Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo
“Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.”—WAGALATIA 6:2.
1. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba sheria ya Kristo ni uvutano wenye nguvu unaotokeza mema leo?
KATIKA Rwanda, Mashahidi wa Yehova Wahutu na Watutsi walihatarisha maisha zao ili kulindana dhidi ya uchinjaji wa kikabila ambao majuzi uliikumba nchi hiyo. Mashahidi wa Yehova huko Kobe, Japani, waliopoteza washiriki wa familia katika tetemeko la dunia lililosababisha uharibifu mkubwa waliathiriwa vibaya sana na hasara waliyopata. Hata hivyo, walitenda upesi kuwaokoa wahasiriwa wengine. Ndiyo, vielelezo vyenye kuchangamsha moyo kutoka ulimwenguni pote huonyesha kwamba sheria ya Kristo inafanya kazi leo. Hiyo ni uvutano wenye nguvu unaotokeza mema.
2. Jumuiya ya Wakristo imeshindwaje kuielewa sheria ya Kristo, nasi twaweza kufanya nini ili kuitimiza sheria hiyo?
2 Wakati uleule, unabii wa Biblia juu ya “siku [hizi] za mwisho” za hatari unatimizwa. Wengi wana “mfano wa utauwa” lakini ‘wanakana nguvu zake.’ (2 Timotheo 3:1, 5) Hasa katika Jumuiya ya Wakristo, mara nyingi dini ni jambo la kidesturi, wala si jambo la moyoni. Je, hilo ni kwa sababu ni vigumu sana kuishi kulingana na sheria ya Kristo? La. Yesu hangetupatia sheria ambayo haingeweza kufuatwa. Jumuiya ya Wakristo imeshindwa tu kuielewa sheria ya Kristo. Imeshindwa kutii maneno haya yaliyopuliziwa: “Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Sisi ‘huitimiza sheria ya Kristo’ kwa kuchukuliana mizigo, wala si kwa kuwaiga Mafarisayo na kuwaongezea ndugu zetu mizigo isivyo haki.
3. (a) Ni zipi baadhi ya amri zinazotiwa ndani katika sheria ya Kristo? (b) Kwa nini lingekuwa kosa kukata maneno kwamba kutaniko la Kikristo halipaswi kuwa na kanuni nyingine zaidi ya zile amri za moja kwa moja za Kristo?
3 Sheria ya Kristo hutia ndani amri zote za Kristo Yesu—ziwe ni kuhubiri na kufundisha, kuliweka jicho likiwa safi na sahili, kujitahidi kudumisha amani na jirani yetu, au kuondoa uchafu kutoka kutanikoni. (Mathayo 5:27-30; 18:15-17; 28:19, 20; Ufunuo 2:14-16) Kwa kweli, Wakristo wanawajibika kushika amri zote zilizomo katika Biblia ambazo zaelekezwa kwa wafuasi wa Kristo. Na kuna mengine zaidi. Tengenezo la Yehova, na pia makutaniko moja-moja, lazima liweke kanuni na taratibu za lazima ili kudumisha utaratibu mzuri. (1 Wakorintho 14:33, 40) Kwani, Wakristo hata hawangekutana pamoja ikiwa hawakuwa na kanuni zozote juu ya wakati, mahali, na jinsi ya kufanya mikutano hiyo! (Waebrania 10:24, 25) Kushirikiana na miongozo yenye kiasi iliyotolewa na wale waliopewa mamlaka katika tengenezo ni sehemu pia ya kuitimiza sheria ya Kristo.—Waebrania 13:17.
4. Ni nini kinachoichochea ibada safi?
4 Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawaruhusu ibada yao iwe mpangilio wa sheria usio na maana. Hawamtumikii Yehova kwa sababu tu mtu fulani au tengenezo fulani lawaambia wafanye hivyo. Badala ya hivyo, kani inayochochea ibada yao ni upendo. Paulo aliandika hivi: “Upendo wa Kristo hutushurutisha.” (2 Wakorintho 5:14, NW, kielezi-chini) Yesu aliwaamuru wafuasi wake wapendane. (Yohana 15:12, 13) Upendo wenye kujidhabihu ndio msingi wa sheria ya Kristo, nao hushurutisha au kuchochea Wakristo wa kweli kotekote, katika familia na katika kutaniko. Acheni tuone ni jinsi gani.
Katika Familia
5. (a) Wazazi waweza kutimizaje sheria ya Kristo nyumbani? (b) Watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi wao, na wazazi fulani wahitaji kushinda vizuizi vipi ili kuutoa?
5 Mtume Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake.” (Waefeso 5:25) Mume amwigapo Kristo na kumtendea mkeye kwa upendo na uelewevu, mume hutimiza sehemu ya maana ya sheria ya Kristo. Zaidi, Yesu aliwaonyesha watoto wadogo shauku waziwazi, akiwakumbatia, akiweka mikono yake juu yao, na kuwabariki. (Marko 10:16) Wazazi wanaotimiza sheria ya Kristo pia huonyesha watoto wao shauku. Ni kweli, kuna wazazi wanaoliona kuwa jambo gumu kuiga kielelezo cha Yesu katika jambo hili. Wengine hawana mwelekeo wa kuonyesha hisia waziwazi. Wazazi, msiruhusu fikira hizo ziwazuie kuwaonyesha watoto wenu upendo mnaohisi kwao! Haitoshi kwako kujua kwamba unawapenda watoto wako. Wao wapaswa kujua hilo pia. Na hawatajua isipokuwa utafute njia za kuonyesha upendo wako.—Linganisha Marko 1:11.
6. (a) Je, watoto wanahitaji kanuni za wazazi, na kwa nini wajibu hivyo? (b) Watoto wahitaji kuelewa sababu gani ya msingi ya kuwa na kanuni za nyumbani? (c) Ni hatari gani zinazoepukwa sheria ya Kristo ieneapo nyumbani?
6 Wakati uleule, watoto wanahitaji mipaka, jambo ambalo lamaanisha kwamba wazazi wao wanahitaji kuweka kanuni na nyakati nyingine kuzitekeleza kanuni hizo kwa kutia nidhamu. (Waebrania 12:7, 9, 11) Hata hivyo, lazima watoto wasaidiwe hatua kwa hatua kuona sababu ya msingi ya kanuni hizo: wazazi wao wawapenda. Nao lazima wajifunze kuwa upendo ndio sababu yao bora ya kuwatii wazazi wao. (Waefeso 6:1; Wakolosai 3:20; 1 Yohana 5:3) Mradi wa mzazi mwenye utambuzi ni kuwafundisha wachanga kutumia ‘nguvu zao za kufikiri’ ili hatimaye waweze kufanya maamuzi mazuri wakiwa peke yao. (Warumi 12:1, NW; linganisha 1 Wakorintho 13:11.) Kwa upande mwingine, kanuni hazipasi kuwa nyingi sana au nidhamu kuwa kali sana. Paulo asema hivi: “Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.” (Wakolosai 3:21; Waefeso 6:4) Sheria ya Kristo ieneapo nyumbani, hakuna nafasi ya nidhamu itolewayo kukiwa na hasira isiyodhibitiwa au usemi wa kuumiza na wenye kudhuru. Katika nyumba ya aina hiyo, watoto huhisi wakiwa wenye usalama na wenye kujengwa, si wenye kulemezwa au kuvunjiwa heshima.—Linganisha Zaburi 36:7.
7. Ni katika njia gani makao ya Betheli yawezavyo kuandaa kielelezo kwa habari ya kuweka kanuni nyumbani?
7 Watu fulani ambao wametembelea makao ya Betheli ulimwenguni pote wanasema kwamba hayo ni vielelezo vizuri vya usawaziko kwa habari ya kanuni kwa ajili ya familia. Ingawa makao ya Betheli huwa na watu wazima, mashirika hayo hutenda kama familia.a Utendaji-kazi wa Betheli ni wenye utata na huhitaji idadi kadhaa ya kanuni—bila shaka nyingi kuliko zihitajiwazo na familia ya kawaida. Hata hivyo, wazee waongozao katika makao, ofisi, na kazi za viwanda vya Betheli, hujitahidi kutumia sheria ya Kristo. Wao huona kuwa mgawo wao si kupanga kazi tu bali pia kuendeleza maendeleo ya kiroho na “shangwe ya Yehova” miongoni mwa wafanyakazi wenzao. (Nehemia 8:10, NW) Kwa hiyo, wao hujitahidi kufanya mambo katika njia ifaayo na yenye kutia moyo na kujaribu kuwa wenye kukubali sababu. (Waefeso 4:31, 32) Si ajabu familia za Betheli hujulikana kwa sababu ya mtazamo wazo wenye shangwe!
Katika Kutaniko
8. (a) Mradi wetu kutanikoni uwe nini sikuzote? (b) Ni zipi baadhi ya hali ambazo chini yazo watu fulani wameomba wapewe kanuni au wamejaribu kufanya kanuni?
8 Katika kutaniko ni mradi wetu vilevile kujengana kwa roho ya upendo. (1 Wathesalonike 5:11) Kwa hiyo Wakristo wote wapaswa kuwa waangalifu wasiongezee mizigo ya wengine kwa kujitwalia daraka la kutoa maoni yao wenyewe katika mambo ya uchaguzi wa kibinafsi. Nyakati nyingine, watu fulani huandikia Watch Tower Society wakiomba wapewe kanuni juu ya mambo kama ni maoni gani wapaswayo kuwa nayo juu ya filamu, vitabu, na hata vichezeo hususa. Walakini, Sosaiti haikupewa mamlaka ya kuchunguza mambo hayo na kutoa maamuzi juu yayo. Katika visa vilivyo vingi, hayo ni mambo ambayo kila mtu mmoja-mmoja au kichwa cha familia apaswa kuamua, ikitegemea kupenda kwake kanuni za Biblia. Wengine huelekea kugeuza madokezo na miongozo ya Sosaiti kuwa kanuni. Kwa kielelezo, katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1996, kulikuwa na makala nzuri iwatiayo moyo wazee kuwafanyia washiriki wa kutaniko ziara za uchungaji za kawaida. Je, kusudi lilikuwa kuweka kanuni? La. Ingawa wale wawezao kufuata madokezo hayo hupata manufaa mengi, wazee fulani hawawezi kufanya hivyo. Vivyo hivyo, ile makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1995, ilionya dhidi ya kupunguza adhama ya pindi ya ubatizo kwa kufanya mambo kupita kiasi, kama karamu zisizodhibitiwa au kupanga misherehekeo. Wengine wametumia shauri hilo komavu kupita kiasi, hata wakiweka kanuni kwamba kutuma kadi ya kutia moyo kwenye pindi hiyo kungekuwa kosa!
9. Kwa nini ni jambo la maana kwamba tuepuke kuwa wenye kuchambuana au kuhukumiana kupita kiasi?
9 Fikiria pia, kwamba ikiwa “sheria kamilifu iliyo ya uhuru” itaenea miongoni mwetu, lazima tukubali kwamba si dhamiri zote za Wakristo zinazofanana. (Yakobo 1:25) Je, tuudhike watu wakiwa na machaguo ambayo hayakiuki kanuni za Kimaandiko? La. Kufanya kwetu hivyo kutakuwa jambo lisababishalo migawanyiko. (1 Wakorintho 1:10) Paulo, alipokuwa akituonya dhidi ya kuhukumu Mkristo mwenzetu, alisema hivi: “Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka. Naam, atasimamishwa, kwa kuwa Bwana aweza kumsimamisha.” (Warumi 14:4) Tusemapo dhidi ya mmoja na mwenzake juu ya mambo yapaswayo kuachiwa dhamiri ya mtu mmoja-mmoja twaingia hatarini mwa kumchukiza Mungu.—Yakobo 4:10-12.
10. Ni nani ambao wamepewa mgawo wa kulinda kutaniko, nasi tuwaungeje mkono?
10 Acheni tukumbuke, pia, kwamba wazee wamepewa mgawo wa kulichunga kundi la Mungu. (Matendo 20:28) Wapo ili wasaidie. Twapaswa kuhisi tukiwa huru kuwafikia ili kupata shauri, kwa kuwa wao ni wanafunzi wa Biblia nao wajua yale ambayo yamezungumziwa katika fasihi za Watch Tower Society. Wazee waonapo mwenendo ambao yamkini utaelekeza kwenye ukiuko wa kanuni za Kimaandiko, wao hutoa bila hofu shauri linalohitajiwa. (Wagalatia 6:1) Washiriki wa kutaniko hufuata sheria ya Kristo kwa kushirikiana na wachungaji hao wapendwa, waongozao miongoni mwao.—Waebrania 13:7.
Wazee Hutumia Sheria ya Kristo
11. Wazee hutumiaje sheria ya Kristo kutanikoni?
11 Wazee wanatamani kuitimiza sheria ya Kristo kutanikoni. Wao huongoza katika kuhubiri habari njema, kufundisha kutokana na Biblia ili wafikie mioyo na, wakiwa wachungaji wenye upendo na upole, husema na “nafsi zilizoshuka moyo.” (1 Wathesalonike 5:14, NW) Wao huepuka mitazamo isiyo ya Kikristo iliyopo katika dini nyingi sana za Jumuiya ya Wakristo. Ni kweli, ulimwengu huu unazorota upesi, na sawa na Paulo, huenda wazee wakahisi hangaiko kwa ajili ya kundi; lakini wao hudumisha usawaziko watendapo kulingana na mahangaiko hayo.—2 Wakorintho 11:28.
12. Mkristo amfikiapo mzee ili kupata msaada, mzee aweza kuitikiaje?
12 Kwa kielelezo, huenda Mkristo akataka kumwona mzee kuhusu jambo la maana ambalo halishughulikiwi na rejezo la moja kwa moja la Kimaandiko au lihitajilo kusawazisha kanuni tofauti za Kikristo. Huenda ikawa amepandishwa cheo kazini kilicho na mshahara mkubwa zaidi lakini chenye madaraka makubwa zaidi. Au baba asiyeamini wa Mkristo mchanga huenda akawa anamdai mwanawe mambo ambayo yangeweza kuathiri huduma yake. Katika hali hizo mzee huepuka kutoa maoni ya kibinafsi. Badala ya hivyo, yamkini atafungua Biblia na kumsaidia mtu huyo kusababu juu ya kanuni zihusikazo. Huenda akatumia kichapo Watch Tower Publications Index, ikiwa chapatikana, ili kupata lile ambalo “mtumwa mwaminifu mwenye akili” amesema juu ya habari hiyo katika kurasa za Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine. (Mathayo 24:45) Namna gani ikiwa baadaye Mkristo huyo afanya uamuzi usioonekana kuwa wenye hekima machoni pa mzee huyo? Ikiwa uamuzi haupingi moja kwa moja kanuni au sheria za Biblia, huyo Mkristo atagundua kwamba huyo mzee anatambua haki ya mtu mmoja-mmoja ya kufanya uamuzi huo, akijua kwamba “kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” Hata hivyo, huyo Mkristo apaswa kukumbuka kwamba “cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”—Wagalatia 6:5, 7.
13. Badala ya kutoa majibu ya moja kwa moja au kutoa maoni yao wenyewe, kwa nini wazee huwasaidia wengine kusababu juu ya mambo?
13 Kwa nini mzee mwenye uzoefu atenda hivyo? Kwa angalau sababu mbili. Kwanza, Paulo aliliambia kutaniko moja kuwa hakuwa ‘bwana-mkubwa juu ya imani yalo.’ (2 Wakorintho 1:24, NW) Huyo mzee, kwa kumsaidia ndugu yake kusababu kwa kutumia Maandiko na kufanya uamuzi wake mwenyewe wenye kutegemea ujuzi, anaiga mtazamo wa Paulo. Yeye anatambua kwamba mamlaka yake ina mipaka, sawa na Yesu alivyotambua kwamba kulikuwa na mipaka katika mamlaka yake. (Luka 12:13, 14; Yuda 9, linganisha NW.) Wakati uleule, wazee hutoa msaada kwa utayari, hata shauri kali la Kimaandiko lihitajiwapo. Pili, yeye anamzoeza Mkristo mwenzake. Mtume Paulo alisema hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:14) Basi, ili kukua kufikia ukomavu, lazima tutumie akili zetu, si kwa kutegemea sikuzote mtu mwingine atupe majibu. Mzee, kwa kumwonyesha Mkristo mwenzake jinsi ya kusababu kwa kutumia Maandiko, kwa njia hiyo anamsaidia kufanya maendeleo.
14. Walio wakomavu waweza kuonyeshaje kwamba wanamtumaini Yehova?
14 Twaweza kuwa na imani kwamba Yehova Mungu kupitia roho yake takatifu atachochea mioyo ya waabudu wa kweli. Hivyo, Wakristo wakomavu huvutia mioyo ya ndugu zao, wakiwasihi, kama alivyofanya mtume Paulo. (2 Wakorintho 8:8; 10:1; Filemoni 8, 9) Paulo alijua kwamba ni wasio waadilifu hasa, wala si waadilifu, wahitajio sheria zinazotia ndani kila kitu ili kuwafanya waenende ifaavyo. (1 Timotheo 1:9) Alionyesha imani katika ndugu zake, wala si hali ya kuwashuku au ukosefu wa kuwatumaini. Aliandikia hivi kutaniko moja: “Tuna uhakika katika Bwana kuhusu nyinyi.” (2 Wathesalonike 3:4, NW) Imani, tumaini na uhakika wa Paulo kwa hakika ulichangia sana kuwachochea Wakristo hao. Wazee na waangalizi wasafirio leo wana makusudi yayo hayo. Wanaume hao waaminifu wanaburudisha kama nini, huku wakilichunga kundi la Mungu kwa upendo!—Isaya 32:1, 2; 1 Petro 5:1-3.
Kuishi Kulingana na Sheria ya Kristo
15. Ni yapi baadhi ya maswali tuwezayo kujiuliza ili kuona ikiwa tunaitumia sheria ya Kristo katika uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu?
15 Sote twahitaji kujichunguza kwa ukawaida tuone ikiwa tunaishi kulingana na, na kuiendeleza sheria ya Kristo. (2 Wakorintho 13:5) Kwa kweli, sisi sote twaweza kunufaika kwa kuuliza: ‘Je, mimi ni mwenye kujenga au mwenye kuchambua? Je, mimi ni mwenye usawaziko au mwenye kupita kiasi? Je, mimi huonyesha wengine ufikirio au husisitizia haki zangu mwenyewe?’ Mkristo hajaribu kuamuru ni hatua zipi ambazo ndugu yake anapaswa au hapaswi kuchukua katika mambo ambayo hayashughulikiwi kihususa katika Biblia.—Warumi 12:1; 1 Wakorintho 4:6.
16. Twaweza kuwasaidiaje wale walio na maoni yasiyofaa juu yao wenyewe, kwa njia hiyo tukitimiza sehemu ya maana ya sheria ya Kristo?
16 Katika nyakati hizi za hatari, ni jambo la maana kwetu kutafuta njia za kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25; linganisha Mathayo 7:1-5.) Tuwatazamapo ndugu na dada zetu, je, sifa zao nzuri si za maana zaidi kwetu kuliko udhaifu wao mbalimbali? Machoni pa Yehova, kila mmoja ni mwenye thamani. Kwa kusikitisha, si wote wahisio hivyo, hata juu yao wenyewe. Wengi huelekea kuona tu makosa na kutokamilika kwao binafsi. Ili kuwatia moyo hao—na wengine—je, twaweza kujaribu kuongea na mtu mmoja au wawili kwenye kila mkutano, tukiwajulisha ni kwa nini twathamini kuwapo kwao na mchango wa maana watoao kutanikoni? Ni furaha kama nini kupunguza mzigo wao kwa njia hiyo na hivyo kutimiza sheria ya Kristo!—Wagalatia 6:2.
Sheria ya Kristo Inafanya Kazi!
17. Unaiona sheria ya Kristo ikifanya kazi katika njia zipi tofauti katika kutaniko lako?
17 Sheria ya Kristo inafanya kazi katika kutaniko la Kikristo. Twaiona kila siku—Mashahidi wenzetu washirikipo kwa bidii habari njema, wafarijianapo na kutiana moyo, wang’ang’anapo kumtumikia Yehova licha ya matatizo yaliyo magumu zaidi, wazazi wajitahidipo kulea watoto wao ili wampende Yehova kwa mioyo yenye shangwe, waangalizi wafundishapo Neno la Mungu kwa upendo na uchangamfu, wakihimiza kundi liwe na bidii yenye kuwaka ya kumtumikia Yehova milele. (Mathayo 28:19, 20; 1 Wathesalonike 5:11, 14) Sisi mmoja-mmoja tuitumiapo sheria ya Kristo maishani mwetu wenyewe, moyo wa Yehova hushangalia kama nini! (Mithali 23:15) Yeye ataka wote wapendao sheria yake kamilifu waishi milele. Katika Paradiso ijayo, tutaona wakati ambapo wanadamu watakuwa wakamilifu, wakati usio na wavunjaji wa sheria, na wakati ambapo kila mwelekeo wa mioyo yetu utadhibitiwa. Ni thawabu iliyoje ya kuishi kulingana na sheria ya Kristo!
[Maelezo ya Chini]
a Makao hayo si kama makao ya watawa ya Jumuiya ya Wakristo. Hakuna “abati,” au “baba,” katika maana hiyo. (Mathayo 23:9) Ndugu wenye kuchukua madaraka hupewa staha, lakini utumishi wao huongozwa na kanuni zilezile ziwaongozazo wazee wote.
Wewe Wafikirije?
◻ Kwa nini Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kuielewa sheria ya Kristo?
◻ Twaweza kuitumiaje sheria ya Kristo katika familia?
◻ Ili kuitumia sheria ya Kristo kutanikoni, tuepuke nini, na lazima tufanye nini?
◻ Wazee waweza kuitiije sheria ya Kristo katika shughuli zao pamoja na kutaniko?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mtoto wako ana uhitaji mkubwa wa upendo
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wachungaji wetu wenye upendo wanaburudisha kama nini!