“Jilindeni na Chachu ya Mafarisayo na Masadukayo”
YESU KRISTO alipoyatamka maneno hayo zaidi ya karne 19 zilizopita, yeye alikuwa akitahadharisha wanafunzi wake juu ya mafundisho na mazoea ya kidini yenye kudhuru. (Mathayo 16:6, 12) Masimulizi katika Marko 8:15 yasema hivi kihususa: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode.” Kwa nini Herode alitajwa? Kwa sababu baadhi ya Masadukayo walikuwa Waherode, chama cha kisiasa.
Kwa nini onyo la kipekee kama hilo lilihitajika? Je, kwani Mafarisayo pamoja na Masadukayo hawakuwa wapinzani wa wazi wa Yesu? (Mathayo 16:21; Yohana 11:45-50) Ndiyo, walikuwa wapinzani wake. Lakini, baadhi yao baadaye wangekubali Ukristo na kisha kujaribu kulazimisha maoni yao katika kutaniko la Kikristo.—Matendo 15:5.
Pia kulikuwa na hatari ya kwamba wanafunzi wenyewe huenda wangeiga viongozi hao wa kidini ambao wanafunzi hao walikuwa wamelelewa chini ya uvutano wao. Nyakati nyingine, kutoka kwa malezi kama hayo tu kuliwazuia wasipate maana ya mafundisho ya Yesu.
Ni nini kilichofanya Ufarisayo na Usadukayo kuwe hatari mno? Mtazamo wa hali za kidini katika siku za Yesu utatupa wazo.
Ufarakano wa Kidini
Kuhusu jumuiya ya Kiyahudi katika karne ya kwanza W.K., mwanahistoria Max Radin aliandika: “Uhuru wa makundi ya Kiyahudi kutokana na moja na jingine ulikuwa halisi sana, na hata ulisisitizwa. . . . Mara nyingi, staha kwa hekalu na jiji takatifu ilipokaziwa zaidi sana, huenda chuki ilikuzwa sana kwa wale waliokuwa na mamlaka kuu kabisa katika nchi hiyo.”
Hali mbaya ya kiroho kama nini! Ni yapi baadhi ya mambo yaliyochangia hali hiyo? Si Wayahudi wote waliishi Palestina. Uvutano wa utamaduni wa Kigiriki, ambao makasisi hawakuwa viongozi wa jumuiya, ulikuwa umechangia kule kudhoofisha staha kwa mpango wa Yehova wa ukuhani. (Kutoka 28:29; 40:12-15) Na sababu nyingine isiyopaswa kupuuzwa ni watu wa kawaida wenye elimu pamoja na waandishi.
Mafarisayo
Jina Mafarisayo, au Peru·shimʹ, laelekea lilimaanisha “watu waliojitenga.” Mafarisayo walijiona kuwa wafuasi wa Musa. Walijiundia ushirika wao wenyewe, au kikundi (kwa Kiebrania, chavu·rahʹ). Ili kuwa mshiriki, lazima mtu aape mbele ya washiriki watatu kwamba atafuata kabisa utakaso wa Kilawi, kuepuka kushirikiana kwa ukaribu na ʽam-ha·ʼaʹrets (watu walio wengi wasio na elimu), na kufuata kabisa malipo ya zaka. Marko 2:16 yasema juu ya “waandishi na Mafarisayo.” Baadhi ya hawa Mafarisayo walikuwa waandishi na walimu stadi, na wengine walikuwa watu wa kawaida.—Mathayo 23:1-7.
Mafarisayo waliamini katika Mungu aliye mahali popote. Wao walisababu kwamba kwa kuwa “Mungu yupo mahali popote, Yeye angeweza kuabudiwa katika au nje ya Hekalu, naye hangeombwa kwa dhabihu pekee. Kwa hiyo walikuza sinagogi kuwa mahali pa ibada, funzo, na sala, na kulitukuza kuwa mahali pakuu na palipo muhimu katika maisha ya watu paliposhindana na Hekalu.”—Encyclopaedia Judaica.
Mafarisayo walikosa uthamini kwa hekalu la Yehova. Hilo laweza kuonwa katika maneno ya Yesu: “Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga. Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au lile hekalu liitakasalo dhahabu? Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo juu yake, amejifunga. Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu iitakasayo sadaka? Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo juu yake.”—Mathayo 23:16-20.
Mafarisayo wangekuja kupotokaje sana katika kusababu kwao? Wao walikuwa wakikosa kuona nini? Ona jambo alilofuatisha kusema Yesu. “Naye aapaye kwa hekalu huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake.” (Mathayo 23:21, italiki ni zetu.) Kuhusu mstari huu, msomi E. P. Sanders aonelea hivi: “Hekalu halikuwa takatifu tu kwa sababu Mungu mtakatifu aliabudiwa hapo, bali pia kwa sababu yeye alikuwa hapo.” (Judaism: Practice and Belief, 63 BCE—66 CE) Hata hivyo, kuwapo kwa Yehova kipekee hakungekuwa na maana sana kwa wale walioamini kwamba alikuwa mahali popote.
Mafarisayo pia waliamini katika wazo la mtu kuamuliwa mambo kimbele pamoja na hiari. Yaani, “kila kitu kimeamuliwa kimbele, lakini kuna uhuru wa kuchagua jambo la kufanya.” Hata hivyo waliamini kwamba Adamu na Hawa waliamuliwa kimbele kufanya dhambi na kwamba hata kujikata kidogo kwenye kidole huamuliwa kimbele.
Huenda Yesu alikuwa akifikiria mawazo hayo ya uongo aliposema kuhusu kuanguka kwa mnara kulikosababisha vifo 18. Yeye aliuliza hivi: “[Waliokufa] walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu?” (Luka 13:4) Kama ilivyo na aksidenti nyingi, hiyo ilitukia kwa sababu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa,” si ajali kama Mafarisayo walivyofundisha. (Mhubiri 9:11, italiki ni zetu.) Je, watu kama hao walioonwa kuwa wenye ujuzi walitumiaje amri za Kimaandiko?
Wao Walikuwa Wabadili-Mambo wa Kidini
Mafarisayo walisisitiza kwamba amri za Kimaandiko zilikuwa lazima zifasiriwe na marabi wa kila kizazi kwa kupatana na habari mpya zaidi. Kwa hiyo, Encyclopaedia Judaica yasema kwamba “hawakupata ugumu wowote wa kupatanisha mafundisho ya Torati na mawazo yao ya kimamboleo, au kupata mawazo yao yakidokezwa au kutajwa katika maneno ya Torati.”
Kwa habari ya Siku ya Kufunika iliyofanywa kila mwaka, wao walitoa nguvu za kufunika dhambi kutoka kwa kuhani mkuu hadi kwa siku yenyewe. (Mambo ya Walawi 16:30, 33) Katika sherehe za Sikukuu ya Kupitwa, wao walikazia zaidi kukaririwa kwa masomo ya masimulizi ya Kutoka walipokuwa wakishiriki divai na mkate usiotiwa chachu kuliko yule mwana-kondoo wa sikukuu ya kupitwa.
Baadaye, Mafarisayo walikuja kuwa watu wenye uvutano katika hekalu. Kisha wao wakaanzisha msafara uliohusisha kubeba maji kutoka kidimbwi cha Siloamu na kumimina maji hayo katika kipindi cha Sikukuu ya Kukusanya, pamoja na kupigwa kwa matawi ya Wilo kwenye madhabahu katika umalizio wa Sikukuu na Sala zinazotolewa kwa ukawaida ambazo hazikuwa na msingi katika Sheria.
“Ya maana hasa” yalikuwa “mambo ya Kifarisayo yaliyobadilishwa kuhusu Sabato,” yasema The Jewish Encyclopedia. Mke alitazamiwa akaribishe Sabato kwa kuwasha taa. Ikiwa ingeonekana kuwa utendaji fulani ungetokeza kazi isiyoruhusiwa, Mafarisayo walikataa usifanywe. Hata walifikia hatua ya kuamuru juu ya tiba nao walikasirika juu ya Yesu kuponya kimwujiza siku ya Sabato. (Mathayo 12:9-14; Yohana 5:1-16) Hata hivyo, wabadili-mambo hao wa kidini hawakuanzisha tu mambo mapya katika kujaribu kutengeneza boma, au ua, wa kulinda sheria za Kimaandiko.
Uondoaji
Mafarisayo walidai kuwa na mamlaka ya kusimamisha kwa muda au kuondoa kabisa sheria za Kimaandiko. Namna wanavyosababu yaonyeshwa katika kanuni hii ya msingi ya Talmud: “Ni afadhali sheria moja iondolewe kuliko Torati nzima isahaulike.” Kielelezo kimoja kilikuwa kuondoshwa kwa Yubile kwa sababu watu walihofu kupoteza madai yao na hivyo kipindi hicho kikaribiapo, hakuna mtu angemkopesha maskini.—Mambo ya Walawi, sura ya 25.
Vielelezo vingine ni kuondolewa kwa kesi ya mwanamke aliyeshukiwa kufanya uzinzi na kesi ya uuaji wa kimakusudi ambayo haikusuluhishwa, kuondolewa kwa muda kwa zile taratibu za ufuniko wa dhambi. (Hesabu 5:11-31; Kumbukumbu la Torati 21:1-9) Muda mrefu haukupita kabla ya Mafarisayo kuondoa takwa la Kimaandiko la mtu kuwaandalia wazazi wake wenye uhitaji.—Kutoka 20:12; Mathayo 15:3-6.
Yesu alionya hivi: “Jilindeni na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.” (Luka 12:1) Ufarisayo, ukiwa na mitazamo isiyo ya kitheokrasi, hakika ulikuwa tu wa kiunafiki—hakika si kitu cha kuletwa katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, vitabu vya marejezo vya Wayahudi hupendelea Mafarisayo kuliko Masadukayo. Ebu sasa tufikirie juu ya kikundi hiki chenye kushikilia desturi.
Masadukayo
Jina Masadukayo yawezekana lilitokana na Zadoki, kuhani mkuu katika siku za Sulemani. (1 Wafalme 2:35, NW, kielezi-chini) Masadukayo walifanyiza kikundi chenye kushikilia desturi kilichowakilisha mapendezi ya hekalu na ukuhani. Tofauti na Mafarisayo, waliodai kuwa na mamlaka kwa sababu ya kusoma na utawa, Masadukayo walitegemeza pendeleo lao la kipekee kwa nasaba na cheo. Wao walipinga mambo ya Kifarisayo yaliyoongezwa hadi wakati wa kuharibiwa kwa hekalu katika 70 W.K.
Kwa kuongezea kukataa kwao wazo la mtu kuamuliwa kimbele, Masadukayo walikataa kukubali fundisho lolote ambalo halikutajwa wazi katika Pentateuki, hata kama lilitajwa mahali pengine katika Neno la Mungu. Hakika, wao “waliliona kuwa jambo zuri kubishania” mambo haya. (The Jewish Encyclopedia) Hilo lakumbusha juu ya pindi ile walipomkabili Yesu kuhusu ufufuo.
Wakitumia kielezi cha mjane mwenye waume saba, Masadukayo waliuliza hivi: “Katika kiyama [“ufufuo,” NW], atakuwa mke wa yupi katika wale saba?” Bila shaka, mjane huyo wa mfano hata angeweza kuwa na waume 14 au 21. Yesu alieleza: “Katika [“ufufuo,” NW] hawaoi wala hawaolewi.”—Mathayo 22:23-30.
Akijua kwamba Masadukayo walikataa waandikaji waliopuliziwa ila tu Musa, Yesu alithibitisha jambo Lake kwa kunukuu kutoka Pentateuki. Yeye alisema hivi: “Kwa habari ya wafu ya kwamba wafufuliwa, hamjasoma katika kitabu cha Musa, Sura ya Kijiti, jinsi Mungu alivyomwambia, akisema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Yeye si Mungu wa wafu bali wa walio hai.”—Marko 12:26, 27.
Wanyanyasi wa Yesu na Wafuasi Wake
Masadukayo waliamini katika kutumia serikali katika kushughulika na mataifa mengine kuliko kungojea Mesiya—ikiwa hata waliamini kuja kwake. Chini ya mapatano na Roma, wao walikuwa waendeshe shughuli za hekalu nao hawakutaka Mesiya yeyote atokee na kuwaharibia mambo. Wakimwona Yesu kuwa tisho kwa cheo chao, wao waliungana na Mafarisayo ili kufanya njama ya kifo chake.—Mathayo 26:59-66; Yohana 11:45-50.
Wakiwa na mtazamo wa kisiasa, Masadukayo kwa kupatana na akili walizusha suala la uaminifu-mshikamanifu kwa Roma na kusema hivi kwa sauti: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” (Yohana 19:6, 12-15) Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, ni Masadukayo waliokuwa katika mstari wa mbele katika kujaribu kuzuia mwenezo wa Ukristo. (Matendo 4:1-23; 5:17-42; 9:14) Baada ya kuharibiwa kwa hekalu katika 70 W.K., kikundi hiki kilitokomea.
Uhitaji wa Kuendelea Kujihadhari
Onyo la Yesu limefaa kama nini! Ndiyo twahitaji ‘kujilinda na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo.’ Mtu anahitaji tu kuona matunda yayo mabaya katika Uyahudi na Jumuiya ya Wakristo leo.
Hata hivyo, wakiwa tofauti kabisa wazee wa Kikristo wenye kustahili katika zaidi ya makutaniko 75,500 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote ‘wanajitunza daima wenyewe na ufundishaji wao.’ (1 Timotheo 4:16, NW) Wao hukubali Biblia nzima kuwa imepuliziwa na Mungu. (2 Timotheo 3:16) Badala ya kubadili mambo au kuendeleza taratibu zao wenyewe za kidini, wao hufanya kazi kwa umoja chini ya mwelekezo wa tengenezo linalotegemea Biblia linalotumia gazeti hili likiwa chombo chalo kikuu cha mafundisho.—Mathayo 24:45-47.
Matokeo ni nini? Mamilioni ya watu ulimwenguni pote huinuliwa kiroho wanapokuja kuelewa Biblia, kuitumia maishani mwao, na kuifundisha wengine. Ili kuona jinsi kazi hiyo inavyokamilishwa, kwa nini usizuru kutaniko la Mashahidi wa Yehova lililo karibu zaidi nawe au uandikie wachapishaji wa gazeti hili?
[Sanduku katika ukurasa wa 26]
YESU ALIWAFIKIRIA WASIKILIZAJI WAKE
YESU KRISTO alifundisha kwa uwazi, akifikiria mawazo ya wasikilizaji wake. Mathalani, alifanya hivyo alipozungumza na Farisayo Nikodemo juu ya suala la “kuzaliwa” tena. Nikodemo aliuliza: “Awezaje mtu kuzaliwa, akiwa mzee? Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?” (Yohana 3:1-5) Kwa nini Nikodemo alishangaa sana, ilhali Mafarisayo waliamini kwamba ni lazima kuzaliwa tena kwa waongofu wa Dini ya Kiyahudi, na msemo mmoja wa kirabi ulifananisha mwongofu kuwa “mtoto aliyetoka kuzaliwa”?
A Commentary on the New Testament From the Talmud and Hebraica, cha John Lightfoot, chatoa ufahamu fulani wa ndani: “Maoni ya kawaida ya Wayahudi juu ya ustahili wa Mwisraeli . . . yangali yanabaki katika akili ya Farisayo huyu” ambaye hawezi “kwa urahisi kuondoa ubaguzi wake wa kwanza . . . : ‘Huku Waisraeli . . . wakiwa na haki ya kuingizwa katika ufalme wa Mesiya, je, wamaanisha kwa usemi huu wako, kwamba ni lazima yeyote aingie tumboni mwa mama yake, ili awe Mwisraeli upya?’”—Linganisha Mathayo 3:9.
Ingawa alikubali kuzaliwa upya kwa waongofu, Nikodemo angeona jambo hilo kuwa haliwezekani kwa Wayahudi wa asili—kama kuingia upya tumbo la uzazi.
Katika pindi nyingine, wengi waliudhika Yesu aliposema juu ya ‘kula mwili wake na kunywa damu yake.’ (Yohana 6:48-55) Hata hivyo, Lightfoot asema kwamba “ilikuwa kawaida sana kwa shule za Kiyahudi kurejezea maneno haya ya ‘kula na kunywa’ katika njia ya mfano.” Yeye alisema pia kwamba Talmud ilitaja “kula Mesiya.”
Kwa hiyo maoni ya Mafarisayo na Masadukayo yalikuwa na athari kubwa katika fikira za Kiyahudi za karne ya kwanza. Hata hivyo, kwa kufaa sikuzote Yesu alifikiria ujuzi na maarifa ya wasikilizaji wake. Hili ni mojapo mambo mengi yaliyomfanya awe Mwalimu Mkubwa.