“Kwa Kuwa Tuna Huduma Hii . . . , Hatuachi”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA RONALD TAYLOR
Katika masika ya 1963, nilijikuta nikipigania uhai wangu. Nilipokuwa nikitembea ukingoni mwa bahari, nilikanyaga shimo hatari na kutumbukia kwa ghafula ndani ya maji yenye kina sana. Nikiwa sijui kuogelea nilikuwa karibu kuzama meta chache tu kutoka ukingoni mwa bahari. Tayari nilikuwa nimedidimia mara tatu na kupukua maji mengi sana ya bahari wakati rafiki mmoja alipoona shida yangu na kunikokota hadi ukingoni mwa bahari. Kwa msaada wa kupuliziwa pumzi haraka, niliokoka.
HII haikuwa mara ya kwanza ambapo nilikuja kuthamini umuhimu wa kutolegea—mambo yajapoonekana kuwa yasiyo na tumaini. Tangu umri wa mapema, ilinibidi nipiganie uhai wangu wa kiroho.
Ilikuwa wakati wa siku zenye huzuni za vita ya ulimwengu ya pili nilipopata Ukristo wa kweli kwa mara ya kwanza. Nilikuwa mmoja wa maelfu ya watoto waliohamishwa kutoka London ili kutoroka hatari ya mashambulizi ya mabomu. Kwa kuwa nilikuwa mwenye umri wa miaka 12, vita haikuwa na maana sana kwangu; ilikuwa kama kujionea mambo.
Nilitunzwa na wenzi wa ndoa wazee-wazee katika Weston-super-Mare, kusini-magharibi mwa Uingereza. Muda mfupi baada ya kufika nyumbani mwa wenzi hao wa ndoa, wahudumu fulani mapainia wakaanza kututembelea. Ilikuwa familia ya Hargreaves; wote wanne—Reg, Mabs, Pamela, na Valeri—walikuwa mapainia wa pekee. Wazazi-walezi wangu walikubali kweli, na baada ya kujifunza kitabu The Harp of God, mimi pia nilifanya uamuzi wa kumtumikia Yehova. Baada ya majuma sita tu, nilialikwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri.
Bado naweza kukumbuka hiyo siku ya kwanza katika utumishi wa shambani. Bila mazoezi yoyote, nilipewa vijitabu kadhaa na kuambiwa: “Wewe hubiri ule upande mwingine wa barabara.” Na hivyo ndivyo nilivyomaliza siku yangu ya kwanza ya kuhubiri. Wakati huo, mara nyingi tulihubiri kwa kutumia sahani za santuri zilizokuwa na mahubiri yenye uzito mwingi. Nyakati zangu za furaha zaidi zilikuwa wakati ningebeba santuri nyumba kwa nyumba na kufungulia hotuba zilizorekodiwa. Nililiona kuwa pendeleo kwelikweli kutumiwa kwa njia hiyo.
Nilitoa ushahidi mwingi sana shuleni, na nakumbuka nikimwangushia mwalimu mkuu seti ya vitabu kadhaa vyenye habari za Biblia. Nikiwa na umri wa miaka 13, nilibatizwa katika kusanyiko lililokuwa karibu katika Bath. Mkusanyiko mwingine wa wakati wa vita ambao sitausahau ulikuwa ule uliofanywa katika Leicester mwaka wa 1941 katika Jumba la De Montfort. Nilienda jukwaani kupokea nakala yangu ya kitabu Children, ambacho ndani yacho mlikuwa na ujumbe wa binafsi kutoka kwa Ndugu Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo. Hotuba yenye kuchochea iliyotolewa kwa wachanga wote waliokuwapo ilichochea tamaa yangu ya kumtumikia Yehova milele.
Hivyo nilitumia miaka miwili yenye furaha nikikua katika kweli nikiwa pamoja na wazazi-walezi wangu. Lakini nikiwa na umri wa miaka 14, ilinibidi kurudi London na kuanza kufanya kazi ili nijisimamie. Ingawa niliungana tena na familia yangu, sasa ilinibidi kujisimamia kiroho, maana hakuna yeyote nyumbani aliyeshiriki imani yangu. Upesi Yehova akatoa msaada. Majuma matatu tu baada ya kufika kwangu London, ndugu mmoja alikuja nyumbani kwetu kumwomba baba yangu ruhusa niende naye kwenye Jumba la Ufalme. Huyu ndugu alikuwa John Barr, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Alikuja kuwa mmoja wa “baba” zangu wa kiroho wakati wa hizo nyakati ngumu za utineja.—Mathayo 19:29.
Nilianza kuhudhuria Kutaniko la Paddington, lililokutana katika Craven Terrace kando ya Makao ya Betheli ya London. Kwa sababu nilikuwa yatima, wa kiroho, ndugu mmoja mzee-mzee mtiwa-mafuta, “Baba” Humphreys, alipewa mgawo wa kunipa upendezi wa pekee. Hakika ilikuwa baraka kubwa kuweza kushirikiana pamoja na ndugu na dada wengi watiwa-mafuta waliotumika katika kutaniko hilo. Sisi wengine tuliokuwa na tumaini la kuishi duniani—tulioitwa Wayonadabu—tulikuwa wachache. Kwa kweli, ni mimi pekee niliyekuwa “Yonadabu” katika Funzo la Kitabu la Kutaniko nililohudhuria. Ijapokuwa sikuwa na ushirika mkubwa na wale wa umri wangu, ushirikiano huo wenye thamani pamoja na ndugu wakomavu ulinifundisha masomo mengi ya maana. Pengine somo lililo la maana zaidi lilikuwa lile la kutoacha kamwe utumishi wa Yehova.
Katika siku hizo, tulikuwa tunatoa mwisho-juma wote kwenye utendaji wa kuhubiri. Nilipewa mgawo wa kutunza “gari lenye kikuza-sauti,” ambalo kwelikweli lilikuwa kigari cha magurudumu matatu kilichoundwa ili kushikilia kifaa cha kikuza sauti na betri ya gari. Kila Jumamosi, nilisafiri kwa kigari hicho na kwenda pembe tofauti-tofauti za barabara za mji, ambapo tulicheza muziki fulani halafu tukasikiliza moja ya hotuba za Ndugu Rutherford. Siku za Jumamosi pia zilitumiwa kwa ajili ya kufanya kazi ya barabarani tukiwa na mikoba yetu ya magazeti. Siku za Jumapili tulifanya kazi ya nyumba kwa nyumba, tukitoa vijitabu na vitabu vilivyojalidiwa.
Ushirika wangu na ndugu wazee-wazee wenye bidii uliwasha tamaa ya upainia ndani yangu. Tamaa hii ilitiwa nguvu niliposikiliza hotuba ya mapainia kwenye mikusanyiko ya wilaya. Mkusanyiko mmoja uliokuwa na uvutano mkubwa sana maishani mwangu ulikuwa ule uliofanywa kwenye Earl’s Court, London, katika 1947. Miezi miwili baadaye, niliingia katika utumishi wa painia, nami nimejitahidi kudumisha roho ya painia tangu wakati huo. Furaha niliyopata kutokana na kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo ilinithibitishia kwamba huu ulikuwa uamuzi ufaao.
Bibi-Harusi Mhispania na Mgawo wa Hispania
Katika mwaka wa 1957, nilipokuwa bado napainia katika Kutaniko la Paddington, nilikutana na dada mmoja Mhispania mwenye kupendeza aitwaye Rafaela. Baada ya miezi michache, tulioana. Mradi wetu ulikuwa kupainia pamoja, lakini kwanza tulienda Madrid ili nikukutane na wazazi wa Rafaela. Ilikuwa ziara iliyobadili maisha yangu. Tulipokuwa Madrid, Ndugu Ray Dusinberre, mwangalizi wa tawi katika Hispania, akaniuliza kama tunaweza kufikiria kutumika katika Hispania, ambapo palikuwa na uhitaji mkubwa sana wa ndugu wenye ujuzi.
Tungeweza kukataaje mwaliko kama huo? Hivyo, katika 1958 tulianza pamoja utumishi wetu wa wakati wote katika Hispania. Wakati huo nchi hiyo ilikuwa ikitawalwa na Franco, na utendaji wetu haukutambuliwa kisheria, jambo lililofanya kazi ya kuhubiri iwe ngumu sana. Zaidi ya hayo, ilinibidi ning’ang’ane na lugha ya Kihispania kwa miaka kadhaa ya kwanza. Kwa mara nyingine tena, lilikuwa jambo la kutoacha, ingawa nililia zaidi ya mara moja kama tokeo la kutojua la kufanya kwa kushindwa kupashana habari na ndugu katika kutaniko.
Uhitaji wa waangalizi ulikuwa mkubwa sana kwamba ingawa singeweza kusema Kihispania chochote, baada ya mwezi mmoja nilikuwa nasimamia kikundi kimoja kidogo. Kwa sababu ya hali ya kuendesha kazi yetu kisiri, tulijipanga kwa vikundi vidogo vilivyokuwa na wahubiri kutoka 15 hadi 20, vilivyotenda kazi kama makutaniko madogo. Mara ya kwanza, ilikuwa vigumu sana kuongoza mikutano, kwa sababu singeweza kila mara kuelewa majibu kutoka kwa wasikilizaji. Lakini, mke wangu aliketi huko nyuma, na alipogundua kwamba sielewi, alinipa ishara ya siri kuthibitisha kwamba jibu lilikuwa sahihi.
Sina kipawa cha asili cha kujua lugha kwa urahisi, na zaidi ya mara moja nilihisi nikitaka kurudi Uingereza, ambapo ningefanya mambo yote kwa urahisi zaidi. Hata hivyo, tangu mwanzo, upendo na urafiki wa ndugu na dada zetu wapendwa Wahispania ulituliza fadhaiko langu la kutojua lugha. Naye Yehova akanibariki kwa mapendeleo ya pekee ambayo yalifanya mambo yote yaonekane kuwa yanastahili. Katika 1958, nilialikwa kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa katika New York nikiwa mgeni kutoka Hispania. Halafu katika 1962, nilipokea mazoezi yenye mafaa sana katika Shule ya Huduma ya Ufalme iliyotayarishwa kwa ajili yetu katika Tangier, Moroko.
Tatizo jingine nililokabili, kando na lugha, lilikuwa hangaiko la kila wakati la kushikwa na polisi. Nikiwa mgeni, nilijua kwamba kushikwa kungemaanisha kurudishwa nyumbani mara moja. Ili kupunguza uwezekano huo, tulifanya kazi tukiwa wawili-wawili. Mmoja akiwa anatoa ushahidi, mwingine angesikiliza dalili zozote za hatari. Baada ya kuzuru mlango mmoja au miwili, mara nyingi ikiwa orofa ya juu katika jengo, tungepita majengo mawili au matatu na kubisha nyumba nyingine mbili au tatu. Tulitumia Biblia sana, na tulibeba vijitabu vichache tu tulivyoweka ndani ya makoti yetu ili kutolea watu wanaopendezwa.
Baada ya mwaka mmoja katika Madrid, tuligawiwa kwenda Vigo, jiji kubwa katika kaskazini-magharibi mwa Hispania, ambako hakukuwa na Mashahidi wowote. Kwa mwezi wa kwanza hivi, Sosaiti ilipendekeza kwamba mke wangu afanye sehemu kubwa ya kutoa ushahidi—ili ionekane kama tulikuwa tukitembelea kama wageni. Ijapokuwa njia hiyo ilikusudiwa kutovuta wengi, mahubiri yetu yalivuta uangalifu. Kwa mwezi mmoja makasisi Wakatoliki wakaanza kutushambulia kwa njia ya redio. Waliwaonya wahudhuriaji wao kwamba kulikuwa na wenzi wa ndoa waliokuwa wakienda nyumba kwa nyumba wakizungumza kuhusu Biblia—kitabu kilichokuwa kama kimepigwa marufuku wakati huo. “Wenzi wa ndoa wanaotafutwa” ni mgeni na mkeye Mhispania, anayefanya karibu mazungumzo yote!
Makasisi waliagiza kwamba kuzungumza tu na wenzi hawa wa ndoa walio hatari lilikuwa kosa ambalo lingesamehewa ikiwa tu litaungamwa mara hiyo kwa kasisi. Na kwa kweli, baada ya mwisho wa mazungumzo mazuri pamoja na mwanamke mmoja, alituambia kwa kusikitika kwamba itambidi aende akaungame. Tulipoondoka nyumbani mwake, tulimwona akiharakisha kuelekea kanisani.
Kuondoshwa
Miezi miwili tu baada ya kufika kwetu katika Vigo, polisi alitushika kwa ghafula. Polisi aliyetushika alikuwa mwenye huruma naye hakutufunga pingu tukielekea kituo cha polisi. Kwenye kituo hicho, tuliona sura tuliyofahamu, mchapa-taipu fulani tuliyekuwa tumemtolea ushahidi karibuni. Kwa wazi aliona aibu sana kutuona tukitendwa kama wahalifu naye akaharakisha kuondoka ili kutuhakikishia kwamba hakutushtaki. Hata hivyo, tulishtakiwa kuwa tunahatarisha hali ya “umoja wa kiroho wa Hispania,” na majuma sita baadaye tulihamishwa.
Lilikuwa pigo, lakini hatukunuia kuacha. Bado kulikuwa na mengi ya kufanya katika Hori ya Iberia. Baada ya miezi mitatu katika Tangier, tulipewa mgawo kwenda Gibraltar—eneo jingine bikira. Kama mtume Paulo asemavyo, ikiwa tunathamini huduma yetu, tutaendelea kufanya kazi nasi tutathawabishwa. (2 Wakorintho 4:1, 7, 8) Hili lilithibitika kuwa kweli kwa habari yetu. Kwenye nyumba ya kwanza kabisa tuliyotembelea katika Gibraltar, tulianzisha funzo la Biblia pamoja na familia hiyo yote. Baada ya muda mfupi, tulikuwa tunaongoza mafunzo 17 kila mmoja wetu. Watu wengi mmoja-mmoja tuliojifunza nao wakawa Mashahidi, na baada ya miaka miwili kulikuwa na kutaniko la wahubiri 25.
Lakini, kama ilivyokuwa katika Vigo, makasisi wakaanza kampeni dhidi yetu. Askofu Mwanglikana wa Gibraltar alimwonya mkuu wa polisi kwamba “hatutakikani,” na njama yake mwishowe ikawa na matokeo. Katika Januari 1962 tuliondoshwa Gibraltar. Tungeenda wapi baadaye? Uhitaji bado ulikuwa mkubwa katika Hispania, kwa hiyo tulirudi huko, tukitumaini kwamba rekodi yetu ya awali ingekuwa imetupwa mbali kufikia sasa.
Jiji la Seville lenye jua lilikuwa makao yetu mapya. Huko tulipata furaha ya kufanya kazi kwa ukaribu na wenzi wa ndoa wengine mapainia, Ray na Pat Kirkup. Ingawa Seville lilikuwa jiji la wakaaji nusu milioni, kulikuwa na wahubiri 21 tu, hivyo kulikuwa na kazi nyingi ya kufanya. Sasa kuna makutaniko 15 yenye wahubiri 1,500. Mwaka mmoja baadaye tulipata jambo la kupendeza; tulialikwa kutumika katika kazi ya kusafiri katika eneo la Barcelona.
Kazi ya mzunguko katika nchi ambapo kazi yetu haikutambuliwa kisheria ilikuwa tofauti kwa njia fulani. Kila juma tulitembelea vikundi vidogo, vingi vikiwa na ndugu wachache sana wenye uwezo. Ndugu hawa wenye bidii walihitaji mazoezi na utegemezo wote ambao tungeweza kuwapa. Tulipenda mgawo huu! Baada ya kutumia miaka kadhaa katika maeneo ambayo yalikuwa na Mashahidi wachache au bila, tulipendezwa kuweza kuwatembelea ndugu na dada wengi tofauti-tofauti. Zaidi ya hayo, kazi ya kuhubiri katika Barcelona ilikuwa rahisi kidogo, na watu wengi walitaka kujifunza Biblia.
Kupigana na Mshuko wa Moyo
Lakini, miezi sita tu baadaye, maisha yangu yakabadilika sana. Likizo yetu ya kwanza ya mapumziko kando ya bahari karibu iwe msiba nilipopata aksidenti iliyosimuliwa awali. Kimwili nilipata nafuu haraka sana kutokana na mshtuko huo wa karibu kuzama, hata hivyo tukio hilo liliacha alama isiyoondoleka kwenye mfumo wangu wa mishipa ya neva.
Kwa miezi michache, nilijikakamua kuendelea na kazi ya kuzunguka, lakini mwishowe ilinibidi kurudi Uingereza kupata matibabu. Baada ya miaka miwili nilipata nafuu kabisa kuweza kurudi Hispania, ambako tulirudia tena kazi ya mzunguko. Hata hivyo, ilikuwa kwa muda mfupi tu. Wazazi wa mke wangu wakawa wagonjwa sana, nasi tukaacha utumishi wa wakati wote ili tuwatunze.
Maisha yakawa magumu hata zaidi katika 1968, nilipopatwa na mvurugiko kamili wa mishipa ya neva. Kuna nyakati Rafaela na mimi tulidhani singepata nafuu kamwe. Ilikuwa kana kwamba, kwa njia tofauti nilikuwa nikizama tena! Kando na kunifanya nijawe na hisia zisizofaa, huo mshuko wa moyo ulininyang’anya nguvu yote. Nilipatwa na vipindi vya uchovu mwingi sana, ulionilazimu kupumzika karibu wakati wote. Wakati huo si ndugu wote waliofahamu aina hii ya tatizo; lakini bila shaka nilijua kwamba Yehova alifahamu. Limekuwa jambo la kuniridhisha sana kusoma nakala za ajabu katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo zimekuwa zenye ufahamu na usaidizi mwingi kwa wale walioshuka moyo.
Katika kipindi hiki chote kigumu, mke wangu alikuwa chanzo cha kitia moyo wakati wote. Kukabili matatizo pamoja kwa kweli kunaimarisha kifungo cha ndoa. Wazazi wa Rafaela wakafa, na baada ya miaka 12, nikapata nafuu kiasi cha kwamba tulihisi tungerudia utumishi wa wakati wote. Katika 1981, kwa mshangao na kupendezwa kwetu, tulialikwa tena kutumika katika kazi ya mzunguko.
Mabadiliko makubwa sana ya kitheokrasi yalikuwa yamefanyika katika Hispania tangu tulipokuwa huko wakati wa kwanza katika huduma ya kusafiri. Kuhubiri kulikuwa huru sasa, hivyo ilinibidi nifahamu hali hizi mpya. Hata hivyo, kutumika nikiwa mwangalizi wa mzunguko kwa mara nyingine tena lilikuwa pendeleo kubwa sana. Kazi ya upainia zijapokuwa hali ngumu ilituwezesha kuwatia moyo mapainia waliokuwa na matatizo. Na mara nyingi tuliweza kuwasaidia wengine kujiunga katika upainia.
Baada ya miaka 11 ya kazi ya kuzunguka katika Madrid na Barcelona, mara nyingine tena afya yetu yenye kudhoofika ilifanya iwe lazima kubadili migawo. Tulipewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee katika jiji la Salamanca, ambapo ningetumika vizuri nikiwa mzee. Ndugu katika Salamanca walifanya tuhisi tumekaribishwa mara moja. Mwaka mmoja baadaye tatizo jingine lilijaribu uvumilivu wetu.
Rafaela akawa hana damu ya kutosha bila sababu yoyote, na majaribio yakaonyesha kwamba alikuwa na kansa ya utumbo mpana. Sasa ilibidi niwe mwenye nguvu na kumpa mke wangu utegemezo wote nilioweza. Jambo la kwanza lilikuwa kutoamini, kukifuatwa na hofu. Je, Rafaela angeokoka hili? Nyakati kama hizi, kumtumaini Yehova kabisa ndiko hutusaidia kuendelea. Nafurahi kusema kwamba upasuaji wa Rafaela ulifaulu, nasi twatumaini kwamba kansa hiyo haitarudi tena.
Ingawa tumepatwa na mazuri na mabaya katika miaka hiyo 36 tuliyotumia katika Hispania, imechangamsha moyo kuishi na kuona wakati huu wa ukuzi wa kiroho. Tumeona kikundi kidogo cha wahubiri 800 katika 1958 kikikua hadi jeshi la wahubiri zaidi ya 100,000 leo. Magumu yetu yamefunikwa na shangwe yetu nyingi—kusaidia wengine wakubali kweli na kukomaa kiroho, kufanya kazi pamoja tukiwa mume na mke, na kuhisi kwamba tumetumia maisha zetu kwa njia bora kabisa.
Paulo asema katika barua yake ya pili kwa Wakorintho: “Kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei [“hatuachi,” NW].” (2 Wakorintho 4:1) Nitazamapo nyuma, naamini kuna mambo kadhaa katika maisha yangu yaliyonizuia kutoacha. Ule mfano wa ndugu watiwa-mafuta waaminifu walionipa upendezi wakati wa miaka yangu ya kwanza ulinipa msingi mzuri. Kuwa na mwenzi anayeshiriki miradi ileile ya kiroho ni msaada wa ajabu; nilipovunjika moyo, Rafaela angeniinua, nami nimefanya vivyohivyo kwake. Kuwa mcheshi ni msaada mkubwa pia. Kuwa na uwezo wa kucheka pamoja na kina ndugu—na kujicheka—kwa njia fulani hufanya matatizo yasionekane kuwa makubwa mno.
Lakini zaidi ya yote, uvumilivu tukabilipo majaribu huhitaji nguvu za Yehova. Mimi hukumbuka maneno ya Paulo: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” Yehova akiwa upande wetu, kamwe hakuna haja ya sisi kuacha.—Wafilipi 4:13.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ronald na Rafaela Taylor katika 1958
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Mkutano wakati wa marufuku katika Hispania (1969)