Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Neno la Mungu Lina Nguvu
“NENO la Mungu li hai, tena lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Maneno haya yamethibitibitika kuwa kweli mara nyingi sana wakati kweli za Biblia zifunuliwapo wazi kwa watu ambao wamedanganywa na dini bandia. Kama ionyeshwavyo na ono lifuatalo kutoka Jamhuri ya Dominika, nguvu za Biblia zaweza kubadili maisha ya watu na kuleta tumaini.
Mashahidi wa Yehova walimtembelea mwanamke mmoja Mkatoliki aliye mashuhuri aliyekuwa tu amefiwa na watoto wadogo wawili. Alishikwa na huzuni sana na kuombolezea msiba wake kila siku. Mashahidi walimwonyesha yale Biblia isemayo kwenye Yohana 5:28, 29 kuhusu tumaini la ufufuo. Baada ya mazungumzo zaidi pamoja na Mashahidi, hakupata faraja katika tumaini la ufufuo tu bali pia alitambua kwamba viongozi wake wa kidini Wakatoliki walikuwa wakimdanganya.
Alijiuzulu upesi kutoka Kanisa Katoliki, akakubali funzo la Biblia la kawaida pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, mume wake hakukubali maoni hayo. Kwa kuwa yeye pia alikuwa Mkatoliki mashuhuri sana, alipanga kwamba marafiki wa kisiasa na wa kidini waliojulikana sana wamtembelee mkeye kwa jitihada ya kumzuia asiendelee na mwendo wake na kumrudisha ndani ya Ukatoliki. Baadaye alitisha kumtaliki mkeye, wakati mmoja hata akijulisha watu wa ukoo wa mkeye na wanadini wenzake kwamba walikuwa wakitalikiana.
Lakini ujanja wake haukufaulu. Kinyume cha hilo, mkeye aliazimia hata zaidi kuendelea na mafunzo yake ya Biblia. Kwa sababu ya ukuzi wake wa kiroho na kusitawisha kwake sifa nzuri za Kikristo, mume aliamua kubaki naye badala ya kutafuta talaka. Siku moja hata alikubali kuchunguza fasihi ya Biblia ambayo mkeye alikuwa akijifunza—lakini kwa sharti fulani. Alitaka kutumia tafsiri yake mwenyewe ya Biblia ya Kikatoliki.
Kwa mshangao wake, alianza kujifunza mambo mapya moja kwa moja kutoka kwa Biblia yake mwenyewe kwa msaada wa fasihi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Alitambua kwamba mkeye alikuwa amechagua mwendo ufaao, na upesi akawa tayari kufuata kielelezo chake. Kwa kweli, aliona uhitaji wa kufanya mabadiliko maishani mwake mwenyewe. Pingamizi moja gumu lilikuwa kuacha tabia ya kuvuta sigareti. Baada ya kusoma toleo la gazeti Amkeni! la Machi 8, 1990, lenye kichwa cha jalada “Kifo Chauzwa—Njia Kumi za Kuacha Kuvuta Sigareti,” aliazimia kuacha tabia hii isiyo ya kimaandiko. Katika mahali pa kawaida pa kuweka paketi ya sigareti mfukoni mwake, alianza kuweka toleo hilo la Amkeni! Kila wakati alipokuwa na hamu ya kuvuta sigareti, alisoma makala hizo juu ya uvutaji wa sigareti. Njia hiyo ilifaulu! Baada ya kusoma makala hizo mara nyingi, aliweza kuacha kuvuta sigareti.
Leo wote wawili mume na mke wanamtumikia Yehova wakiwa wahudumu waliobatizwa. Hali zinaporuhusu, yeye hutumikia akiwa mhudumu wa wakati wote, akitumia wakati wake mwingi kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, naye hutumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova. Yeye na mkeye wanatazama mbele kwenye ufufuo wakati wawezapo kukaribisha watoto wao kwenye uhai tena katika ulimwengu mpya. Ndiyo, Neno la Mungu, Biblia li hai na lina nguvu!