Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 11/15 kur. 4-7
  • Wafu Wako Wapi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wafu Wako Wapi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nani Wanaoenda Mbinguni?
  • Wale Wasioenda Mbinguni
  • Kulala Katika Kifo
  • Maisha Mapya kwa Wazazi Wetu wa Kale Waliokufa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Ni Nani Wanaoenda Mbinguni, na kwa Sababu Gani?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Inakuwaje kwa Wapendwa Wetu Waliokufa?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Je! Watu Wote Wema Wanakwenda Mbinguni? . . .
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 11/15 kur. 4-7

Wafu Wako Wapi?

“DUNIA ni soko; mbinguni ndio kwetu,” wasema Wayoruba wa Afrika Magharibi. Wazo hili husemwa katika dini nyingi. Linatoa wazo la kwamba dunia ni kama soko tunalotembelea kwa muda mfupi halafu tunaondoka. Kulingana na imani hii, tunapokufa tunaenda mbinguni, makao yetu ya kweli.

Biblia hufundisha kwamba wachache huenda mbinguni. Yesu Kristo aliwaambia mitume wake waaminifu: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi. . . . naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.”—Yohana 14:2, 3.

Maneno ya Yesu hayamaanishi ya kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni au kwamba mbingu ni makao ya binadamu. Wengine wanapelekwa mbinguni kwa ajili ya kuitawala dunia. Yehova Mungu alijua kwamba serikali za wanadamu hazingefaulu kamwe kusimamia mambo katika dunia. Kwa hiyo, alifanya mpango kwa ajili ya serikali ya kimbingu, au Ufalme, ambao mwishowe ungechukua mamlaka ya dunia na kuigeuza kuwa Paradiso aliyoikusudia tangu mwanzo. (Mathayo 6:9, 10) Yesu angekuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Danieli 7:13, 14) Wengine wangechaguliwa kutoka kwa wanadamu wakatawale pamoja naye. Biblia ilitabiri kwamba wale wanaoenda mbinguni wangekuwa “ufalme na makuhani kwa Mungu wetu” nao “wangetawala wakiwa wafalme juu ya dunia.”—Ufunuo 5:10, New Word Translation.

Nani Wanaoenda Mbinguni?

Tukifikiria daraka kubwa sana ambalo hawa watawala wa kimbingu wangekuwa nalo, si ajabu kwamba wangelazimika kufikia matakwa makali. Ni lazima wale wanaoenda mbinguni wapate ujuzi sahihi wa Yehova na lazima wamtii. (Yohana 17:3; Warumi 6:17, 18) Wanatazamiwa wajizoeze imani katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Na bado, mengi yanahusika. Lazima waitwe na kuchaguliwa na Mungu kupitia Mwanaye. (2 Timotheo 1:9, 10; 1 Petro 2:9) Zaidi ya hayo, lazima wawe Wakristo waliobatizwa ambao ‘wamezaliwa mara ya pili,’ wakafanywa kuwa wana kwa roho takatifu ya Mungu. (Yohana 1:12, 13; 3:3-6) Wao wanapaswa pia kudumisha uaminifu wa kimaadili kwa Mungu hadi kifo.—2 Timotheo 2:11-13; Ufunuo 2:10.

Mamilioni mengi ya watu walioishi na kufa hawakufikia matakwa haya. Wengi hawajapata fursa ya kujifunza juu ya Mungu wa kweli. Wengine hawajapata kamwe kusoma Biblia na wanajua kidogo tu au hawajui lolote kuhusu Yesu Kristo. Hata miongoni mwa Wakristo wa kweli duniani leo, ni wachache wamechaguliwa na Mungu kwa ajili ya uhai wa kimbingu.

Kwa sababu hiyo, idadi ya wale wanaoenda mbinguni ingekuwa ndogo kwa ulinganifu. Yesu aliwarejezea hao kuwa “kundi dogo.” (Luka 12:32) Baadaye, ilifunuliwa kwa mtume Yohana kwamba wale “walionunuliwa katika nchi” wakatawale pamoja na Kristo mbinguni wangekuwa 144,000 tu. (Ufunuo 14:1, 3; 20:6) Wanapolinganishwa na mabilioni ya watu waliowahi kuishi duniani, hiyo ni hesabu ndogo kwelikweli.

