Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 10/15 kur. 4-7
  • Ni Nini Hali ya Wafu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Hali ya Wafu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Binadamu Hakukusudiwa Afe
  • Ahadi Gani?
  • Mawasiliano Kutoka kwa Makao ya Roho
  • Yehova, Mungu wa Kweli na Upendo
  • Inakuwaje kwa Wapendwa Wetu Waliokufa?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Kuna Sababu ya Kuwaogopa Wafu?
    Amkeni!—2009
  • Uhai Baada ya Kifo—Jinsi Gani, Wapi, Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Je, Una Roho Isiyoweza Kufa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 10/15 kur. 4-7

Ni Nini Hali ya Wafu?

WOGA wa wafu husababishwa na jambo fulani—la kwamba mtu aliyekufa ana nafsi au roho ambayo huendelea kuishi baada ya kifo. Ikiwa Biblia hufundisha waziwazi kuwa wazo hili ni la uongo, basi swali la kama wafu waweza kukudhuru limejibiwa kabisa. Kwa hiyo basi, Biblia husema nini?

Kuhusu hali ya wafu, Neno la Mungu husema: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja; wala hawana sehemu tena katika jambo lo lote lililofanyika chini ya jua.”—Mhubiri 9:5, 6.

Kwa msingi huo, je, wafu waweza kukusaidia au kukudhuru? Maandiko hujibu la. Wafu hawana fahamu na wako katika hali ya unyamavu. Hawawezi kuwasiliana na walio hai wala kuonyesha hisia zozote—upendo au chuki—au kufanya tendo lolote. Hupaswi kuwa na woga wowote kwa ajili yao.

‘Ndiyo, hiyo yaweza kuwa kweli ikiwa warejezea kifo cha mwili halisi,’ wengine waweza kusema. ‘Lakini kifo halisi si mwisho wa uhai; hicho huifungua tu roho kutoka mwilini. Roho hiyo yaweza kusaidia au kudhuru walio hai.’ Mamilioni ya watu ulimwenguni pote huhisi hivyo.

Kwa mfano, katika Madagaska uhai huonwa kuwa kitu kinachogeuka tu, hivyo mazishi na kufukua mfu huonwa kuwa ya maana kuliko arusi. Inafikiriwa kwamba mtu alitoka kwa mababu wake waliokufa naye huwarudia anapokufa. Kwa sababu hiyo, nyumba za walio hai zimejengwa kwa mbao na matofali, vifaa viharibikavyo baada ya muda, lakini makaburi, “makao” ya wafu, kwa ujumla ni mazuri zaidi na yenye kudumu. Wakati wa kufukua mfu, watu wa familia na marafiki huhisi kuwa watabarikiwa, na wanawake huamini kuwa ikiwa watagusa mifupa ya mtu wa ukoo aliyekufa, watapata uwezo wa kuzaa. Lakini, tena, Neno la Mungu husemaje?

Binadamu Hakukusudiwa Afe

Ni jambo la kupendeza kufahamu kwamba Yehova Mungu aliumba mwanadamu aishi, na alitaja kifo kuwa tu matokeo ya kutotii. (Mwanzo 2:17) Kwa huzuni, mwanamume na mwanamke wa kwanza walifanya dhambi, na kama tokeo, dhambi ikaenea kwa binadamu wote ikiwa urithi wenye kuleta kifo. (Warumi 5:12) Hivyo ungeweza kusema kwamba kifo kimekuwa uhakika wa maisha tangu kutotii kwa binadamu wawili wa kwanza, ndiyo, uhakika wenye uchungu wa maisha. Tuliumbwa tuishi, jambo ambalo kwa upande mmoja hueleza kwa nini ni vigumu sana kwa mamilioni mengi ya watu kukubali kwamba kifo ni mwisho wa mambo.

Kulingana na maelezo ya Biblia, Shetani alijaribu kudanganya binadamu wawili wa kwanza kuhusu kifo kwa kupinga onyo la Mungu kwamba kutokutii kungeleta kifo. (Mwanzo 3:4) Hivyo, kwa kupita kwa wakati, ilikuja kuonekana waziwazi kwamba binadamu hufa kama vile Mungu alisema wangefanya. Hivyo, kwa karne nyingi Shetani aliitikia kwa uongo mwingine—kwamba sehemu fulani ya roho ya mwanadamu huokoka kifo cha mwili. Uongo kama huo wafaana na Shetani Ibilisi, ambaye Yesu alimtaja kama ‘baba wa uongo.’ (Yohana 8:44) Kwa upande mwingine, jibu la Mungu juu ya kifo ni ahadi inayotia moyo.

Ahadi Gani?

Ni ahadi ya ufufuo wa wengi. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ufufuo” ni a·naʹsta·sis. Lamaanisha “kuinuka tena” kihalisi nalo linarejezea kuinuka kutoka kwa wafu. Ndiyo, mwanadamu hulala chini katika kifo, lakini Mungu kwa uweza wake aweza kuinua mtu tena. Mwanadamu hupoteza uhai, lakini Mungu aweza kumpa uhai tena. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alisema kwamba “saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Mtume Paulo alieleza “tumaini [lake] kwa Mungu . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo, pia alitangaza tumaini lake katika ufufuo: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. Wewe [Mungu] ungeita, nami ningekujibu.”—Ayubu 14:14, 15.

Ahadi iliyo wazi ya ufufuo je, haionyeshi kuwa ni wazo la uongo kwamba wafu wako hai katika mwili wa kiroho? Ikiwa wafu wangekuwa hai na kufurahia kuishi mbinguni au katika ulimwengu fulani wa roho, kusudi la ufufuo lingekuwa nini? Je, hawangekuwa wamepokea thawabu au matokeo yao? Funzo la Neno la Mungu hufunua kwamba wafu hakika wamekufa, hawana fahamu, wamelala hadi uamsho mkuu wa ufufuo katika ulimwengu mpya—paradiso—iliyoahidiwa na Baba yetu mwenye upendo, Yehova. Lakini ikiwa kifo hakimaanishi kutenganisha mwili na roho na ikiwa roho haiendelei kuishi, vipi juu ya habari zionekanazo kama mawasiliano kutoka ulimwengu wa roho?

Mawasiliano Kutoka kwa Makao ya Roho

Habari nyingi sana za mawasiliano zionekanazo kuwa zimepokewa kutoka kwa makao ya roho zimeripotiwa. Chanzo chazo hasa ni nini? Biblia hutuonya sisi kwamba “Shetani mwenyewe hujifanya kuwa kama malaika wa nuru. Hivyo basi ni jambo rahisi kwa wajumbe wake kujifanya kuwa wajumbe wa mema.” (2 Wakorintho 11:14, 15, The New English Bible) Ndiyo, ili kudanganya na kupotosha watu kwa urahisi zaidi, mashetani (malaika waasi) wamewasiliana na walio hai, nyakati nyingine wakijifanya kuwa wenye kusaidia.

Mtume Paulo anatoa onyo zaidi kwa jitihada hiyo ya kueneza udanganyifu: “Wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani.” (1 Timotheo 4:1) Kwa hiyo itikio lolote linalodhaniwa latoka kwa mashetani ambao wanajifanya kuwa “wajumbe wa mema” na kueneza uongo wa kidini, hufunga watu katika utumwa wa ushirikina ambao huwapotosha kutoka kwa kweli ya Neno la Mungu.

Ikihakikisha kwamba wafu hawawezi kusema lolote, kufanya lolote, au kuhisi chochote, Zaburi 146:3, 4, New World Translation, hueleza: “Msiweke tumaini lenu kwa wakuu, wala kwa mwana wa binadamu, ambaye hana wokovu. Roho yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yamekwisha.” Ni roho gani hiyo ambayo “hutoka”? Ni kani ya uhai ya mtu ambayo hutegemezwa na kupumua. Hivyo basi, wakati aliyekufa aliacha kupumua, hisi zake ziliacha kufanya kazi. Aliingia katika hali ya kutofahamu lolote. Hivyo haiwezekani kwake kutawala walio hai.

