“Utumishi Mtakatifu Pamoja na Nguvu Zenu za Kufikiri”
“Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”—WARUMI 12:1, NW.
1, 2. Ni kwa njia gani kujifunza kutumia kanuni za Biblia ni kama kujifunza lugha mpya?
JE, UMEPATA kujaribu kujifunza lugha mpya? Ikiwa ndivyo, bila shaka utakubali kwamba hiyo ni kazi ngumu. Kwani, kuna mengi zaidi yanayohusika kuliko kujifunza tu maneno mapya. Utumiaji sanifu wa lugha pia huhitaji kujua vizuri sarufi yayo. Ni lazima ujue jinsi maneno yanavyohusiana na jinsi yanavyoungana kufanyiza mawazo kamili.
2 Ndivyo ilivyo na kutwaa kwetu ujuzi wa Neno la Mungu. Mengi zaidi yanahusika kuliko kujifunza tu Andiko moja-moja. Ni lazima pia tujifunze sarufi ya Biblia. Tunahitaji kuelewa jinsi maandiko yanavyohusiana na jinsi yanavyotumika yakiwa kanuni ziwezazo kutumiwa katika maisha ya kila siku. Hivyo, twaweza kuwa ‘kamili, tukiwa tumekamilishwa kupata kutenda kila tendo jema.’—2 Timotheo 3:17.
3. Kuhusu utumishi kwa Mungu, ni badiliko gani lililotokea katika 33 W.K.?
3 Katika mpango wa kanuni ya Sheria ya Kimusa, uaminifu ungeweza kuonyeshwa, kwa kadiri kubwa, kwa kushika kabisa sheria zilizofafanuliwa wazi. Hata hivyo, katika 33 W.K., Yehova alifutilia mbali Sheria, ‘akiipigilia misumari kwenye mti wa mateso’ ambao Mwana wake aliuawa juu yao. (Wakolosai 2:13, 14, NW) Baadaye, watu wa Mungu hawakupewa orodha ndefu ya dhabihu za kutoa na sheria za kufuata. Badala ya hivyo, wao waliambiwa: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.” (Warumi 12:1, NW) Ndiyo, Wakristo walikuwa wajikakamue kwa moyo wao wote, nafsi yao yote, akili zao zote, na nguvu zao zote katika utumishi wa Mungu. (Marko 12:30; linganisha Zaburi 110:3.) Lakini yamaanisha nini kutoa “utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri”?
4, 5. Ni nini kinachohusika katika kumtumikia Yehova kwa nguvu zetu za kufikiri?
4 Maneno haya ‘nguvu za kufikiri’ yametafsiriwa kutoka kwa neno la Kigiriki lo·gi·kosʹ, limaanishalo “-a kiakili” au “-erevu.” Watumishi wa Mungu huhimizwa kutumia dhamiri iliyozoezwa na Biblia. Badala ya kutegemeza maamuzi yao kwa sheria nyingi zilizowekwa tayari, Wakristo wapaswa kuchanganua kanuni za Biblia kwa uangalifu. Wao wahitaji kuelewa “sarufi” ya Biblia, au jinsi kanuni zayo mbalimbali zinavyohusiana. Hivyo, wao waweza kufanya maamuzi yenye usawaziko kwa kutumia nguvu zao za kufikiri.
5 Je, hilo lamaanisha kwamba Wakristo hawana sheria? Hapana. Kwa wazi Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalikataza ibada ya sanamu, ukosefu wa adili katika ngono, uuaji wa kimakusudi, uwongo, uwasiliani-roho, matumizi mabaya ya damu, na dhambi nyinginezo nyingi. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Lakini, kwa kadiri kubwa zaidi ya vile Waisraeli walihitajika, ni lazima tutumie nguvu zetu za kufikiri kujifunza na kutumia kanuni za Biblia. Ni kama kujua lugha mpya, jambo hilo huchukua wakati na jitihada. Nguvu zetu za kufikiri zaweza kusitawishwaje?
Kusitawisha Nguvu Zako za Kufikiri
6. Kujifunza Biblia huhusisha nini?
6 Kwanza, ni lazima tuwe wanafunzi wa Biblia wenye hamu. Neno la Mungu lililopulizwa “lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki.” (2 Timotheo 3:16) Si lazima sikuzote tutarajie kupata suluhisho la tatizo katika mstari mmoja wa Biblia. Badala ya hivyo, huenda tukawajibika kusababu juu ya maandiko kadhaa yaangazayo nuru kwa hali au tatizo fulani hususa. Tutahitaji kutafuta sana mawazo ya Mungu juu ya jambo hilo. (Mithali 2:3-5, NW) Pia twahitaji uelewevu, kwa kuwa “mwenye uelewevu ndiye hupata mwongozo wenye ustadi.” (Mithali 1:5, NW) Mtu mwenye uelewevu aweza kutenganisha mambo hususa ya suala fulani kisha atambue jinsi yanavyohusiana. Kama ilivyo na kuunganisha picha za mchezo wa fumbo, mtu mwenye uelewevu huunganisha kila kijambo pamoja ili aweze kuona picha nzima.
7. Wazazi wanaweza kusababu kwa njia gani juu ya kanuni za Biblia kuhusu nidhamu?
7 Kwa kielelezo, ebu chukua suala la kuwa wazazi. Mithali 13:24, NW, lasema kwamba baba apendaye mwana wake “humwangalia ili kumtia nidhamu.” Likitumiwa peke yalo, andiko hilo laweza kutumiwa vibaya katika kutetea adhabu kali, isiyokoma. Lakini, Wakolosai 3:21 laandaa himizo lenye usawaziko: “Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.” Wazazi ambao hutumia nguvu zao za kufikiri na kupatanisha kanuni hizi hawatatoa nidhamu iwezayo kutajwa kuwa “kutenda vibaya.” Wao watatendea watoto wao kwa uchangamfu, uelewevu, na kwa staha. (Waefeso 6:4) Hivyo, kuhusu kuwa mzazi au katika jambo jingine lolote linalohusu kanuni za Biblia, twaweza kusitawisha nguvu zetu za kufikiri kwa kuchanganua mambo yote yanayohusiana. Kwa njia hii, twaweza kung’amua “sarufi” ya kanuni za Biblia, kusudi la Mungu lilikuwa nini na jinsi ya kulitimiza.
8. Tunaweza kuepukaje kushikilia sana maoni bila kubadilikana kwa habari ya vitumbuizo?
8 Njia ya pili ambayo twaweza kusitawisha nguvu zetu za kufikiri ni kwa kuepuka kushikilia sana maoni, bila kubadilikana. Mtazamo usiobadilikana huzuia ukuzi wa nguvu zetu za kufikiri. Fikiria suala la vitumbuizo. Biblia yasema: ‘Dunia yote hukaa katika yule mwovu.’ (1 Yohana 5:19) Je, hilo lamaanisha kwamba kila kitabu, sinema, au programu yoyote ya televisheni inayotokezwa na ulimwengu ni yenye ufisadi na ni ya kishetani? Maoni kama hayo hayawezi kuwa yenye kusababu kuzuri. Bila shaka, huenda wengine wakaamua kuepuka kabisa televisheni, sinema, au vichapo vya kilimwengu. Hiyo ni haki yao, nao hawapaswi kuchambuliwa kwa jambo hilo. Lakini wao pia hawapaswi kujaribu kuwekea wengine masharti magumu kama hayo. Sosaiti imechapisha makala zenye kutaja kanuni za Biblia zinazopasa kutuwezesha kuwa wenye hekima katika uteuzi wetu wakati wa kustarehe au wa vitumbuizo. Kutenda kinyume cha miongozo hiyo na kujihatarisha kwa fikira zisizo za maadili, ujeuri mbaya, au uwasiliani-roho zinazopatikana katika sehemu kubwa ya vitumbuizo vya ulimwengu huu si jambo la hekima hata kidogo. Hakika, uchaguzi mzuri wa vitumbuizo huhitaji kwamba tutumie nguvu zetu za kufikiri ili kutumia kanuni za Biblia na kupata dhamiri safi mbele ya Mungu na mwanadamu.—1 Wakorintho 10:31-33.
9. Ni nini kinachomaanishwa na “ufahamu kamili”?
9 Sehemu kubwa ya vitumbuizo vya leo kwa wazi haifai Wakristo.a Kwa hiyo, ni lazima tuzoeze mioyo yetu ‘kuchukia uovu’ ili tusiwe kama wengine katika karne ya kwanza waliokuwa ‘wameishiwa na utambuzi wote wa adili.’ (Zaburi 97:10; Waefeso 4:17-19, NW) Ili kusababu vizuri juu ya mambo hayo, twahitaji “ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” (Wafilipi 1:9, NW) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ufahamu” laonyesha “hisi nyepesi ya kiadili.” Neno hilo larejezea hisi halisi za wanadamu, kama vile hisi ya kuona. Kwa habari ya vitumbuizo au jambo jingine lolote linalohitaji uamuzi wa binafsi, hisi yetu ya kiadili yapaswa iwe makini ili tuweze kuona si mambo ambayo yameelezwa wazi tu, bali pia tuweze kuona mambo yasiyofafanuliwa wazi. Kwa wakati uo huo, twapaswa kujaribu kuepuka kutumia kanuni za Biblia kupita kiasi na kusisitiza kwamba ndugu zetu wote wafanye vivyo hivyo.—Wafilipi 4:5.
10. Tunawezaje kuja kuelewa utu wa Yehova kama unavyoonyeshwa katika Zaburi 15?
10 Njia ya tatu ya kusitawisha nguvu zetu za kufikiri ni kujua njia ya kufikiri ya Yehova na kuikaza kikiki mioyoni mwetu. Katika Neno lake, Yehova hufunua utu wake na viwango vyake. Kwa mfano, katika Zaburi 15, twasoma juu ya mtu ambaye Yehova aalika kuwa mgeni katika hema lake. Mtu huyo hutenda kwa uadilifu, husema kweli moyoni mwake, huwa mwadilifu kwa ahadi zake, naye hatumii wengine vibaya. Unaposoma zaburi hii, jiulize, ‘Je, sifa hizi zinanifafanua? Je, Yehova angenialika kuwa mgeni katika hema lake?’ Nguvu zetu za kufikiri huimarishwa tunapojipatanisha na njia na kufikiri kwa Yehova.—Mithali 3:5, 6; Waebrania 5:14.
11. Mafarisayo ‘waliachaje mambo ya adili, na upendo wa Mungu’?
11 Ni kwa habari hii Mafarisayo walishindwa kabisa. Mafarisayo walijua Sheria kabisa lakini hawakujua “sarufi” yayo. Wao wangeweza kukariri mambo mengi sana madogo-madogo ya Sheria, lakini walishindwa kuelewa utu wa Yehova. Yesu aliwaambia: “Mwatoa zaka za mnanaa na mchicha na kila mboga, na huku mwaacha mambo ya adili, na upendo wa Mungu.” (Luka 11:42) Wakiwa na akili zisizobadilikana na mioyo migumu, Mafarisayo walishindwa kutumia nguvu zao za kufikiri. Kusababu kwao kusikopatana kulikuja kuwa wazi waliposhutumu wanafunzi wa Yesu kwa kukwanyua masuke na kuzila mbegu siku ya Sabato; lakini, baadaye siku hiyohiyo, hawakuhisi kuchomwa na dhamiri walipopanga kumwua Yesu!—Mathayo 12:1, 2, 14.
12. Twaweza kujipatanishaje zaidi na Yehova akiwa Mtu?
12 Twataka kuwa tofauti na Mafarisayo. Ni lazima ujuzi wetu wa Neno la Mungu utusaidie kupatana zaidi na Yehova akiwa Mtu. Twaweza kufanyaje hivyo? Baada ya kusoma sehemu fulani ya Biblia au kichapo chenye kutegemea Biblia, wengine wamesaidiwa kwa kutafakari maswali kama haya, ‘Habari hii inanifundisha nini juu ya Yehova na sifa zake? Naweza kuonyeshaje sifa za Yehova nishughulikapo na wengine?’ Kutafakari maswali kama hayo husitawisha nguvu zetu za kufikiri na kutuwezesha kuwa ‘waigaji wa Mungu.’—Waefeso 5:1, NW.
Watumwa wa Mungu na Kristo, Si wa Wanadamu
13. Mafarisayo walitendaje kama watawala wa mambo ya kiadili?
13 Ni lazima wazee waruhusu wale walio chini ya utunzi wao watumie nguvu zao za kufikiri. Washiriki wa kutaniko si watumwa wa watu. “Kama ningekuwa hata sasa nawapendeza wanadamu,” akaandika Paulo, “singekuwa mtumwa wa Kristo.” (Wagalatia 1:10; Wakolosai 3:23, 24) Kwa kinyume, Mafarisayo walitaka watu waamini kwamba ilikuwa muhimu zaidi kupata kibali cha wanadamu kuliko cha Mungu. (Mathayo 23:2-7; Yohana 12:42, 43) Mafarisayo walijiweka wenyewe kuwa watawala wa mambo ya kiadili waliojifanyizia sheria zao wenyewe kisha kuhukumu wengine kwa namna walivyojipatanisha na sheria hizo. Watu waliofuata Mafarisayo walidhoofishwa katika matumizi yao ya dhamiri iliyozoezwa na Biblia, kwa njia hiyo wakija kuwa watumishi wa wanadamu.
14, 15. (a) Wazee wanawezaje kujionyesha kuwa wafanyakazi wenzi wa kundi? (b) Wazee wapaswa kushughulikiaje mambo ya dhamiri?
14 Wazee wa Kikristo leo wanajua kwamba sanasana kundi haliwajibiki kwao. Ni lazima kila Mkristo abebe mzigo wake. (Warumi 14:4; 2 Wakorintho 1:24; Wagalatia 6:5) Hilo lafaa. Kwa kweli ikiwa washiriki wa kundi wangekuwa watumwa wa wanadamu, wakitii kwa sababu tu ya kuchunguzwa, je, wangefanya nini wakati wanadamu hao hawako? Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kuwa na shangwe juu ya Wafilipi: “Kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” Hakika, wao walikuwa watumwa wa Kristo, bali si wa Paulo.—Wafilipi 2:12.
15 Basi, kwa habari ya dhamiri, wazee hawafanyi maamuzi kwa wale walio chini ya utunzi wao. Wao hueleza kanuni za Biblia zinazohusika katika jambo na kisha kuruhusu mtu mmoja-mmoja anayehusika kutumia nguvu zao za kufikiri ili kufanya uamuzi. Hilo ni daraka zito sana, lakini ni lile ambalo ni lazima mtu mwenyewe alibebe.
16. Ni mfumo gani uliokuwa katika Israeli wa kushughulikia matatizo?
16 Fikiria kile kipindi ambacho Yehova alitumia waamuzi kuongoza Israeli. Biblia yatuambia hivi: “Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.” (Waamuzi 21:25) Lakini Yehova aliandalia watu wake njia ya kupata mwongozo. Kila jiji lilikuwa na wanaume wazee ambao wangeandaa msaada mkomavu kwa maswali na matatizo. Kwa kuongezea, makuhani wa Kilawi walitenda wakiwa kani ya mema kwa kuelimisha watu sheria za Mungu. Hasa mambo magumu yalipotokea, kuhani mkuu angetafuta shauri kwa Mungu kwa kutumia Urimu na Thumimu. Insight on the Scriptures chaeleza: “Mtu aliyekubali maandalio hayo, aliyepata ujuzi wa sheria ya Mungu na kuitumia, alikuwa na mwongozo mzuri kwa dhamiri yake. Kufanya kwake ‘yaliyo sawa machoni pake’ katika hali hiyo hakungetokeza mabaya. Yehova aliruhusu watu kuonyesha mtazamo na mwendo wa hiari au usio wa hiari.”—Buku 2, kurasa 162-163.b
17. Wazee wanaweza kuonyeshaje kwamba wao hushauri kwa kupatana na viwango vya Mungu badala ya vyao?
17 Kama waamuzi na makuhani Waisraeli, wazee wa kutaniko huandaa msaada mkomavu kwa matatizo na kutoa shauri lenye thamani. Nyakati nyingine, wao hata ‘hukaripia, hukemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho.’ (2 Timotheo 4:2) Wao hufanya hivyo kwa kupatana na viwango vya Mungu, si vyao. Linakuwa jambo lenye matokeo kama nini wazee wawekapo kielelezo kizuri na kujaribu kufikia mioyo!
18. Kwa nini ni jambo la kutumika zaidi hasa kwa wazee kufikia mioyo?
18 Moyo ni “injini” ya utendaji wetu wa Kikristo. Kwa hiyo Biblia yasema: “Ndiko zitokako chemchemi za uzima.” (Mithali 4:23) Wazee ambao huchochea mioyo watapata kwamba wale walio katika kutaniko huchochewa kufanya yote wawezayo katika utumishi wa Mungu. Wao watajianzisha wenyewe, wasihitaji sikuzote kusukumwa na wengine. Yehova hataki utii wa kulazimishwa. Yeye anataka utii unaotoka katika moyo uliojaa upendo. Wazee waweza kutia moyo utumishi huo wenye kuchochewa na moyo kwa kusaidia watu katika kundi wasitawishe nguvu zao za kufikiri.
Kusitawisha “Akili ya Kristo”
19, 20. Kwa nini ni muhimu kwetu kusitawisha akili ya Kristo?
19 Kama ilivyotajwa, haitoshi kujua tu sheria za Mungu. “Unifahamishe,” akaomba mtunga-zaburi, “nami nitaishika sheria yako, naam, nitaitii kwa moyo wangu wote.” (Zaburi 119:34) Yehova amefunua katika Neno lake “akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16, NW) Akiwa alimtumikia Yehova kwa nguvu zake za kufikiri, Yesu alituachia kigezo kikamilifu. Yeye alielewa sheria na kanuni za Mungu, naye alizitumia bila kukosea. Kwa kujifunza kielelezo chake, ‘kwa ukamili tuweze kufahamu kiakili ni nini kilicho upana na urefu na kimo na kina, na kuujua upendo wa yule Kristo uzidio ujuzi.’ (Waefeso 3:17-19, NW) Ndiyo, yale tunayojifunza katika Biblia kuhusu Yesu yanahusu mengi zaidi ya kushika mambo akilini tu; yanatupa picha kamili ya jinsi Yehova mwenyewe alivyo.—Yohana 14:9, 10.
20 Hivyo, tujifunzapo Neno la Mungu, twaweza kutambua fikira za Yehova juu ya mambo na kufikia maamuzi yenye usawaziko. Jambo hilo litahitaji jitihada. Ni lazima tuwe wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu, tukiwa wepesi kuona utu na viwango vya Yehova. Ni kama tunajifunza sarufi mpya. Na wale wafanyao hivyo watakuwa wakifuata himizo la Paulo la ‘kutoa miili yao iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zao za kufikiri.’—Warumi 12:1.
[Maelezo ya chinis]
a Hii haingetia ndani vitumbuizo vya kishetani, pornografia, au vyenye ukatili, na vilevile vile viitwavyo eti vitumbuizo vya familia nzima vinavyoendeleza mawazo ya ukosefu wa maadili au kuendekeza mambo ambayo Wakristo hawawezi kukubali.
b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Ulijifunza Nini?
◻ Ni badiliko gani kuhusu utumishi kwa Mungu lililotukia katika 33 W.K.?
◻ Tunaweza kusitawishaje nguvu zetu za kufikiri?
◻ Wazee wanawezaje kusaidia wale walio katika kundi kuwa watumwa wa Mungu na Kristo?
◻ Kwa nini tusitawishe “akili ya Kristo”?
[Picha katika ukurasa wa23]
Wazee husaidia wengine kutumia nguvu zao za kufikiri