Wale Wasioenda Mbinguni

Ni nini linalotokea kwa wale wasioenda mbinguni? Je, wanateseka katika mahali pa mateso ya milele, kama vile dini fulani hufundisha? Bila shaka sivyo, kwa maana Yehova ni Mungu wa upendo. Wazazi wenye upendo hawatupi watoto wao ndani ya moto, na Yehova hawatesi watu kwa njia kama hiyo.—1 Yohana 4:8.

Taraja la walio wengi sana kati ya wale waliokufa ni ufufuo katika paradiso ya kidunia. Biblia husema kwamba Yehova aliiumba dunia “ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mtunga-zaburi alitangaza: “Mbingu ni mbingu za BWANA, bali nchi amewapa wanadamu.” (Zaburi 115:16) Ni dunia, si mbingu, itakayokuwa makao ya kudumu ya wanadamu.

Yesu alitabiri: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake [ya Yesu, “Mwana wa Adamu”]. Nao watatoka.” (Yohana 5:27-29) Mtume Mkristo Paulo alithibitisha: “Nina tumaini kwa Mungu . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Kwenye mti wa mateso, Yesu alimwahidi mtenda dhambi mwenye kutubu uhai kupitia kwa ufufuo katika paradiso ya kidunia.—Luka 23:43.

Lakini, wafu watakaofufuliwa wapate uhai duniani wako katika hali gani? Tukio katika huduma ya Yesu latusaidia kujibu swali hili. Rafiki yake Lazaro alikuwa amekufa. Kabla Yesu hajaenda kumfufua, Yeye aliwaambia wanafunzi Wake: “Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha.” (Yohana 11:11) Hivyo Yesu alifananisha kifo na usingizi, usingizi mzito bila ndoto.

Kulala Katika Kifo

Maandiko mengine hukubaliana na wazo hili la kulala katika kifo. Hayafundishi kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa inayopita na kwenda kwenye ulimwengu wa roho wakati wa kufa. Badala ya hivyo, Biblia husema: “Wafu hawajui neno lolote . . . Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi] uendako wewe.” (Mhubiri 9:5, 6, 10) Zaidi ya hayo, mtunga-zaburi alisema kwamba mtu “huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.

Maandiko haya hufunua kwamba wale wanaolala katika kifo hawawezi kutuona au kutusikia. Hawana uwezo wa kuleta wala baraka wala msiba. Hawako mbinguni, wala hawakai katika jamii ya mababu waliokufa. Hawana uhai, hawaishi.

Wakati wa Mungu ufikapo, wale sasa wamelala katika kifo na walio katika kumbukumbu lake wataamshwa kwenye uhai katika dunia paradiso. Itakuwa dunia iliyoondolewa uchafu wa hewa, matatizo, na shida ambazo wanadamu wanakabili sasa. Utakuwa wakati wa kufurahisha kama nini! Katika Paradiso hiyo watakuwa na taraja la kuishi milele, maana Zaburi 37:29 hutuhakikishia: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”

[Sanduku katika ukurasa wa 6, 7]

NILIACHA KUABUDU WAFU

“Nilipokuwa mvulana, nilikuwa nikimsaidia baba yangu wakati wa dhabihu zake za kawaida kwa baba yake aliyekufa. Pindi moja wakati baba yangu alipopata nafuu kutokana na ugonjwa mbaya sana, mwasiliani-roho alimwambia kwamba kwa kuonyesha uthamini wa kupona kwake apaswa kutoa dhabihu ya mbuzi, viazi vikuu, njugu za kola, na kileo kwa baba yake mfu. Baba yangu alishauriwa pia kuwasihi mababu wake waliokufa kuzuia magonjwa mengine na msiba.

“Mama yangu alinunua kilichohitajiwa kwa ajili ya dhabihu, ambayo ingefanywa kwenye kaburi la babu yangu. Kaburi lilikuwa kando tu ya nyumba yetu, kulingana na desturi za kwetu.

“Marafiki, watu wa ukoo, na majirani walialikwa kuona dhabihu ikitolewa. Baba yangu, aliyevalia vizuri sana kwa ajili ya pindi hiyo, akaketi kwenye kiti kuelekeana na madhabahu ambapo mafuvu ya mbuzi yaliyotumiwa wakati wa dhabihu za mbeleni yalikuwa yamepangwa kwa mstari. Kazi yangu ilikuwa kumwaga divai kutoka kwenye chupa ndani ya bilauri, niliyompa baba yangu. Naye aliimwaga chini kama dhabihu. Baba yangu akaliita jina la baba yake mara tatu na kumwomba amwokoe kutokana na msiba wakati ujao.

“Njugu za kola zilitolewa, na kondoo-dume alichinjwa, akachemshwa, na kuliwa na wote waliokuwapo. Nilishiriki kula na kucheza dansi kwa nyimbo na ngoma. Baba yangu alicheza dansi vizuri sana na kwa nguvu, ijapokuwa alikuwa mzee. Pindi kwa pindi aliwaomba mababu wake waliokufa kubariki wale wote waliokuwapo, huku watu, kutia ndani mimi, tukijibu Ise, kumaanisha ‘Na iwe hivyo.’ Nilimtazama baba yangu kwa kupendezwa na kuvutiwa sana na kutamani siku ambayo ningekuwa na umri wa kutosha kutoa dhabihu kwa mababu waliokufa.

“Dhabihu zile nyingi zijapotolewa, bado amani haikupatikana katika familia. Ingawa kulikuwa na wana watatu waliokuwa hai wa mama yangu, hakuna binti kati ya wale watatu aliozaa aliyeishi kwa muda mrefu; wote walikufa wakiwa watoto. Mama yangu alipopata mimba tena, baba yangu alitoa dhabihu sana ili mtoto azaliwe kwa usalama.

“Mama akazaa msichana mwingine. Miaka miwili baadaye mtoto akawa mgonjwa na kufa. Baba yangu akamwendea yule mwasiliani-roho, aliyesema kwamba adui alihusika kwa kifo hicho. Mwasiliani-roho akasema kwamba ili ‘nafsi’ ya mtoto ipigane, kipande cha mti wenye moto, chupa ya kileo, na mbwa mchanga walihitajiwa kwa ajili ya dhabihu. Mti wenye moto ulikuwa uwekwe kwenye kaburi, kileo kilikuwa kimiminwe kwenye kaburi, na mbwa mchanga alikuwa azikwe akiwa hai karibu na kaburi. Hii ilipaswa kuamsha nafsi ya msichana aliyekufa kulipiza kisasi kifo chake.

“Nilipeleka chupa ya kileo na mti wenye kuwaka moto kwenye kaburi, na baba yangu akabeba mtoto wa mbwa, aliyemzika kulingana na maagizo ya mwasiliani-roho. Sisi sote tuliamini kwamba katika siku saba nafsi ya msichana aliyekufa ingeharibu mtu aliyesababisha kifo chake cha mapema. Miezi miwili ikapita, na hakuna kifo kilichoripotiwa katika ujirani. Nikavunjika moyo.

“Nilikuwa na umri wa miaka 18 wakati huo. Muda mfupi baadaye nilikutana na Mashahidi wa Yehova, walionionyesha kutoka katika Maandiko kwamba wafu hawawezi kufanya chochote kizuri wala kibaya kwa walio hai. Ujuzi wa Neno la Mungu ulipoendelea kupata mizizi katika moyo wangu, nilimwambia baba yangu singeweza tena kuandamana naye kutoa dhabihu kwa wafu. Mwanzoni alinighadhabikia kwa kumwacha, kama alivyosema. Lakini alipoona kwamba sikuwa nataka kuikana imani yangu mpya, hakupinga ibada yangu kwa Yehova.

“Katika Aprili 18, 1948, nilionyesha wakfu wangu kwa ubatizo wa maji. Tangu wakati huo, nimeendelea kumtumikia Yehova kwa furaha nyingi na kwa uradhi, nikiwasaidia wengine kuacha ibada ya mababu waliokufa, ambao hawawezi kutusaidia wala kutudhuru.”—Imechangwa na J. B. Omiegbe, Benin City, Nigeria.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kutakuwa furaha kubwa sana wafu watakapofufuliwa katika paradiso duniani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki