Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Yohana wa Kwanza 4:18, hutuambia hivi: “Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu.” Lakini Petro aliandika hivi: “Iweni na upendo kwa ushirika wote wa akina ndugu, iweni katika hofu ya Mungu.” (1 Petro 2:17, NW) Twaweza kuhusianishaje mistari hiyo miwili?
Petro na vilevile Yohana walikuwa mitume waliokuwa wamejifunza moja kwa moja kutoka kwa Yesu Kristo mwenyewe. Hivyo twaweza kuwa na hakika kwamba waliyoandika yanapatana. Kuhusu mistari iliyonukuliwa juu, suluhisho ni kwamba mitume hao wawili walikuwa wakizungumza juu ya aina mbalimbali za hofu.
Kwanza ebu tufikirie shauri la Petro. Kama muktadha unavyoonyesha, Petro alikuwa akiwapa Wakristo wenzake shauri lililovuviwa juu ya mtazamo wao kuelekea wale walioko mamlakani. Kwa maneno mengine, alikuwa akitoa maelezo juu ya mwelekeo ufaao wa ujitiisho katika maeneo fulani. Hivyo, aliwashauri Wakristo kujitiisha kwa watu waliokuwa na vyeo vyenye mamlaka katika serikali za kibinadamu, kama vile wafalme na magavana. (1 Petro 2:13, 14) Akiendelea, Petro aliandika hivi: “Heshimuni watu wa namna zote, iweni na upendo kwa ushirika wote wa akina ndugu, iweni katika hofu ya Mungu, iweni na heshima kwa mfalme.”—1 Petro 2:17, NW.
Kwa kufikiria muktadha, ni wazi kwamba Petro aliposema kwamba Wakristo wapaswa wawe “katika hofu ya Mungu,” alimaanisha kwamba twapaswa kuwa na staha ya kina kirefu kwa Mungu, hofu ya kutomchukiza mwenye mamlaka ya juu zaidi.—Linganisha Waebrania 11:7.
Namna gani juu ya maelezo ya mtume Yohana? Mapema katika 1 Yohana sura 4, (NW) mtume huyo alizungumzia uhitaji wa kujaribu “semi zilizopuliziwa” zitokazo kwa manabii wa uwongo. Kwa hakika semi hizo hazitokani na Yehova Mungu; zatoka kwa ulimwengu mwovu.
Kinyume cha hayo, Wakristo watiwa mafuta ‘watokana na Mungu.’ (1 Yohana 4:1-6) Jambo hilo likiwa ndivyo lilivyo, Yohana alisihi hivi: “Wapenzi, na tupendane; kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu.” Mungu alikuwa wa kwanza kuonyesha upendo—yeye ‘alimtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.’ (1 Yohana 4:7-10) Tuitikieje?
Kwa wazi, twapaswa kubaki katika muungano pamoja na Mungu wetu mwenye upendo. Hatupaswi kuogofya au kutetemeka tutazamiapo kumkaribia katika sala. Mapema Yohana alishauri hivi: “Mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake.” (1 Yohana 3:21, 22) Ndiyo, dhamiri safi hutupa uhuru wa kumkaribia Mungu bila kutetemeka au kujibana kwa woga. Kwa upendo, tunahisi uhuru wa kujieleza, au kumkaribia, Yehova katika sala. Kupatana na hilo, “katika pendo hamna hofu.”
Basi ebu tuunganishe mawazo hayo mawili. Lazima Mkristo sikuzote awe na hofu yenye staha kwa Yehova, iletwayo na heshima ya kina kirefu ya cheo chake, uwezo, na haki. Lakini pia twampenda Mungu akiwa Baba yetu na kuhisi ukaribu kwake na uhuru wa kumkaribia. Badala ya kubanwa na ogofyo lolote kwake, twatumaini kwamba twaweza kumkaribia, kama mtoto ahisivyo uhuru kumkaribia mzazi mwenye upendo.—Yakobo 4:8.