Chanzo cha Moyo Mkuu wa Daima
“SAUTI kama ya nyoka ilifanya tusimame ghafula. Kisha, kutoka katika kichaka kilichokuwa upande wetu wa kushoto, ndege wawili walikimbia kutuelekea mabawa yao yakiwa yamepanuliwa wazi. Mbele yetu kulikuwa na mayai mawili katika shimo dogo ardhini. Ndege hao walituzuia tusikanyage kiota chao bila kujua. Kila wakati tulipojaribu kusonga karibu zaidi ili kupiga picha ya mayai hayo maridadi yenye rangi ya maji ya kunde, ndege hao walirudia wonyesho wao wa kututisha. ‘Wana moyo mkuu kama nini,’ tukafikiri.”
Hilo lilikuwa ona la watu wazima wanne walipokaribia kiota cha ndege dikopu mwenye madoa-madoa. Ndege mwingine mdogo zaidi ni fundichuma. Katika kitabu Everyone’s Guide to South African Birds, wataalamu wa ndege Sinclair na Mendelsohn waeleza: “[Ndege] wawili wenye makinda hulinda kwa bidii kiota chao na makinda yao nao huwa wakali sana kwa kitu chochote kikaribiapo. Wao hawatishwi na ukubwa wa hao wavuka-njia nao huruka wakilia kwa sauti kali, wikirukia hata wanadamu bila kuogopa katika kujaribu kuwaonya.”
Watu fulani wameona ndovu wakubwa mmoja mmoja wakielekea kiota cha fundichuma bila kukusudia, kumbe waanzisha wonyesho wa ndege huyo. Mara nyingi ndovu hao hukubali kwa kubadili njia zao.
Ndege wanapata wapi moyo mkuu kama huo wa wazi? Huo watokana na Yule aliyewaumba. Yehova Mungu amewekea viumbe hivyo vidogo silika fulani ya kuzuia wanyama wakubwa wasidhuru viota vyao au makinda yao.
Somo kwa Wakristo
Wakristo waweza kujifunza somo kutokana na ono hili, hata ingawa wao wapaswa kufanya zaidi ya kuwa na moyo mkuu wa kisilika. Wao huombwa kuiga Bwana-Mkubwa wao, Yesu Kristo, aliyetii amri za Mungu bila hofu. (Waebrania 12:1-3) Biblia yashutumu waoga wanaojizuia wasimtumikie Mungu. (Waebrania 10:39; Ufunuo 21:8) Wakati uo huo, Yehova huelewa maumbile yetu ya kutokamilika naye ajua kwamba nyakati nyingine twaweza kutenda dhambi au kukosa moyo mkuu unaohitajiwa kufanya mapenzi yake kikamili. (Zaburi 103:12-14) Mtu aweza kufanya nini hofu imfanyapo asitende yaliyo sawa?
Ni lazima Mkristo amwendee Mungu kwa sala ili apate nguvu za kukabili majaribu na kuendelea kufanya mapenzi ya kimungu. Biblia ina ahadi hii inayotoa uhakikisho juu ya msaada wa Yehova: “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Haya vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.” (Isaya 40:29-31) Wanadamu wengi wasiokamilika wameona ukweli wa maneno hayo nao ‘wametiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu.’ (Waebrania 11:34) Kielelezo kizuri kilikuwa Mkristo mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote.”—2 Timotheo 4:17.
Hata watu wapya ambao wameanza kupendezwa wanaotaka kuwa wafuasi wa Yesu Kristo waweza kupata msaada kama huo wenye kuimarisha. Fikiria mtu mmoja wa Afrika Kusini aitwaye Henry, aliyekuwa mweka-hazina wa kanisa lao na aliyekuwa jirani wa pasta wake. Henry alikuwa akitafuta ile kweli. Ujapokuwa uhusiano wake na kanisa, siku moja alikubali kuwa na funzo la Biblia la nyumbani bila malipo pamoja na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda, alitaja kwamba alitaka kuwa Shahidi naye aliuliza hatua alizotakikana kuchukua ili kufikia mradi huo. Alielezwa kwamba kwanza ilikuwa ni lazima ajiuzulu kutoka kwa kanisa lake. (Ufunuo 18:4) Kwa kuwa yule pasta alikuwa jirani yake na rafiki yake, Henry alihisi kwamba hangeweza kuandika tu barua ya kujiuzulu bali alihitaji kueleza jambo hilo ana kwa ana. Naye alifanya hivyo kwa moyo mkuu.
Pasta huyo alishtuka sana na baadaye alichukua modereta na washiriki wengine wa kanisa kumtembelea Henry. Walitaka kujua sababu iliyomfanya aache kanisa lao awe mshiriki wa dini ambayo, kulingana nao, haina roho takatifu ya Mungu. “Mwanzoni, nilikuwa mwoga kuwajibu,” akaeleza Henry, “kwa sababu sikuzote walikuwa na uvutano mkubwa sana juu yangu. Lakini nilisali kwa Yehova kwa ajili ya msaada, naye aliniwezesha kujitetea hivi: ‘Kati ya dini zote za kimataifa, ni ipi pekee inayotumia jina la Mungu, Yehova? Je, si Mashahidi wa Yehova? Je, mwafikiri Mungu angewaruhusu watumie jina lake na asiwape pia roho yake takatifu?’” Maofisa hao wa kanisa walishindwa kukanusha kutoa sababu kwa njia hiyo. Akishukuru kwa ajili ya ujuzi na nguvu ambayo Mungu huandaa, Henry sasa ashiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa moyo mkuu katika huduma ya nyumba kwa nyumba.
Naam, kuwa Mkristo wa kweli kwahitaji moyo mkuu. Mwisho wa ulimwengu huu ukaribiapo, majaribu ya imani yataongezeka. Shetani anataka kuwanyang’anya watumishi wa Mungu tumaini lao ajabu la uhai wa milele kwa kujaribu kuvunja uaminifu wao wa maadili kwa Yehova. (Linganisha Ufunuo 2:10.) Lakini tusishindwe kamwe. Hata tukishindwa kidogo kwa sababu ya hofu, Yehova aweza kutusaidia kurudia hali yetu. Endelea kumtazamia akupe nguvu ya kuendelea kufanya mapenzi yake. Kumbuka, yeye aliyewaumba ndege hao wenye moyo mkuu ndiye Chanzo cha moyo mkuu wa daima. Kwa kweli, Wakristo wa kweli wapaswa “kuwa wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa. Mtu aweza kunifanya nini?’”—Waebrania 13:6, NW.