Uhai Baada ya Kifo—Jinsi Gani, Wapi, Lini?
MUUMBA na Mpaji-Uhai wa mwanadamu hutoa uhakikisho wake mwenyewe kwamba kifo cha kibinadamu si lazima kimalize uhai milele. Zaidi, Mungu hutuhakikishia kwamba haiwezekani tu kuishi tena tukiwa na urefu wa uhai wenye kikomo bali kuishi tukiwa na taraja la kutokabili kifo tena kamwe! Mtume Paulo alitaarifu hivi waziwazi, hata hivyo kwa uhakika: “Naye [Mungu] ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua [Kristo Yesu] kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:31, NW.
Bila shaka, hilo bado laacha maswali matatu ya msingi bila kujibiwa: Mtu aliyekufa aweza kurudije kwenye uhai? Hilo litatendeka lini? Ni wapi ambapo uhai mpya huo huja kuwako? Ulimwenguni kote, majibu yanayotofautiana yametolewa kwa maswali hayo, lakini ufunguo wa maana wa kuonyesha kweli ya jambo hilo ni kuelewa kwa usahihi linalowapata wanadamu wakati wa kifo chao.
Je, Hali ya Kutokufa Ndiyo Jibu?
Itikadi ambayo imeenea sana ni kwamba sehemu fulani ya wanadamu wote ina hali ya kutokufa na kwamba ni miili yao tu ndiyo hufa. Bila shaka umesikia dai hilo. Sehemu hiyo inayodaiwa kuwa na hali ya kutokufa hurejezewa kwa njia tofauti-tofauti kuwa “nafsi” au “roho.” Sehemu hiyo yasemekana husalimika kifo cha mwili na huendelea kuishi kwingineko. Kwa kweli, itikadi hiyo haikutokana na Biblia. Ni kweli kwamba, watu wa kale katika Biblia ya Kiebrania walitazamia uhai baada ya kifo, lakini si kwa kusalimika kwa sehemu fulani yao yenye hali ya kutokufa. Walitazamia kwa uhakika kurudi kwenye uhai duniani wakati ujao kupitia muujiza wa ufufuo.
Mzee wa ukoo Abrahamu ni kielelezo chenye kutokeza cha mtu aliyekuwa na imani katika ufufuo wa wafu wa wakati ujao. Likifafanua utayari wa Abrahamu wa kumtoa mwanawe Isaka katika dhabihu, Waebrania 11:17-19 hutuambia hivi: “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; . . . akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano,” kwa kuwa Mungu hakutaka kwamba Isaka atolewe akiwa dhabihu. Akishuhudia zaidi ile itikadi ya mapema miongoni mwa Waisraeli kwamba wangerudi kwenye uhai tena wakati fulani baadaye (badala ya kuendelea kwa uhai mara moja katika makao ya roho), nabii Hosea aliandika hivi: “Nitawakomboa na nguvu za kaburi; nitawaokoa na mauti.”—Hosea 13:14.
Kwa hiyo wazo la hali ya kutokufa kwa kibinadamu kiasili ilikuja kuingia katika kuwaza na itikadi za Kiyahudi lini? Kichapo Encyclopaedia Judaica chakiri kwamba “labda fundisho la hali ya kutokufa kwa nafsi liliingia katika Dini ya Kiyahudi chini ya uvutano wa Kigiriki.” Hata hivyo, Wayahudi wenye ujitoaji kufikia wakati wa Kristo bado waliamini na kutazamia ufufuo wa wakati ujao. Twaweza kuona hilo waziwazi kutokana na mazungumzo ya Yesu pamoja na Martha wakati wa kifo cha nduguye Lazaro: “Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. . . . Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”—Yohana 11:21-24.
Hali ya Wafu
Hapa tena, hakuna haja ya kukisia jambo hilo. Kweli sahili ya Biblia ni kwamba wafu “wamelala,” hawana fahamu, wasio na hisia wala ujuzi wowote. Kweli hiyo haitokezwi katika Biblia kwa njia tata, iliyo ngumu kufahamika. Fikiria maandiko haya yaliyo rahisi kuelewa: “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote . . . Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.” (Mhubiri 9:5, 10) “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:3, 4.
