Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 6/1 kur. 20-25
  • Tulipewa Lulu ya Thamani ya Juu Sana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tulipewa Lulu ya Thamani ya Juu Sana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tukio la Kukumbukwa
  • Utamaduni Mpya
  • Kujifunza Kihispania na Kuanza Kazi
  • Mitihani ya Mapema Katika Madrid
  • Maono Mazuri Ajabu Katika Madrid
  • Huduma Yenye Matokeo Pamoja na Mwanajeshi
  • Funzo la Biblia Lisilo la Kawaida
  • Mwaliko wa Kushangaza
  • Kulazimika Kuacha Mgawo Wetu wa Mishonari
  • Kuhubiri Katikati ya Dawa za Kulevya na Jeuri
  • Uamuzi Mgumu
  • “Kwa Kuwa Tuna Huduma Hii . . . , Hatuachi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Maisha Yenye Mambo Yasiyotazamiwa Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • ‘Wenye Furaha Ni Wale Wanaoendelea Kumngoja Yehova’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Madrid Jiji Kuu Lililojengwa kwa Ajili ya Mfalme
    Amkeni!—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 6/1 kur. 20-25

Tulipewa Lulu ya Thamani ya Juu Sana

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RICHARD GUNTHER

Ilikuwa Septemba 1959. Tulikuwa katika meli ya Italia iitwayo, Julio Caesar tukivuka Bahari ya Atlantiki kutoka New York hadi Cádiz, Hispania. Watch Tower Society ilikuwa imenipa mgawo, nikiwa na mke wangu, Rita, pamoja na Paul na Evelyn Hundertmark, wenzi wa ndoa wengine, katika nchi hiyo ya Iberia. Tulikuwa tukienda kukabili magumu mengi. Lakini ilikuwaje kwamba tulianza kazi ya mishonari?

RITA na mimi tulibatizwa kuwa Mashahidi wa Yehova katika 1950 katika New Jersey, Marekani. Muda mfupi baadaye, tulifanya uamuzi ambao baada ya muda ungeweka mikononi mwetu lulu ya thamani ya juu sana. Tulikuwa katika kutaniko lenye ndugu na dada wengi wa kutosha kutumikia eneo hilo. Hivyo tulihisi kuwajibika kujitolea kutumika mahali palipokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri. Kwenye kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova katika New York City katika kiangazi cha 1958, tulifanya ombi la utumishi wa mishonari.

Muda mfupi baadaye, tulialikwa Watchtower Bible School of Gilead, na katika kipindi cha mwaka mmoja tulikuwa tukisafiri kuelekea Hispania tukiwa wamishonari. Tukiwa tumehusika sana katika mipango mingi na kujawa na msisimuko, hatukutambua wakati huo kile tulichokuwa tumepewa. Yesu alikuwa amezungumza juu ya lulu ya thamani ya juu sana. (Mathayo 13:45, 46) Ingawa pendeleo letu la mishonari halikuwa ndilo maana ya mfano wake, pendeleo letu la kutumika tukiwa wamishonari kwetu lililingana na lulu hiyo. Tutazamapo nyuma, sasa tunathamini zaidi sana zawadi hii ya utumishi yenye thamani katika tengenezo la Yehova.

Tukio la Kukumbukwa

Wakati huo mtaala wa mishonari wa Gileadi ulikuwa ukifanywa katika maeneo ya mashambani yenye kupendeza katika eneo la Finger Lakes la Jimbo la New York. Huko, tulitumia miezi sita ya ajabu tukijihusisha kabisa katika funzo la Biblia na uhusiano wa Kikristo ulio kwelikweli, tukiwa tumetengwa kutoka kwa mambo na matatizo ya ulimwengu huu. Wanafunzi wenzetu walikuwa wametoka sehemu nyingi za ulimwengu, kutia ndani Australia, Bolivia, New Zealand, Ugiriki, na Uingereza. Hata hivyo, siku ya kuhitimu ilifika haraka. Katika Agosti 1959, tuliagana tukiwa na machozi machoni tulipoanza kuabiri kuelekea migawo yetu ya mishonari. Mwezi mmoja baadaye tulifika Hispania.

Utamaduni Mpya

Tulitua katika bandari ya Algeciras iliyo upande wa kusini, kando ya Mwamba wa Gibraltar ulio mkubwa. Usiku huo sote wanne, Rita, na mimi pamoja na akina Hundertmark, tukapanda gari-moshi kuelekea Madrid. Tulienda Hotel Mercador, tungojee hapo hadi washiriki wa ofisi ya tawi ya siri ya Sosaiti wawasiliane na sisi. Hispania ilikuwa chini ya utawala wa kimabavu wa Generalissimo Francisco Franco. Hii ilimaanisha kwamba dini iliyotambuliwa kisheria ilikuwa Kanisa Katoliki ya Kiroma peke yalo. Ilikuwa kinyume cha sheria kuendesha dini nyingine peupe, na kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku. Hata mikutano ya kidini ilikuwa imekatazwa, hivi kwamba Mashahidi wa Yehova, wapatao 1,200 katika makutaniko 30 katika Hispania wakati huo, hawangeweza kukutanika katika Majumba ya Ufalme kama ilivyokuwa katika nchi nyinginezo. Ilibidi tukutane kisiri katika nyumba za watu binafsi.

Kujifunza Kihispania na Kuanza Kazi

Tatizo letu la kwanza lilikuwa kujifunza lugha. Mwezi wa kwanza tulitumia muda wa saa 11 kila siku tukijifunza Kihispania—muda wa saa 4 kila asubuhi darasani, halafu muda wa saa 7 tukijifunza peke yetu. Mwezi wa pili ilikuwa vivyo hivyo asubuhi, lakini alasiri zilitumiwa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Waweza kuwazia? Tukiwa bado hatujaijua lugha hiyo na tukiwa na maelezo ya msingi yaliyokaririwa yaliyokuwa yameandikwa kwenye kikaratasi, Rita na mimi tulienda katika kazi ya nyumba kwa nyumba peke yetu!

Nakumbuka nikibisha mlango katika Vallecas, sehemu ya Madrid iliyokaliwa na wafanyakazi. Nikiwa nimeshika kikaratasi changu mkononi, nisije nikasahau la kusema, nikasema kwa Kihispania: “Habari ya asubuhi. Tunafanya kazi ya Kikristo. Biblia husema (tungesoma andiko). Tungependa upate kijitabu hiki.” Mwanamke huyo alitazama tu, kisha akachukua kijitabu hicho. Tulipofanya rudio, alitukaribisha ndani, na tulipokuwa tukizungumza, yeye alitazama tu. Tulianzisha funzo la Biblia kwa kadiri tulivyoweza, na wakati wa mafunzo, yeye alitazama na kusikiliza tu. Baada ya muda mwishowe alituambia kwamba hakuwa ameelewa tuliyokuwa tumesema katika ziara yetu ya kwanza lakini alikuwa amesikia neno Dios (Mungu) na kwamba hili lilitosha kumjulisha kwamba kilikuwa kitu kizuri. Baada ya muda, alitwaa ujuzi mwingi sana wa Kibiblia akabatizwa, na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Kujifunza Kihispania kulikuwa kugumu sana kwangu. Nilipokuwa nikisafiri jijini, nilizoea kukariri viunganishi-kitenzi. Yale niliyokariri juma moja niliyasahau juma lililofuata! Ilinivunja moyo sana. Mara kadhaa karibu niache kujifunza. Kwa kuwa nilizungumza Kihispania kibaya sana, ilibidi ndugu Wahispania kuwa wenye subira sana nilipokuwa nikichukua uongozi miongoni mwao. Kwenye mkusanyiko mmoja wa wilaya, ndugu fulani alinipa tangazo lililokuwa limeandikwa kwa mkono nisome kwenye jukwaa. Nikiwa natatizika kusoma maandishi yake, nilitangaza: “Leteni muletas (mikongojo) yenu katika stediamu kesho.” Lilipaswa liwe, “Leteni maletas (mizigo) yenu katika stediamu kesho.” Bila shaka umati ukacheka, na kama ilivyo kawaida niliaibika.

Mitihani ya Mapema Katika Madrid

Hiyo miaka michache ya kwanza katika Madrid ilikuwa migumu sana kihisia-moyo kwa Rita na mimi. Tulitamani nyumbani kwetu na marafiki zetu sana. Kila wakati tulipopokea barua kutoka Marekani, tungehisi kukosa nyumbani sana. Hivyo vipindi vya kukosa nyumbani vilikuwa vigumu sana, lakini vilipita. Kwani, tulikuwa tumeacha nyumba, familia, na marafiki ili tupokee lulu ya thamani ya juu sana. Tulihitaji kujipatanisha na hali.

Tulipofika Madrid mara ya kwanza, tulikuwa tukiishi katika nyumba ya wageni iliyokuwa ovyo sana. Tulikuwa na chumba chetu na milo mitatu kwa siku. Kilikuwa chumba kidogo chenye giza, na magodoro yalikuwa ya majani. Kodi ya nyumba katika mwezi ilichukua rudishio letu dogo la fedha lote. Kwa kawaida tulikuwa tukipata chakula cha mchana hapo kwenye nyumba ya wageni, na mwanamke mwenye mahali hapo alikuwa akiacha chakula chetu kwenye jiko kukipasha joto ili kwamba usiku sana tungekuwa na kitu cha kula. Hata hivyo, tulipokuwa tukitembea barabarani tukiwa katika kazi ya kuhubiri mchana na jioni, tulikuwa tukihisi njaa sana. Ikiwa tungeishiwa na rudishio la fedha, tungetumia pesa zetu chache za binafsi kununua chokoleti ya bei ya chini kabisa tuliyoweza kupata. Hata hivyo, mwangalizi wa Sosaiti wa kanda ya dunia alipotutembelea, upesi hali hii ilibadilika. Aliona shida yetu naye akasema kwamba tutafute jengo dogo ili litumike kuwa makao ya mishonari. Tukiwa na nyumba yetu wenyewe ingekuwa bora zaidi kuliko kuoga tukiwa tumesimama tukitumia beseni kwenye sakafu jikoni. Sasa tungeweza kuoga kwa maji ya juu, na kuwa na friji ya kuweka chakula, na jiko la stima ambalo tungepikia chakula chetu. Tulishukuru sana kwa hali yetu kufikiriwa.

Maono Mazuri Ajabu Katika Madrid

Kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilifanywa kwa busara nyingi sana. Shughuli za kila siku katika Madrid zilitusaidia, zikitufunika ili tusitokeze sana. Tulijaribu kuvalia na kutenda kama wengine ili kwamba tusionekane kuwa wageni. Njia yetu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilikuwa kuingia katika jengo, kubisha mlango, kuzungumza na mtu, kisha kuondoka jengo hilo, barabara, na eneo hilo. Kila wakati kulikuwa na uwezekano kwamba mwenye nyumba angeita polisi, na hivyo basi halikuwa jambo la hekima kukaa katika ujirani huo. Kwa kweli, ingawa walikuwa wenye busara katika kutumia njia hii, Paul na Evelyn Hundertmark walishikwa na kufukuzwa kutoka nchi hiyo katika 1960. Walienda nchi jirani ya Ureno, wakitumika huko kwa miaka kadhaa, Paul akitumikia ofisi ya tawi ya siri. Leo yeye ni mwangalizi wa jiji katika San Diego, California.

Hata hivyo, kwetu sisi usawaziko ulitokea. Miezi michache tu baadaye, wamishonari sita waliopewa mgawo wa kwenda Ureno waliamuriwa waondoke nchi hiyo! Jambo hilo lilileta mambo mazuri kwa sababu Eric na Hazel Beveridge, waliokuwa katika darasa letu la Gileadi, sasa waliagizwa watoke Ureno na kuja Hispania. Kwa hiyo katika Februari 1962, mara nyingine tena tulienda Hotel Mercador—wakati huu kuwakaribisha Eric na Hazel walipofika.

Ilikuwa katika hizo siku za mapema katika Madrid ambapo Rita na mimi tulipata ono la kwanza la unafiki wa kidini. Tulijifunza Biblia na wenzi wa ndoa fulani, Bernardo na Maria, walioishi kwenye kibanda kilichojengwa kwa visehemu vyovyote vya mabaki ya vifaa vya kujenga ambavyo Bernardo angeweza kupata. Tulijifunza nao usiku sana, na baada ya funzo, walizoea kutupatia mkate, divai na jibini au chochote walichokuwa nacho. Niliona kwamba jibini hiyo ilikuwa tu kama jibini ya Marekani. Usiku mmoja baada ya funzo, walileta mkebe ambao jibini hiyo ilikuwa imewekwa. Ulikuwa umeandikwa kwa maandishi makubwa, kwa Kiingereza, “Kutoka kwa watu wa Marekani kwa watu wa Hispania—isiuzwe.” Familia hii maskini ilipataje jibini hiyo? Kanisa Katoliki lilitumiwa na serikali kuigawa kwa maskini. Lakini kasisi alikuwa akiiuza!

Huduma Yenye Matokeo Pamoja na Mwanajeshi

Baada ya muda mfupi jambo fulani la ajabu lilitokea ambalo lingekuja kuwa baraka kwetu na kwa wengine wengi. Tulipokea barua kutoka ofisi ya tawi ikituomba tumtembelee kijana mmoja kwa jina Walter Kiedaisch, aliyekuwa akiishi katika kituo cha Wanahewa wa Marekani katika Torrejón, kilichokuwa kilometa chache nje ya Madrid. Tuliwatembelea yeye na mkeye, tukaanzisha funzo la Biblia pamoja nao na wenzi wa ndoa wengine wa Wanahewa huko.

Wakati huo, nilikuwa nikiongoza karibu mafunzo ya Biblia matano pamoja na Wanahewa wa Marekani, bila shaka, wote kwa Kiingereza. Kati yao, saba baadaye walibatizwa, na baada ya kurudi Marekani, wanne wa watu hao wakawa wazee wa kutaniko.

Huu ulikuwa wakati ambapo ilikuwa vigumu sana kuingiza vitabu, magazeti, na Biblia nchini kwa sababu ya marufuku ya kazi yetu. Hata hivyo, fasihi fulani iliingizwa na watalii na watu wale waliokuwa wakileta vichapo kutoka Marekani. Nilipewa mgawo na tawi kuendesha depo ya siri ya fasihi. Ilikuwa katika chumba cha akiba nyuma ya duka la kuuza vifaa vya ofisi katika Vallecas. Mke wa mwenye duka hilo alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ingawa mwenye duka hilo hakuwa Shahidi, aliheshimu kazi yetu, na hata kwa kujihatarisha sana na kuhatarisha biashara yake, aliniruhusu kutumia mahali hapo nyuma kutayarisha vifurushi vya fasihi kuvipeleka majijini nchini kote. Kwa kuwa chumba hiki sikuzote kilipaswa kuonekana kama kilivyopaswa kuwa—chumba chenye vumbi jingi, shaghala-baghala kilichojaa makatoni—ilinibidi kujenga ubao wa kufanyia kazi na maktaba ya vitabu ambavyo vingesimamishwa tayari kufanyiwa kazi haraka na kufunikwa haraka sana. Mwishoni mwa siku, ningengoja hadi watu wote waondoke dukani kisha niondoke haraka na vifurushi vyangu.

Lilikuwa pendeleo kwelikweli kushiriki katika kugawa fasihi ya mambo ya kiroho, kama vile magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na fasihi nyingineyo, kwa makutaniko nchini kote. Hizo zilikuwa nyakati zenye kusisimua.

Rita alipata shangwe ya kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 16, ambao karibu nusu yao wakawa Mashahidi wa Yehova waliobatizwa. Dolores alikuwa mwanamke mchanga aliyeolewa aliyetumia nyakati za baridi za kipupwe kitandani kwa sababu ya tatizo la moyo. Katika nyakati za kuisha kwa kipupwe angeamka na kuwa mwenye nguvu kiasi fulani. Imani ya Dolores ilikuwa yenye nguvu, kwa hiyo wakati ulipofika wa mkusanyiko wetu wa wilaya katika Toulouse, Ufaransa, alitaka sana kwenda. Alitahadharishwa na daktari kwamba haingekuwa hekima kwa sababu ya hali ya moyo wake. Akiwa amevalia nguo ya kawaida na sapatu bila mzigo, alienda kwenye kituo cha gari-moshi kuwaaga mumeye, mama yake, na wengine. Machozi yakimtoka, hakuvumilia kuwaona wakienda bila yeye, hivyo akapanda gari-moshi, na kusafiri hadi Ufaransa! Rita hakujua kwamba hili lilikuwa limefanyika. Lakini huko mkusanyikoni, alistaajabu kama nini alipomwona Dolores, akitabasamu sana!

Funzo la Biblia Lisilo la Kawaida

Hatuwezi kumaliza simulizi hili la mgawo wetu wa Madrid bila kutia ndani Don Benigno Franco, “el profesor.” Shahidi wa mahali hapo alinipeleka kumtembelea mwanamume mmoja mzee-mzee aliyekuwa akiishi na mkeye katika jengo moja la watu maskini. Nilianzisha funzo la Biblia pamoja naye. Baada ya kujifunza kwa karibu mwaka mmoja na nusu, aliomba abatizwe na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Mwanamume huyu mzee-mzee, Don Benigno Franco, alikuwa binamu wa Francisco Franco, aliyekuwa mtawala wa kimabavu wa Hispania wakati huo. Inaonekana kwamba Don Benigno sikuzote alikuwa mtu mwenye kupenda uhuru. Wakati wa Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Hispania, alihurumia chama cha Republic na kumpinga binamu yake—Jenerali aliyeshinda vita hiyo na kuanzisha utawala wa kimabavu wa Kikatoliki. Daima tangu 1939, Don Benigno alikuwa amenyimwa haki ya kuajiriwa, naye alikuwa na mapato kidogo sana. Kwa hiyo ikawa kwamba binamu ya Generalissimo Francisco Franco, mtawala wa kimabavu wa Hispania, alikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Mwaliko wa Kushangaza

Katika 1965 ofisi ya tawi ya Hispania ilitualika kuanza kusafiri katika kazi ya mzunguko katika Barcelona. Hii ilimaanisha kuwaacha ndugu wote wapendwa ambao tulikuwa na ukaribu sana nao katika Madrid. Sasa tulikuwa tuanze si ono jipya tu bali pia, mtihani, kwangu. Ono hilo lilikuwa lenye kutisha kwa sababu sikuzote nilitilia shaka uwezo wangu. Najua vizuri sana kwamba ilikuwa ni Yehova aliyeniwezesha kuwa na matokeo katika eneo hili la utumishi.

Kutembelea kutaniko kila juma kulimaanisha kuishi nyumba mbalimbali za akina ndugu. Hatukuwa na makao kamili, na karibu kila majuma mawili, tulihamia nyumba nyingine. Jambo hili hasa ni gumu kwa mwanamke. Lakini baada ya muda mfupi José na Roser Escudé, walioishi Barcelona, walitualika kukaa nao kwa siku kadhaa zenye kufuatana kila wakati. Hili lilikuwa jambo la upendo sana kwa upande wao, kwa kuwa lilimaanisha kwamba tungekuwa na mahali pa kudumu pa kuweka vitu vyetu na mahali pa kawaida kurudi nyumbani jioni za Jumapili.

Rita na mimi tulitumia miaka minne iliyofuata katika kazi ya mzunguko katika mkoa wa Katalonia, uliokuwa kwenye Pwani ya Mediterania. Mikutano yetu yote ya Biblia ilifanywa kisiri katika nyumba za binafsi, na mahubiri yetu ya nyumba kwa nyumba pia yalifanywa kwa busara ili tusivute fikira za watu. Nyakati nyingine kutaniko lote lilikusanyika pamoja Jumapili kwa “mandari” misituni, hasa tulipokuwa tukifanya kusanyiko la mzunguko.

Sikuzote tutawaheshimu ndugu wengi wenye kujitoa waliohatarisha kazi na uhuru wao, wakijikakamua kuweka makutaniko yakiwa yameungamana na yenye kutenda. Wengi wao waliongoza katika kupanua kazi katika miji nje ya jiji. Hii ilifanyiza msingi wa ongezeko kubwa katika Hispania baada ya marufuku kuondolewa na kupewa uhuru wa kidini katika 1970.

