Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 5/1 kur. 26-29
  • Badiliko la Mgawo Nikiwa na Umri wa Miaka 80

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Badiliko la Mgawo Nikiwa na Umri wa Miaka 80
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kweli ya Biblia Yageuza Maisha Zetu
  • Vielelezo Vilivyotutia Nguvu
  • Kupainia Katika East Anglia
  • Wakati wa Vita na Familia
  • Uamuzi Wetu wa Kwenda Hispania
  • “Kwa Kuwa Tuna Huduma Hii . . . , Hatuachi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Akina Mama—Jifunzeni Kutokana na Mfano wa Eunike
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kukaza Macho na Moyo Kwenye Tuzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 5/1 kur. 26-29

Badiliko la Mgawo Nikiwa na Umri wa Miaka 80

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GWENDOLINE MATTHEWS

Nilipofika umri wa miaka 80, mume wangu nami tuliamua kufunga vitu vyote tulivyokuwa navyo, tukaviweka katika gari la kukodi na kuondoka Uingereza kwenda Hispania. Hatukuzungumza Kihispania, na tulikuwa tukienda kusini-magharibi mwa Hispania, mbali na watalii wenye kuzungumza Kiingereza waliozuru mara nyingi. Wengi wa rafiki zetu walifikiri tulikuwa na kichaa, lakini nilijikumbusha kwa uchangamfu kwamba, Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75 alipoondoka Uru.

KAMA ilivyotokea kuwa, miaka ambayo tumeishi Hispania tangu tuwasili hapa katika Aprili 1992, imekuwa baadhi ya miaka yenye kuthawabisha zaidi maishani mwetu. Lakini kabla ya kuwaeleza sababu iliyotufanya tuhame, acheni niwaambie jinsi maisha katika utumishi wa Yehova yalivyotuongoza kufanya uamuzi mkubwa hivyo.

Kweli ya Biblia Yageuza Maisha Zetu

Nililelewa katika nyumba ya kidini huko kusini-magharibi mwa London, Uingereza. Mama alikuwa akipeleka dada yangu nami kwenda mahali tofauti-tofauti pa ibada alipokuwa akitafuta kujitosheleza kiroho. Baba yangu, aliyekuwa na ugonjwa wa kudumu wa kifua kikuu, hakuwa akiandamana nasi. Lakini alikuwa msomaji mwenye bidii wa Biblia, naye aliipiga mstari kila mara alipoona kifungu chenye kumwelimisha. Mojawapo ya mali zangu nizithaminizo sana, ni Biblia hiyo iliyochakaa sana ambayo ilikuwa yenye maana kubwa kwa Baba.

Mwaka wa 1925, nilipokuwa na umri wa miaka 14, trakti fulani iliwekwa chini ya mlango wetu, nayo ilitualika kwenda kwenye hotuba ya watu wote kwenye jumba la mji huko West Ham. Mama yangu na jirani fulani waliamua kuhudhuria hiyo hotuba, na dada yangu nami tukaandamana nao. Ile hotuba, “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” ilipanda mbegu za kweli ya Biblia moyoni mwa Mama.

Miezi michache baadaye, Baba alikufa akiwa na umri wa miaka 38. Kifo chake kilikuwa pigo kubwa, kwa kuwa kilituacha tukiwa tumevunjika moyo na tukiwa fukara. Kwenye ibada ya ukumbusho, iliyofanywa katika Kanisa la Uingereza la mahali hapo, Mama alishtuka kumsikia kasisi akidai kwamba nafsi ya Baba ilikuwa mbinguni. Alijua kutoka katika Biblia kwamba wafu wanalala kaburini, na aliamini kwa dhati kwamba siku moja Baba angefufuliwa kwenye uhai udumuo milele duniani. (Zaburi 37:9-11, 29; 146:3, 4; Mhubiri 9:5; Matendo 24:15; Ufunuo 21:3, 4) Akiwa amesadikishwa kwamba ilimpasa ashirikiane na watu waliofunza Neno la Mungu, aliazimia kusitawisha kufahamiana kwake na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.

Kwa kuwa hatukuwa na fedha za usafiri, kila juma tulitembea kwa muda wa saa mbili kutoka nyumbani kwetu hadi kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Baadaye, tulitumia saa nyingine mbili tukitembea kwa uchovu kurudi nyumbani. Lakini tuliithamini mikutano hiyo sana, na hatukukosa hata mmoja, hata wakati ambapo ule ukungu mbaya wa London ulikuwa umelikumba hilo jiji. Punde si punde Mama akaamua kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa, na mwaka wa 1927, nikabatizwa pia.

Licha ya magumu yetu ya kiuchumi, sikuzote Mama alinifunza kutanguliza mambo ya kiroho. Andiko la Mathayo 6:33 lilikuwa mojawapo ya maandiko aliyopenda zaidi, na kwa kweli ‘alitafuta ufalme kwanza.’ Mwaka wa 1935, alipokufa kabla ya wakati kwa sababu ya kansa, alikuwa akipanga kujiunga na wahudumu wa wakati wote ambao wangeweza kuhamia Ufaransa, wakatumikie huko.

Vielelezo Vilivyotutia Nguvu

Katika miaka hiyo ya mapema, watu fulani waliohudhuria mikutano katika London walitaka kujulisha maoni yao, nao walianzisha mabishano na mifoko mikali. Hata hivyo, sikuzote Mama alisema kwamba, lingekuwa jambo la kukosa uaminifu-mshikamanifu kuliacha tengenezo la Yehova baada ya yale yote tuliyokuwa tumejifunza kutokana nalo. Ziara za Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society wakati huo, zilituchochea kuendelea kutumikia kwa uaminifu-mshikamanifu.

Namkumbuka Ndugu Rutherford kuwa mwanamume mwenye fadhili na mwenye kufikika. Nilipokuwa bado tineja, Kutaniko la London lilikuwa na matembezi ambayo yeye alikuwapo. Aliniona—tineja ambaye kwa njia fulani alikuwa mwenye haya—nikiwa na kamera, akaniuliza ikiwa nilitaka kumpiga picha. Picha hiyo ilipata kuwa kumbukumbu lenye kuthaminiwa sana.

Baadaye zaidi, jambo lililonipata lilikazia akilini mwangu tofauti kati ya wale wenye kuongoza katika kutaniko la Kikristo na wanadamu mashuhuri wa ulimwengu. Nilikuwa nikitumikia nikiwa mhudumu wa mezani katika nyumba kubwa huko London ambamo Franz von Papen, mmoja wa wajumbe wa Hitler, alikuwa amealikwa kwa chakula cha mchana. Alipokuwa akila, alikataa kuvua upanga wake uvaliwao na mavazi rasmi, na nilijikwaa kwa sababu ya huo upanga na kumwaga mchuzi niliokuwa nikibeba. Alisema kwa hasira kwamba kule Ujerumani, kutojali kama huko kungefanya nipigwe risasi. Kwa muda uliosalia wa mlo huo, nilikaa mbali kabisa naye!

Mwaka wa 1931, mkusanyiko wa maana sana ulifanywa katika Alexandra Palace ambako nilimsikia Ndugu Rutherford akizungumza. Huko, tulikubali kwa shauku jina letu jipya, Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10, 12) Mwaka wa 1933, miaka miwili baadaye, nilijiunga na utumishi wa painia, kama vile huduma ya wakati wote iitwavyo. Baraka nyingine nikumbukayo ambayo niliipata miaka hiyo, ilikuwa ushirika nilioweza kuwa nao pamoja na vijana wanaume wazuri, ambao baadaye walipata kuwa wamishonari katika sehemu za mbali sana za dunia. Hao walitia ndani Claude Goodman, Harold King, John Cooke, na Edwin Skinner. Vielelezo hivyo vya uaminifu vilinifanya nitake kutumikia katika shamba la kigeni.

Kupainia Katika East Anglia

Mgawo wangu wa painia ulikuwa katika East Anglia (mashariki mwa Uingereza), na kuhubiri huko kulihitaji shauku na bidii. Ili kuhubiri eneo letu kubwa, tulisafiri kwa baiskeli kutoka mji hadi mji na kutoka kijiji hadi kijiji na kukaa katika vyumba vya kukodi. Hakukuwa na makutaniko yoyote katika eneo hilo, kwa hiyo mwenzangu nami tulizungumzia peke yetu sehemu zote za mikutano ya kawaida ya kila juma. Katika huduma yetu, tuliangusha mamia ya vitabu na vijitabu vilivyoeleza makusudi ya Mungu.

Tulifanya ziara moja ya kukumbukwa kwenye nyumba ya pasta ambako tulizungumza na kasisi wa mahali hapo wa Kanisa la Uingereza. Katika maeneo mengi, tuliahirisha ziara yetu ya kwenda kwa huyo kasisi Mwanglikana hadi akawa wa mwisho kutembelewa, kwa sababu mara nyingi alifanya mambo yawe magumu kwetu alipojua kwamba tulikuwa tukihubiri habari njema katika hilo eneo. Lakini katika kijiji hicho, kila mtu alimsifu huyo kasisi. Aliwatembelea wagonjwa, akawaazima vitabu waliofurahia kusoma, na hata kuwazuru nyumbani waparokia wake na kuwaeleza juu ya Biblia.

Kwa kweli, tulipomzuru, alikuwa mwenye urafiki sana, akakubali vitabu kadhaa. Alituhakikishia pia kwamba, ikiwa yeyote kijijini humo alitaka kuwa na baadhi ya vitabu vyetu lakini hakuweza kuvilipia, yeye angeweza kuwalipia. Tulipata habari kwamba mambo yenye kuogofya yaliyompata katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalikuwa yamemfanya aazimie kuendeleza amani na nia njema katika parokia yake. Kabla ya sisi kuondoka, alitubariki na kututia moyo tuendelee na kazi yetu nzuri. Maneno yake ya kutuaga yalikuwa yale ya Hesabu 6:24: “Bwana awabariki, na kuwatunza.”—King James Version.

Mama alikufa miaka miwili baada ya mimi kuanza kupainia, nami nikarudi London bila fedha wala familia. Shahidi kutoka Scotland mwenye kuthaminiwa sana alinikaribisha kwake, akanisaidia kukabiliana na kifo cha Mama, na kunitia moyo niendelee na huduma ya wakati wote. Kwa hiyo nilirudi East Anglia pamoja na Julia Fairfax, painia mwenzi mpya. Tulitengeneza gari la zamani (trela) ili litumike likiwa makao yaendayo; tulitumia tingatinga au lori kuyahamisha kwenda hapa na pale. Tukiwa pamoja na wenzi wa ndoa Albert na Ethel Abbott, waliokuwa wenye umri mkubwa zaidi, ambao pia walikuwa wamefanya gari dogo kuwa makao, tuliendelea kuhubiri. Albert na Ethel walikuwa kama wazazi kwangu.

Nilipokuwa nikipainia huko Cambridgeshire, nilijuana na John Matthews, ndugu mzuri Mkristo ambaye tayari alikuwa amethibitisha uaminifu-maadili wake kwa Yehova chini ya hali ngumu. Tulioana mwaka wa 1940, muda mfupi baada ya kuanza kwa vita ya ulimwengu ya pili.

Wakati wa Vita na Familia

Tulipokuwa wenzi wapya wa ndoa, nyumba yetu ilikuwa gari dogo mno, ukubwa wake ukiwa karibu sawa na chumba kidogo cha kupikia, na tulisafiri katika huduma yetu kwa kutumia pikipiki yenye kutegemeka. Mwaka mmoja baada ya kuoana, John alihukumiwa kufanya kazi ngumu katika shamba wakati ambapo alikataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya masadikisho yake yenye kuitegemea Biblia. (Isaya 2:4) Ingawa hilo lilimaanisha kutoendelea na upainia wetu, hukumu ya John ilithibitika kuwa yenye kufaa kwa kuwa nilikuwa mja mzito na angeweza kututegemeza.

Wakati wa miaka ya vita, tulifurahia mikutano ya pekee iliyofanywa kujapokuwa na shida mbalimbali. Mwaka wa 1941, John nami nikiwa na mimba ya mtoto wetu wa kwanza tulisafiri kwa pikipiki yetu hadi Manchester, umbali wa kilometa 300. Tulipata miji mingi njiani, iliyokuwa imeharibiwa kwa mabomu, na tulijiuliza ikiwa mkutano ungeweza kufanywa chini ya hali kama hizo. Ulifanywa. Mashahidi kutoka sehemu nyingi za Uingereza walijaza jumba liitwalo The Free Trade Hall katikati ya Manchester, na sehemu zote kwenye programu zilitolewa.

Kwenye umalizio wa hotuba yake, msemaji wa mwisho wa mkusanyiko aliwaambia wasikilizaji kwamba walipaswa kuondoka mahali hapo mara moja, kwa kuwa shambulio la ndege lilitarajiwa. Hilo onyo lilikuwa la wakati ufaao. Hatukuwa tumeenda mbali sana na hilo jumba, wakati ambapo tulisikia ving’ora na bunduki za kutungua ndege. Tukitazama nyuma tuliona idadi kubwa ya ndege ikiangusha mabomu katikati ya hilo jiji. Huko mbali, katikati ya mioto na moshi, tuliliona lile jumba ambamo tulikuwa tumetoka tu kuketi; liliharibiwa kabisa! Tulifurahi kwamba, hakuna yeyote wa ndugu au dada zetu Wakristo aliyeuawa.

Tulipowalea watoto wetu, hatukuweza kupainia, lakini tuliwakaribisha nyumbani kwetu waangalizi wasafirio na mapainia waliokuwa bila mahali pa kulala. Wakati mmoja, mapainia sita walikaa nyumbani mwetu kwa miezi kadhaa. Bila shaka kushirikiana na watu kama hao, kulikuwa sababu moja iliyomfanya binti yetu Eunice achague kuanza upainia mwaka wa 1961 alipokuwa na umri wa miaka 15 tu. Yasikitisha kusema kwamba mwana wetu, David, hakuendelea kumtumikia Yehova alipokuwa mtu mzima, naye Linda, binti yetu mwingine, alikufa wakati wa vita chini ya hali zenye kuhuzunisha.

Uamuzi Wetu wa Kwenda Hispania

Kielelezo na kitia-moyo cha Mama kilikuwa kimechochea ndani yangu tamaa ya kuwa mishonari, mradi ambao sikuusahau kamwe. Hivyo, tulipendezwa wakati ambapo Eunice aliondoka Uingereza mwaka wa 1973 kwenda Hispania, ambako uhitaji wa wapiga-mbiu wa Ufalme ulikuwa mkubwa. Bila shaka, tulisikitika kumwona akienda, lakini pia tuliona fahari kwamba alitaka kutumikia katika nchi ya kigeni.

Tulimzuru Eunice kwa miaka mingi, na tulipata kuijua Hispania vizuri. Kwa kweli, John nami tulimzuru kwenye migawo minne kati ya migawo yake tofauti. Kisha miaka ilipopita, nguvu zetu zilianza kupungua. John alianguka na afya yake ikaathiriwa sana, nami nilikuwa na matatizo ya moyo na ya kikoromeo. Mbali na hayo, sisi wawili tuliugua yabisi-kavu. Ingawa kwa kweli tulihitaji msaada wa Eunice, hatukutaka aache mgawo wake kwa ajili yetu.

Tulizungumza pamoja na Eunice juu ya machaguo yetu, na kusali ili tupate mwongozo. Alikuwa tayari kuja nyumbani kutusaidia, lakini tuliamua kwamba utatuzi ulio bora ungekuwa John nami tuishi naye huko Hispania. Ikiwa mimi mwenyewe singeweza kuwa mishonari, angalau ningemwunga mkono binti yangu na waandamani wake wawili mapainia katika utumishi wa wakati wote. Kufikia wakati huo, John nami tuliwaona Nuria na Ana, mapainia wenzi wa Eunice kwa miaka ipatayo 15, kuwa binti zetu wenyewe. Nao walifurahia tuishi nao kokote kule ambako wangeweza kugawiwa kwenda.

Zaidi ya miaka sita imepita tangu tulipofanya uamuzi huo. Afya yetu haijaadhoofika zaidi, na kwa hakika maisha zetu zimepata kuwa za kuvutia zaidi. Bado siwezi kuzungumza Kihispania sana, lakini jambo hilo halinizuii kuhubiri. John nami hujisikia nyumbani tukiwa katika kutaniko letu dogo lililoko Extremadura, kusini-magharibi mwa Hispania.

Kuishi Hispania kumenifunza mengi kuhusu hali ya kimataifa ya kazi yetu ya kuhubiri Ufalme, na sasa naelewa kwa wazi zaidi sana jinsi, kama vile Yesu Kristo alivyosema, “shamba ndio ulimwengu.”—Mathayo 13:38.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikipainia katika miaka ya 1930

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki