Kujifunza Kupata Furaha Katika Kumhofu Yehova
“Njoni, enyi wana, mnisikilize, nami nitawafundisha kumcha [“kumhofu,” “New World Translation”] BWANA.”—ZABURI 34:11.
1. Hofu itaondolewaje na Ufalme wa Mungu, lakini je, hilo lamaanisha hofu yote?
WATU kila mahali hutamani kupata uhuru kutoka katika hali ya hofu—kuhofu uhalifu na ujeuri, kuhofu kutokuwa na kazi ya kuajiriwa, kuhofu ugonjwa mahututi. Itakuwa siku tukufu kama nini uhuru huo unapokuwa halisi chini ya Ufalme wa Mungu! (Isaya 33:24; 65:21-23; Mika 4:4) Hata hivyo, si kuhofu kote kutakakoondolewa wakati huo, wala hatupaswi kujaribu kusukumia mbali kuhofu kote kutoka maishani mwetu sasa. Kuna hofu iliyo nzuri na hofu iliyo mbaya.
2. (a) Ni hofu ya aina gani iliyo mbaya, na ni ya aina gani iliyo yenye kutamanika? (b) Hofu ya kimungu ni nini, na maandiko yaliyotajwa huonyeshaje jambo hilo?
2 Hofu yaweza kuwa sumu ya akilini, ikidhoofisha uwezo wa mtu wa kutumia akili. Yaweza kudhoofisha moyo mkuu na kuharibu tumaini. Hofu hii yaweza kumpata mtu anayetishwa kimwili na adui fulani. (Yeremia 51:30) Yaweza kumpata mtu ambaye huwekea umaana sana jambo la kupata kibali cha wanadamu fulani mashuhuri. (Mithali 29:25) Lakini pia kuna ile hofu yenye mtazamo ufaao, aina ambayo hutuzuia tusifanye jambo lolote bila kujali, na tusijidhuru. Hofu ya kimungu hutia ndani hata mengi zaidi ya hayo. Huo ni woga kuelekea Yehova, staha nyingi kuelekea yeye, pamoja na ogofyo lifaalo la kutompendeza. (Zaburi 89:7) Hofu hiyo ya kutompendeza Mungu hutokana na uthamini kuelekea fadhili zake zenye upendo na wema wake. (Zaburi 5:7; Hosea 3:5) Yatia ndani pia ufahamu wa kwamba Yehova ndiye Hakimu Mkuu Zaidi ya Wote na Mweza Yote, aliye na nguvu za kupasisha adhabu, hata kifo, juu ya wale wakataao kumtii.—Warumi 14:10-12.
3. Kumhofu Yehova kunatofautianaje na hofu iliyoshirikishwa na miungu fulani ya kipagani?
3 Hofu ya kimungu ni sifa yenye mtazamo ufaao, si yenye kuhuzunisha. Humchochea mtu awe imara kwa yale yaliyo sawa, si kuyaacha kwa kufanya mabaya. Si kama ile hofu inayoshirikishwa na yule mungu wa kale wa Kigiriki Fobos, aliyesimuliwa kuwa mungu mkatili aliyeamsha hofu kuu. Wala si kama ile hofu inayoshirikishwa na yule mungu-mke wa Kihindu aitwaye Kali, ambaye nyakati nyingine huonyeshwa akiwa mwenye hamu ya kumwaga damu, akitumia maiti, nyoka, na mafuvu ya vichwa kuwa mapambo. Hofu ya kimungu huvutia; haichukizi. Imefungamanishwa na upendo na uthamini. Hivyo, hofu ya kimungu hutuvuta kwa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; Zaburi 2:11.
Sababu kwa Nini Wengine Wanayo na Wengine Hawana
4. Kama vile ilivyoonyeshwa na mtume Paulo, jamii ya kibinadamu imefikia hali gani, na hali hiyo imesababishwa na nini?
4 Wanadamu kwa ujumla hawachochewi na sifa hiyo ya hofu ya kimungu. Kwenye Warumi 3:9-18, mtume Paulo asimulia kadiri ambayo wanadamu wametumbukia kutoka kwenye hali ya kwanza ya ukamilifu. Baada ya kusema kwamba wote wako chini ya dhambi, Paulo anukuu kutoka kwenye Zaburi, akisema hivi: “Hakuna mwenye haki hata mmoja.” (Ona Zaburi 14:1.) Kisha atoa maelezo zaidi kwa kutaja mambo kama vile kupuuza kwa wanadamu kumtafuta Mungu, ukosefu wao wa fadhili, usemi wao wenye udanganyifu, kulaani, na umwagaji wa damu. Hilo lasimulia ulimwengu wa leo kwa usahihi kama nini! Watu walio wengi hawapendezwi na Mungu wala makusudi yake. Mara nyingi watu huonyesha fadhili wakati tu ambapo kufanya hivyo kutawafaidi. Kusema uwongo na kutumia lugha chafu ni mambo ya kawaida. Umwagaji wa damu hauonyeshwi tu katika habari bali pia huonyeshwa katika kitumbuizo. Ni nini husababisha hali hii? Ni kweli kwamba sisi sote ni wazao wa yule mtenda-dhambi Adamu, lakini watu wanapochagua kufuata maishani mwao yale mambo yanayosimuliwa na mtume Paulo, kuna jambo jingine zaidi ya hilo linalohusika. Mstari wa 18 waeleza jambo hilo ni nini, ukisema: “Kumcha [“kumhofu,” NW] Mungu hakupo machoni pao.”—Ona Zaburi 36:1.
5. Kwa nini watu wengine wana hofu ya kimungu, hali wengine hawana?
5 Lakini, kwa nini watu wengine wana hofu ya kimungu hali wengine hawana? Ikisemwa kwa urahisi, ni kwa sababu watu wengine huisitawisha, hali wengine hawaisitawishi. Hakuna yeyote kati yetu anayezaliwa nayo, lakini sisi sote tuna uwezo wa kuwa nayo. Hofu ya kimungu ni jambo ambalo ni lazima tujifunze. Kisha, ili iwe kani yenye nguvu ya kuchochea maishani mwetu, twapaswa kuisitawisha.
Mwaliko Wenye Kuvutia
6. Ni nani anayetupa sisi mwaliko uliorekodiwa kwenye Zaburi 34:11, na andiko hili huonyeshaje kwamba ni lazima mtu ajifunze hofu ya kimungu?
6 Katika Zaburi 34 tunatolewa mwaliko wenye kuvutia wa kujifunza kumhofu Yehova. Hii ni zaburi ya Daudi. Naye Daudi aliwakilisha nani? Si mwingine ila Bwana Yesu Kristo. Unabii ambao mtume Yohana alitumia hasa kumhusu Yesu umerekodiwa katika mstari wa 20 wa zaburi hii. (Yohana 19:36) Katika siku yetu, Yesu ndiye anayetoa mwaliko kama ule ulio katika mstari wa 11: “Njoni, enyi wana, mnisikilize, nami nitawafundisha kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.” Hilo laonyesha kwa wazi kwamba hofu ya kimungu ni jambo ambalo mtu aweza kujifunza, na Yesu Kristo astahili sana kutufundisha. Kwa nini?
7. Kwa nini Yesu hasa ni mtu ambaye twaweza kujifunza hofu ya kimungu kutoka kwake?
7 Yesu Kristo ajua umaana wa hofu ya kimungu. Waebrania 5:7, lasema hivi kumhusu yeye: “Siku hizo za mwili wake [Kristo], alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu [“kwa sababu ya hofu yake ya kimungu,” NW].” Hofu hiyo ya kimungu ilikuwa sifa ambayo Yesu Kristo alidhihirisha hata kabla ya yeye kukabiliwa na kifo juu ya mti wa mateso. Kumbuka, katika Mithali sura ya 8, Mwana wa Mungu anasimuliwa kuwa hekima-umbo-mtu. Na kwenye Mithali 9:10, tunaambiwa hivi: “Kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ni mwanzo wa hekima.” Kwa hiyo hofu ya kimungu ilikuwa sehemu ya msingi ya utu wa Mwana wa Mungu muda mrefu kabla ya yeye kuja duniani.
8. Kwenye Isaya 11:2, 3, sisi twajifunza nini juu ya kumhofu Yehova?
8 Zaidi ya hayo, Isaya 11:2, 3 lasema hivi kumhusu Yesu akiwa Mfalme wa Kimesiya: “Roho ya BWANA [i]takaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA; na furaha yake itakuwa katika kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.” Hilo linaelezwa kwa uzuri kama nini! Kumhofu Yehova si jambo lisilopendeza. Ina mtazamo ufaao na ni yenye kujenga. Ni sifa itakayoenea katika milki yote ambayo Kristo atawala juu yayo akiwa Mfalme. Yeye anatawala sasa, naye anawapa wote wanaokusanywa kuwa raia zake, mafundisho katika kumhofu Yehova. Jinsi gani?
9. Yesu Kristo anatufundishaje kumhofu Yehova, naye ataka tujifunze nini juu ya kuhofu huko?
9 Kupitia mikutano yetu ya kutaniko, makusanyiko, na mikusanyiko, Yesu, akiwa Kichwa cha kutaniko kilichowekwa rasmi na akiwa Mfalme wa Kimesiya, hutusaidia tuelewe kwa wazi kile kimaanishwacho na hofu ya kimungu na kwa nini hiyo ni yenye manufaa sana. Hivyo yeye hujaribu kuongeza uthamini wetu kuelekea sifa hiyo ili tujifunze kupata furaha katika kumhofu Yehova kama vile yeye hupata.
Je, Wewe Utajitahidi?
10. Tunapohudhuria mikutano ya Kikristo, ni lazima tufanye nini ikiwa tutaelewa kumhofu Yehova?
10 Bila shaka, kusoma kwetu Biblia tu au kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme hakutatoa uhakikisho kwamba tutakuwa na hofu ya kimungu. Angalia lile tunalohitaji kufanya ikiwa kwa kweli tutaelewa kumhofu Yehova. Mithali 2:1-5 lasema hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha [“utakapoelewa kumhofu,” NW] BWANA, na kupata kumjua Mungu.” Kwa hiyo, tuhudhuriapo mikutano, twahitaji kusikiliza kwa uangalifu yale yanayosemwa, tujitahidi sana kukaza fikira na kukumbuka mawazo makuu, tufikirie sana jinsi ambavyo njia twahisi juu ya Yehova yapasa kuathiri mtazamo wetu kuelekea shauri linalotolewa—ndiyo, kufungua mioyo yetu. Kisha tutaelewa kumhofu Yehova.
11. Ili kusitawisha hofu ya kimungu, twapaswa kufanya nini kwa bidii na mara nyingi?
11 Zaburi 86:11 lavuta fikira kwenye jambo jingine la maana, yaani sala. “Ee BWANA, unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako,” akasali mtunga-zaburi. “Ungamanisha moyo wangu kuhofu jina lako.” (NW) Yehova alikubali sala hiyo, kwani yeye aliagiza irekodiwe ndani ya Biblia. Ili kusitawisha hofu ya kimungu, sisi pia twahitaji kusali kwa Yehova kumwomba msaada wake, nasi tutanufaika kwa kusali kwa bidii na mara nyingi.—Luka 18:1-8.
Moyo Wako Unahusika
12. Kwa nini ni lazima moyo upewe uangalifu wa pekee, na huo watia ndani nini?
12 Kuna jambo jingine tupaswalo kuona kwenye Zaburi 86:11. Mtunga-zaburi hakuwa akiomba tu kuwa na ufahamu wa kiakili juu ya kumhofu Mungu. Yeye ataja moyo wake. Kusitawishwa kwa hofu ya kimungu huhusisha moyo wa kitamathali, ambao hutaka uangalifu wa pekee kwa sababu huo ni mtu wa ndani kama adhihirishwavyo katika utendaji wetu wote wa maisha na watia ndani mawazo yetu, mitazamo yetu, tamaa zetu, makusudio yetu, miradi yetu.
13. (a) Ni nini kiwezacho kuonyesha kwamba moyo wa mtu umegawanyika? (b) Tusitawishapo hofu ya kimungu, twapaswa kujitahidi kufikia mradi gani?
13 Biblia hutuonya kwamba moyo wa mtu waweza kuwa umegawanyika. Waweza kuwa mdanganyifu. (Zaburi 12:2; Yeremia 17:9) Waweza kutuchochea tushiriki katika utendaji mbalimbali ufaao—kwenda kwenye mikutano ya kutaniko na kwenda katika huduma ya shambani—lakini waweza pia kutufanya tupende sehemu fulani za njia ya maisha ya ulimwengu. Hilo laweza kutuzuia tusiwe wenye nafsi yote kikweli katika kuendeleza masilahi ya Ufalme. Kisha moyo huo mdanganyifu waweza kujaribu kutushawishi kwamba, kwa vyovyote, sisi tunafanya mengi kadiri ileile ambayo wengine wengi wanafanya. Au, labda shuleni au mahali pa kazi yetu ya kimwili, moyo waweza kuathiriwa na hali ya kumhofu mwanadamu. Likiwa tokeo, huenda tukasita tukiwa katika mazingira hayo, kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova na huenda hata tukafanya mambo yasiyofaa kwa Wakristo. Hata hivyo, baadaye, dhamiri yetu yatusumbua. Hatutaki kuwa watu wa aina hiyo. Kwa hiyo, pamoja na mtunga-zaburi twasali kwa Yehova hivi: “Ungamanisha moyo wangu kuhofu jina lako.” (NW) Sisi twataka yule mtu wote wa ndani, kama adhihirishwavyo na utendaji wetu wote wa maisha, atoe uthibitisho wa kwamba ‘twamhofu Mungu wa kweli na kuzishika amri zake.’—Mhubiri 12:13.
14, 15. (a) Alipokuwa akitabiri juu ya kurudishwa kwa Israeli kutoka katika utumwa wa Babiloni, Yehova aliahidi kuwapa watu wake nini? (b) Yehova alifanya nini ili kutia hali ya kumhofu Mungu mioyoni mwa watu wake? (c) Kwa nini Israeli waligeuka kando kutoka kwa njia za Yehova?
14 Yehova aliahidi kwamba angewapa watu wake moyo huo umhofuo Mungu. Yeye alitabiri kurudishwa kwa Israeli akasema hivi, kama tusomavyo kwenye Yeremia 32:37-39: “Nitawaleta tena hata mahali hapa, nami nitawakalisha salama salimini; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; nami nitawapa moyo mmoja, na njia moja, wapate kunicha [“kunihofu,” NW] sikuzote; kwa mema yao, na ya watoto wao baada yao.” Katika mstari wa 40, ahadi ya Mungu inakaziwa hivi: “Nami nitatia kicho changu [“kunihofu kwangu,” NW] mioyoni mwao, ili wasiniache.” Katika 537 K.W.K., Yehova kwa hakika aliwarudisha Yerusalemu, kama vile alivyokuwa ameahidi. Lakini namna gani ile sehemu nyingine ya ahadi hiyo—kwamba angewapa ‘moyo mmoja wapate kumhofu sikuzote’? Kwa nini taifa la Israeli la kale lilimwacha Yehova baada ya yeye kuwarudisha kutoka Babiloni, hivi kwamba hekalu lao liliharibiwa katika 70 W.K., lisipate kujengwa tena kamwe?
15 Hiyo haikuwa kwa sababu ya kushindwa kokote kwa upande wa Yehova. Kwa kweli, Yehova alichukua hatua za kutia hali ya kumhofu Mungu mioyoni mwa watu wake. Kwa rehema aliyoonyesha katika kuwakomboa kutoka Babiloni na kuwarudisha kwenye bara lao, yeye aliwapa sababu za kutosha za kumstahi sana. Mungu aliimarisha yote hayo na vikumbusha, shauri, na karipio kupitia manabii Hagai, Zekaria, na Malaki; kupitia Ezra, aliyetumwa kwao akiwa mwalimu; kupitia Gavana Nehemia; na kupitia Mwana wa Mungu mwenyewe. Nyakati nyingine watu walisikiliza. Wao walifanya hivyo walipojenga tena hekalu la Yehova kwa kuhimizwa na Hagai na Zekaria, na wakati walipowafukuza wake wa kigeni katika siku za Ezra. (Ezra 5:1, 2; 10:1-4) Lakini ni mara nyingi zaidi kwamba hawakutii. Hawakuendelea kusikiliza kwa uangalifu; hawakuendelea kuitikia shauri; hawakuendelea kuwa na mioyo iliyofunguka. Waisraeli hawakuwa wakisitawisha hofu ya kimungu, na tokeo likawa kwamba, hiyo haikuwa kani yenye nguvu ya kuchochea maishani mwao.—Malaki 1:6; Mathayo 15:7, 8.
16. Yehova ametia hofu ya kimungu katika mioyo ya nani?
16 Hata hivyo, ahadi ya Yehova ya kutia hofu ya kimungu mioyoni mwa watu wake haikushindwa. Yeye alifanya agano jipya pamoja na Israeli wa kiroho, wale Wakristo aliowatolea tumaini la kimbingu. (Yeremia 31:33; Wagalatia 6:16) Katika 1919, Mungu aliwarudisha kutoka katika utumwa wa Babiloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Yeye ametia imara hali ya kumhofu mioyoni mwao. Hilo limeleta manufaa nyingi sana kwao na kwa “umati mkubwa,” walio na tumaini la uhai wakiwa raia wa kidunia wa Ufalme. (Yeremia 32:39; Ufunuo 7:9, NW) Hali ya kumhofu Yehova imekuja kuwa mioyoni mwao pia.
Jinsi Hofu ya Kimungu Hutiwa Mioyoni Mwetu
17. Yehova ametiaje hofu ya kimungu mioyoni mwetu?
17 Yehova ametiaje hofu hiyo ya kimungu mioyoni mwetu? Kupitia utendaji wa roho yake. Nasi tuna nini ambacho ni zao la roho takatifu? Biblia, Neno la Mungu lililopuliziwa. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa yale ambayo amefanya katika wakati uliopita, kwa kushughulika kwake na watumishi wake sasa katika kutimiza Neno lake la kiunabii, na kwa unabii mwingi wa mambo yatakayokuja, Yehova hutuandalia sisi sote msingi thabiti ili tusitawishe hofu ya kimungu.—Yoshua 24:2-15; Waebrania 10:30, 31.
18, 19. Mikusanyiko, makusanyiko, na mikutano ya kutaniko hutusaidiaje tujipatie hofu ya kimungu?
18 Yastahili kuonwa kwamba, kama ilivyoripotiwa kwenye Kumbukumbu la Torati 4:10, Yehova alimwambia Musa hivi: “Nikusanyieni watu hawa, nami nitawasikizisha maneno yangu, ili wajifunze kunicha [“kunihofu,” NW] mimi siku zote watakazoishi duniani, wakapate na kuwafundisha watoto wao.” Vivyo hivyo leo, Yehova ametoa maandalizi mengi ili kusaidia watu wake wajifunze kumhofu yeye. Kwenye mikusanyiko, makusanyiko, na mikutano ya kutaniko, sisi husimulia uthibitisho wa fadhili za Yehova zenye upendo na wema wake. Hilo ndilo jambo tulilokuwa tukifanya tulipokuwa tukijifunza kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Funzo hilo lilikuathirije wewe na mtazamo wako kumwelekea Yehova? Ulipoona sehemu mbalimbali za utu mtukufu wa Baba yetu wa kimbingu zikionyeshwa na Mwana wake, je, hilo halikuimarisha tamaa yako ya kutomchukiza Mungu kamwe?—Wakolosai 1:15.
19 Kwenye mikutano yetu, sisi hujifunza pia masimulizi juu ya Yehova kuwakomboa watu wake katika nyakati zilizopita. (2 Samweli 7:23) Kuhusu matendo yote hayo ya Mungu, Zaburi 66:5 lasema hivi: “Njoni yatazameni matendo ya Mungu; hutisha [“hutia hofu,” NW] kwa mambo awatendayo wanadamu.” Ndiyo, yakionwa ifaavyo, matendo hayo ya Mungu hutia mioyoni mwetu hali ya kumhofu Yehova, staha iliyo nyingi. Hivyo twaweza kuona jinsi Yehova Mungu atimizavyo ahadi yake: “Nitatia kicho changu [“kunihofu kwangu,” NW] mioyoni mwao, ili wasiniache.”—Yeremia 32:40.
20. Ili hofu ya kimungu itiwe ndani sana mioyoni mwetu, ni nini kinachotakwa kwa upande wetu?
20 Hata hivyo, ni wazi kwamba hofu hiyo ya kimungu haipati kuwa mioyoni mwetu bila jitihada kwa upande wetu. Matokeo hayaji yenyewe tu. Yehova hufanya sehemu yake. Ni lazima tufanye sehemu yetu kwa kusitawisha hofu ya kimungu. (Kumbukumbu la Torati 5:29) Waisraeli wa asili walishindwa kufanya hivyo. Lakini kwa kumtegemea Yehova, Waisraeli wa kiroho na waandamani wao tayari wanajionea manufaa nyingi zinazowajia wale wamhofuo Mungu. Tutachunguza baadhi ya manufaa hizo katika makala inayofuata.
Ungejibuje?
◻ Hofu ya kimungu ni nini?
◻ Tunafunzwaje kupata furaha katika kumhofu Yehova?
◻ Ili kuwa na hofu ya kimungu, ni jitihada gani inayotakwa kwa upande wetu?
◻ Kwa nini kujipatia hofu ya kimungu huhusisha sehemu zote za moyo wetu wa kitamathali?
[Picha katika ukurasa wa 12, 13]
Funzo lenye bidii-nyendelevu linatakwa ili kuelewa kumhofu Yehova