Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 7/1 kur. 23-27
  • Toka Ufukara Hadi Utajiri Mkubwa Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Toka Ufukara Hadi Utajiri Mkubwa Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutafuta Kitu Bora Zaidi
  • Kusisimuliwa na Tumaini la Biblia
  • Kunufaika kwa Sababu ya Kuonyesha Ukaribishaji-Wageni
  • Kuvumilia Mnyanyaso
  • Kufurahia Utajiri Mkubwa Zaidi
  • Tumejionea Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu Katika Njia Nyingi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • ‘Wenye Furaha Ni Wale Wanaoendelea Kumngoja Yehova’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kukubali Mialiko ya Yehova Huthawabisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 7/1 kur. 23-27

Toka Ufukara Hadi Utajiri Mkubwa Zaidi

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MANUEL DE JESUS ALMEIDA

Nilizaliwa Oktoba 1916, nikiwa kitindamimba kati ya watoto 17. Ndugu na dada zangu wakubwa tisa walikuwa wamekufa kutokana na ugonjwa na utapiamlo, kwa hiyo sikupata kuwajua kamwe. Sisi wanane tuliosalia tuliishi na wazazi wetu katika kijiji kidogo karibu na Porto, Ureno.

MAKAO yetu duni yalikuwa chumba kidogo cha mezani na chumba kimoja cha kulala. Tulipata maji ya kunywa kutoka katika kisima kilichokuwa umbali wa karibu nusu kilometa, na mapishi yetu yalikuwa ya kikale sana.

Mara ndugu zangu walipojiweza kimwili, walianza kufanya kazi katika mashamba ya mahindi. Mapato yao yalisaidia kuandalia familia kiasi fulani cha chakula. Kwa msaada wao nikawa mtoto pekee aliyesoma kidogo. Ingawa maisha yetu yalikuwa magumu, tulikuwa washiriki waaminifu sana kwa Kanisa Katoliki, tukitumaini kwamba hilo lingesaidia maisha yetu kwa njia fulani.

Mwezi wa Mei, kanisa lilikuwa na ibada iliyoitwa novena. Siku tisa mfululizo, tulitembea kwa miguu kwenda kanisani asubuhi na mapema kukiwa na giza bado. Tukiwa huko tulisali, tukiamini kwamba kufanya hivyo kungeleta baraka kutoka kwa Mungu. Pia tulidhani kwamba kasisi ni mtu mtakatifu, mwakilishi wa Mungu. Lakini, hatimaye, maoni hayo yakabadilika.

Kutafuta Kitu Bora Zaidi

Tuliposhindwa kulipa kodi ya kanisa, kasisi hakujali hali yetu mbaya ya kiuchumi. Hilo lilituvunja moyo. Maoni yangu juu ya kanisa yakabadilika sana, kwa hiyo nilipokuwa na umri wa miaka 18, nikaamua kuiacha familia yangu nikatafute ikiwa kuna kitu kingine bora zaidi maishani kuliko kufanya kazi mashambani na kubishana na kanisa. Nikawasili Lisbon, jiji kuu la Ureno, mwaka wa 1936.

Huko nilikutana na Edminia. Ingawa nilihisi kuwa nilikuwa nimedanganywa na dini, tulifuata desturi na kuoana katika Kanisa Katoliki. Kisha mwaka wa 1939, Vita ya Ulimwengu ya Pili ikaanza. Wakati wa vita hiyo, nilisimamia maghala 18, nasi kwa siku moja tulikuwa tukipeleka malori yapatayo 125 yenye zana za vita.

Vitisho vya vita pamoja na kuhusika sana kwa Kanisa Katoliki kuliniathiri sana. Nilijiuliza, ‘Je, kwa kweli Mungu anawajali wanadamu? Twapaswa kumwabuduje?’ Miaka kadhaa baadaye, mwaka wa 1954, mzee mmoja muungwana, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliongea nami juu ya swali nililokuwa nalo. Mazungumzo hayo yalibadili maisha yangu yote.

Kusisimuliwa na Tumaini la Biblia

Mwanamume huyo mwenye fadhili, Joshua, alinieleza kwamba Ufalme wa Mungu ndio utatuzi pekee wa matatizo ya ulimwengu na kwamba amani na usalama zingepatikana kupitia utawala wa Ufalme tu. (Mathayo 6:9, 10; 24:14) Mambo aliyosema yalinipendeza, lakini sikukubali mara moja maelezo yake kwa sababu ya mambo niliyokuwa nimejionea katika dini. Alipojitolea kujifunza Biblia nami, nilikubali maadamu tu asiniombe fedha na asiongee juu ya siasa. Akakubali, akinihakikishia kwamba alikuwa akijitolea bure.—Ufunuo 22:17.

Uhakika wangu katika Joshua ukaongezeka haraka. Kwa hiyo, nikamwomba kitu fulani ambacho nilikuwa nimekitamani tangu nilipokuwa kijana. “Je, ningeweza kupata nakala yangu mwenyewe ya Biblia?” Baada ya kuipokea, nilifurahi kama nini kusoma kwa mara ya kwanza kabisa kutoka katika Neno la Muumba mwenyewe ahadi kama vile: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja [na wanadamu]. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali”!—Ufunuo 21:3, 4.

Ahadi za Biblia hasa juu ya kuondolewa kwa umaskini na ugonjwa zilinifariji. Yule mwanamume mwaminifu Elihu alisema hivi juu ya Mungu: “Hutoa chakula kwa ukarimu.” (Ayubu 36:31) Na chini ya utawala mwadilifu wa Ufalme wa Mungu, Biblia husema, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Yehova Mungu anapendezwa kama nini na wanadamu! Jinsi nilivyozidi kupendezwa na ahadi zake!

Nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova Aprili 17, 1954. Ulikuwa mkutano wa pekee—Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Tangu wakati huo na kuendelea, nilihudhuria mikutano kwa ukawaida sana. Upesi nikaanza kuwahubiria wengine habari njema nilizokuwa nikijifunza. Siku hizo nchini Ureno, tulikuwa na tafrija kila mwezi karibu na ufuo, kisha tukawa na ubatizo. Miezi saba baada ya Joshua kuongea nami, nilijitoa wakfu kwa Yehova Mungu na kuuonyesha kwa kubatizwa majini katika bahari.

Mapema mwaka wa 1954 kulikuwa na Mashahidi wapatao mia moja tu katika nchi nzima ya Ureno. Kwa hiyo, kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wanaume wa kuongoza katika kazi ya kuhubiri. Nilifanya maendeleo ya kiroho haraka, na punde si punde nikapewa madaraka kutanikoni. Mwaka wa 1956, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko, kama vile mwangalizi msimamizi alivyoitwa wakati huo, katika kutaniko la pili la Mashahidi wa Yehova huko Lisbon. Leo, kuna makutaniko zaidi ya mia moja katika jiji hilo na viunga vyake.

Kunufaika kwa Sababu ya Kuonyesha Ukaribishaji-Wageni

Ingawa Edminia nami tulikuwa na fedha chache, sikuzote tuliwakaribisha ndugu zetu Wakristo. Mwaka wa 1955, painia mmoja, kama waitwavyo waeneza-evanjeli wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, alipitia Ureno akitoka nyumbani kwake Brazili akielekea katika Kusanyiko la kimataifa la “Ushindi wa Ufalme” huko Ujerumani. Kwa sababu ya matatizo ya kusafiri, alikaa nyumbani kwetu kwa mwezi mmoja, nasi tulinufaika kiroho kama nini kutokana na ziara yake!

Wageni wengine waliokaa nyumbani kwetu wakati huo walitia ndani washiriki wa familia ya makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, kama vile Hugo Riemer na ndugu aliyeishi pamoja naye, Charles Eicher. Walikula mlo pamoja nasi na kutolea ndugu Wareno hotuba mbalimbali. Kama vifaranga waliotoka kuanguliwa wenye midomo wazi, tulisubiri urojorojo mtamu wa kiroho waliotuandalia.

Waangalizi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova pia walikaa kwetu wakati wa ziara zao. Mgeni mwenye kukumbukwa mwaka wa 1957 alikuwa Álvaro Berecochea, mwangalizi wa ofisi ya tawi ya Morocco, aliyepewa mgawo wa kuzuru Ureno ili kuwatia moyo akina ndugu. Alihudhuria funzo la kitabu nyumbani kwetu, nasi tukasisitiza akae nasi wakati wote uliosalia ambao angekuwa Ureno. Tulibarikiwa sana na kunenepeshwa kiroho wakati wa ziara yake ya mwezi mzima, naye Álvaro akinenepa kimwili kutokana na mapishi mazuri ya mke wangu mpendwa Edminia.

Ufukara, kama ule tuliokuwa nao nikiwa mtoto, waweza kumdhuru mtu sana kwa muda mrefu. Hata hivyo, nilikuja kufahamu kwamba kadiri tunavyomtolea Yehova na watumishi wake waaminifu, ndivyo anavyozidi kutubariki. Jambo hilo limekaziwa kwangu tena na tena tulipokuwa tukiwaonyesha ukaribishaji-wageni wote tulioweza.

Kwenye mkusanyiko huko Porto mwaka wa 1955, tangazo lilitolewa juu ya mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova ambao ungefanyiwa Yankee Stadium, New York City, mwaka wa 1958. Sanduku la michango liliwekwa katika kila Jumba la Ufalme nchini—yaliyokuwa machache wakati huo—ili kusaidia kulipia gharama za kuwatuma wajumbe wa Ureno kwenye mkusanyiko huo. Waweza kuwazia shangwe yetu wakati ambapo mke wangu nami tulichaguliwa kuwa miongoni mwa wajumbe hao? Ilikuwa furaha kama nini kutembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn tulipokuwa kwenye mkusanyiko wa Marekani!

Kuvumilia Mnyanyaso

Mwaka wa 1962, kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku nchini Ureno, na wamishonari—kutia ndani Eric Britten, Domenick Piccone, Eric Beverdge, na wake zao—wakafukuzwa. Baadaye, hatukuruhusiwa kufanya mikutano katika Majumba ya Ufalme, kwa hiyo tuliifanya kisiri katika nyumba za watu; wala haikuwezekana tena kuwa na mikusanyiko mikubwa nchini Ureno. Kwa hiyo, likawa daraka langu kupangia ndugu na dada zetu Wakristo usafiri ili waweze kuhudhuria mikusanyiko hiyo katika nchi nyingine.

Haikuwa rahisi kupangia idadi kubwa ya Mashahidi wasafiri kwenda nchi nyingine. Hata hivyo, jitihada hizo hazikuwa kazi bure, hasa kwa kufikiria manufaa ya kiroho ambayo ndugu hao Wareno walipokea. Lilikuwa jambo lenye kujenga imani kama nini walipohudhuria mikusanyiko nchini Uswisi, Uingereza, Italia, na Ufaransa! Mikusanyiko hiyo pia iliwaandalia fursa ya kurudi nchini wakiwa na fasihi. Miaka yote hiyo, tulitoa maombi mengi ya kusajiliwa tukiwa tengenezo la kidini nchini Ureno, lakini maombi yote hayo yalikataliwa.

Baada ya wamishonari kufukuzwa mapema mwaka wa 1962, polisi wa usalama walianza kuzidisha kampeni zao za kusimamisha kazi yetu ya kuhubiri. Ndugu na dada zetu kadha wa kadha walikamatwa na kupelekwa mahakamani. Ripoti za visa kadhaa halisi vya matukio haya zilichapishwa katika jarida hili na gazeti jenzile, Amkeni!a

Painia mmoja ambaye nilikuwa nimemhubiria habari njema ya Ufalme wa Mungu alikuwa miongoni mwa wale waliotiwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri. Kwa kuwa polisi walipata anwani yangu miongoni mwa mali yake, niliitwa na kuhojiwa.

Baadaye, maofisa wawili wa polisi wakaja nyumbani kwangu. Walitwaa vichapo vyangu vya kujifunza Biblia pamoja na nakala 13 za Biblia. Waliendelea kutusumbua, wakirudi jumla ya mara saba ili kupekua makao yetu. Kila mara, walituuliza maswali mengi.

Niliitwa mara kadhaa nitoe ushahidi kwa niaba ya Mashahidi katika kesi za mahakamani. Ingawa sikuwa na elimu nyingi ya kilimwengu, Yehova alinipa ‘hekima ambayo wapingaji wote wakiwa pamoja hawakuweza kukinza au kubisha.’ (Luka 21:15) Pindi moja hakimu alishangazwa sana na ushuhuda wangu hivi kwamba akauliza nilikuwa na elimu kiasi gani. Watu wote kotini walicheka niliposema kwamba nilikuwa nimefika darasa la nne tu.

Mnyanyaso ulipozidi kuongezeka, idadi ya wale walioukubali ujumbe wa Ufalme iliongezeka pia. Kwa hiyo, wale Mashahidi waliopungua 1,300 nchini Ureno mwaka wa 1962 waliongezeka na kupita 13,000 kufikia mwaka wa 1974! Wakati huohuo, mwezi wa Mei 1967, nilialikwa nitumikie nikiwa mwangalizi asafiriye. Katika kazi hiyo nilitembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ili kuyaimarisha kiroho.

Kufurahia Utajiri Mkubwa Zaidi

Mwezi wa Desemba 1974, nilipata pendeleo la kuhusika katika kusajiliwa kulikohalalisha kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ureno. Mwaka uliofuata mke wangu nami tukawa washiriki wa familia ya Betheli ya Mashahidi wa Yehova mjini Estoril. Pia niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ureno.

Imekuwa shangwe kama nini kuona kazi ya kuhubiri ikisitawi nchini Ureno na katika maeneo yaliyo chini ya uangalizi wa ofisi yetu ya tawi! Nchi hizo zatia ndani Angola, Azores, Cape Verde, Madeira, na São Tomé na Príncipe. Kwa miaka kadhaa limekuwa jambo lenye kusisimua kuona wamishonari kutoka Ureno wakitumwa kutumikia katika nchi hizo, ambamo upendezi mkubwa sana katika ujumbe wa Ufalme umeonyeshwa. Wazia shangwe yetu sasa kuwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 88,000 katika sehemu hizo, kutia ndani zaidi ya 47,000 nchini Ureno! Hudhurio la ukumbusho katika nchi hizo mwaka wa 1998 lilipita 245,000, likilinganishwa na linalopungua 200 nilipopata kuwa Shahidi mwaka wa 1954.

Edminia nami twakubaliana kwa moyo mzima na mtunga-zaburi wa Biblia aliyesema kwamba “siku moja tu maskani mwako, ni bora kuliko siku elfu mahali pengine.” (Zaburi 84:10, Biblia Habari Njema) Nikumbukapo nilivyoanza katika ufukara na kulinganisha na utajiri wa kiroho ambao nimepata tangu wakati huo, nahisi kama alivyohisi nabii Isaya: “Ee BWANA, wewe u Mungu wangu; nitakutukuza na kulihimidi jina lako; kwa kuwa umetenda mambo ya ajabu . . . Maana umekuwa ngome ya maskini, ngome ya mhitaji katika dhiki yake.”—Isaya 25:1, 4.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Amkeni! la Mei 22, 1964, ukurasa wa 8-16 katika Kiingereza, na Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1966, ukurasa wa 581-592, katika Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Juu: Ndugu Almeida jijini Lisbon akitangaza mpango wa kutuma wajumbe kwenye mkusanyiko wa 1958 huko New York

Katikati: Nikiongoza kigezo cha mkutano wa watumishi kwenye Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” lililofanywa jijini Paris

Chini: Mabasi yaliyokodishwa yakitayarishwa kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya nchini Ufaransa

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiongoza ibada ya asubuhi katika ofisi ya tawi ya Ureno

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ofisi ya tawi ya Ureno, iliwekwa wakfu mwaka wa 1988

[Picha katika ukurasa wa 26]

Hotuba za ndugu Hugo Riemer alipozuru kutoka Betheli ya Brooklyn zilitutia moyo

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na mke wangu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki