Ni Kosa la Nani?
MWANADAMU wa kwanza, Adamu, alianza ule mwelekeo. Baada ya kutenda dhambi alimwambia Mungu hivi: “Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala.” Yaani, alikuwa akisema: “Si kosa langu!” Mwanamke wa kwanza, Hawa, alifanya vivyo hivyo aliposema hivi: “Nyoka alinidanganya, nikala.”—Mwanzo 3:12, 13.
Hivyo, kawaida ilianzishwa katika shamba la Edeni ya binadamu kukataa kukubali daraka kwa vitendo vyao wenyewe. Je, umewahi kuwa na hatia ya hili? Matatizo yazukapo, je, wewe hulaumu wengine upesi? Au wewe huchanganua hali ili kuona kosa ni la nani hasa? Katika maisha ya kila siku, ni rahisi sana kunaswa katika kulaumu wengine kwa makosa yetu wenyewe na kusema, “Si kosa langu!” Acheni tuchunguze hali za kawaida na kuona lile watu fulani huelekea kufanya. La maana zaidi, fikiria lile ungelifanya chini ya hali zinazofanana na hizo.
Magumu ya Kifedha
“Si kosa langu—ni uchumi, wanabiashara waliopotoka, gharama za maisha zilizopanda,” wengine huenda wakasema wanapojikuta wenyewe katika matatizo makubwa ya kifedha. Lakini mambo haya ni ya kulaumiwa kweli? Labda hali fulani ziliwaongoza kwenye biashara za kukisia-kisia au zinazotilika shaka. Nyakati fulani pupa hufunika uhalisi, na watu hujikuta wenyewe katika biashara wasizozijua, wakija kuwa windo la wanabiashara wenye pupa na hila. Wao husahau mithali ya kale, “Si chote kimetacho kilicho dhahabu.” Wao hutafuta mashauri wanayotaka kusikia, lakini magumu ya kiuchumi yazukapo, wao hutafuta mtu mwingine wa kulaumu. Kwa kusikitisha, hili nyakati fulani hutukia hata katika kutaniko la Kikristo.
Wengine wamenaswa katika mipango ya biashara isiyo ya kihekima au yenye kutilika shaka, kama vile kununua almasi ambazo hazikuwapo, kulipia gharama za programu za televisheni zinazofaulu sana zilizokwisha haraka, au kutegemeza usitawi wa mashamba na nyumba uliofilisika. Tamaa isiyotoshelezwa ya utajiri huenda ilififisha kumbukumbu lao juu ya shauri hili la Biblia: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi . . . na kujichoma kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.
Utumizi usiozuiwa waweza kuongoza kwenye angamizo la kifedha. Wengine huhisi kwamba ni lazima waonekane kama watu walio katika magazeti ya fashoni ya karibuni zaidi, wachukue likizo zenye kugharimu sana, wale katika mikahawa ya hali ya juu, na wanunue “vichezeo” vya watu wazima vya karibuni zaidi—magari ya tafrija, mashua, kamera, vyombo vya muziki. Bila shaka, baada ya muda huenda wengine wakaweza kupata vitu hivi kupitia mipango ya werevu na kujiwekea akiba. Lakini wale walio na haraka kuvipata huenda wakajikuta wenyewe katika deni kubwa. Ikiwa wajikuta hivyo, ni kosa la nani? Ni wazi wamepuuza shauri timamu la Mithali 13:18: “Umaskini na fedheha zitampata yeye akataaye kurudiwa.”
Kutofanikiwa kwa Watoto
“Ni kosa la wazee kwamba watoto wangu waliacha kweli,” huenda wakasema wazazi fulani. “Hawakutoa uangalifu wa kutosha kwa watoto wangu.”
Wazee wana daraka la kuchunga na kutunza kundi, lakini namna gani wazazi wenyewe? Je, wanaweka kielelezo kizuri katika kudhihirisha tunda la roho ya Mungu katika yote wafanyayo? Je, funzo la Biblia la familia liliongozwa kwa ukawaida? Je, wazazi walionyesha bidii katika utumishi wa Yehova na kusaidia watoto kutayarisha kwa ajili yalo? Je, walitahadhari kuhusu washiriki wa watoto wao?
Vilevile, ni rahisi kwa mzazi kusema kuhusiana na kazi ya shule: “Ni kosa la walimu kwamba mwana wangu hakufanya vizuri katika shule. Hawakumpenda mwana wangu. Na kwa vyovyote shule hiyo ina kiwango cha chini sana cha elimu.” Lakini, je, mzazi huyo aliwasiliana kwa ukaribu na shule hiyo? Je, mzazi alipendezwa na mafunzo na masomo ya mtoto huyo? Je, masomo yake ya kufanyia nyumbani yaliratibiwa, na msaada ulitolewa ulipohitajika? Je, yawezekana tatizo kuu ni suala la mtazamo au uvivu kwa upande wa mtoto au mzazi?
Badala ya wazazi kulaumu mfumo wa shule, ni yenye matokeo zaidi ikiwa wangechukua hatua chanya ili kuhakikisha kuwa watoto wao wana mtazamo ufaao na kwamba wanatumia fursa za kujifunza wazipatazo shuleni.
Kukosa Kusitawi Kiroho
Mara kwa mara sisi husikia mtu fulani akisema: “Ningekuwa na nguvu kiroho, lakini si kosa langu kwamba siko hivyo. Wazee hawatoi uangalifu wa kutosha kwangu. Sina marafiki wowote. Roho ya Yehova haiko juu ya kutaniko hili.” Wakati uleule, wengine kutanikoni wana marafiki, wana furaha, na wafanya maendeleo mazuri ya kiroho; na kutaniko labarikiwa kwa ukuzi na ufanisi wa kiroho. Kwa hiyo, ni kwa sababu gani wengine wanakuwa na matatizo?
Ni watu wachache watakao kuwa waandamani wa karibu wa wale wadhihirishao roho iliyo hasi na ya kunung’unika. Ulimi mkali, unaokata na kunung’unika kusikokoma kwaweza kuvunja moyo zaidi. Wakiwa hawataki kudhoofishwa kiroho, wengine huenda wakawekea mipaka ushirika wao wa kijamii na watu kama hao. Kwa kuchukulia hili kuwa ubaridi kwa upande wa kutaniko, huenda mtu akaanza uhamaji, akihama kwanza kwenye kutaniko moja, halafu kwenye jingine, na jingine tena. Kama kundi la wanyama wahamaji wa nyanda za Afrika ambao nyakati zote hutafuta majani mabichi zaidi, Wakristo hawa “wahamaji” nyakati zote hutafuta kutaniko linalowafaa vizuri. Badala ya hivyo, jinsi wangekuwa na furaha ikiwa wangeangalia, sifa nzuri katika watu wengine na kujitahidi kudhihirisha kwa ukamili lile tunda la roho ya Mungu katika maisha zao wenyewe!—Wagalatia 5:22, 23.
Wengine hufanya hivyo kwa kufanya bidii ya kipekee kusema na mtu tofauti katika kila mkutano kwenye Jumba la Ufalme na kumpongeza kwa unyoofu katika jambo jema. Ingeweza kuwa ni kuhusu watoto wake wenye tabia njema, ukawaida katika mikutano ya Kikristo, maelezo yaliyotayarishwa vyema katika Funzo la Mnara wa Mlinzi, ukarimu wake kwa kuruhusu nyumba yake itumiwe kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko na mikutano ya utumishi wa shambani, na kadhalika. Kwa kufanya liwe lengo lako kuona sifa bora ambazo mwanzoni zaweza kufunikwa na kutokamilika, utagundua sifa bora katika ndugu na dada zako Wakristo. Hili litafanya wakupende, na utakuta kwamba huna uhaba wa marafiki waaminifu-washikamanifu.
Kisingizio Kikuu
“Ni mapenzi ya Mungu.” “Mlaumu Ibilisi.” Yamkini kisingizio kikuu ni kumlaumu Mungu au Ibilisi kwa mapungukio yetu wenyewe. Ni kweli kwamba Mungu au Shetani huenda wakaathiri matukio fulani maishani mwetu. Hata hivyo, wengine huamini kwamba kwa kweli kila kitu, kizuri au kibaya, maishani mwao ni tokeo la uingilio wa Mungu au wa Shetani. Ni kana kwamba hakuna chochote kilichowapata kilikuwa tokeo la matendo yao wenyewe. “Mungu akitaka nipate gari hilo jipya, atahakikisha kuwa nimelipata.”