Kulazimika Kuacha Mgawo Wetu wa Mishonari

Wakati wa miaka yetu kumi katika Hispania, kufurahia kwetu baraka hii ya pekee ya kutumikia Yehova kulikuwa kumevurugwa na hali ya wazazi wetu. Pindi kadhaa, tulikuwa karibu kuacha mgawo wetu na kurudi nyumbani kuwatunza mama na baba yangu. Hata hivyo, kwa ajili ya ndugu na dada wenye upendo katika makutaniko yaliyo karibu na wazazi wetu, tuliweza kuendelea katika Hispania. Ndiyo, pendeleo la kutumika miaka hiyo katika kazi ya mishonari liliwezekana kwa sehemu kwa sababu ya wengine walioshiriki nasi katika kuweka masilahi ya Ufalme wa Mungu kwanza.

Mwishowe, katika Desemba 1968, tulienda nyumbani kumtunza mama yangu. Mwezi huohuo baba yangu akafa, na sasa mama yangu akawa ameachwa peke yake. Bado tukiwa na uhuru wa kiasi fulani kutumika wakati wote, tulipokea mgawo kutumika katika kazi ya mzunguko, lakini wakati huu katika Marekani. Kwa miaka 20 iliyofuata, tulitumika katika mizunguko ya Kihispania. Ingawa tulikuwa tumepoteza lulu ya thamani ya juu ya mishonari, tulikuwa na nyingine iliyowekwa mikononi mwetu.

Kuhubiri Katikati ya Dawa za Kulevya na Jeuri

Sasa tulikuwa tukitumika pamoja na ndugu na dada wengi waliokuwa wakiishi katika sehemu zilizojaa jeuri jijini. Lile juma la kwanza katika kazi ya mzunguko katika Brooklyn, New York, Rita alinyang’anywa mfuko wake wa vitabu.

Katika pindi moja Rita na mimi tulikuwa pamoja na kikundi tukishiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba katika sehemu nyingine ya New York City. Tulipopiga kona, tuliona watu fulani wakiwa wamepiga mstari mbele ya shimo fulani katika ukuta wa jengo tupu lililoachwa. Tulipopiga hatua chache barabarani, tuliona kijana fulani akisimama kando ya njia akitutazama. Kulikuwa na mwingine mbali kwenye kona akichungulia magari ya polisi. Tulikuwa tumetembea katikati ya kituo cha ulanguzi wa dawa za kulevya! Mchunguliaji wa kwanza alishtuka, kisha akaona gazeti la Mnara wa Mlinzi naye akatulia. Hata hivyo, ningalikuwa polisi! Kisha akapaza sauti kwa Kihispania, “¡Los Atalayas! ¡Los Atalayas!” (Minara ya Mlinzi! Minara ya Mlinzi!) Walitujua, wakitutambua kwa sababu ya gazeti, na kila kitu kikawa sawa. Nilipopita karibu naye, nilisema, “¿Buenos dias, como está?” (Habari ya asubuhi, u hali gani?) Yeye alijibu kwa kuniambia nimwombee!

Uamuzi Mgumu

Katika 1990 ilionekana kwamba ingenibidi kuwa na mama yangu kila siku. Tulikuwa tumejaribu sana kubaki katika kazi ya mzunguko, lakini kwa hekima tuliona kwamba haikuwezekana kutimiza madaraka yote mawili. Tulitaka kuwa na hakika kwamba mama alitunzwa kwa upendo. Lakini mara nyingine tena ilitubidi kuacha lulu ya thamani ya juu sana, kitu kilichokuwa chenye thamani sana kwetu. Vito vyote halisi ulimwenguni na yote viwezavyo kumfanyia mtu ni machache sana yakilinganishwa na vito vya kutumika ukiwa mishonari au ukiwa mwangalizi asafiriye katika tengenezo la Yehova.

Rita na mimi sasa tumo katika miaka yetu ya 60. Tumeridhika sana nasi twaona shangwe kutumika pamoja na kutaniko la hapa la Kihispania. Tutazamapo miaka yetu ya nyuma katika utumishi wa Yehova, twamshukuru kwa kutukabidhi lulu za thamani ya juu sana.

[Picha katika ukurasa wa23]

Nikiwa pamoja na Rita na Paul na Evelyn Hundertmark (kulia) nje ya uwanja wa mchezo wa kupigana na fahali katika Madrid

[Picha katika ukurasa wa24]

Tukitumikia kutaniko moja kwenye “mandari” misituni

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki