Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Habari Njema za Ufalme Zitahubiriwa
KWA karne nyingi adui mkuu wa Mungu, Shetani Ibilisi, ametumia kwa ufundi serikali za kisiasa na dini bandia katika jitihada zake za kuzuia kuenezwa kwa Ukristo wa kweli. Lakini mbinu hizi hazitafaulu. Yesu alitabiri kwamba “habari njema ya ufalme itahubiriwa [si, “huenda ikahubiriwa” au, “ingeliweza kuhubiriwa”] katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:14, italiki ni zetu.
Kushindwa kwa Shetani kumekuwa dhahiri katika Ugiriki. Katika nchi hiyo Kanisa Orthodoksi la Kigiriki limejaribu kuzuia Mashahidi wa Yehova kuhubiri habari njema za Ufalme. Lakini kama inavyokaziwa na ono lifuatalo, hatimaye kweli za Biblia zafikia watu wenye mioyo minyoofu japo upinzani.
Yapata miaka kama 30 iliyopita, kasisi wa Orthodoksi ya Kigiriki alikubali habari njema na hata kueleza tamaa yake ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, watu wake wa ukoo walipinga sana hatua hii na kumshurutisha aache ushirika wake pamoja na Mashahidi. Ili kupendeza familia yake, aliendelea kufuatia kazi-maisha yake akiwa kasisi; lakini, alitambua nyakati zote kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamemsaidia kujifunza kweli na kwamba aliiacha kwa sababu ya cheo cha umashuhuri katika dini bandia.
Walakini, nyakati nyingine yeye alisema kwa kuunga mkono Mashahidi wa Yehova fursa ilipojitokeza. Katika pindi kadhaa hata aliwashauri watu kwamba ikiwa wangetaka kujifunza kweli za Biblia, wanapaswa kujifunza pamoja na Mashahidi. Kwa miaka ambayo imepita baadhi yao wamefuata pendekezo lake.
Hivi karibuni kasisi huyo alikuwa mgonjwa sana na kugundua kuwa huenda angekufa baada ya muda mfupi. Akiwa hospitalini, aliita watoto wake, nao walikusanyika wote kando ya kitanda chake.a Halafu akawaelezea kwamba ikiwa angekufa, huenda wangekutana naye tena. Alizungumza nao kuhusu fundisho la Biblia juu ya binadamu kufufuliwa na Yehova ili aishi katika paradiso duniani, lakini iwapo walitaka kwelikweli kuona hilo likitukia, iliwapasa kujifunza kweli kutoka kwenye Biblia na kujitenga na dini bandia. Aliwasihi washirikiane na Mashahidi wa Yehova na kujifunza kutoka kwao jinsi ya kuwa Wakristo wa kweli.
Muda mfupi baada ya hapo kasisi huyo alikufa. Hata hivyo, wasia wake kwa watoto wake ulikuwa na matokeo mazuri. Binti yake, sawa na watu wake wa ukoo, alikuwa amechukia Mashahidi wa Yehova na kazi yao. Lakini hangeweza kupuuza ombi nyoofu la babaye aliyekuwa akifa, hivyo mara moja aliwasiliana na Mashahidi wa Yehova na kuanza kujifunza Biblia. Hivi karibuni yeye mwenyewe alikuja kuwa Shahidi, akiweka maisha yake wakfu kwa Yehova Mungu na kuufananisha kwa ubatizo wa maji.
Katika Ugiriki, kama ilivyo katika nchi nyinginezo 230, Mashahidi wa Yehova hutegemea uwezo wa roho takatifu ya Mungu. Ni kwa utegemezo kamili wa roho takatifu kwamba wao hushiriki katika utimizo wa unabii wa Yesu: “Mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu [“roho takatifu,” NW]; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”—Matendo 1:8.
[Maelezo ya Chini]
a Kanisa Orthodoksi la Kigiriki huruhusu kasisi wao kuoa.y