Mwisho wa Chuki Ulimwenguni Pote
MIAKA elfu mbili hivi iliyopita, kikundi kidogo ndicho kilichochukiwa. Tertullian aeleza hivi mtazamo wenye kuenea wa Warumi kuelekea Wakristo wa mapema: “Ikiwa mbingu hazitoi mvua, ikiwa kuna tetemeko la dunia, ikiwa kuna njaa kuu au magonjwa, mara hiyo yowe ni, ‘Wapelekeni Wakristo wakaliwe na simba!’”
Wakristo wa mapema walikataa jaribu la kulipiza kisasi cha kutotendewa kwa haki, ijapokuwa walikuwa watu wa kuchukiwa na watu wote. Katika Mahubiri yake ya Mlimani yajulikanayo sana, Yesu Kristo alisema: “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako. Lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.”—Mathayo 5:43, 44.
Lilikuwa ndilo pokeo la mdomo tu la Wayahudi lililoshikilia itikadi ya kwamba ‘kuchukia adui’ kulikuwa ndilo jambo lifaalo. Hata hivyo, Yesu, alisema ni lazima tumpende adui yetu, si rafiki yetu tu. Jambo hili ni gumu lakini lawezekana. Kupenda adui hakumaanishi kupenda njia au matendo yake yote. Neno la Kigiriki lipatikanalo katika simulizi la Mathayo limetokana na a·gaʹpe, lielezalo upendo ambao hutenda kwa kupatana na kanuni. Mtu adhihirishaye a·gaʹpe, upendo wa kanuni, hufanya mema hata kwa adui anayemchukia na kumtenda vibaya. Kwa nini? Kwa sababu ndiyo njia ya kumwiga Kristo, na ndiyo njia ya kushinda chuki. Msomi mmoja wa Kigiriki alionelea hivi: “[A·gaʹpe] hutusaidia kushinda mwelekeo wetu wa asili wa kuwa na hasira na uchungu.” Lakini je, hili lawezekana katika ulimwengu huu wa leo wenye kujaa chuki?
Inakubaliwa kwamba, sio wote wanaodai kuwa Wakristo huazimia kufuata kielelezo cha Kristo. Ule ukatili wa juzijuzi katika Rwanda ulifanywa na vikundi vya kikabila, ambavyo wengi wavyo hudai kuwa Wakristo. Pilar Díez Espelosín, mtawa wa kike wa Katoliki ya Kiroma ambaye amefanya kazi katika Rwanda kwa miaka 20, anakumbuka tukio moja lenye kuchoma moyo. Mwanamume fulani alikaribia kanisa akiwa na mkuki mkononi ambao bila shaka alikuwa akiutumia. Huyo mtawa wa kike akamuuliza hivi: “Unafanya nini ukienda ukiwaua watu? Je, humfikirii Kristo?” Alidai kuwa alikuwa akimfikiria naye akaanza kuingia kanisani, kupiga magoti, na kurudia maneno ya Tasbihi kwa bidii. Lakini alipomaliza, huyo akatoka na kuendelea kuua. “Hilo laonyesha kwamba hatufundishi gospeli kwa njia inayofaa,” mtawa huyo wa kike akakubali. Hata hivyo, kushindwa huko, hakumaanishi kwamba ujumbe wa Yesu ni wenye kasoro. Chuki inaweza kushindwa na wale wafuatao Ukristo wa kweli.
Kuishinda Chuki Katika Kambi ya Mateso
Max Liebster ni Myahudi wa asili aliyeokoka Maangamizi Makubwa. Ingawa jina lake la ziada humaanisha “mpendwa,” ameona chuki nyingi sana. Yeye aeleza aliyojifunza katika Ujerumani ya Nazi juu ya upendo na chuki.
“Nililelewa karibu ya Mannheim, Ujerumani, wakati wa miaka ya 1930. Hitler alidai kwamba Wayahudi wote walikuwa matajiri wenye kujifaidi waliokuwa wakinyonya watu wa Ujerumani. Lakini ukweli ni kwamba baba yangu alikuwa mshona-viatu tu wa hali ya chini. Hata hivyo, kwa sababu ya propaganda za Nazi, majirani walianza kugeuka dhidi yetu. Nilipokuwa tineja, mwanakijiji alinipaka kinguvu damu ya nguruwe kwenye kipaji cha uso wangu. Ubaya huu mkubwa ulikuwa mwonjo tu wa yale yaliyokuwa yakija. Katika 1939 Gestapo walinikamata na kutwaa mali yangu yote.
“Kutoka Januari 1940 hadi Mei 1945, niling’ang’ana kuishi katika kambi tano za mateso: Sachsenhausen, Neuengamme, Auschwitz, Buna, na Buchenwald. Baba yangu, aliyepelekwa pia Sachsenhausen, alikufa wakati wa majira ya baridi kali sana ya 1940. Mimi mwenyewe nilibeba maiti yake hadi mahali pa kuchomea maiti, ambapo rundo la miili iliyokuwa imekufa ilikuwa imelala ikingoja kuchomwa. Kwa jumla, wanane wa familia yangu walikufa katika kambi hizo.
“Miongoni mwa wafungwa kapos walichukiwa sana hata kuliko askari wa SS. Hao kapos walikuwa wafungwa walioshirikiana na askari wa SS na hivyo kufurahia mapendeleo fulani. Waliwekwa kusimamia ugavi wa chakula, na pia waliwapiga mijeledi kijeuri wafungwa wengineo. Mara nyingi walitenda isivyo haki na kwa ukatili. Nafikiri nilikuwa na sababu ya kutosha kuchukia askari wa SS na kapos, lakini wakati wa kifungo changu, nilijifunza kwamba upendo una nguvu nyingi zaidi kuliko chuki.
“Uimara wa wafungwa waliokuwa Mashahidi wa Yehova ulinihakikishia kwamba imani yao ilikuwa na msingi wa Maandiko—nami mwenyewe nikawa Shahidi. Ernst Wauer, Shahidi niliyemkuta katika kambi ya mateso ya Neuengamme, alinisihi nisitawishe mtazamo wa akilini wa Kristo. Biblia husema kwamba “yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.” (1 Petro 2:23) Nilijaribu kufanya vivyo hivyo, kuacha kisasi mikononi mwa Mungu, aliye Hakimu wa wote.
“Miaka yangu katika kambi hizo ilinifunza kwamba watu mara nyingi hufanya mambo maovu kwa kutojua. Hata si askari wa SS wote waliokuwa wabaya—kulikuwa na mmoja aliyeokoa uhai wangu. Wakati mmoja niliugua ugonjwa mbaya sana wa kuhara nami nikawa dhaifu sana nisiweze kutembea kutoka kazini kwenda kwenye kambi. Ningalipaswa asubuhi iliyofuata nipelekwe kwenye vyumba vya gesi ya sumu yenye kuua ya Auschwitz, lakini askari mmoja wa SS, tuliyetoka sehemu moja naye ya Ujerumani, akaingilia mambo kwa niaba yangu. Alifanya mpango nifanye kazi katika chumba cha vyakula cha askari wa SS, ambamo niliweza kupata pumziko la kiasi fulani hadi nilipopata nafuu. Siku moja alikiri kwangu hivi: ‘Max, nahisi nikiwa ndani ya gari-moshi linaloendeshwa kwa mwendo wa kasi sana bila udhibiti. Nikiruka, nitauawa. Nikikaa ndani, nitaangamia!’
“Watu hawa walihitaji upendo sawa na nilivyohitaji. Kwa kweli, ulikuwa upendo na huruma, pamoja na imani yangu katika Mungu, ulioniwezesha kukabiliana na hali hiyo ngumu na tisho la kila siku la kuuawa. Siwezi kusema kwamba niliokoka bila kuumia, lakini majeraha yangu ya kihisia-moyo yalikuwa machache.”
Uchangamfu na fadhili ambazo bado Max anaonyesha miaka 50 baadaye ni ushahidi wenye nguvu wa kweli ya maneno yake. Kisa cha Max si cha pekee. Yeye alikuwa na sababu ya kutosha kuishinda chuki—alitaka kumwiga Kristo. Wengine ambao maisha zao zimeongozwa na Maandiko wametenda kwa njia hiyohiyo. Simone, mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoka Ufaransa, aeleza jinsi alivyojifunza maana hasa ya upendo usio na ubinafsi.
“Mama yangu Emma, aliyekuja kuwa Shahidi muda mfupi kabla ya vita ya ulimwengu ya pili, alinifundisha kwamba mara nyingi watu hufanya mambo mabaya kwa sababu ya kutojua mambo yalivyo. Yeye alieleza kwamba tukiwachukia vilevile, sisi si Wakristo wa kweli, kwa kuwa Yesu alisema tunapaswa kuwapenda adui zetu na kusali kwa niaba ya wale wanaotunyanyasa.—Mathayo 5:44.
“Nakumbuka hali moja iliyokuwa ngumu sana iliyotahini sadikisho hili. Wanazi walipotwaa Ufaransa, mama aliteseka sana kwa sababu ya jirani katika jengo letu. Jirani huyo alimshtaki mama kwa Gestapo, na kama tokeo, mama yangu akatumia miaka miwili katika kambi ya mateso ya Ujerumani, ambako alinusurika kifo. Baada ya vita, askari wa Ufaransa walitaka mama atie sahihi karatasi ya kumtia mwanamke huyu katika hatia ya kuwa msaidizi wa Wajerumani. Lakini mama yangu alikataa, akisema kwamba ‘Mungu ndiye Hakimu na Mthawabishaji wa mema na mlipiza-kisasi wa uovu.’ Miaka michache baadaye, jirani huyohuyo akaugua kansa yenye kufisha. Badala ya kufurahia msiba wake, mama yangu alitumia saa nyingi akifanya miezi ya mwisho ya maisha ya huyo mama kuwa yenye kustarehesha iwezekanavyo. Mimi sitasahau kamwe ushindi huu wa upendo dhidi ya chuki.”
Vielelezo hivi viwili vinatoa kielezi cha nguvu za upendo wa kanuni wakati wa kukabiliwa na ukosefu wa haki. Walakini, Biblia yenyewe husema kwamba kuna “wakati wa kupenda, na wakati wa kuchukia.” (Mhubiri 3:1, 8) Hili lawezekanaje?
Wakati wa Kuchukia
Mungu hakatazi chuki yote. Kuhusu Yesu Kristo, Biblia husema: “Umependa haki, umechukia maasi.” (Waebrania 1:9) Hata hivyo, kuna tofauti, kati ya kuchukia kosa na kuchukia mtu afanyaye kosa hilo.
Yesu alionyesha kwa kielelezo usawaziko ufaao kati ya upendo na chuki. Yeye alichukia unafiki, lakini alijaribu kuwasaidia wanafiki wabadili njia yao ya kufikiri. (Mathayo 23:27, 28; Luka 7:36-50) Yeye alilaumu jeuri, lakini aliomba kwa niaba ya wale waliomuua. (Mathayo 26:52; Luka 23:34) Na ingawa ulimwengu ulimchukia bila sababu, aliutoa uhai wake mwenyewe ili aupe ulimwengu uhai. (Yohana 6:33, 51; 15:18, 25) Alituachia kielelezo kikamilifu cha upendo wa kanuni na chuki ya kimungu.
Huenda ukosefu wa haki ukaamsha ghadhabu ya kiadili ndani yetu, kama Yesu. (Luka 19:45, 46) Hata hivyo, Wakristo, hawaruhusiwi kulipiza kisasi. “Msimlipe mtu ovu kwa ovu,” Paulo aliwashauri Wakristo katika Rumi. “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Msijilipize kisasi . . . Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.” (Warumi 12:17-21) Tunapokataa kusitawisha chuki moyoni au kulipiza kisasi juu ya jambo baya, upendo hupata ushindi.
Ulimwengu Usio na Chuki
Ili chuki iondoke ulimwenguni pote, mielekeo iliyoimarika ya mamilioni ya watu lazima ibadilike. Hili laweza kutimizwaje? Profesa Ervin Staub afanya pendekezo lifuatalo: “Tushushe tuwaumizao na kuthamini tuwasaidiao. Tunapothamini sana watu tuwasaidiao na kuhisi uradhi unaotokana na kusaidia, tunakuja kujiona pia tukiwa wenye kujali na wenye kusaidia mmojapo miradi yetu. Lazima kuunda jamii ambazo katika hizo mna uwezekano mkubwa wa kushiriki kufanya mambo kwa niaba ya wengine.”—The Roots of Evil.
Kwa maneno mengine, kuondolea mbali chuki huhitaji uundaji wa jamii ambayo katika hiyo watu hujifunza kupenda kwa kusaidiana, jamii ambamo watu husahau uadui wote uletwao na chuki isiyo na sababu nzuri, utukuzo wa taifa, ubaguzi wa rangi, na ukabila. Je, kuna jamii kama hiyo? Fikiria ono hili la mtu aliyekabili mwenyewe chuki wakati wa Mapinduzi ya Kitamaduni katika China.
“Mapinduzi ya Kitamaduni yalipoanza, tulifundishwa kwamba hakuna nafasi ya kuridhiana, katika ‘pigano la kitabaka.’ Chuki ndiyo iliyokuwa mwelekeo wenye kutokeza. Nikawa mshiriki wa Red Guard nami nikaanza kuwatafuta kila mahali ‘maadui wa kitabaka’—hata miongoni mwa familia yangu. Ingawa nilikuwa tineja tu wakati huo, nilishiriki katika upekuzi wa kila nyumba ambao katika huo tulikuwa tukitafuta uthibitisho wa ‘mielekeo ya kupinga maendeleo fulani.’ Hata niliongoza mkutano wa peupe ulioshutumu ‘mpinga mapinduzi.’ Bila shaka, mashtaka haya wakati mwingine yalikuwa na msingi wa uadui wa kibinafsi kuliko kuwa mielekeo ya kisiasa.
“Niliwaona watu wengi—wachanga kwa wazee, waume kwa wake—wakipewa adhabu ya kutandikwa viboko iliyokuwa ya ukatili zaidi na zaidi. Mmoja wa walimu wangu wa shule—mtu mzuri—alitembezwa barabarani kana kwamba alikuwa mhalifu. Miezi miwili baadaye mwalimu mwingine aliyeheshimiwa sana katika shule yangu alipatikana amekufa katika Mto Suzhou, na mwalimu wangu wa Kiingereza alilazimika kujinyonga. Nilishtuka na kufadhaika. Hawa walikuwa watu wema. Kuwatendea hivi kulikuwa kosa! Hivyo nikajitenga kabisa na Red Guards.
“Sidhani kipindi hiki cha chuki kilichokumba China kwa muda mfupi kilikuwa tukio la kipekee. Katika karne hii kumekuwa na matukio mengi sana ya chuki. Hata hivyo, ninasadiki sana kwamba upendo unaweza kushinda chuki. Ni jambo ambalo nimejionea mwenyewe. Nilipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, nilivutiwa na upendo wa kweli walioonyesha watu wa aina na malezi tofautitofauti. Natazamia mbele wakati ambao, kama vile Biblia inavyoahidi, Watu wote watakuwa wamejifunza kupendana mmoja na mwenzake.”
Ndiyo, jamii ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova ni ithibati halisi kwamba chuki yaweza kumalizwa kabisa. Bila kujali malezi yao, Mashahidi wanajitahidi kuondoa ubaguzi na mahali pa huo kuonyeshana heshima na kuondolea mbali baki lolote la ukabila, ubaguzi, au utukuzo wa taifa. Msingi mmoja wa kufaulu kwao ni azimio lao la kumwiga Yesu Kristo katika kuonyesha upendo unaoongozwa na kanuni. Msingi mwingine ni kwamba wanatazamia mbele Ufalme wa Mungu ulete mwisho wa ukosefu wowote wa haki ambao kwa huo huenda wakawa wanateseka.
Ufalme wa Mungu ndio suluhisho hasa liwezalo kuleta ulimwengu usio na chuki, ulimwengu ambao katika huo hakutakuwa hata na uovu wa kuchukia. Ikifafanuliwa katika Biblia kuwa “mbingu mpya” serikali hii ya kimbingu itahakikisha kuwe na ulimwengu usio na ukosefu wa haki. Itatawala juu ya “dunia mpya,” (NW) au jamii mpya ya watu watakaokuwa wameelimishwa kupendana. (2 Petro 3:13; Isaya 54:13) Elimu hii inaendelea sasa, kama vile maono ya Max, Simone, na wengine wengi yashuhudiavyo. Huu ni mwonjo wa programu ya ulimwenguni pote ya kuondolea mbali chuki na visababishi vyayo.
Kupitia nabii wake Isaya, Yehova aeleza tokeo: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Mungu mwenyewe atakuwa ametangaza kikomo cha chuki. Utakuwa wakati wa kupenda kwelikweli.
[Picha katika ukurasa w7]
Wanazi walichanja nambari ya mfungwa kwenye mkono wa kushoto wa Max Liebster
[Picha katika ukurasa wa8]
Karibuni chuki itakuwa jambo la wakati uliopita