‘Wenye Furaha Ni Wale Wanaoendelea Kumngoja Yehova’
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA DOMENICK PICCONE
Wazazi wangu walihama Italia kwenda United States miaka ya mapema ya 1920 na hatimaye wakakaa Filadelfia Kusini, iliyojulikana wakati huo kuwa Italia Ndogo. Kufikia 1927 walikuwa wakishirikiana na wanafunzi wa Biblia ambao baadaye walijulikana kuwa Mashahidi wa Yehova.
NILIZALIWA katika 1929 na hivyo kweli ya Biblia ikawa inapatikana kwangu tangu utoto. Naweza kukumbuka kwamba Mashahidi walikuwa wakikutana nyumbani mwetu kabla ya kwenda mahubiri katika miji ilioko katika eneo la Pennsylvania la kuchimbia makaa-mawe iliyoshikilia sana imani ya Katoliki ya Kiroma, ambako ndugu walikamatwa mara nyingi. Nilibatizwa katika 1941 kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika St. Louis, Missouri. Halafu mambo yakaanza kuharibika.
Nilianza kushirikiana na vijana wabaya katika ujirani na kuanza kuvuta sigareti na kucheza kamari kwenye kona za barabara. Kwa furaha, wazazi wangu waliona kwamba walikuwa wakishindwa kunidhibiti wakaamua kuhamia eneo jingine la jiji. Sikufurahi, kwa kuwa nilipoteza marafiki wangu wote wa barabarani. Hata hivyo, ninapokumbuka yaliyotukia namshukuru sana baba yangu. Kwa kweli alitoa dhabihu ya kifedha ili kuniondoa katika mazingira hayo. Ingawa mbeleni aliweza kwenda kazini kwa miguu, sasa alilazimika kusafiri mwendo mrefu kwa gari-moshi inayopita chini ya ardhi. Lakini kuhama huko kulinirudisha ndani ya mazingira ya kitheokrasi.
Mbegu ya Misionari Yapandwa
Karibu kila mwaka tulisafiri kwenda South Lansing, New York, kuhudhuria kuhitimu kwa Watchtower Bible School of Gilead. Kuona wamisionari hao wakitumwa kotekote ulimwenguni kulipanda moyoni mwangu tamaa ya utumishi wa misionari. Kwa hiyo, baada ya kuhitimu shule ya sekondari, nilijiandikisha kuwa mhudumu painia wa kawaida, kuanzia Mei 1947.
Paina mwingine mchanga katika kundi letu alikuwa Elsa Schwarz, naye alikuwa mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Wazazi wake walikuwa wamemtia moyo sikuzote awe misionari, kwa hiyo yaelekea waweza kukisia tokeo. Tulioana katika 1951. Tulipokuwa tukitumikia pamoja tukiwa mapainia huko Pennsylvania, tulipeleka maombi ya kuhudhuria shule ya misionari ya Gileadi. Katika 1953 tulialikwa kwenye darasa la 23 la Gileadi. Baada ya miezi mitano ya kujifunza na kujitayarisha sana katika Gileadi, tulihitimu kwenye mkusanyiko huko Toronto, Kanada, na kupokea mgawo wetu—Hispania!
Matatizo Katika Hispania
Tulipokuwa tukijitayarisha kwenda kwenye mgawo wetu wa misionari katika 1955, Elsa nami tulikuwa na maswali mengi. Hispania! Ingekuwaje? Taifa lilikuwa chini ya utawala wa Kamanda Mkuu Francisco Franco dikteta Mkatoliki, na kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku. Tungekabilianaje na hali hizo?
Tulikuwa tumearifiwa na ndugu kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn kwamba Frederick Franz aliyekuwa wakati huo makamu wa msimamizi wa Watch Tower Society, na Alvaro Berecochea, misionari kutoka Argentina, pamoja na ndugu wengine walikuwa wamekamatwa. Kusanyiko la siri lilikuwa limepangwa msituni karibu na Barcelona. Hata hivyo, polisi walipata kujua kuhusu kusanyiko hilo la siri nao walikuwa wamekamata wengi wa wale waliokuwapo.a
Tulikuwa tumeambiwa kwamba labda hakuna yeyote ambaye angeweza kutulaki tuwasilipo Barcelona. Maagizo yetu yalikuwa: “Tafuteni mahali pa kukaa hotelini, kisha arifuni Sosaiti katika New York kuhusu anwani ya hoteli hiyo.” Tulikumbuka maneno ya Isaya: “Heri [wenye furaha, NW] wote wamngojao [wanaoendelea kumngoja, NW] [Yehova]. na masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni.” (Isaya 30:18, 21) Tungepaswa kuendelea tu kumngojea Yehova na kufuata mwelekezo wa tengenezo lake.
Tuliagana na wazazi na marafiki wetu waliokuja New York kutuaga, na baada ya muda mfupi meli yetu, Saturnia, ikawa ikisafiri kwenye Mto Hudson kuelekea Bahari Atlantiki. Huo ulikuwa wakati wangu wa mwisho kumwona baba yangu. Miaka miwili baadaye, nilipokuwa ng’ambo, alikufa baada ya ugonjwa wa muda mrefu.
Hatimaye tulifika kwenye mgawo wetu, Barcelona jiji la bandari. Ilikuwa siku mbaya, yenye mvua nyingi, lakini tulipokuwa tukipitia sehemu ya forodha, tuliona “kianga” cha nyuso zenye kutabasamu kwa shangwe. Alvaro Berecochea, pamoja na ndugu wengine Wahispania, alikuwa hapo kutulaki. Tulifurahi sana kujua kwamba ndugu zetu walikuwa wamewekwa huru.
Sasa wakati wa kujifunza Kihispania ukafika. Siku hizo wamisionari walilazimika kujifunza lugha kwa njia ngumu—bila vitabu vya kujifunzia wala walimu. Mitaala ya lugha haikuwako wakati huo. Tulipaswa tutimize saa zilizotakiwa katika kazi ya kuhubiri na wakati ule ule—kujifunza ile lugha.
Kuhubiri Chini ya Udikteta wa Kikatoliki
Wakati huo tengenezo la Yehova lilikuwa likianza-anza tu katika Hispania. Katika 1955 kulikuwako kilele cha wahubiri 366 katika nchi yenye watu milioni 28. Kulikuwako makundi kumi tu katika nchi nzima. Je, ingeendelea hivyo kwa muda mrefu? Mara mke wangu nami tulipoanza kuhubiri nyumba kwa nyumba, tulipata kwamba Hispania ilikuwa kama paradiso ya kuenezea habari njema. Naam, watu walikuwa na njaa kwa ajili ya kweli.
Lakini kazi ya kuhubiri ilifanywaje, kwa kuwa ilikuwa imepigwa marufuku? Kwa kawaida hatukutembelea kila nyumba kwenye barabara moja, wala nyumba zote katika jengo moja. Barcelona ina majengo mengi yenye orofa tano na sita, nasi tuliagizwa tuanzie orofa ya juu kabisa na kisha kuendelea na za chini. Tulikuwa tunatembelea labda nyumba moja tu kwenye kila orofa au hata kuacha orofa kadhaa. Njia hiyo ilifanya iwe vigumu zaidi kwa polisi kutukamata ikiwa mwenye nyumba mshupavu aliarifu polisi juu yetu.
Mikutano ya kundi ilifanywa katika nyumba za faragha, makundi yakiwa na vikundi vya mafunzo vitatu hadi vinne. Hilo lilimwezesha mtumishi wa kundi atembelee kila moja ya mafunzo hayo ya kitabu mara moja kwa mwezi. Kiongozi wa funzo la kitabu alikuwa na daraka la kuongoza mikutano yote, yaliyofanywa siku mbili tofuati za juma kwa vikundi vya watu 10 hadi 20.
Tulilazimika kujifunza njia mpya ya maisha. Wakati huo mipango ya nyumba ya misionari haikuwako katika Hispania. Ilipowezekana, tuliishi pamoja na ndugu katika nyumba zao. Kujifunza kupika kwa jiko la makaa lilikuwa tatizo kubwa kwa Elsa! Hatimaye tuliweza kununua jiko dogo la mafuta ya taa, hali ikawa bora zaidi.
Mnyanyaso na Kufukuzwa Nchini
Baada ya muda mfupi tulisikia kwamba wimbi la mnyanyaso lilikuwa likianza katika Andalusia, ambako painia wa pekee alikuwa amekamatwa. Kwa kusikitisha, alikuwa akibeba kijitabu kilichokuwa na majina na anwani za ndugu katika sehemu zote za nchi. Tuliendelea kupokea ripoti kwamba ndugu zetu walikuwa wakikamatwa katika jiji moja baada ya jingine. Uvamizi huo wa ghafula wa maofisa wa sheria ulikuwa ukikaribia Barcelona zaidi na zaidi. Mwishowe, mnyanyaso ukafika Barcelona.
Miezi michache mapema kidogo, polisi walikuwa wamenipeleka kwenye makao makuu kunihoji. Baada ya saa kadhaa niliachiliwa, nami nikafikiri kwamba mambo yalikuwa yameishia hapo. Kisha Ubalozi wa Amerika uliwasiliana nami na kudokeza kwamba ili niepuke aibu ya kurudishwa nyumbani, ingefaa niondoke nchini kwa hiari yangu. Muda mfupi baadaye, polisi walituarifu kwamba tulipaswa kuondoka nchini katika muda wa siku kumi tu. Kwa sababu hatukuwa na wakati wa kuandikia Watch Tower Society, tungepaswa kufanyaje? Hali zilionekana kudokeza kwamba tungepaswa kuelekea shamba la umisionari nje ya Hispania lililokuwa karibu zaidi—Ureno, upande wa magharibi.
Mgawo Mwingine Lugha Nyingine
Mara tulipofika Lisbon, Ureno, katika Julai 1957, tulipewa mgawo kuwa wamisionari katika Porto, mji ulio kaskazini kabisa mwa Lisbon. Lilionwa kuwa jiji kuu la pili la nchi nalo lilikuwa katika eneo mashuhuri kwa sababu ya divai nyekundu yalo aina ya port. Kundi lenye kusitawi lilifanya mikutano yalo katika chumba cha chini cha jengo lililokuwa mjini. Kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku katika Ureno pia, kwa kuwa nchi ilikuwa chini ya udikteta wa Salazar. Hata hivyo hali zilikuwa tofauti kabisa na zile za Hispania. Mikutano ilifanywa nyumbani mwa ndugu, na vikundi vya watu 40 hadi 60 vilihudhuria. Hakukuwa ishara zozote kwamba nyumba hizo zilikuwa mahali pa kukutania pa Mashahidi wa Yehova. Hata ingawa sikusema Kireno hata kidogo, niliwekwa kuwa mtumishi wa kundi. Mara nyingine tena, tulijifunza lugha mpya kwa njia ngumu.
Karibu mwaka mmoja baadaye, tulipewa mgawo kwenda Lisbon. Hapo, kwa mara ya kwanza, tulikuwa na mahali petu wenyewe pa kukaa, nyumba ambayo kutoka juu yayo tungeweza kuona jiji la Lisbon. Tulipewa mgawo tutumikie mzunguko—Jamhuri nzima ya Ureno. Tulipowasili Ureno, kulikuwako wahubiri 305 na makundi matano tu.
Wakati wa Matatizo Waanza
Kwenye ramani nyingine zinazoonyesha Ureno na koloni zayo, kulikuwako ule msemo: “Jua halishuki kamwe katika maeneo ya Ureno.” Hiyo ilikuwa kweli, kwa kuwa Ureno ilikuwa na koloni katika sehemu nyingi za ulimwengu, mbili kubwa zaidi kati yazo zikiwa Msumbiji na Angola katika Afrika. Katika 1961 ilionekana kwamba matatizo yalikuwa yakianza katika koloni hizo, na Ureno iliona uhitaji wa kuongeza majeshi yayo.
Sasa, ndugu vijana wangefanya nini walipoandikishwa katika utumishi wa kijeshi? Wengine waliweza kuachiliwa kwa sababu ya afya mbaya, lakini walio wengi walichukua msimamo imara wa kutokuwamo kwa Kikristo. Upesi wimbi la mnyanyaso lenye nguvu likaanza. Tawi lilipokea ripoti kwamba mapainia wa pekee walikuwa wakikamatwa na kupigwa vikali na polisi wa siri, wale P.I.D.E. (Polícia Internacional e Defesa do Estado) wenye sifa mbaya. Wengine kati yetu wamisionari waliitwa kwenye makao makuu ya polisi kuhojiwa. Kisha, wenzi wa ndoa watatu walipewa siku 30 kuondoka nchini. Sisi sote tukakata rufani uamuzi huo ubadilishwe.
Wenzi wa ndoa wamisionari waliitwa kwenye makao makuu ya polisi wahojiwe na mkurugenzi wa P.I.D.E. Kwanza mtumishi wa tawi, Eric Britten, na mkewe, Christina, walihojiwa. Kisha, Eric Bveridge na mkewe, Hazel, na hatimaye Elsa nami tukahojiwa. Mkuu wa polisi alitushtaki kwa uwongo kwamba tulikuwa tukitumiwa na Wakomunisti kuudhoofisha ulimwengu wa Magharibi kwa mafundisho yetu juu ya kutokuwamo. Rufani yetu haikufanikiwa.
Lilikuwa jambo la kuhuzunisha kama nini kuwaacha ndugu na dada 1,200 waliokuwa wakipitia nyakati ngumu kwa sababu ya utawala wenye ukatili wa dikteta asiyetaka kusikia maoni ya wengine! Akina Beveridge walipokwenda Hispania na akina Britten wakarudi Uingereza, mgawo wetu ambao ungefuata ungekuwa nini? Nchi ya Kiislamu ya Moroko!
Kuhubiri Katika Moroko ya Kiislamu
Kwa mara nyingine tena, tulikuwa tukiendelea kumngojea Yehova. Mgawo mpya, desturi mpya, na lugha mpya! Kiarabu, Kifaransa, na Kihispania zilikuwa lugha za taifa za Ufalme wa Moroko, ambako walikuwako Mashahidi 234 katika makundi manane. Dini ya taifa ya nchi hiyo ilikuwa Kiislamu, na kujaribu kuongoa miongoni mwa Waislamu lilikuwa jambo lililokatazwa kisheria. Kwa hiyo tungeweza kuhubiria tu watu wa Ulaya wasio Waislamu.
Mara wamisionari walipoanza kuwasili katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1950, maongezeko yalianza kuonekana. Lakini serikali ya Moroko ilianza kuwabana watu wa Ulaya, watu wengi wa nchi za nje wakaanza kuondoka, kutia na ndugu wengi.
Kwa kuwa idadi ya watu wasio Waislamu ilipungua, tulipata kwamba ilikuwa lazima tutafute njia za busara za kuongea na Waislamu, na hilo lilitokeza malalamiko yaliyopelekwa kwa polisi. Kadiri malalamiko yalivyozidi kuongezeka katika Tangier na miji mingine, tuliambiwa hatimaye kwamba tulikuwa na siku 30 tu za kuondoka nchini humo. Katika Mei 1969, Elsa nami tukafukuzwa katika mgawo mwingine bado.
Mgawo wa Muda Mfupi?
Tuliambiwa turudi Brooklyn, nami nikaalikwa nihudhurie mkutano wa watumishi wa tawi uliofanywa kiangazi hicho. Nilipokuwa huko, niliarifiwa kwamba mgawo wetu mpya ungekuwa El Salvador, Amerika ya Kati, na kwamba ningetumikia huko nikiwa mtumishi wa tawi. Niliambiwa kwamba yaelekea mgawo huo ungekuwa wa muda wa miaka mitano hivi, muda mrefu zaidi ambao wamisionari walikubaliwa kukaa katika nchi hiyo, kwa kuwa kazi yetu haikutambuliwa kisheria huko.
El Salvador—ulikuwa mgawo mzuri kama nini! Walikuwako wahubiri 1,290, kutia na mapainia 114 kwa wastani wakiripoti kila mwezi. Watu walikuwa wenye kumhofu Mungu, wenye kuipenda Biblia, na wakaribishaji-wageni. Katika karibu kila mlango, walikuwa wakitukaribisha ndani tuongee nao. Kwa muda mfupi, tulikuwa na mafunzo mengi sana ya Biblia.
Tulipokuwa tukiona ongezeko na uhitaji mkubwa uliokuwa huko, tulikuwa na huzuni kwamba tungelazimika kuacha mgawo huo baada ya miaka mitano tu. Kwa hiyo ikaamuliwa kwamba tujaribu kuhalalisha kisheria kazi ya Mashahidi wa Yehova. Katika December 1971, tulitolea serikali karatasi zilizohitajiwa, Aprili 26, 1972, tulifurahi kusoma katika gazeti la serikali, Diario Oficial, kwamba ombi letu lilikuwa limekubaliwa. Wamisionari wasingelazimika tena kuondoka baada ya miaka mitano bali wangepata ukaaji wa kudumu katika nchi hiyo.
Majaribu na Mibaraka
Katika miaka ambayo imepita ya migawo yetu mbalimbali, tumefanya marafiki wengi wazuri na kuona matokeo katika huduma yetu. Elsa aliona jambo zuri katika San Salvador kuhusu mwalimu na mume wake aliyekuwa askari. Rafiki mmoja wa mwalimu huyo alipendezwa na kweli pia. Mwanzoni mume wa mwalimu huyo hakuonyesha kupendezwa katika Biblia; hata hivyo, tulimtembelea alipokuwa hospitalini, naye alikuwa mwenye urafiki. Hatimaye alijifunza Biblia, akaacha kazi-maisha yake ya kijeshi, akaanza kuhubiri pamoja nasi.
Wakati ule ule, bibi fulani alikuja kwenye Jumba la Ufalme na kumwuliza Elsa kama alikuwa akisoma na yule mtu ambaye hapo zamani alikuwa askari. Ilitokea kwamba alikuwa amekuwa hawara wa askari huyo! Alikuwa pia akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kwenye mkusanyiko wa wilaya, yule mtu aliyekuwa askari hapo zamani, mke wake, rafiki wa mke wake, na yule aliyekuwa hawara wake wote wakabatizwa!
Ongezeko Katika El Salvador
Kwa sababu ya ongezeko kubwa, Majumba ya Ufalme mengi yamejengwa, na nchi sasa ina Mashahidi zaidi ya 18,000 wenye kutenda kazi. Hata hivyo maendeleo hayo, hayakuwa bila majaribu. Kwa miaka kumi, ndugu wamepaswa kufanya mapenzi ya Yehova katikati ya vita ya wao kwa wao. Lakini wamedumisha kutokuwamo kwao wakaendelea kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Yehova.
Kati yetu wawili, Elsa na mimi tumekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 85. Tumeona kwamba tunapoendelea kumngojea Yehova na kusikiliza ‘neno nyuma yake, likisema, Njia ni hii, ifuate,’ hatutamauki kamwe. Kwa kweli tumefurahia maisha yenye kuridhisha na yenye kuthawabisha tukiwa watumishi wa Yehova wa wakati wote.
[Maelezo ya Chini]
a Kupata maelezo zaidi, ona Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1978 (katika Kiingereza) kurasa 177-9.
[Picha of Domenick and Elsa Piccone katika ukurasa wa 23]
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kusanyiko katika msitu huko Hispania, 1956
[Picha katika ukurasa wa 25]
Tulikuwa tukihubiria wasio Waislamu katika Moroko
[Picha katika ukurasa wa 26]
Tawi katika El Salvador, mgawo wetu wa sasa