Yaeleweka basi, sababu iliyomfanya Yesu Kristo kurejezea kifo kuwa usingizi. Mtume Yohana arekodi mazungumzo kati ya Yesu na wanafunzi wake: “Akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha. Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.”—Yohana 11:11-14.
Mtu Kamili Hufa
Kifo cha mwanadamu huhusisha mtu kamili, wala si kifo cha mwili tu. Kulingana na taarifa zilizo wazi za Biblia, lazima tufikie mkataa kwamba mwanadamu hana nafsi yenye hali ya kutokufa iwezayo kusalimika kifo cha mwili wake. Maandiko huonyesha waziwazi kwamba nafsi yaweza kufa. “Tazama! nafsi zote—ni mali yangu mimi. Kama vile nafsi ya baba ndivyo ilivyo nafsi ya mwana—ni mali yangu mimi. Nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4, NW) Hakuna popote ambapo maneno “kutokufa” au “hali ya kutokufa” yanatajwa yakiwa asili ya wanadamu.
Kichapo New Catholic Encyclopedia chaandaa habari hii ya msingi yenye kupendeza juu ya maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa kuwa “nafsi” katika Biblia: “Nafsi katika AK [Agano la Kale] ni nepeš, katika AJ [Agano Jipya] [psy·kheʹ]. . . . Nepeš hutokana na mzizi wa neno la awali ambalo huenda wamaanisha kupumua, na hivyo . . . kwa kuwa pumzi hutofautisha wanaoishi na wafu, neno nepeš likaja kumaanisha uhai au mwenyewe au kwa usahili uhai wa mtu mmoja-mmoja. . . . Hakuna dikotomia [mgawanyiko katika sehemu mbili] ya mwili na nafsi katika AK. Mwisraeli aliona mambo kwa njia yenye kugusika, kwa ukamili wayo, na hivyo aliwaona wanadamu kuwa watu wala si walio na sehemu mbalimbali. Neno nepeš, ingawa latafsiriwa na neno letu nafsi, halimaanishi kamwe nafsi ikiwa tofauti na mwili au mtu mmoja-mmoja. . . . Neno [psy·kheʹ] ndilo neno la AJ linalolingana na nepeš. Laweza kumaanisha kanuni ya uhai, uhai wenyewe, au kiumbe hai.”
Hivyo waweza kuona kwamba wakati wa kifo, mtu aliyekuwa hai, au nafsi hai, hukoma kuwako. Mwili hurudi “mavumbini” au kwenye elementi za dunia, ama hatua kwa hatua kupitia maziko na kuoza kunakofuata ama haraka kupitia kuteketezwa kwa maiti. Yehova alimwambia Adamu: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Basi, uhai wawezekanaje baada ya kifo? Ni kwa sababu Mungu ana kumbukumbu lake mwenyewe la mtu aliyekufa. Yehova ana nguvu za kimuujiza na uwezo wa kuumba wanadamu, kwa hiyo haipaswi kushangaza kwamba yeye katika kumbukumbu lake aweza kuhifadhi rekodi ya kiolezo cha maisha cha mtu mmoja-mmoja. Ndiyo, mataraja yote ya kuishi tena humtegemea Mungu.
Hii ndiyo maana ya neno “roho,” inayozungumziwa kuwa inamrudia Mungu wa kweli aliyeitoa. Akifafanua matokeo hayo, mwandikaji aliyepuliziwa wa kitabu cha Mhubiri aeleza hivi: “Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.”—Mhubiri 12:7.
Mungu tu ndiye awezaye kumfanya mtu aishi. Mungu alipomuumba mwanadamu katika Edeni na kupuliza katika mianzi ya pua yake “pumzi ya uhai,” zaidi ya kujaza hewa katika mapafu ya Adamu, Yehova alifanya kani ya uhai ihuishe seli zote mwilini mwake. (Mwanzo 2:7) Kwa sababu kani hiyo ya uhai yaweza kupitishwa kutoka kwa wazazi hadi watoto kupitia utaratibu wa kuchukua mimba na kuzaa, uhai wa kibinadamu waweza kwa kufaa kusemwa kuwa watokana na Mungu ingawa, bila shaka, hupokewa kupitia wazazi.
Ufufuo—Wakati Wenye Furaha
Ufufuo wapaswa kutofautishwa na kuzaliwa upya katika umbo jingine, jambo ambalo halina utegemezo wowote katika Maandiko Matakatifu. Kuzaliwa upya katika umbo jingine ni itikadi ya kwamba baada ya mtu kufa, yeye huzaliwa tena katika kuwako kumoja au zaidi kwenye kufuatana. Hilo husemekana kutukia katika kiwango cha kuwako cha juu zaidi au chini zaidi kwa kulinganishwa na maisha ya mtu yaliyotangulia, ikitegemea rekodi ambayo yadhaniwa alijijengea katika maisha yake yaliyotangulia. Kulingana na itikadi hiyo mtu aweza “kuzaliwa upya” ama akiwa binadamu ama akiwa mnyama. Hilo lahitilafiana kwelikweli na yale ambayo Biblia hufundisha.
Neno “ufufuo” limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki a·naʹsta·sis, ambalo kihalisi humaanisha “kusimama tena.” (Waebrania wanaotafsiri Kigiriki wametumia neno a·naʹsta·sis pamoja na maneno ya Kiebrania techi·yathʹ ham·me·thimʹ, wakimaanisha “kuhuishwa kwa wafu.”) Ufufuo huhusisha kutendeshwa upya kwa tabia, matendo, mielekeo, na mambo mengineyo ambayo Mungu ameweka katika kumbukumbu lake. Kulingana na mapenzi ya Mungu kwa mtu mmoja-mmoja, mtu arudishwa ama katika mwili wa kibinadamu ama katika mwili wa kiroho; na bado adumisha utambulisho wake wa kibinafsi, akiwa na utu uleule na makumbukumbu yaleyale aliyokuwa nayo alipokufa.
Ndiyo, Biblia husema juu ya aina mbili za ufufuo. Mmoja ni ufufuo wa kwenda mbinguni katika mwili wa roho; huo ni wa watu wachache kwa kulinganishwa. Yesu Kristo alipokea ufufuo huo. (1 Petro 3:18) Naye alionyesha kwamba hilo lingewapata wale walioteuliwa miongoni mwa wafuasi wa nyayo zake, kuanzia na mitume waaminifu, ambao aliwapa ahadi hii: “Naenda kuwaandalia mahali. . . . nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.” (Yohana 14:2, 3) Biblia hurejezea huo kuwa “ufufuo wa kwanza,” wa kwanza katika wakati na cheo. Maandiko hufafanua wale wanaofufuliwa hivyo kwenye uhai wa kimbingu kuwa makuhani wa Mungu na wakitawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 20:6) “Ufufuo [huo] wa kwanza” ni wa idadi yenye kikomo, na Maandiko yenyewe hufunua kwamba ni 144,000 tu watakaochukuliwa kutoka miongoni mwa wanaume na wanawake waaminifu. Watakuwa wamethibitisha uaminifu-maadili wao kwa Yehova Mungu na Kristo Yesu kufikia kifo chao, wakiwa wamekuwa watendaji katika kutolea wengine ushahidi juu ya imani yao.—Ufunuo 14:1, 3, 4.
Bila shaka, ufufuo wa wafu ni wakati wa furaha isiyo na mipaka kwa wale watakaofufuliwa kwenye uhai mbinguni. Lakini furaha haiishii hapo, kwa kuwa ufufuo kwenye uhai papa hapa duniani umeahidiwa pia. Watakaofufuliwa watajiunga na idadi isiyo na mpaka ya watakaosalimika mwisho wa mfumo mwovu uliopo. Baada ya kuona ile idadi ndogo ya watu inayostahili ufufuo wa kimbingu, mtume Yohana alipewa ono la “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Huo utakuwa wakati wa furaha kama nini mamilioni, labda hata mabilioni, ya watu watakaporudi kwenye uhai hapa duniani!—Ufunuo 7:9, 16, 17.
Itakuwa Lini?
Shangwe na furaha yoyote ingekuwa ya muda mfupi ikiwa watu wangerudi kwenye dunia iliyojawa na zogo, umwagikaji wa damu, uchafuzi, na jeuri—jinsi hali ilivyo leo. La, ufufuo lazima ungojee kuundwa kwa “dunia mpya.” Ebu wazia, sayari iliyosafishwa isiwe na watu na mashirika ambayo kufikia sasa yaonekana yameazimia kuiharibu dunia na kuharibu uzuri wayo wa awali, zaidi ya ile huzuni nyingi ambayo yameletea wakazi wayo.—2 Petro 3:13; Ufunuo 11:18, linganisha NW.
Kwa wazi, wakati wa ufufuo wa ujumla wa wanadamu ungali mbele. Hata hivyo habari njema ni kwamba hauko mbali sana. Ni kweli kwamba, lazima ungojee mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo wa sasa. Hata hivyo, uthibitisho mwingi huthibitisha kwamba wakati wa mwanzo wa ghafla wa “dhiki kubwa” u karibu, ukifikia upeo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi”—irejezewayo kwa ukawaida kuwa Har–Magedoni. (Mathayo 24:3-14, 21; Ufunuo 16:14, 16, linganisha NW.) Hilo litatokeza kuondolewa kwa uovu wote kutoka kwenye sayari hii yenye kupendeza, Dunia. Kufuatia hilo Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu utakuja, dunia itakapoletwa katika hali ya paradiso hatua kwa hatua.
Biblia hufunua kwamba wakati wa utawala huo wa Mileani, ufufuo wa binadamu wafu utatukia. Ndipo itakapotimia ahadi ya Yesu aliyotoa alipokuwa duniani: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; . . . kwa ufufuo.”—Yohana 5:28, 29.
Tokeo la Tumaini la Ufufuo
Taraja hili la ufufuo ni tumaini la wakati ujao la ajabu kama nini—wakati ambapo wafu watarudi kwenye uhai tena! Jinsi linavyotutia moyo tukabilipo ugumu wa umri unaoongezeka, ugonjwa, misiba isiyotazamiwa na huzuni, na mikazo tu ya kila siku na matatizo ya maisha! Huondoa umo la kifo—hauondoi huzuni kabisa bali hututenga na wale ambao hawana tumaini la wakati ujao. Mtume Paulo alikiri tokeo hilo lenye kufariji la tumaini la ufufuo kwa maneno haya: “Ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye.”—1 Wathesalonike 4:13, 14.
Huenda ikawa kwamba tayari tumejionea kweli ya jambo jingine lililoonwa na yule mtu wa Mashariki Ayubu: “Mwanadamu huharibika kama kitu kilichooza, kama vazi lililoliwa na nondo. Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke ni wa siku chache na zenye kujaa taabu. Huchanuka kama ua na kunyauka; kama kivuli chenye kupita haraka, yeye hadumu.” (Ayubu 13:28–14:2, New International Version) Sisi pia, twajua juu ya ukosefu wa uhakika wa maisha na uhalisi usiopendeza wa kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” laweza kumpata yeyote miongoni mwetu. (Mhubiri 9:11, NW) Kwa hakika, hakuna yeyote miongoni mwetu anayefurahia lile wazo la kukabili hatua ya kufa. Bado, tumaini hakika la ufufuo kwa kweli husaidia kuondoa hofu yenye kulemea ya kifo.
Basi, uwe na moyo mkuu! Tazama mbali zaidi ya usingizi uwezekanao katika kifo kwenye kurudia uhai tena kupitia muujiza wa ufufuo. Tazama mbele kwa uhakika kwenye taraja la uhai wa wakati ujao usiokoma, na uongezee hilo shangwe ya kujua kwamba wakati huo wenye baraka u katika wakati ujao ulio karibu.