Watu kama hao mara nyingi huishi maisha yao kijahili, wakifanya maamuzi ya kifedha na mengine katika wazo la kwamba Mungu atawaokoa. Matendo yao yasiyo na busara yakitokeza msiba, kiuchumi au vingine, wanalaumu Ibilisi. Kufanya jambo kwa kutofikiri bila ‘kuhesabu gharama’ kwanza halafu kulaumu Shetani kwa kutofaulu, au kwa ubaya zaidi, kutazamia Yehova aingilie, hakungekuwa umbelembele tu bali pia kinyume cha Maandiko.—Luka 14:28, 29.
Shetani alijaribu kumfanya Yesu afikiri hivyo na kutochukua daraka kwa matendo Yake. Kuhusu jaribu la pili, Mathayo 4:5-7 huripoti hivi: “Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; na mikononi mwao watakuchukua; usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.” Yesu alitambua kuwa hangelitazamia Yehova aingilie ikiwa angechukua mwendo ambao kwa wazi ulikuwa wa kipumbavu, na hata wa ujiuaji. Kwa hiyo, yeye alijibu hivi: “Imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako.”
Wale walio na maelekeo ya kumlaumu Ibilisi au Mungu kwa matendo yao yenye kutilika shaka wafanana sana na wafuasi wa astrolojia, ambao huweka nyota mahali pa Mungu au Ibilisi. Wakisadikishwa kabisa kwamba karibu kila kitu kitokeacho ni chenye kupita udhibiti wao, wao hupuuza ile kanuni rahisi itajwayo katika Wagalatia 6:7: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”
Kukabili Uhalisi
Hakuna atakayepinga kwamba tunaishi katika ulimwengu usiokamilika. Matatizo yaliyozungumziwa hapa ni halisi. Watu watatupunja kifedha. Waajiri fulani watakuwa waonevu. Watu tuwajuao huenda wakaathiri watoto wetu vibaya. Waalimu na shule fulani zahitaji marekebisho. Nyakati fulani wazee wangeliweza kuwa wenye upendo na wenye kushughulikia mambo zaidi. Lakini lazima tukubali athari za kutokamilika na kwamba, kama Biblia inayotaja, “dunia [“ulimwengu,” NW] yote pia hukaa katika yule mwovu.” Kwa hivyo, si jambo lililo halisi kutazamia kwamba kijia chetu kupitia maisha kitakuwa shwari kila wakati.—1 Yohana 5:19.
Kwa kuongezea, lazima tukumbuke kutokamilika kwetu wenyewe na udhaifu na tutambue kwamba mara nyingi matatizo yetu ni tokeo la upumbavu wetu wenyewe. Paulo alionya Wakristo katika Roma hivi: “Namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia.” (Warumi 12:3) Shauri hilo latumika na nguvu ileile kwetu leo. Jambo fulani liendapo vibaya maishani mwetu, hatutawaiga mara moja wazazi wetu wa kale Adamu na Hawa na kusema: “Si kosa langu!” Badala ya hivyo, tutajiuliza, ‘Ningelifanya nini tofauti ili kuepuka tokeo hili lenye kuhuzunisha? Je, nilifanya uamuzi timamu katika jambo hilo na kutafuta shauri kutoka chanzo chenye hekima? Je, nilichukulia yule mwingine au wale wengine waliohusika kuwa wasio na hatia nikiwapa heshima?’
Tukifuata kanuni za Kikristo na kujizoeza uamuzi timamu, tutakuwa na marafiki wengi na matatizo haba. Mengi ya matatizo yasiyo na maana katika maisha yetu ya kila siku yatapunguzwa. Tutapata shangwe katika kushughulika kwetu na wengine na hatutasumbuliwa na lile swali: “Ni kosa la nani?”
[Picha katika ukurasa wa 28]
Wazazi waweza kufanya mengi ili kusaidia watoto wao wasitawi kiroho