Kumkana Mungu Katika Karne ya 20
“Watu wamekubali wazo la kutokuwapo kwa Mungu na wanapanga maisha zao kivyao, kwa wema au kwa ubaya, na bila kumfikiria Mungu hata kidogo.” —One Hundred Years of Debate Over God—The Sources of Modern Atheism.
INGAWA mara ya kwanza ni wenye kuvutia, baadaye mti mrefu huonwa kuwa kitu cha kawaida. Kuwapo kwao ni kwa kawaida; urefu wake si wenye kicho tena.
Ndivyo ilivyo na kukataa kuwapo kwa Mungu. Ingawa kulitokeza mijadala mingi katika karne ya 19, kukana kuwapo kwa Mungu siku hizi hakushangazi wala kusumbua. Enzi ya kuachilia mambo imeruhusu wazo la kukataa kuwapo kwa Mungu likubalike kwa amani pamoja na imani katika Mungu.
Si kwamba watu wengi hukana Mungu waziwazi; kinyume na hilo, matokeo ya uchunguzi kutoka nchi 11 kotekote Amerika, Ulaya, na Asia yafunua kwamba, kwa wastani, idadi ipitayo kidogo asilimia 2 wadai kuwa hawaamini kuwapo kwa Mungu. Hata hivyo, roho ya kukataa kuwapo kwa Mungu imeenea—hata miongoni mwa wengi wanaoamini kwamba Mungu yupo. Hili lawezekanaje?
Kukana Mamlaka ya Mungu
“Nyakati fulani kukataa kuwapo kwa Mungu hurejezea tu kumkataa Mungu au kumpuuza kwa matendo,” chasema The Encyclopedia Americana. Kwa sababu hii, The New Shorter Oxford English Dictionary hutoa ufafanuzi wa pili ufuatao wa “mtu anayekataa kuwapo kwa Mungu”: “Mtu ambaye humkana Mungu kiadili; mtu asiye wa Mungu.”—Italiki ni zetu.
Ndiyo, kukataa kuwapo kwa Mungu kwaweza kumaanisha kukana kuwapo kwa Mungu au mamlaka yake au zote mbili. Biblia hutaja roho hii ya kukataa kuwapo kwa Mungu katika Tito 1:16: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana.”—Linganisha Zaburi 14:1.
Kukataa mamlaka ya Mungu kama huko kwaweza kufuatiwa nyuma hadi wakati wa watu wawili wa kwanza. Hawa alitambua kuwapo kwa Mungu; hata hivyo alitaka ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ Maana yake ilikuwa kwamba angekuwa ‘mwenye kujiamulia mambo’ na kutengeneza kanuni zake mwenyewe za maadili. Baadaye Adamu aliungana na Hawa katika kukana mamlaka ya Mungu.—Mwanzo 3:5, 6.
Je, mtazamo huo umeenea leo? Ndiyo. Kukataa kuwapo kwa Mungu kwa ujanja kunaonyeshwa katika utafutaji wa uhuru. “Watu leo wamechoka kuishi wakitazamwa na Mungu,” chasema kitabu One Hundred Years of Debate Over God—The Sources of Modern Atheism. “Wanapendelea . . . kuishi katika uhuru.” Kanuni za maadili za Biblia zinakataliwa kuwa hazifai na si halisi. Wengi huwaza kama Farao wa Misri ambaye kwa ukaidi alitangaza: “BWANA ni nani, hata niisikilize sauti yake . . . ? Mimi simjui BWANA.” Alikataa mamlaka ya Yehova.—Kutoka 5:2.
Kumkana Mungu kwa Jumuiya ya Wakristo
Kukana mamlaka ya Mungu kwenye kushtua sana hutokana na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, ambao wamebadili desturi za wanadamu kwa kweli safi za Biblia. (Linganisha Mathayo 15:9.) Kwa kuongezea, wamechangia vita zenye umwagaji mkubwa zaidi wa damu za karne ya 20, hivyo wakikataa amri ya Biblia ya kuonyesha upendo wa kweli.—Yohana 13:35.
Makasisi pia wamemkana Mungu kwa kugeuzia visogo vyao kanuni za maadili—kwa mfano, kama ionyeshavyo, na kesi nyingi sana dhidi ya makuhani wanaofanya ngono na watoto. Hali ya Jumuiya ya Wakristo yafanana na ile ya Israeli na Yuda ya kale. “Nchi imejaa damu nao mji umejaa kupotosha hukumu,” nabii Ezekieli aliambiwa, “maana husema, BWANA ameiacha nchi hii, naye BWANA haoni.” (Ezekieli 9:9; linganisha Isaya 29:15.) Si ajabu kwamba wengi wameacha kabisa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo! Lakini, je, ni lazima waache imani katika Mungu?
Je, Ni Sababu Zifaazo za Kukataa Kuwapo kwa Mungu?
Ikiwa wameona unafiki wa dini au sivyo, wengi wa wasioamini kuwapo kwa Mungu hawawezi kupatanisha imani katika Mungu na kule kuteseka kuliopo katika ulimwengu. Pindi moja Simone de Beauvoir alisema hivi: “Ilikuwa rahisi kwangu kufikiri juu ya ulimwengu usio na muumba kuliko muumba aliyejazwa mambo yote yenye kupingana ya ulimwengu.”
Je, mambo yasiyo ya haki ya ulimwengu—kutia ndani yale yaliyochochewa na wanadini wanafiki—yanathibitisha kwamba hakuna Mungu? Fikiria: Kisu kikitumiwa kwa kutisha, kudhuru, au hata kuua kimakusudi mtu asiye na hatia, je, hili lamaanisha kwamba kisu hakikuwa na mbuni? Je, badala yake haionyeshi kwamba kitu hicho kilitumiwa vibaya? Sawa na hilo, huzuni nyingi ya wanadamu huthibitisha kwamba wanadamu wanatumia vibaya uwezo wao waliopewa na Mungu na dunia vilevile.
Hata hivyo, wengine huhisi kwamba si jambo la akili kumwamini Mungu, maana hatuwezi kumwona. Lakini vipi hewa, mawimbi ya sauti, na harufu? Hatuwezi kuona vyovyote vya vitu hivi, hata hivyo tunajua kwamba vipo. Mapafu yetu, masikio, na mapua hutuambia hivyo. Kwa kweli tunaamini katika yale yasiyoweza kuonekana ikiwa tuna uthibitisho.
Baada ya kufikiria uthibitisho halisi—kutia ndani elektroni, protoni, atomu, amino-asidi, na ubongo ulio mgumu kuufahamu—mwanasayansi wa mambo ya asili Irving William Knobloch alisukumwa kusema: “Naamini katika Mungu kwa sababu kwangu kuwapo Kwake Kimungu ndiko njia pekee ya akili ya kueleza jinsi vitu vilivyo.” (Linganisha Zaburi 104:24.) Vilevile, mwanafisiolojia Marlin Books Kreider asema: “Nikiwa wa kawaida, na pia nikiwa mtu aliyetoa maisha yake kwa masomo ya kisayansi na uchunguzi, sina shaka lolote juu ya kuwapo kwa Mungu.”
Watu hao hawako peke yao. Kulingana na profesa wa fizikia Henry Margenau, “ukiwachukua wanasayansi mashuhuri, utapata wachache sana miongoni mwao wasioamini kuwapo kwa Mungu.” Wala maendeleo ya sayansi wala kushindwa kwa dini hakupaswi kutufanya tuache kumwamini Muumba. Acha tuchunguze sababu.
Tofauti ya Dini ya Kweli
Katika 1803, rais wa Marekani Thomas Jefferson aliandika hivi: “Ufisadi wa Ukristo, mimi naupinga kwelikweli; bali si mafundisho manyoofu ya Yesu mwenyewe.” Ndiyo, kuna tofauti kati ya Jumuiya ya Wakristo na Ukristo. Mengi ya mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo yanatokana na mapokeo ya wanadamu. Tofauti na hilo, Ukristo wa kweli hutegemea itikadi zao katika Biblia. Hivyo, Paulo aliwaandikia Wakolosai wa karne ya kwanza kwamba wanapaswa kujipatia “maarifa,” “hekima,” na “ufahamu wa rohoni.”—Wakolosai 1:9, 10.
Haya ndiyo tunapaswa kutazamia kutoka kwa Wakristo wa kweli, maana Yesu aliwaamuru wafuasi wake hivi: ‘Mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.’—Mathayo 28:19, 20, italiki ni zetu.
Leo, Mashahidi wa Yehova wanatii amri hii katika nchi 231 ulimwenguni pote. Wameitafsiri Biblia katika lugha 12 na kuchapisha zaidi ya nakala 74,000,000. Zaidi ya hayo, kwa njia ya programu ya funzo la Biblia nyumbani, kwa sasa wanasaidia zaidi ya watu 4,500,000 ‘kuyashika yote aliyoamuru Yesu.’
Programu hii ya elimu ina matokeo ya kutazamisha sana. Inaleta uelewevu wa kweli, maana haitegemei msingi wa mawazo ya mwanadamu, bali inategemea hekima ya Mungu. (Mithali 4:18) Zaidi ya hayo, inasaidia watu kutoka kwa mataifa na rangi zote kufanya jambo ambalo “Enzi ya Kuerevuka” kwa mwanadamu hakungeweza kutimiza kamwe—‘kuvaa utu mpya’ unaowasaidia kusitawisha upendo wa kweli kwa mmoja na mwenzake.—Wakolosai 3:9, 10.
Dini ya kweli inasitawi katika karne yetu ya 20. Haimkani Mungu—wala kuwapo kwake wala mamlaka yake. Tunakukaribisha ujionee mambo haya wewe mwenyewe kwa kuwatembelea Mashahidi wa Yehova katika moja ya Majumba ya Ufalme yao.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
KUIMARISHA MIZIZI YA KUKATAA KUWAPO KWA MUNGU
Katikati ya karne ya 18, mwanafalsafa Denis Diderot aliamriwa kutafsiri buku moja la ensaiklopedia kutoka lugha ya Kiingereza hadi Kifaransa. Hata hivyo, alitimiza matazamio ya mwajiri wake kwa mbali sana. Diderot alitumia karibu miongo mitatu akikusanya Encyclopédie yake, mabuku-28 yaliyoonyesha kabisa mtazamo wa enzi hiyo.
Ingawa Encyclopédie hiyo ilikuwa na habari zenye mafaa sana, ilikazia hekima ya mwanadamu. Kulingana na seti ya vitabu Great Ages of Man, “ilijasiria kuhubiri mawazo [ya wanafalsafa] ya kwamba mwanadamu angeweza kuboresha hali yake kama angeacha kuamini na kutumia kusababu kuwa kanuni ya kumwongoza.” Haikutaja Mungu. “Katika mazungumzo yao,” chasema kitabu The Modern Heritage, “wahariri walihakikisha kwamba dini haikuwa moja ya vitu ambavyo watu walihitaji kujua.” Bila shaka kanisa lilijaribu kuikandamiza ile Encyclopédie. Mkuu wa sheria aliilaumu kuwa yenye uzushi wa siasa, maadili na dini.
Ijapokuwa maadui yacho, Encyclopédie ya Diderot iliagizwa na watu karibu 4,000—idadi ya kushangaza sana, ukifikiria bei yayo ghali sana. Ni muda mfupi tu ulibaki kabla ya kukataa kuwapo kwa Mungu kulikokuwa kudogo kusitawi kuwe kumkana Mungu waziwazi.