasa
The Origin of Species kilitoa mtazamo mpya juu ya tabia za kibinadamu. Kwa nini taifa moja hufaulu kulishinda taifa jingine? Kwa nini jamii moja hushinda nyingine? The Origin of Species, kwa mkazo wacho juu ya uteuzi asilia na halisalimika kwa wafaao zaidi, kilitoa maelezo ambayo yalichochea wanafalsafa mashuhuri wa karne ya 19.
Friedrich Nietzsche (1844-1900) na Karl Marx (1818-1883) walikuwa wanafalsafa waliokuwa na athari kubwa juu ya siasa. Wote wawili walivutiwa na mageuzi. “Kitabu cha Darwin ni muhimu,” akasema Marx, “nacho chanitolea msingi wa kisayansi wa asili kwa ajili ya ming’ang’ano ya tabaka za kijamii katika historia.” Mwanahistoria Will Durant alimwita Nietzsche “mtoto wa Darwin.” Kile kitabu Philosophy—An Outline-History kilitoa muhtasari wa mojapo itikadi za Nietzsche hivi: “Watu wenye nguvu, jasiri, wenye kutamalaki, wenye kujivuna, wafaa kuliko wote katika jamii ya wakati ujao.”
Darwin aliamini—na aliandika kwenye barua kwa rafikiye—kwamba katika wakati ujao “idadi isiyo na mwisho ya jamii za tabaka la chini zitakuja kufyekwa na jamii za tabaka la juu zilizostaarabika kotekote ulimwenguni.” Alitumia kama kielelezo ushindi wa Wanaulaya kwa wengine na kuelekeza jambo hili kuwa “mng’angano ili kuishi.”
Wenye nguvu walikuwa na haraka kutumia taarifa kama hizo kwa manufaa yao. H. G. Wells aliandika hivi katika The Outline of History: “Watu wenye kushinda kufikia mwisho wa karne ya kumi na tisa waliamini kwamba walishinda kwa msingi wa Mng’angano ili Kuishi, ambao katika huo wenye nguvu na wajanja huwashinda walio dhaifu na wenye kuaminika. Na zaidi waliamini kwamba walihitaji kuwa wenye nguvu, wenye nishati, wakatili, ‘wenye ustadi,’ wenye kushindana.”
Hivyo, “halisalimika kwa wafaao zaidi” ikachukua maana ya kifalsafa, kijamii na kisiasa, mara nyingi ikivuka ilichomaanisha. “Kwa wengine vita vikawa ‘ulazima wa kibiolojia,’” kikasema kitabu Milestones of History. Na kitabu hiki kilionelea kwamba wakati wa karne iliyofuata, “maoni ya Darwin yalifanyiza sehemu muhimu ya imani ya Hitler ya ukuu wa kijamii.”
Bila shaka, wala Darwin, wala Marx, wala Nietzsche hawakuishi kuona jinsi maoni yao yangetumiwa—ama kutumiwa vibaya. Hakika, walitazamia kwamba ule mng’ang’ano ili kuishi ungeboresha njia ya maisha ya mwanadamu. Darwin aliandika katika The Origin of Species kwamba “nyenzo zote za kimwili na kiakili zitaelekea kukua kuelekea ukamilifu.” Padri na mwanabiolojia wa karne ya 20 Pierre Teilhard de Chardin alikubaliana na hili, akinadharia kwamba hatimaye kungetukia ‘mageuzi ya akili zote za jamii ya kibinadamu; kila mtu angefanya kazi kwa upatano kuelekea lengo moja.’
Kudhoofika, Si Kuboreka
Je, unaona kuboreka kama huko kukitukia? Kile kitabu Clinging to a Myth chataja juu ya mwelekeo chanya wa De Chardin hivi: “De Chardin lazima awe alikosa uelewevu kuhusu historia ya umwagaji damu wa mwanadamu na mifumo ya kubagua jamii kama vile ubaguzi wa rangi katika Afrika Kusini. Yeye asikika kama mwanadamu ambaye haishi katika ulimwengu huu.” Badala ya kusonga mbele kuelekea umoja, jamii ya binadamu katika karne hii imepatwa na migawanyiko ya kijamii na kitaifa kwa kiwango kisichowazika.
Lile tumaini lililotolewa katika The Origin of Species, kwamba mwanadamu angesonga mbele kuelekea ukamilifu, ama angalau kuboreka, liko mbali na kutimizwa. Na tumaini hilo huendelea kunyong’onyea kwa kupita kwa wakati, kwani tangu kukubali mageuzi kwa ujumla, familia ya binadamu mara nyingi imezidi kudidimia kwenye unyanyaswaji wa kijamii. Ebu fikiria: Zaidi ya watu milioni 100 wameuawa katika vita vya karne hii, yapata milioni 50 katika Vita ya Ulimwengu 2 peke yake. Pia fikiria machinjo ya kikabila ya hivi majuzi katika mahali kama vile Rwanda na iliyokuwa Yugoslavia.
Je, hiyo ni kusema kwamba hakukuwa na vita na ukatili katika karne zilizopita? La hasha, hakika vilikuwapo. Lakini kule kukubali nadharia ya mageuzi, kule kuingiwa na mtazamo huu wa kwamba ni lazima kuwe na mng’ang’ano ili kuishi, maoni hayo ya halisalimika kwa wafaao zaidi, hayajatumika kuboresha njia ya maisha ya mwanadamu. Kwa hiyo, ingawa mageuzi hayawezi kulaumiwa kwa matatizo yote ya mwanadamu, hayo yamesaidia kusukuma familia ya kibinadamu ndani ya chuki, uhalifu, jeuri, ukosefu wa adili, na mdhoofiko mkubwa hata zaidi. Kwa kuwa yakubaliwa kwa mapana kwamba binadamu walitokana na hayawani, si ajabu kwamba watu wengi zaidi na zaidi wanatenda kama hayawani.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa hakika, Biblia haifunzi kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita halisi (saa 144). Kwa habari zaidi kuhusu kueleweka vibaya huku, ona Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?, kurasa 25-37, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
‘Kitabu cha Darwin chanitolea msingi wa kisayansi kwa ajili ya mng’ang’ano wa tabaka za kijamii katika historia.’ —Karl Marx
[Blabu katika ukurasa wa 6]
‘Jamii za tabaka la chini zitakuja kufyekwa na jamii za tabaka la juu zilizostaarabika.’—Charles Darwin
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Picha ya U.S. National Archives
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Haki zote za kunukuu zimehifadhiwa na British Museum