Mizizi ya Kukataa Kuwapo kwa Mungu
TUNAISHI katika sayari iliyojaa mchafuko; kutazama kwa ufupi tu habari kuu magazetini kwathibitisha jambo hilo kila siku. Hali yenye kukatisha tamaa ya ulimwengu wetu imefanya wengi watilie shaka kuwapo kwa Mungu. Wengine, wakidai kuwa wasioamini kuwapo kwa Mungu, hata kukana kuwapo kwake. Ndivyo ilivyo kwako?
Kuamini au kutoamini katika Mungu kwaweza kuathiri sana mtazamo wako juu ya wakati ujao. Bila Mungu, kuokolewa kwa jamii ya wanadamu kunabaki kabisa-kabisa mikononi mwa mwanadamu—ni wazo lisilopendeza kufikiria uwezo wa mwanadamu wa kusababisha uharibifu. Ikiwa waamini kwamba Mungu yupo, basi yaelekea wakubali kwamba uhai katika sayari hii una kusudi—kusudi ambalo litakuja kutimizwa.
Ingawa kukana kuwapo kwa Mungu ni jambo ambalo limetokea mara moja moja katika historia, ni katika karne za karibuni tu kwamba kukataa kuwapo kwa Mungu kumeenea. Je, wajua sababu ni nini?
Kuitambua Mizizi
Mti mrefu ni wenye kuvutia. Hata hivyo, macho huona majani, matawi, na kisiki tu. Mizizi—chanzo cha uhai wa mti—imefichwa chini sana ardhini.
Ndivyo ilivyo na kukataa kuwapo kwa Mungu. Kama vile mti mrefu sana, kukana kuwapo kwa Mungu kulienea kwa kutazamisha sana katika karne ya 19. Je, uhai na ulimwengu wote mzima ungeweza kuwapo bila Chanzo cha Mwanzilishi asiye wa kibinadamu? Je, kuabudu Muumba kama huyo ni kupoteza wakati? Majibu ya wanafalsafa mashuhuri wa siku hizo yalikuwa wazi na yenye mkazo. “Kama vile tusivyohitaji maongozi ya kimaadili, wala hatuhitaji dini,” akasema Friedrich Nietzsche. “Dini ni ndoto ya akili ya kibinadamu,” akasisitiza Ludwig Feuerbach. Naye Karl Marx, ambaye maandishi yake yalipata umashuhuri katika miongo iliyofuata, alisema hivi kwa ujasiri: “Nataka kuongeza uhuru wa akili kutokana na minyororo ya dini.”
Wengi walivutiwa. Hata hivyo, waliyoyaona, yalikuwa majani, matawi, na kisiki pekee cha kukataa kuwapo kwa Mungu. Mizizi ilikuwapo nayo ilikuwa inachipuka zamani kabla ya karne ya 19 kuanza. Kwa kushangaza, ukuzi wa siku hizi wa kukataa kuwapo kwa Mungu ulichochewa na dini za Jumuiya ya Wakristo! Jinsi gani? Kwa sababu ya ufisadi, mashirika hayo ya kidini yalisababisha kuvunjika moyo kwingi na mateto makubwa sana.
Mbegu Zapandwa
Wakati wa Enzi za Kati, Kanisa Katoliki lilikuwa limekandamiza wafuasi walo. “Makasisi walionekana kukosa maarifa ya kutunza mahitaji ya watu ya kiroho,” yasema The Encyclopedia Americana. “Makasisi wa cheo cha juu, hasa maaskofu, walitoka kwa jamii ya maisha ya juu nao waliona vyeo vyao kuwa hasa chanzo cha umashuhuri na nguvu.”
Wengine, kama John Calvin na Martin Luther, walijaribu kurekebisha kanisa. Hata hivyo, njia zao mara nyingi hazikuwa kama za Kristo; kuachilia mambo na umwagaji wa damu vilitia alama Marekebisho hayo. (Linganisha Mathayo 26:52.) Mashambulizi mengine yalikuwa yenye ukatili hivi kwamba karne tatu baadaye rais wa tatu wa Marekani, Thomas Jefferson aliandika hivi: “Ni afadhali kutoamini mungu yeyote, kuliko kumkufuru yeye kwa matendo makatili ya Calvin.”a
Kwa wazi, Marekebisho hayo hayakurudisha ibada safi. Hata hivyo, yalipunguza nguvu za Kanisa Katoliki. Vatikani haikudhibiti imani ya kidini sana. Wengi walijiunga na madhehebu mapya ya Waprotestanti. Wengine wakiwa wamevunjwa moyo na dini, walifanya akili ya mwanadamu kuwa ibada yao. Mwelekeo wa kukubali mambo zaidi ukafuatwa, ukiruhusu kutokea kwa maoni mbalimbali kuhusu Mungu.
Shaka Lachipuka
Kufikia karne ya 18, kwa ujumla kufikiri kuzuri kulitukuzwa kuwa ponyo la matatizo ya ulimwengu. Mwanafalsafa Mjerumani Immanuel Kant alisisitiza kwamba maendeleo ya mwanadamu yalikuwa yakizuiliwa na kutegemea kwake siasa na dini ili kupata mwongozo. “Jaribu kujua!” alihimiza. “Pata ujasiri wa kutumia akili yako mwenyewe!”
Ile Enzi ya Kuerevuka, iliyoitwa pia Enzi ya Kusababu, ilikuwa pia na mtazamo huo. Ukidumu katika karne ya 18, hiki kilikuwa kipindi cha kutafuta sana kupata ujuzi. “Shaka lilichukua nafasi ya imani bila ujuzi,” chasema kitabu Milestones of History. “Desturi zote za kale zilitiliwa shaka.”
Moja ya ‘desturi za kale’ iliyochunguzwa ilikuwa dini. “Wanadamu walibadili maoni yao juu ya dini,” chasema kitabu The Universal History of the World. “Hawakuridhika tena na ahadi za thawabu mbinguni; walikuwa wakidai maisha bora duniani. Wakaanza kupoteza imani yao katika mwenye uwezo kuliko mwanadamu.” Kwa kweli, wanafalsafa walio wengi wa ile Enzi ya Kuerevuka waliidharau dini. Hasa waliwalaumu viongozi wa Kanisa Katoliki wenye pupa ya cheo kwa kuwaacha watu katika ujinga bila maarifa.
Wakikosa kuridhika na dini, wengi wa wanafalsafa hawa wakawa na imani katika Mungu; lakini walisisitiza kwamba alikuwa hana haja na wanadamu.b Wachache wakawa shupavu katika kutoamini kuwapo kwa Mungu, kama vile mwanafalsafa Paul Henri Thiry Holbach, aliyedai kwamba dini ilikuwa “chanzo cha migawanyiko, ukichaa, na uhalifu.” Miaka iliposonga, wengi zaidi wakachoshwa na Jumuiya ya Wakristo na kukubali maneno ya Holbach.
Ni jambo la kushangaza kama nini kwamba Jumuiya ya Wakristo ilichochea kukataa kuwapo kwa Mungu! “Makanisa yalikuwa chanzo cha kukataa kuwapo kwa Mungu,” aandika mwanatheolojia profesa Michael J. Buckley. “Dhamiri ya watu wa Magharibi iliudhika sana na kukirihishwa na dini zenye kuungama dhambi. Makanisa na madhehebu ya kidini yalikuwa yameharibu Ulaya, yalikuwa yamechochea mauaji, yalidai ukinzani wa kidini au mapinduzi, yakafanya bidii ya kupindua wafalme.”
Kukataa Kuwapo kwa Mungu Kwafikia Kiwango Chake cha Juu Zaidi
Kufikia karne ya 19, kumkana Mungu kulikuwa wazi na kusitawi. Wanafalsafa na wanasayansi hawakupata tulizo kutangaza kwa ujasiri maoni yao. “Adui wetu ni Mungu,” akatangaza waziwazi shupavu mmoja asiyekubali kuwapo kwa Mungu. “Kumchukia Mungu ni chanzo cha maarifa. Ikiwa mwanadamu atafanya maendeleo kikweli, lazima yawe chini ya msingi wa kukataa kuwapo kwa Mungu.”
Hata hivyo, badiliko dogo lilitokea katika karne ya 20. Kumkana Mungu kukapungua; aina tofauti ya kukataa kuwapo kwa Mungu kukaanza kuenea, kukiathiri hata wale wanaodai kumwamini Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Madhehebu ya Waprotestanti yaliyotokezwa na yale Marekebisho yalidumisha mafundisho mengi yasiyo ya kimaandiko. Ona makala za Amkeni! za Juni 8, 1990, kurasa 16-20, na Julai 8, 1990, kurasa 11-15.
b Wenye imani katika Mungu lakini kwamba hana haja na wanadamu walidai kwamba, kama vile mtengenezaji wa saa, Mungu aliviweka viumbe wake katika mwendo halafu akaacha mambo yajiendeshe, na kukosa kuhusika bila kujali. Kulingana na kitabu The Modern Heritage, wenye imani katika Mungu, “waliamini kwamba kukataa kuwapo kwa Mungu ni kosa lililotokezwa na kutojua la kufanya lakini pia kwamba hali ya mamlaka ya Kanisa Katoliki lenye ugumu na kutovumilia mafundisho yao ilikuwa ya kulaumika hata zaidi.”
[Picha katika ukurasa wa 3]
Karl Marx
[Picha katika ukurasa wa 3]
Ludwig Feuerbach
[Picha katika ukurasa wa 3]
Friedrich Nietzsche
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
JALADA: Earth: By permission of the British Library; Nietzsche:- Copyright British Museum (see also page 3); Calvin: Musée Historique de la Réformation, Genève (Photo F. Martin); Marx: U.S. National Archives photo (see also page 3); Planets, instruments, crusaders, locomotive: The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck; Feuerbach: The Bettmann Archive (see also page 3)