Dini Yako—Je, Ni Merikebu Isiyopaswa Kuachwa?
MERIKEBU katikati ya dhoruba kali. Wafanyakazi wayo, wanang’ang’ana kabisa ili kuokoa chombo chao, wanakabiliwa na uamuzi wenye kutazamisha: ama wakae ndani ama waiache merikebu na kujiokoa. Je, ulijua kwamba ono hilo lenye kuogofya linatumika likiwa kielezi cha mafundisho ya kidini?
Wanatheolojia, hasa wasomi Wakatoliki, mara nyingi hulinganisha dini yao na merikebu inayokabiliwa na dhoruba. Wanasema kwamba merikebu hii, Yesu au Petro wakiwa nahodha, ndiyo njia pekee ya kuokoka. Msimamo wa makasisi ni, ‘Usiiache kamwe merikebu. Kanisa limepitia matatizo makubwa hapo awali, lakini hilo ni merikebu iliyokabili dhoruba zote katika historia.’ Wengine husema, ‘Kwa nini uiache? Ni mambo gani mengine yaliyopo ya kugeukia? Kwa nini usikae na kusaidia kuiongoza hadi kwenye maji yenye utulivu?’
Kwa kupatana na lugha hii ya mfano, watu wengi, wa dini za aina nyingi, wanasababu hivi, ‘Najua kwamba dini yangu inakosea katika mambo mengi, lakini natumaini itabadilika. Sitaki kuiacha. Ningependa kushiriki katika kuisaidia ishinde matatizo yayo.’ Kusababu kwa aina hii kwaweza kuongozwa na shauku ya unyoofu kwa dini ya mababu au hata kwa woga wa “kuisaliti.”
Mfano mzuri ni ule wa Hans Küng, mwanatheolojia Mkatoliki aliye mpinzani ajulikanaye sana, aliyesababu hivi: “Je, niiache mashua wakati wa dhoruba, nikiwaacha wale nilioabiri nao hadi sasa wakabili upepo, wavute maji, na labda kupigania wokovu?” Yeye alijibu hivi: “Mimi sitaacha kutoa msaada wangu kwa kanisa.” Jambo jingine lingekuwa “kuachana na kanisa hili, kwa sababu ya kasoro yalo, kwa ajili ya kupenda maadili ya hali ya juu, na pengine, kuwa Wakristo asilia.”—Die Hoffnung bewahren.
Lakini, je, mtu anaweza kukaa ndani ya mashua ya kanisa lake mwenyewe akiwa na tumaini kwamba Mungu, kwa huruma zake, atazipa dini zote kipindi kisicho na kikomo cha kurekebisha mambo? Hilo ni swali la kufikiriwa sana. Kama ionyeshwavyo na kielezi hicho, kuondoka haraka kutoka kwa merikebu iliyohatarishwa na kuingia katika mitumbwi isiyo salama kungekuwa hatari kama vile kukaa ndani ya merikebu inayozama. Je, ni hekima kukaa katika kanisa kwa vyovyote, bila kujali hali yalo? Kuna uwezekano gani kwamba dini za leo zitarekebisha mambo? Mungu ataziruhusu kwa muda gani kutenda dhidi ya mapenzi yake?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Chesnot/Sipa Press