Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Sweden
SWEDEN iko kwenye upande wa mashariki mwa peninsula ya Skandinevia na kupanuka juu ya Kizio cha Aktiki. Ikisifiwa ulimwenguni pote kwa mapambo ya misitu ya kijani kibichi, pamoja na maziwa ya maji, na milima, Sweden ni mojapo ya nchi za Ulaya ambayo haina mfinyano wa watu. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wametafuta na wamepata wapenda kweli huko tangu mwishoni mwa miaka ya 1800. Ona kielelezo cha juzijuzi.
Mwanamke mmoja alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi, lakini mumeye hakupendezwa na jambo hilo. Akamwambia mkeye aache kujifunza, naye akaacha. Mtu huyu alifanya kazi katika duka la kuuza vitu vya kutengeneza pombe. Siku moja dereva wa lori akaja katika duka hilo akiwa na mjukuu wake mwenye umri wa miaka kumi. Babu huyo akamwomba mtu huyo amtunzie mvulana huyo apakiapo lori lake. Akitaka mazungumzo tu, mtu huyo akamuuliza mvulana huyo ni zawadi zipi alikuwa amepokea kwa ajili ya siku yake ya kuzaliwa ya hivi majuzi. Kwa mshangao wa mtu huyo, mvulana huyo alimwambia kwamba yeye na familia yake hawasherehekei siku za kuzaliwa kwa sababu wao ni Mashahidi wa Yehova. Mvulana huyo pia alimwambia kwamba alikuwa akipokea zawadi nyakati nyinginezo mwakani naye hakukosa chochote, kwa kuwa alikuwa na familia changamfu sana na yenye upendo. Hakuna zawadi zinazolingana na hayo, yeye akaongezea.
Mvulana huyo alirudi na babu yake mara kadhaa. Kila wakati, mtu huyo angemuuliza mvulana huyo maswali mengi sana, naye alipendezwa sana na jinsi mvulana huyo alivyotoa majibu manyoofu, na ya moja kwa moja bila kusitasita. Pia yeye alivutiwa na uthamini wa mvulana huyo wa mambo ya maana. Usiku mmoja baada ya mtu huyo kutazama programu ya televisheni iliyoonyesha hali mbaya sana ulimwenguni, alitambua kwamba alipaswa kuchunguza mambo ya kiroho kwa makini zaidi. Akampigia simu Shahidi aliyejifunza pamoja na mkeye akamwomba arudi. Baada ya muda mfupi mtu huyo alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Shahidi fulani, na akafanya maendeleo haraka. Alibatizwa katika Aprili 10, 1994. Mkeye pia amebatizwa sasa.
Ukuzi Huhitaji Ujenzi
Sweden ni makao ya wakimbizi wengi kutoka nchi nyinginezo, nao Mashahidi Wasweden wamepata matokeo mazuri katika kuwahubiri. Kwa ujumla kazi imefanikiwa hivi kwamba Majumba ya Ufalme mapya yamehitajiwa kwa ajili ya mpanuko. Kuanzia 1986 hadi 1993, Majumba ya Ufalme 37 yalijengwa kwa njia ya ujenzi wa haraka, huku majumba 8 yakipanuliwa na kurekebishwa upya. Katika 1994 pekee, Majumba ya Ufalme saba zaidi yalijengwa, na matatu yakarekebishwa upya.
Kwa sasa, kuna makutaniko 65 yanayongoja msaada wa kujenga Jumba la Ufalme jipya au kupanua au kurekebisha upya walilo nalo. Wajitoleaji karibu 2,500 husaidia katika kazi hizo za ujenzi, nayo makutaniko huthamini sana msaada wao wenye upendo.
Upande wa kaskazini wa Sweden, uliopanuka juu ya Kizio cha Aktiki, nyakati nyingine huitwa nchi ya jua la usiku wa manane. Hii ni kwa sababu wakati wa sehemu ya kiangazi jua halitui huko. Hata hivyo, katika Sweden yote, mwangaza wa kweli pia unaendelea kung’aa sana. Kwa baraka ya Yehova, mwangaza huo wa kiroho hautafifia kamwe bali utaendelea kung’aa zaidi na zaidi.
[Sandukupage 8]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1994
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 24,246
UWIANO: Shahidi 1 kwa Watu 362
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 40,372
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 2,509
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 11,306
IDADI YA WALIOBATIZWA: 850
IDADI YA MAKUTANIKO: 358
OFISI YA TAWI: ARBOGA
[Picha katika ukurasa wa9]
Ofisi ya tawi na Makao ya Betheli katika Arboga
[Picha katika ukurasa wa9]
Mashahidi wa mapema katika Hjo walitumia hili basi dogo kuhubiri eneo la kilometa 5,000 za mraba.