Jina la Mungu Latamkwa Nchini Israeli
KWA karne nyingi, Dini ya Kiyahudi ya kidesturi imewakataza katakata wafuasi wake wasilitamke jina la Mungu, Yehova. Kulingana na Mishnah, yeyote atamkaye jina la Mungu hatakuwa na “urithi katika ulimwengu ujao.”—Sanhedrin 10:1.a
Aliyekuwa rabi mkuu Msefardi nchini Israel alilitamka kimakusudi jina la Mungu Januari 30, 1995. Alifanya hivyo akikariri tikkun, sala ya Kabala ya kusahihisha. Sala hiyo hutolewa ili Mungu arudishe kadiri fulani ya upatano katika ulimwengu, ambao, kulingana na waabudu hao, umevurugwa na nguvu za uovu. Gazeti Yedioth Aharonoth, la Februari 6, 1995, lilitaarifu hivi: “Hii ni liturjia yenye nguvu nyingi sana hivi kwamba maneno yake yapatikana katika kijitabu maalumu pekee ambacho hakiuziwi umma.” Yadhaniwa kwamba kuliitia jina la Mungu katika muktadha huo huongezea ombi hilo nguvu maalumu.
Yafaa kukumbukwa kwamba Biblia huwaamuru watumishi wa Mungu walitumie jina la Mungu, Yehova. (Kutoka 3:15; Mithali 18:10; Isaya 12:4; Sefania 3:9) Katika maandishi ya awali ya Kiebrania ya Biblia, jina hilo lapatikana karibu mara 7,000. Hata hivyo, Biblia yaonya dhidi ya kulitumia jina la Mungu vibaya. Amri ya tatu ya zile Amri Kumi yasema hivi: “Usilitaje bure jina la BWANA, Mungu wako, maana BWANA hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.” (Kutoka 20:7) Jina la Mungu laweza kutajwaje bure? Maelezo fulani yaliyotolewa na The Jewish Publication Society yataja kwamba neno la Kiebrania lililotafsiriwa “bure” laweza kutia ndani “utumizi wa kipuuzi” wa jina la Mungu na pia “kukariri baraka isiyohitajiwa.”
Basi, twapaswa kuonaje sala ya Kikabala ya kusahihisha ya tikkun? Asili yake ni nini? Katika karne ya 12 na ya 13 W.K., namna fulani ya Dini ya Kiyahudi ya kifumbo, iliyoitwa Kabala, ilianza kupata umaarufu. Katika karne ya 16, rabi fulani aliyeitwa Isaac Luria aliingiza “tikkunim” katika liturjia ya Kikabala. Jina la Mungu lilitumiwa kama hirizi ya kifumbo yenye nguvu maalumu, nalo likawa sehemu ya desturi ya Kikabala. Je, wewe unaona kuwa huo ni utumizi mzuri wa jina la Mungu?—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.
Hata jibu lako liweje kwa swali hilo, utakubali kwamba kutamkwa waziwazi kwa jina la Mungu katika Israeli ya leo kulikuwa tukio lisilo la kawaida. Ingawa hivyo, Mungu mwenyewe alitabiri hivi: “Katika siku hiyo mtasema, Mshukuruni BWANA [“Yehova,” NW], liitieni jina lake; yatangazeni matendo yake kati ya mataifa, litajeni jina lake kuwa limetukuka. Mwimbieni BWANA; kwa kuwa ametenda makuu; na yajulikane haya katika dunia yote.”—Isaya 12:4, 5.
Kwa furaha, Mashahidi wa Yehova nchini Israeli, kama ilivyo katika nchi zaidi ya 230 ulimwenguni pote, wanafanya kila jitihada kuwasaidia jirani zao wapate ujuzi sahihi juu ya Yehova. Wanatumaini kwamba watu wengi zaidi watakuja kutambua maana ya maandiko kama vile Zaburi 91:14: “Kwa kuwa amekaza kunipenda [mimi Yehova] nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kwa kuwa amenijua Jina langu.”
[Maelezo ya Chini]
a Mishnah ni mkusanyo wa maelezo ambayo ni nyongeza ya sheria ya Kimaandiko, yanayotegemea maelezo ya marabi waitwao Tannaim (walimu). Yalikusanywa katika maandishi mwishoni mwa karne ya pili na mwanzoni mwa karne ya tatu W.K.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Hapa katika Negebu, watu wa Yehova wanajulisha jina na Neno lake
[Picha katika ukurasa wa 29]
Bango likionyesha jina la Mungu