Hiyo ndiyo sababu Biblia hulinganisha kifo cha binadamu na kile cha mnyama, ikieleza kwamba wote hufikia kukosa fahamu wakati wa kifo na kurudi katika ardhi ambayo waliumbwa nayo. Mhubiri 3:19, 20 husema: “Kwa maana linalowatukia wanadamu linawatukia wanyama; jambo moja lawatukia; anavyokufa huyu ndivyo anavyokufa huyu; naam, wote wanayo pumzi moja; wala mwanadamu hana kitu cha kumpita mnyama; kwa maana yote ni ubatili. Wote huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”

Akijua kwamba mashetani hujaribu kudanganya watu katika kufikiri kwamba wanaweza kuwasiliana na kuathiriwa na wafu, Yehova Mungu aliwaonya watu wake, Waisraeli wa kale: “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Kwa wazi, wazo la kwamba wafu wanaweza kutudhuru halitokani na Mungu. Yeye ni Mungu wa kweli. (Zaburi 31:5; Yohana 17:17) Na ana wakati ujao wa ajabu uliowekwa kwa ajili ya wapenda kweli wanaomwabudu “kwa roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.

Yehova, Mungu wa Kweli na Upendo

Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, “asiyeweza kusema uongo,” ametoa ahadi yake: Mamilioni na mamilioni waliokufa na kuwekwa ndani ya makaburi watafufuliwa wakiwa na tumaini la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu! (Tito 1:1, 2; Yohana 5:28) Ahadi hii ya upendo ya ufufuo huonyesha kwamba Yehova anapendezwa sana na hali njema ya viumbe vyake vya kibinadamu na tamaa ya moyoni ya kuondolea mbali kifo, kilio, na maumivu. Hivyo hakuna haja kuwaogopa wafu au kujihusisha isivyopasa kuwahusu na mataraja yao. (Isaya 25:8, 9; Ufunuo 21:3, 4) Mungu wetu mwenye upendo na haki, Yehova, anaweza na atawafufua, na kufungua uchungu wa kifo.

Neno la Mungu, Biblia, lajaa maelezo kuhusu jinsi hali ya dunia itakavyokuwa katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ulioahidiwa. (Zaburi 37:29; 2 Petro 3:13) Utakuwa wakati wa amani na furaha na upendo kwa watu wote. (Zaburi 72:7; Isaya 9:7; 11:6-9; Mika 4:3, 4) Wote watakuwa na makao yaliyo salama na mazuri, pamoja na kazi yenye kufurahisha. (Isaya 65:21-23) Kutakuwa na chakula kingi kizuri kwa wote. (Zaburi 67:6; 72:16) Wote watafurahia afya bora. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Ingawa mitume na wengine wachache watatawala mbinguni pamoja na Yesu, Biblia haitaji hali za baraka katika mbingu kwa ajili ya nafsi za wengine baada ya kifo. (Ufunuo 5:9, 10; 20:6) Hili lingekuwa gumu ikiwa mabilioni ya wale waliokufa huishi baada ya kufa.

Lakini si jambo gumu tunapojua mafundisho dhahiri ya Biblia: Wafu wameacha kuwapo wakiwa nafsi zinazoishi. Hawawezi kukudhuru. Wale walio katika makaburi ya kumbukumbu wanapumzika tu, bila fahamu hadi ufufuo wao wakati wa Mungu ufikapo. (Mhubiri 9:10; Yohana 11:11-14, 38-44) Basi, matumaini yetu na tamaa yetu, yategemea Mungu. “Na tushangilie na kuufurahia wokovu wake.”—Isaya 25:9.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kama ionyeshwavyo wazi na Neno la Mungu, wafu hawawezi kufanya lolote hadi wakati wa ufufuo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki