Je, Unapaswa Kusali kwa Yesu?
WATU fulani wanafikiri kwamba ni sawa kusali kwa Yesu. Katika Ujerumani wengi wamefundishwa wakiwa watoto kwamba kabla ya kula chakula wanapaswa kukunja mikono yao na kumshukuru Yesu Kristo.
Kulingana na Biblia, kwa kweli Yesu ana cheo kikubwa sana mbinguni. Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kusali kwake? Waweza kuwa kati ya wale wanaosali kwa Yesu kwa ajili ya kumpenda, lakini Yesu anazionaje sala kama hizo?
Kwanza, kwa nini maswali haya yanazushwa? Kwa sababu Biblia humwita Yehova Mungu ni “Msikiaji wa sala.” Basi, si ajabu kwamba watumishi wa Mungu katika nyakati za kale, kama vile Waisraeli, walisali kwa Yehova Mungu pekee, aliye Mweza Yote.—Zaburi 5:1, 2; 65:2, NW.
Je, mambo yalibadilika wakati Yesu, Mwana wa Mungu, alipokuja duniani kuokoa wanadamu katika dhambi na kifo? La, sala bado zilielekezwa kwa Yehova. Alipokuwa duniani Yesu mwenyewe alisali mara nyingi kwa Baba yake wa mbinguni, naye aliwafundisha wengine kufanya vivyo hivyo. Ebu fikiria sala ya kiolezo, ambayo nyakati nyingine huitwa Sala ya Bwana au Baba Yetu, ambayo ni mojapo sala zinazojulikana zaidi ulimwenguni. Yesu hakutufundisha tusali kwake; alitupa kiolezo hiki: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.”—Mathayo 6:6, 9; 26:39, 42.
Sasa acha tuangalie habari hii kwa makini zaidi kwa kuchunguza maana halisi ya sala.
Sala Ni Nini?
Kila sala ni aina ya ibada. The World Book Encyclopedia chathibitisha jambo hili, kikisema: “Sala ni aina ya ibada ambayo mtu aweza kujitoa, kushukuru, kuungama, au kumsihi Mungu.”
Katika pindi moja Yesu alisema: “Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” Yesu alishikamana na kweli ya msingi kwamba ibada—na hivyo sala pia—zinapaswa kuelekezwa kwa Baba yake pekee, Yehova Mungu.—Luka 4:8; 6:12.
Kumtambua Yesu Katika Sala Zetu
Yesu alikufa akiwa dhabihu ya fidia kwa wanadamu, akafufuliwa na Mungu, na kupewa cheo cha juu zaidi. Kama unavyoweza kufikiri, haya yote yalileta badiliko kuhusu sala zenye kukubalika. Kwa njia gani?
Mtume Paulo anafafanua uvutano mkubwa ambao cheo cha Yesu huleta kuhusu sala akisema: “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:9-11.
Je, maneno “kwa jina la Yesu kila goti lipigwe” yamaanisha kwamba tusali kwake? (Italiki ni zetu.) La. Neno la Kigiriki linalohusika hapa “humaanisha jina linalounganisha wale wapigao goti, wote (πᾶν γόνυ) wakiabudu katika muungano huo. Jina ambalo Yesu alipata huwasukuma wote katika umoja wa ibada.” (A Grammar of the Idiom of the New Testament, cha G. B. Winer) Kwa kweli, ili sala ikubalike, lazima isemwe “kwa jina la Yesu,” hata hivyo, inaelekezwa kwa Yehova Mungu nayo humtukuza. Kwa sababu hiyo, Paulo alisema: “Katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.”—Wafilipi 4:6, italiki ni zetu.
Kama vile kijia kiongozacho kwenye lengo, vivyo hivyo Yesu ni “njia” iongozayo kwa Mungu Mweza Yote. “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” ndivyo Yesu alivyowafundisha mitume. (Yohana 14:6) Hivyo, tunapaswa kusali kwa Mungu kupitia Yesu na si moja kwa moja kwa Yesu.a
‘Lakini,’ wengine waweza kuuliza hivi, ‘je, Biblia hairipoti kwamba mfuasi Stefano na mtume Yohana walizungumza na Yesu akiwa mbinguni?’ Hilo ni kweli. Hata hivyo, matukio haya hayakuhusu sala, maana Stefano na Yohana, kila mmoja alimwona Yesu katika njozi na kuzungumza naye moja kwa moja. (Matendo 7:56, 59; Ufunuo 1:17-19; 22:20) Ufahamu kwamba kuzungumza tu hata na Mungu hakumaanishi kwamba tumesali kwake. Adamu na Hawa walizungumza na Mungu, wakitoa visababu kwa dhambi yao kubwa, wakati Yeye aliwahukumu baada ya dhambi yao katika Edeni. Kuzungumza na Mungu kwa njia kama hiyo hakukuwa kusali. (Mwanzo 3:8-19) Hivyo, ingekuwa makosa kutaja mazungumzo ya Stefano na Yohana pamoja na Yesu kuwa ushahidi wa kwamba tunapaswa kusali kwa Yesu.
Jina la Yesu ‘Linaitiwaje’?
Je, bado una shaka ukifikiri kwamba ni sawa kusali kwa Yesu? Mwanamke mmoja aliandikia ofisi ya tawi ya Watch Tower Society akisema: “Kwa kusikitisha, bado sijasadiki kwamba Wakristo wa kwanza hawakusali kwa Yesu.” Mwanamke huyo alikuwa akifikiria juu ya maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 1:2, mahali aliposema “pamoja na wote wanaoliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kila mahali.” (Italiki ni zetu.) Hata hivyo, mtu apaswa kujua kwamba, katika lugha ya asili, usemi “kuliitia” waweza kumaanisha mambo mengine tofauti na sala.
Jina la Kristo “liliitiwaje” kila mahali? Njia moja ni kwamba wafuasi wa Yesu wa Nazareti walimtangaza waziwazi kuwa Mesiya na “Mwokozi wa ulimwengu,” wakifanya matendo mengi ya kimuujiza kwa jina lake. (1 Yohana 4:14; Matendo 3:6; 19:5) Kwa hiyo, The Interpreter’s Bible yasema kwamba kifungu “kuliitia jina la Bwana wetu . . . chamaanisha kukiri kuwa yeye ni bwana wala si kusali kwake.”
Kumkubali Kristo na kujizoeza imani katika damu yake iliyomwagwa, inayofanya msamaha wa dhambi uwezekane, pia lamaanisha “kuliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo.” (Linganisha Matendo 10:43 na 22:16.) Na kihalisi tunataja jina la Yesu tunaposali kwa Mungu kupitia kwake. Hivyo, ingawa inaonyesha kwamba tunaweza kuliitia jina la Yesu, Biblia haionyeshi kwamba tunapaswa kusali kwake.—Waefeso 5:20; Wakolosai 3:17.
Mambo Ambayo Yesu Anaweza Kutufanyia
Yesu aliwaahidi wanafunzi wake kwa udhahiri hivi: “Nanyi mkiomba [“mkisali,” NW] lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya.” Je, hilo lataka kusali kwake? La. Kusali kunaelekezwa kwa Yehova Mungu—lakini kwa jina la Yesu. (Yohana 14:13, 14; 15:16) Tunamsihi Mungu kwamba Mwanaye, Yesu, atumie uweza wake mkuu kwa niaba yetu.
Yesu huwasilianaje na wafuasi wake wa kweli leo? Ufafanuzi wa Paulo wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta watumika kama kielezi. Alilifananisha na mwili, na Yesu Kristo na kichwa. Kwa njia ya “viungo na mishipa,” “kichwa” hugawia mahitaji washiriki wacho wa mwili wa kiroho au kupitia kwa mipango ya kugawia kutaniko chakula cha kiroho cha kutosha na mwongozo. (Wakolosai 2:19) Kwa njia iyo hiyo, Yesu leo hutumia “zawadi katika wanadamu,” au wanaume waliokomaa kiroho, kuongoza katika kutaniko, hata kutoa karipio inapokuwa lazima kufanya hivyo. Hakuna mwandalio wa washiriki wa kutaniko kuwasiliana na Yesu moja kwa moja au kusali kwake, lakini wanapaswa—ndio, ni lazima—wasali kwa Yehova Mungu, Baba ya Yesu.—Waefeso 4:8-12.
Unamheshimuje Yesu?
Kuhusu wokovu wa wanadamu, Yesu ana fungu kubwa jinsi gani! Mtume Petro alisema: “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” (Matendo 4:12) Je, unajua umuhimu wa jina la Yesu?
Kwa kutoelekeza sala moja kwa moja kwa Yesu mwenyewe, hatukosi kuheshimu cheo chake. Badala ya hivyo, Yesu anaheshimiwa tunaposali kwa kutumia jina lake. Na kama vile watoto huheshimu wazazi wao kwa kuwa watiifu, sisi huheshimu Yesu Kristo kwa kutii amri zake, hasa ile amri mpya ya kupendana.—Yohana 5:23; 13:34.
Sala Zinazokubalika
Je, unatamani kutoa sala zinazokubalika? Basi zielekeze kwa Yehova Mungu, na ufanye hivyo kwa jina la Mwanaye, Yesu. Ufahamu mapenzi ya Mungu na sala zako zionyeshe ufahamu huo. (1 Yohana 3:21, 22; 5:14) Pata nguvu kutoka kwa maneno ya Zaburi 66:20: “Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu [“sala zangu,” NW], wala kuniondolea fadhili zake.”
Kama vile tumeona, sala ni namna ya ibada inayopewa Mungu Mweza Yote pekee. Kwa kuelekeza sala zetu zote kwa Yehova Mungu, tunaonyesha kwamba tunatii mwongozo wa Yesu wa kusali: “Baba yetu uliye mbinguni.”—Mathayo 6:9.
[Maelezo ya Chini]
a Wengine waweza kusali kwa Yesu kwa sababu wanaamini kwamba yeye ni Mungu. Lakini Yesu ni Mwana wa Mungu, naye alimwabudu Yehova, Baba yake. (Yohana 20:17) Kwa mazungumzo zaidi juu ya haba- ri hii, ona Je! Uamini Utatu?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.