Kubali Biblia Kama Ilivyo kwa Kweli
“Sisi nasi twamshukuru Mungu bila kukoma, kwa kuwa, mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.”—1 WATHESALONIKE 2:13.
1. Ni habari ya aina gani katika Biblia inayofanya kitabu hicho kiwe chenye kutokeza kwelikweli?
BIBLIA TAKATIFU ndiyo kitabu kilichotafsiriwa zaidi na kugawanywa zaidi ulimwenguni. Inakubaliwa kwa urahisi kuwa mojapo vitabu vikuu vya fasihi. Hata hivyo, la maana zaidi, Biblia huandaa mwongozo unaohitajiwa sana na watu wa kila jamii na kila taifa, hata wawe na kazi gani au cheo gani maishani. (Ufunuo 14:6, 7) Kwa njia iridhishayo akili na moyo, Biblia yajibu maswali kama haya: Kusudi la uhai wa binadamu ni nini? (Mwanzo 1:28; Ufunuo 4:11) Kwa nini serikali za wanadamu hazijafanikiwa kuleta amani na usalama wa kudumu? (Yeremia 10:23; Ufunuo 13:1, 2) Kwa nini watu hufa? (Mwanzo 2:15-17; 3:1-6; Warumi 5:12) Katika ulimwengu huu wenye matatizo, twaweza kukabilije matatizo ya maisha kwa mafanikio? (Zaburi 119:105; Mithali 3:5, 6) Wakati ujao una nini kwetu?—Danieli 2:44; Ufunuo 21:3-5.
2. Kwa nini Biblia huandaa majibu yanayotegemeka kabisa kwa maswali yetu?
2 Kwa nini Biblia yajibu maswali hayo ikiwa na mamlaka? Kwa sababu hiyo ni Neno la Mungu. Alitumia wanadamu kuiandika, lakini kama isemwavyo wazi katika 2 Timotheo 3:16, ‘kila andiko lina pumzi ya Mungu.’ Hiyo si tokeo la ufasiri wa binafsi wa matukio ya kibinadamu. ‘Unabii [matangazo ya mambo yatakayokuja, amri za kimungu, kiwango cha maadili cha Biblia] haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na roho takatifu.’—2 Petro 1:21.
3. (a) Toa mifano ionyeshayo jinsi Biblia imethaminiwa sana na watu katika nchi mbalimbali. (b) Kwa nini watu mmoja-mmoja walikuwa tayari kuhatarisha uhai wao ili wasome Maandiko?
3 Wakithamini thamani ya Biblia, watu wengi wamejihatarisha kufungwa gerezani, hata kuuawa, ili wawe nayo na kuisoma. Ndivyo ilivyokuwa katika miaka iliyopita katika Hispania ya Katoliki, ambako makasisi waliogopa kwamba uvutano wao ungedhoofishwa ikiwa watu wangesoma Biblia katika lugha yao wenyewe; ndivyo ilivyokuwa pia katika Albania, ambako adhabu kali ilitolewa chini ya utawala huo ambao haukuamini kuwako kwa Mungu ili kukomesha uvutano wowote wa kidini. Lakini, watu mmoja-mmoja wenye kuhofu Mungu walithamini sana nakala za Maandiko, wakazisoma, na kuzishiriki na wengine. Katika kipindi cha Vita ya Ulimwengu 2, katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, Biblia ilikuwa ikipitishwa kwa uangalifu mno kutoka jengo moja la korokoro hadi jingine (ingawa tendo hilo lilikuwa limekatazwa), na wale walioipata walikariri visehemu vyayo ili kuvishiriki na wengine. Katika miaka ya 1950, katika ile iliyokuwa wakati huo Ujerumani Mashariki ya Kikomunisti, Mashahidi wa Yehova waliofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao walijihatarisha kuwekwa katika kifungo cha upweke cha muda mrefu walipopeana visehemu vidogo vya Biblia ili visomwe wakati wa usiku. Kwa nini walifanya hivyo? Kwa sababu walitambua kwamba Biblia ni Neno la Mungu, nao walijua kwamba “mwanadamu haishi kwa mkate tu” bali kwa “kila litokalo katika kinywa cha BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 8:3) Maneno hayo, yaliyoandikwa katika Biblia, yaliwawezesha Mashahidi hao kuendelea kuwa hai kiroho wajapotendwa kwa ukatili wa kinyama.
4. Biblia yapasa iwe na mahali gani maishani mwetu?
4 Biblia si kitabu cha kuwekwa tu katika rafu na kufanyiwa marejezo ya pindi kwa pindi, wala si ya kutumiwa tu wakati waamini wenzi wakusanyikapo kwa ajili ya ibada. Kila siku inapaswa kutumiwa kuangaza nuru katika hali zinazotukabili na kutuonyesha njia ifaayo ya kwenda.—Zaburi 25:4, 5.
Ilikusudiwa Isomwe na Kueleweka
5. (a) Ikiwezekana, kila mmoja wetu apaswa kuwa na nini? (b) Katika Israeli ya kale, watu walijuaje yaliyokuwa katika Maandiko? (c) Zaburi 19:7-11 yaathirije mtazamo wako kuelekea usomaji wa Biblia?
5 Katika siku zetu, nakala za Biblia hupatikana kwa urahisi katika nchi nyingi, na twahimiza kila msomaji wa Mnara wa Mlinzi kupata nakala moja. Katika kipindi ambacho Biblia ilikuwa ikiandikwa, hakukuwa matbaa za uchapishaji. Watu kwa ujumla hawakuwa na nakala zao binafsi. Lakini Yehova alipanga ili watumishi wake wasikie yale yaliyokuwa yameandikwa. Kwa hiyo, Kutoka 24:7 laripoti, baada ya Musa kuandika yale ambayo Yehova alikuwa ameagiza, “akakitwaa kitabu cha agano akakisoma masikioni mwa watu.” (Italiki ni zetu.) Baada ya kujionea maonyesho hayo ya uwezo upitao wa kibinadamu kwenye Mlima Sinai, wao walitambua kwamba Musa aliwasomea yale yaliyotoka kwa Mungu na kwamba wao walihitaji kujua habari hii. (Kutoka 19:9, 16-19; 20:22) Sisi pia twahitaji kujua yale yaliyoandikwa katika Neno la Mungu.—Zaburi 19:7-11.
6. (a) Kabla ya taifa la Israeli kuingia katika Bara Lililoahidiwa, Musa alifanya nini? (b) Twaweza kuigaje kielelezo cha Musa?
6 Taifa la Israeli lilipojitayarisha kuvuka Mto Yordani na kuingia katika Bara Lililoahidiwa, na hivyo wakiacha maisha yao ya kuhama-hama nyikani, ilifaa kwao kupitia Sheria ya Yehova na shughuli zake pamoja nao. Akisukumwa na roho ya Mungu, Musa alipitia Sheria pamoja nao. Aliwakumbusha juu ya mambo madogo-madogo ya Sheria, naye akakazia pia kanuni na mitazamo ya msingi ambayo ingekuwa na uvutano juu ya uhusiano wao pamoja na Yehova. (Kumbukumbu la Torati 4:9, 35; 7:7, 8; 8:10-14; 10:12, 13) Tuanzapo migawo mipya au tukabilipo hali zilizo mpya maishani, itafaa kwetu pia kufikiria jinsi shauri la Maandiko lapaswa kuwa na uvutano juu ya kile tufanyacho.
7. Muda mfupi baada ya Waisraeli kuvuka Yordani, ni nini kilichofanywa kukazia Sheria ya Yehova akilini na mioyoni mwao?
7 Muda mfupi baada ya Israeli kuvuka Mto Yordani, watu walikusanyika tena ili kupitia yale Yehova alikuwa amewaambia kupitia Musa. Taifa hilo lilikusanyika karibu kilometa 50 kaskazini mwa Yerusalemu. Nusu ya makabila hayo yalikuwa mbele ya Mlima Ebali, na nusu yalikuwa mbele ya Mlima Gerizimu. Huko Yoshua “alisoma maneno yote ya torati, baraka na laana.” Hivyo, wanaume, wanawake, na watoto, pamoja na wakaaji-wageni, walisikia rudio hilo lililofaa la sheria zilizoongoza mwenendo ambao ungefanya wakose kibali cha Yehova na juu ya baraka ambazo wangepokea ikiwa wangemsikiliza Yehova. (Yoshua 8:34, 35) Wao walihitaji kuweka wazi akilini yale yaliyokuwa mazuri na yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova. Isitoshe, walihitaji kukaza mioyoni mwao yaliyo mema na kuchukia yaliyo mabaya, kama ilivyo na kila mmoja wetu leo.—Zaburi 97:10; 119:103, 104; Amosi 5:15.
8. Ni nini iliyokuwa manufaa ya usomaji wa kawaida wa Neno la Mungu katika makusanyiko fulani ya taifa lote katika Israeli?
8 Kwa kuongezea usomaji wa Sheria katika pindi hizo za kihistoria, andalio la kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu lilitajwa katika Kumbukumbu la Torati 31:10-12. Kila mwaka wa saba taifa zima lilikuwa likusanyike ili kusikia usomaji wa Neno la Mungu. Hilo liliandaa chakula cha kiroho kwao. Hilo liliendeleza katika akili na mioyo yao zile ahadi kuhusu ile Mbegu na hivyo kutumika kuelekeza waaminifu kwa yule Mesiya. Mipango ya ulishaji wa kiroho iliyoanzishwa Israeli lilipokuwa lingali nyikani haikukoma lilipoingia Bara Lililoahidiwa. (1 Wakorintho 10:3, 4) Badala ya hivyo, Neno la Mungu lilitajirishwa kwa kuongezwa kwa mafunuo mengine zaidi ya manabii.
9. (a) Je, Waisraeli walisoma Maandiko walipokusanyika katika vikundi vikubwa pekee? Eleza. (b) Maagizo ya Maandiko yalitolewaje katika familia moja-moja, na kwa lengo gani?
9 Pitio la shauri la Neno la Mungu halikufanywa katika zile pindi ambapo watu walikusanyika katika kikundi kikubwa pekee. Visehemu vya Neno la Mungu na kanuni zayo zilikuwa zizungumzwe kila siku. (Kumbukumbu la Torati 6:4-9) Katika mahali pengi leo, inawezekana kwa vijana kuwa na nakala ya binafsi ya Biblia, na inawanufaisha sana kuwa nayo. Lakini hali haikuwa hivyo katika Israeli ya kale. Wakati huo, wazazi walipotoa maagizo kutoka kwa Neno la Mungu, ilikuwa lazima wategemee yale waliyokuwa wamekariri na zile kweli ambazo walikuwa wamethamini sana mioyoni mwao, pamoja na madondoo yoyote madogo ambayo huenda walikuwa wameandika. Kwa kuyarudia mara kwa mara, wao walijaribu kujenga katika watoto wao upendo kwa Yehova na njia zake. Lengo halikuwa kupata tu ujuzi bali lilikuwa kusaidia kila mshiriki wa familia kuishi kwa njia ya kuonyesha upendo kwa Yehova na Neno lake.—Kumbukumbu la Torati 11:18, 19, 22, 23.
Usomaji wa Maandiko Katika Masinagogi
10, 11. Ni programu gani ya usomaji wa Maandiko iliyofuatwa katika masinagogi, na Yesu alizionaje pindi hizo?
10 Muda fulani baada ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni katika Babiloni, masinagogi yalianzishwa yakiwa mahali pa ibada. Ili Neno la Mungu lisomwe na kuzungumzwa mahali hapo mbalimbali pa kukutania, nakala nyingi zaidi za Maandiko zilifanyizwa. Hii ilikuwa sababu kubwa iliyofanya nakala za kale zenye visehemu vya Maandiko ya Kiebrania zipatazo 6,000 zilizoandikwa kwa mkono kuokoka.
11 Sehemu muhimu ya ibada ya sinagogi ilikuwa usomaji wa Torati, inayolingana na vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia zetu za kisasa. Matendo 15:21 laripoti kwamba katika karne ya kwanza W.K, usomaji huo ulifanywa kila Sabato, na Mishnah inaonyesha kwamba kufikia karne ya pili, kulikuwa pia usomaji wa Torati katika siku za pili na tano za juma. Idadi fulani ya watu walishiriki katika kusoma visehemu vilivyogawiwa, mmoja baada ya mwingine. Desturi ya Wayahudi walioishi katika Babiloni ilikuwa kusoma Torati nzima kila mwaka; desturi iliyokuwa katika Palestina ilikuwa kuratibu usomaji kwa kipindi cha miaka mitatu. Kisehemu kutoka kwa Manabii kilisomwa pia na kufafanuliwa. Ilikuwa desturi ya Yesu kuwapo kwa programu za usomaji wa Biblia za Sabato mahali alipoishi.—Luka 4:16-21.
Itikio la Binafsi na Matumizi
12. (a) Musa aliposomea watu Sheria, watu walinufaikaje? (b) Watu waliitikiaje?
12 Kusoma Maandiko yaliyopuliziwa hakukukusudiwa kuwa jambo la kufanywa kivivi-hivi tu. Hakukufanywa ili kuridhisha tu udadisi wa watu. Musa aliposoma “kitabu cha agano” kwa Israeli katika tambarare iliyokabili Mlima Sinai, yeye alifanya hivyo ili wao wajue madaraka yao mbele ya Mungu na kuyatimiza. Je, wangefanya hivyo? Usomaji ulihitaji itikio. Watu walitambua hilo, nao wakasema: “Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda, nasi tutatii.”—Kutoka 24:7; linganisha Kutoka 19:8; 24:3.
13. Yoshua aliposoma laana za kutotii, watu walikuwa wafanye nini, kwa lengo gani?
13 Baadaye, Yoshua aliposomea taifa baraka zilizoahidiwa na zile laana, itikio lilihitajika. Baada ya kila laana, agizo lilitolewa: “Na watu wote waseme, Amina.” (Kumbukumbu la Torati 27:4-26) Hivyo, jambo kwa jambo, walirekodiwa kuwa walikubali mashutumu ya Yehova kwa mabaya yaliyotajwa. Ni lazima hilo lilikuwa tukio lenye kuvutia kama nini taifa lote lilipokubali kwa sauti kuu!
14. Katika siku za Nehemia, kwa nini usomaji wa peupe wa Sheria ulikuwa wenye manufaa hasa?
14 Katika siku za Nehemia, watu wote walipokusanyika katika Yerusalemu kusikia Sheria, waliona kwamba hawakuwa wakitekeleza vizuri maagizo yaliyoandikwa humo. Katika pindi hiyo walitumia mara hiyo yale waliyojifunza. Tokeo likawa nini? “Furaha kubwa sana.” (Nehemia 8:13-17) Baada ya juma la usomaji wa Biblia kila siku katika kipindi hicho cha msherehekeo, wao walitambua kwamba kuna mengi zaidi yaliyohitajika. Kwa sala wao walipitia historia ya shughuli za Yehova pamoja na watu wake tangu siku za Abrahamu na kuendelea. Hayo yote yaliwachochea kula kiapo cha kujipatanisha na matakwa ya Sheria, kuepuka kufunga ndoa na watu wa kigeni, na kukubali wajibu wa kudumisha hekalu na utumishi walo.—Nehemia, sura 8-10.
15. Maagizo katika Kumbukumbu la Torati 6:6-9 yanaonyeshaje kwamba, katika familia, maagizo katika Neno la Mungu hayakuwa yawe ya kivivi-hivi?
15 Vivyo hivyo, katika familia, kufundisha Maandiko hakukukusudiwa kuwa jambo la kivivi-hivi tu. Kama tulivyokwisha kuona, katika semi za kitamathali kwenye Kumbukumbu la Torati 6:6-9, watu waliambiwa ‘wayafunge maneno ya Mungu yawe dalili juu ya mikono yao’—hivyo wakionyesha kwa kielelezo na kwa tendo upendo wao kwa njia za Yehova. Nao walipaswa kuweka maneno ya Mungu kama ‘utepe katikati ya macho yao’—hivyo wakikumbuka daima kanuni zinazohusika katika Maandiko na kuzitumia kuwa msingi wa maamuzi yao. (Linganisha lugha iliyotumiwa katika Kutoka 13:9, 14-16.) Wao walikuwa ‘wayaandike juu ya miimo ya nyumba zao na juu ya malango yao’—hivyo wakitambulisha nyumba zao na jumuiya zao kuwa mahali ambapo neno la Mungu linastahiwa na kutumika. Yaani, maisha zao zilikuwa zitoe uthibitisho mwingi kwamba wao walipenda na kutumia kanuni za uadilifu za Yehova. Hilo lingenufaisha kama nini! Je, Neno la Mungu linatokeza sana hivyo katika maisha ya kila siku ya nyumba zetu? Kwa kusikitisha, Wayahudi waligeuza mpango huo wote kuwa kitu cha kivivi-hivi tu, wakivalia makasha yenye maandiko kana kwamba hayo ni hirizi. Ibada yao ilikoma kutoka moyoni nayo ilikataliwa na Yehova.—Isaya 29:13, 14; Mathayo 15:7-9.
Daraka la Wale Wenye Vyeo vya Uangalizi
16. Kwa nini usomaji wa kawaida wa Maandiko ulikuwa muhimu kwa Yoshua?
16 Kuhusu habari ya usomaji wa Maandiko, uangalifu wa pekee ulielekezwa kwa wale waliokuwa waangalizi wa taifa. Yehova alimwambia Yoshua: “Uangalie kutenda sawasawa na sheria yote.” Ili atimize daraka hilo, yeye aliambiwa: “Yatafakari maneno yake [“Lazima ukisome kwa sauti ya chini,” New World Translation] mchana na usiku, . . . maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.” (Yoshua 1:7, 8) Kama ilivyo kweli kwa mwangalizi Mkristo yeyote, usomaji wa Maandiko wa kawaida wa Yoshua ulimsaidia kuweka wazi akilini amri hususa ambazo Yehova alikuwa amewapa watu Wake. Pia Yoshua alihitaji kuelewa jinsi Yehova alivyokuwa ameshughulika na watumishi Wake chini ya hali mbalimbali. Aliposoma taarifa za kusudi la Mungu, ilikuwa muhimu kwake kufikiria daraka lake mwenyewe kwa habari ya kusudi hilo.
17. (a) Ili wafalme wanufaike na usomaji wa Maandiko katika njia ambayo Yehova alitaja, ni nini kilichohitajiwa pamoja na usomaji wao? (b) Kwa nini usomaji wa kawaida wa Biblia na kutafakari ni muhimu sana kwa wazee Wakristo?
17 Yehova alielekeza kwamba mtu yeyote aliyetumika akiwa mfalme juu ya watu Wake alikuwa, mwanzoni mwa utawala wake, afanyize nakala ya Sheria ya Mungu, akiitegemeza kwa nakala iliyowekwa na makuhani. Kisha alikuwa “asome humo siku zote atakazoishi.” Lengo halikuwa kukariri tu yaliyomo. Badala ya hivyo, lengo lilikuwa ‘ili apate kujifunza kumhofu Yehova, Mungu wake’ na kwamba “moyo wake usije ukainuliwa juu ya ndugu zake.” (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Baadhi ya wafalme waonekana walifikiri kwamba walikuwa wenye shughuli mno na kazi za usimamizi kuweza kufanya hivyo, na taifa zima liliumia kwa sababu ya kukosa kufanya hivyo. Fungu la wazee katika kutaniko la Kikristo bila shaka si fungu la wafalme. Hata hivyo, kama ilivyokuwa kweli kwa wafalme, ni muhimu kwamba wazee wasome na kutafakari juu ya Neno la Mungu. Kufanya hivyo kutawasaidia kudumisha maoni yafaayo juu ya wale waliokabidhiwa utunzi wao. Pia kutawawezesha kutimiza daraka lao wakiwa walimu kwa njia ambayo kwa kweli inamheshimu Mungu na kuimarisha Wakristo wenzi kiroho.—Tito 1:9; linganisha Yohana 7:16-18; tofautisha na 1 Timotheo 1:6, 7.
18. Usomaji na funzo la kawaida la Biblia litatusaidia kuiga kielelezo gani kilichowekwa na mtume Paulo?
18 Mtume Paulo, aliyekuwa mwangalizi Mkristo wa karne ya kwanza, alijua sana Maandiko yaliyopuliziwa. Alipotolea ushahidi watu wa Thesalonike la kale, aliweza kusababu nao kwa mafanikio kutoka kwa Maandiko na kuwasaidia kuelewa umaana. (Matendo 17:1-4) Yeye alifikia mioyo ya wasikilizaji wenye mioyo minyoofu. Hivyo, wengi waliomsikia wakawa waamini. (1 Wathesalonike 2:13) Kutokana na programu yako ya usomaji na funzo la Biblia, je, unaweza kusababu kwa mafanikio kutoka kwa Maandiko? Je, mahali umeupa usomaji wa Biblia maishani mwako na jinsi unavyoufanya watoa uthibitisho kwamba kwa kweli unathamini umaana wa kuwa Neno la Mungu? Katika makala ifuatayo, tutaona jinsi hata watu wenye ratiba zilizojaa mno waweza kuitikia sawa kwa maswali hayo.
Ungejibuje?
◻ Kwa nini watu wamekuwa tayari kuhatarisha uhai na uhuru ili wasome Biblia?
◻ Tunanufaikaje kwa kupitia maandalizi yaliyofanyiwa Israeli ya kale ili kusikia Neno la Mungu?
◻ Tufanye nini na yale tusomayo katika Biblia?
◻ Kwa nini usomaji wa Biblia na kutafakari ni muhimu hasa kwa wazee Wakristo?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Yehova alimwambia Yoshua hivi: “Lazima ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku”