Manufaa za Kumhofu Mungu wa Kweli
“Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—ISAYA 48:17.
1. Ni misiba ipi ambayo ingaliweza kuzuiwa na hofu ya kimungu?
IKIWA Adamu angalisitawisha hofu ya kimungu, hiyo ingaliweza kumzuia asitende ile dhambi iliyoongoza kwenye kifo chake mwenyewe cha milele na kwenye maelfu ya miaka yenye huzuni kwa wazao wake. Ikiwa taifa la Israeli la kale lingalikuwa limetii shauri la Yehova la kumhofu na kumpenda, taifa hilo lisingalichukuliwa mateka Babiloni, wala lisingalimkataa Mwana wa Mungu na kuwa na hatia ya kumwaga damu yake. Ikiwa ulimwengu leo ungemhofu Mungu, kusingekuwa na ufisadi katika serikali wala katika biashara, kusingekuwa na uhalifu, kusingekuwa na vita.—Mithali 3:7.
2. Zijapokuwa hali katika ulimwengu unaotuzunguka, kwa nini tusitawishe hali ya kumhofu Yehova?
2 Hata hivyo, yajapokuwa mambo yafanywayo na ulimwengu unaotuzunguka, sisi tukiwa watu mmoja-mmoja, tukiwa familia, na tukiwa makutaniko ya watumishi wa Yehova twaweza kunufaika kwa kusitawisha hali ya kumhofu Mungu wa kweli. Hili lapatana na kikumbusha ambacho Musa alitolea taifa la Israeli: “BWANA, Mungu wako, anataka nini kwako, ila umche [“umhofu,” NW] BWANA, Mungu wako, na kwenda katika njia zake zote, na kumpenda, na kumtumikia BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho [“nafsi,” NW] yako yote; kuzishika amri za BWANA . . . upate uheri?” (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Ni zipi baadhi ya manufaa zinazotujia tunapomhofu Yehova, aliye Mungu wa kweli?
Hekima—Yenye Thamani Kubwa Kuliko Dhahabu
3. (a) Ni nini manufaa ya kwanza kabisa ambayo twaweza kupokea? (b) Ni nini maana ya Zaburi 111:10?
3 Manufaa ya kwanza kabisa ni hekima ya kweli. Zaburi 111:10 latangaza hivi: “Kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ndio mwanzo wa hekima.” Hilo lamaanisha nini? Hekima ni uwezo wa kutumia ujuzi kwa mafanikio kusuluhisha matatizo, kujikinga na hatari, na kufikia miradi fulani. Huhusisha uamuzi timamu. Mwanzo, yaani sehemu ya kwanza, msingi wa hekima hiyo, ni kumhofu Yehova. Kwa nini? Kwa sababu uumbaji wote ni kazi ya mikono yake. Unamtegemea. Yeye aliipa jamii ya kibinadamu hiari lakini hakuipa uwezo wa kuongoza hatua zayo yenyewe kwa mafanikio pasipo mwongozo wake. (Yoshua 24:15; Yeremia 10:23) Twaweza kuwa na mafanikio ya kudumu ikiwa tu twang’amua mambo hayo ya hakika ya msingi kuhusu maisha na twaishi kwa kupatana nayo. Ujuzi wetu kumhusu Yehova ukitupa sisi usadikisho usiotikisika wa kwamba kwa kweli mapenzi ya Mungu yatafanikiwa na kwamba ahadi yake na uwezo wake wa kuthawabisha uaminifu ni wa hakika, basi hofu ya kimungu itatuchochea tutende kwa hekima.—Mithali 3:21-26; Waebrania 11:6.
4, 5. (a) Kwa nini elimu ya chuo kikuu ya kijana fulani ilimwacha akiwa hana hekima ya kweli? (b) Mtu huyo na mke wake walijipatiaje hekima halisi baadaye, na hilo lilibadili maisha zao kwa njia gani?
4 Fikiria kielelezo hiki. Miongo kadhaa iliyopita, kijana mmoja alikuwa akisoma kwenye Chuo Kikuu cha Saskatchewan, katika Kanada. Mtaala ulitia ndani biolojia, naye alifundishwa mageuzi. Baada ya kuhitimu, yeye alifanya masomo maalumu katika fizikia ya atomi, akipokea tuzo ya kulipiwa elimu ili kuendelea na masomo yake kwenye Chuo Kikuu cha Toronto. Alipokuwa akijifunza, aliona uthibitisho mzuri ajabu wa utaratibu na ubuni katika miundo ya atomi. Lakini majibu hayakutolewa kwa maswali haya: Ni nani aliyebuni hivi vyote? Vilibuniwa wakati gani? Na kwa nini? Bila majibu hayo, je, kweli yeye angeweza kutumia ujuzi wake kwa hekima katika ulimwengu uliokuwa vitani wakati huo? Ni nini kingemwongoza? Utukuzo wa taifa? Tamaa ya kupata vitu vya kimwili? Je, kweli, alikuwa amejipatia hekima ya kweli?
5 Muda mfupi baada ya kuhitimu kwake, kijana huyo pamoja na mke wake walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kutoka katika Neno la Mungu mwenyewe, wao walianza kupata yale majibu waliyokuwa wameshindwa kupata hapo awali. Walikuja kumjua Muumba, Yehova Mungu. Walipokuwa wakijifunza juu ya Musa kwenye Bahari Nyekundu na juu ya Danieli na waandamani wake katika Babiloni, walijifunza umaana wa kumhofu Mungu si wanadamu. (Kutoka 14:10-31; Danieli 3:8-30) Hofu hiyo ya kimungu pamoja na kumpenda Yehova kihalisi kulianza kuwachochea. Upesi mwendo mzima wa maisha zao ulibadilika. Hatimaye kijana huyo alijua Yule ambaye yeye alikuwa amejifunza juu ya kazi zake katika biolojia. Alianza kuelewa kusudi la Yule ambaye yeye alikuwa ameona hekima yake ikionekana katika masomo yake ya fizikia. Badala ya kutumia ujuzi wake kuunda vyombo ambavyo vingeharibu wanadamu wenzake, yeye pamoja na mke wake walitaka kuwasaidia wengine wampende Mungu na kupenda jirani yao. Walijiandikisha katika utumishi wa wakati wote wakiwa wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu. Baadaye, walihudhuria Watchtower Bible School of Gilead wakatumwa kuwa wamishonari.
6. Ikiwa tuna hekima inayotegemea kumhofu Yehova, sisi tutaepuka kufuatia mambo yapi yasiyodumu, nasi tutakuwa tukifanya nini badala ya hivyo?
6 Bila shaka, si kila mtu awezaye kuwa mishonari. Lakini sisi sote twaweza kufurahia ile hekima inayotegemea kumhofu Yehova. Tukisitawisha hekima hiyo, hatutakuwa tukifuata kwa hamu falsafa za wanadamu ambao kwa kweli wanakisia-kisia tu kusudi la uhai. Tutakuwa tukijitahidi kujifunza Biblia, iliyopuliziwa na Chanzo cha uhai, Yehova Mungu, yule awezaye kutupa sisi uhai wa milele. (Zaburi 36:9; Wakolosai 2:8) Badala ya kuwa watumwa wa mfumo wa kibiashara ambao wenyewe watikisika ukiwa karibu kuangamia, tutatii shauri la Yehova la kuridhika na chakula na mavazi, huku tukifanya uhusiano wetu pamoja na Mungu kuwa jambo la kwanza kabisa maishani. (1 Timotheo 6:8-12) Badala ya kutenda kana kwamba wakati wetu ujao wategemea kuwa na cheo kizuri katika ulimwengu huu, tutaliamini Neno la Yehova lituambiapo kwamba ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu milele.—1 Yohana 2:17.
7. (a) Mithali 16:16 latusaidiaje tuwe na maoni yenye usawaziko juu ya mambo yenye thamani? (b) Ni thawabu zipi zinazotokana na kufanya mapenzi ya Mungu yawe kitovu cha maisha zetu?
7 Mithali 16:16 latutia moyo kwa kusema kwa kweli hivi: “Si afadhali kupata hekima [hekima ianzayo na kumhofu Yehova] kuliko dhahabu? Naam, yafaa kuchagua ufahamu [“uelewevu,” NW] kuliko fedha.” Hekima na uelewevu huo utatusukuma tufanye utendaji wa mapenzi ya Mungu uwe kitovu cha maisha zetu. Na Mungu amewakabidhi Mashahidi wake kazi gani kwa kipindi hiki cha historia ya kibinadamu? Kuhubiri juu ya Ufalme wake na kusaidia wale wenye mioyo yenye kufuatia haki wawe wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Hiyo ni kazi ambayo thawabu zayo ni uradhi wa kweli na furaha tele. Basi, ni kwa sababu nzuri kwamba Biblia husema hivi: “Heri [“mwenye furaha ni,” NW] mtu yule aonaye hekima.”—Mithali 3:13.
Ulinzi Dhidi ya Kutenda Mabaya
8. (a) Taja manufaa ya pili inayotokana na kumhofu Mungu. (b) Ni nini yale mabaya ambayo twalindwa dhidi yayo? (c) Hofu ya kimungu inakujaje kuwa kani yenye nguvu ya kuchochea?
8 Manufaa ya pili inayotokana na kumhofu Mungu ni kwamba hivyo sisi tunalindwa dhidi ya kufanya yaliyo mabaya. Wale wanaomstahi Mungu sana hawajiamulii wenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya. Hawaoni yale ambayo Mungu asema ni mema, kuwa mabaya, wala hawaoni mambo ambayo Mungu asema ni mabaya kuwa mema. (Zaburi 37:1, 27; Isaya 5:20, 21) Zaidi ya hayo, mtu anayechochewa na hofu ya kimungu haoni kwamba yatosha tu kujua yale ambayo Yehova asema ni mema na yale ambayo asema ni mabaya. Mtu huyo hupenda yale ambayo Yehova hupenda na huchukia yale ambayo Yehova huchukia. Likiwa tokeo, yeye hutenda kwa kupatana na viwango vya Mungu. Hivyo, kama isemavyo kwenye Mithali 16:6, “kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu.” Hofu hiyo ya kimungu huwa kani yenye nguvu ya kuchochea ili kutimiza yale ambayo huenda mtu asiweze kufanya kwa nguvu zake mwenyewe.
9. Tamaa yenye nguvu ya kutompendeza Mungu iliathirije uamuzi wa mwanamke fulani katika Mexico, na tokeo likawa nini?
9 Hata ingawa hofu ya kimungu yaanza tu kukua katika mtu fulani, yaweza kumwimarisha aepuke kufanya jambo fulani ambalo angeweza kujuta kwa muda wote wa maisha yake yanayobaki. Kwa kielelezo, mwanamke mmoja mja mzito katika Mexico alimuuliza mmoja wa Mashahidi wa Yehova juu ya utoaji wa mimba. Shahidi huyo alimsomea mwanamke huyo maandiko kadhaa kisha akasababu hivi: “Kwa Muumba, uhai ni jambo la maana sana, hata uhai wa wale ambao hawajazaliwa bado.” (Kutoka 21:22, 23; Zaburi 139:13-16) Uchunguzi wa kitiba ulikuwa umedokeza kwamba huenda mtoto wake akazaliwa na kasoro fulani. Lakini sasa, kwa kuchochewa na yale aliyokuwa ameona katika Neno la Mungu, mwanamke huyo aliamua kumzaa mtoto wake. Daktari wake alikataa kumwona tena, na mume wake alitisha kumwacha, lakini yeye alikuwa imara. Hatimaye, alimzaa msichana—asiye na kasoro yoyote, mwenye afya, na mwenye sura ya kupendeza. Kwa kusukumwa na shukrani, yeye aliwatafuta Mashahidi, naye akaanza kujifunza Neno la Mungu pamoja nao. Katika mwaka mmoja yeye na mume wake walibatizwa. Miaka michache baadaye kwenye mkusanyiko wa wilaya, walifurahi kukutana tena na yule Shahidi wa kwanza nao wakamjulisha kwa binti yao mzuri mwenye miaka minne. Kumstahi Mungu ifaavyo na tamaa yenye nguvu ya kumpendeza huwa kwa hakika na uvutano mwingi wenye nguvu maishani mwa mtu.
10. Hofu ya kimungu yaweza kuimarisha watu wajiweke huru na namna zipi za kutenda mabaya?
10 Hofu ya kimungu hutuimarisha dhidi ya namna nyingi za kutenda mabaya. (2 Wakorintho 7:1) Inapositawishwa ifaavyo, hiyo yaweza kumsaidia mtu akomeshe dhambi za siri, zijulikanazo kwake mwenyewe na kwa Yehova pekee. Yaweza kumsaidia ajiweke huru na utumwa wa matumizi mabaya ya kileo au matumizi mabaya ya madawa. Mtu mmoja katika Afrika Kusini aliyekuwa mraibu wa madawa ya kulevya hapo awali alieleza: “Nilipokuwa nikipata ujuzi kumhusu Mungu, nilisitawisha pia hofu ya kuumiza maoni yake au kutompendeza. Nilijua yeye alikuwa akichungulia, nami nikatamani sana kukubaliwa machoni pake. Hiyo ilinisukuma kuharibu madawa ya kulevya niliyokuwa nayo kwa kuyapiga maji chooni.” Hofu ya kimungu imesaidia maelfu zaidi kwa njia kama hizo.—Mithali 5:21; 15:3.
Ulinzi Dhidi ya Kuogopa Wanadamu
11. Kumhofu Yehova kunakofaa hutulinda dhidi ya mtego upi ulio wa kawaida?
11 Kumhofu Mungu kunakofaa hutulinda pia dhidi ya hali ya kumhofu binadamu. Watu walio wengi wanasumbuliwa na hali hiyo ya kumhofu binadamu kwa kadiri kubwa zaidi au ndogo zaidi. Hata mitume wa Yesu Kristo walimwacha na kukimbia alipokamatwa na askari-jeshi katika bustani ya Gethsemane. Baadaye, katika ua wa kuhani wa cheo cha juu, akiwa amekosa usawaziko na kunaswa na hofu, Petro alikanusha kwamba alikuwa mmoja wa wanafunzi wa Yesu na kwamba hata alimjua. (Marko 14:48-50, 66-72; Yohana 18:15-27) Lakini mitume walisaidiwa kupata tena usawaziko wa kiroho. Kwa upande ule mwingine, katika siku za Mfalme Yehoyakimu, Uriya mwana wa Shemaya alilemewa na hofu sana hivi kwamba aliacha utumishi wake akiwa nabii wa Yehova akakimbia kutoka nchi hiyo, hatimaye kukamatwa tu na kuuawa.—Yeremia 26:20-23.
12. (a) Mithali 29:25 laelekeza kwenye ulinzi upi dhidi ya hali ya kumhofu binadamu? (b) Kumtumaini Mungu hukuzwaje?
12 Ni nini kiwezacho kumsaidia mtu ashinde hali ya kumhofu binadamu? Baada ya kuonya kwamba “kuwaogopa [“kuwahofu,” NW] wanadamu huleta mtego,” Mithali 29:25 laongeza hivi: “Amtumainiye BWANA atakuwa salama.” Kumtumaini Yehova ndio ufunguo. Kutumaini huko kunategemea ujuzi na uzoefu. Kwa kujifunza Neno lake, twaona uthibitisho wa uhaki wa njia za Yehova. Twaja kufahamu matukio yanayoonyesha kutegemeka kwake, uhakika wa ahadi zake (kutia ndani ile ya ufufuo), upendo wake na nguvu zake zenye uweza wote. Kisha tunapotenda kwa kupatana na ujuzi huo, tukifanya mambo ambayo Yehova aelekeza na kukataa kwa uthabiti yale anayoonya yasifanywe, twaanza kujionea wenyewe utunzaji wake wenye upendo na kutegemeka kwake. Sisi binafsi twaona uthibitisho wa kwamba nguvu zake hutumiwa ili kutimiza mapenzi yake. Uhakika wetu katika yeye huongezeka, na pia, upendo wetu kwake na tamaa yetu yenye bidii ya kuepuka kutompendeza. Kutumaini huko kunajengwa juu ya msingi thabiti. Hutumika kama nguzo dhidi ya hali ya kumhofu binadamu.
13. Hofu ya kimungu yaweza kutusaidiaje katika kazi yetu ya kimwili, nyumbani, na shuleni?
13 Kumtumaini kwetu Yehova, pamoja na hofu ya kimungu, kutatufanya tuwe imara kwa yale yaliyo sawa ikiwa mwajiri wa kazi atutisha kwamba tutapoteza kazi yetu kwa sababu ya kukataa kushiriki katika mazoea ya kibiashara yasiyofuatia haki. (Linganisha Mika 6:11, 12.) Hofu hiyo ya kimungu huwezesha maelfu mengi ya Wakristo wadumu katika ibada ya kweli wakabilipo upinzani kutoka kwa washiriki wa familia wasioamini. Hiyo pia huwapa vijana wanaoenda shuleni moyo mkuu wa kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova, na kuwaimarisha wakabiliane na dhihaka kutoka kwa wanadarasa wenzao wanaodharau viwango vya Biblia. Hivyo, Shahidi mmoja tineja alisema hivi: “Maoni yao hayana maana sana. Maoni ya Yehova ndiyo yenye maana.”
14. Watumishi wa Yehova wanawezaje kushinda hata wakati uhai wao unapotishwa?
14 Usadikisho uo huo huwaimarisha Wakristo wa kweli washikamane kwa uthabiti na njia za Yehova hata wakati uhai wao unapotishwa. Wao wajua kwamba ni lazima watazamie mnyanyaso kutoka kwa ulimwengu. Wao wang’amua kwamba mitume walipigwa viboko na kwamba Yesu Kristo mwenyewe alipigwa mijeledi na kuuawa na watu waovu. (Marko 14:65; 15:15-39; Matendo 5:40; linganisha Danieli 3:16-18.) Lakini watumishi wa Yehova wana uhakika kamili kwamba yeye aweza kuwaimarisha ili wavumilie; kwamba kwa msaada wa Mungu wao waweza kushinda; kwamba kwa hakika Yehova atawathawabisha wale walio waaminifu—ikiwa lazima hata kwa ufufuo kwenye uhai katika ulimwengu wake mpya. Kumpenda kwao Mungu pamoja na hofu ya kimungu huwachochea kwa nguvu waepuke kufanya jambo lolote lile ambalo lisingempendeza.
15. Ni nini kilichowawezesha Mashahidi wa Yehova wadumishe uaminifu-maadili wao katika kambi za mateso za Nazi?
15 Kichocheo hicho kiliwawezesha Mashahidi wa Yehova wavumilie zile hali mbaya sana za kambi za mateso za Nazi katika miaka ya 1930 na 1940. Wao walizingatia moyoni shauri la Yesu kwenye Luka 12:4, 5: “Nawaambia ninyi rafiki zangu, msiwaogope [“msiwahofu,” NW] hao wauuao mwili, kisha baada ya hayo hawana wawezalo kutenda zaidi. Lakini nitawaonya mtakayemwogopa [“mtakayemhofu,” NW]; mwogopeni [“mhofuni,” NW] yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni [“mhofuni,” NW] huyo.” Hivyo, Gustav Auschner, Shahidi aliyekuwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, aliandika hivi baadaye: ‘Polisi wa SS walimpiga risasi August Dickmann wakatisha kutupiga risasi sisi wengine ikiwa tusingetia sahihi taarifa ya kukana imani yetu. Hakuna yeyote kati yetu aliyeitia sahihi. Tulihofu zaidi kutompendeza Yehova kuliko risasi zao.’ Kumhofu binadamu huongoza kwenye kukana imani, lakini kumhofu Mungu humwimarisha mtu kwa yale yaliyo sawa.
Kuhifadhiwa kwa Uhai
16. Ni nini kilichomwezesha Noa adumishe mwendo ulio sawa mwongo baada ya mwongo hadi wakati wa Gharika, na tokeo likawa nini kwake na kwa watu wa nyumbani mwake?
16 Noa aliishi kupitia siku za mwisho za ulimwengu wa kabla ya gharika. Yehova alikuwa ameazimia kuharibu ulimwengu mwovu wa wakati huo kwa sababu ya ubaya wa binadamu. Hata hivyo, wakati uo huo, Noa alikuwa katika ulimwengu huo uliojaa ujeuri, ukosefu mbaya sana wa adili, na mtazamo wa kutojali kuelekea mapenzi ya kimungu. Kujapokuwa kuhubiri kwa Noa juu ya uadilifu, ‘hawakutambua, hata gharika ikaja, ikawachukua wote.’ (Mathayo 24:39) Hata hivyo Noa hakukengeushwa kutoka kwenye kazi ambayo Mungu aliweka mbele yake. Alifanya “sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwanzo 6:22) Ni nini kilichomwezesha Noa afuate mwendo ufaao mwaka baada ya mwaka hadi wakati wa Gharika? Waebrania 11:7 lajibu hivi: “Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu [“alionyesha hofu ya kimungu,” NW].” Likiwa tokeo, yeye na mke wake na wana wake na wake zao walihifadhiwa kupitia Gharika.
17. (a) Yajapokuwa yale ambayo watu wengine hufanya, sisi twapaswa kufanya nini? (b) Kwa nini wale wamhofuo Yehova ni wenye furaha kwelikweli?
17 Sisi twaishi katika kipindi kifananacho na siku ya Noa kwa njia nyingi. (Luka 17:26, 27) Onyo linatolewa tena. Ufunuo 14:6, 7, (NW) lasimulia juu ya malaika fulani arukaye katika mbingu ya kati ambaye huwasihi watu wa kila taifa na kabila na lugha ‘wamhofu Mungu na kumpa utukufu.’ Iwe ni nini linalofanywa na ulimwengu unaokuzunguka, tii maneno hayo, kisha utoe mwaliko huo kwa wengine. Kama vile Noa, tenda kwa imani na uonyeshe hofu ya kimungu. Kufanya kwako hivyo kwaweza kuongoza kwenye kuhifadhiwa kwa uhai wako na kwa uhai wa wengine wengi. Tutafakaripo manufaa zinazofurahiwa na wale wamhofuo Mungu wa kweli, twaweza kukubaliana tu na mtunga-zaburi aliyepuliziwa ambaye aliimba hivi: “Heri [“mwenye furaha ni,” NW] mtu yule amchaye [“amhofuye,” NW] BWANA, apendezwaye sana na maagizo yake.”—Zaburi 112:1.
Ungejibuje?
◻ Ni zipi baadhi ya manufaa zenye kutokeza zinazotokana na kumhofu Mungu wa kweli?
◻ Hekima inayotegemea hofu ya kimungu yaweza kutulindaje?
◻ Kwa nini hofu ya kimungu hutufanya tugeukie mbali na mabaya?
◻ Hofu ya kimungu hutulindaje dhidi ya hali ya kumhofu binadamu?
◻ Hofu ya kimungu inahusuje mataraja ya uhai wetu wa wakati ujao?
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
“Heri [“mwenye furaha ni,” “NW”] mtu yule amchaye [“amhofuye,” “NW”] BWANA, apendezwaye sana na maagizo yake.”—Zaburi 112:1