Kwa Nini Kuhofu Mungu, Si Wanadamu?
“KUTETEMEKA kwa sababu ya wanadamu ndiko hutega mtego, lakini yeye ambaye hutegemea Yehova atapata kinga.” (Mithali 29:25, NW) Kwa maneno haya mithali ya kale hutuweka chonjo tuone aina ya hofu ambayo ni sumu ya kiakili kweli kweli—hofu kwa mwanadamu. Inalinganishwa na mtego. Kwa nini? Kwa sababu mnyama mdogo, kama sungura, anakuwa hoi anaponaswa katika mtego. Anataka kukimbia, lakini ule mtego unamshika bila kumwachilia. Inakuwa kana kwamba mateka huyo amelemazwa kabisa.
Tukishikwa na hofu kwa wanadamu, sisi tunakuwa sana kama sungura huyo. Huenda tukajua tunalopaswa kufanya. Hata huenda tukataka kulifanya. Lakini hofu hutufanya watumwa. Tunalemazwa kabisa na kushindwa kutenda.
Mtego wa Kuhofu Mwanadamu
Fikiria vielelezo fulani vya nyakati za Biblia vya wale walionaswa na mtego wa hofu. Katika siku za Yoshua, wanaume 12 walipelekwa wakapeleleze bara la Kanaani kabla ya Waisraeli kupanga kulivamia. Wapelelezi hao walirudi wakaripoti kwamba bara lilikuwa lenye rutuba na lenye utajiri, kama vile Mungu alivyokuwa amesema. Lakini kumi kati ya wapelelezi wale waliogopeshwa mno na nguvu za wakaaji. Hivyo, kwa kuhofu mwanadamu, walitolea Waisraeli ripoti iliyotiwa chumvi juu ya nguvu hii na kusababisha taifa zima lishikwe na hofu. Waisraeli walikataa kutii amri ya Mungu ya kupiga miguu waingie Kanaani na kulitwaa bara. Kama tokeo, wakati wa miaka 40 iliyofuata, idadi yote ya watu wazima wa kiume wa wakati huo, isipokuwa wachache tu, walikufa jangwani.—Hesabu 13:21–14:38.
Yona alikuwa mwingine aliyehofu mwanadamu. Alipopewa mgawo wa kuhubiria lile jiji kubwa la Ninawi, yeye “akaondoka akimbilie Tarshishi, apate kujiepusha na uso wa BWANA [Yehova, NW].” (Yona 1:3) Kwa nini? Waninawi walikuwa na sifa ya kuwa watu wasio na huruma na wajeuri, na bila shaka Yona alijua hivyo. Kuhofu mwanadamu kulimfanya akimbilie upande unaoelekea mbali na Ninawi. Ni kweli, hatimaye yeye alikubali mgawo wake lakini ilikuwa ni baada tu ya kupokea nidhamu isiyo ya kawaida kutoka kwa Yehova.—Yona 1:4, 17.
Hata wafalme waweza kuhofu wanadamu. Katika pindi moja, Mfalme Sauli alikosa kutii moja kwa moja amri iliyosemwa waziwazi kutoka kwa Mungu. Udhuru wake? “Nimeipita amri ya Yehova na maneno yako, kwa sababu mimi niliwahofu watu na hivyo nikatii sauti yao.” (1 Samweli 15:24, NW) Karne kadhaa baadaye, wakati Yerusalemu lilipokuwa likishambuliwa na Wababuloni, Yeremia, mnabii mwaminifu, alishauri Mfalme Sedekia asalimu amri na hivyo aepushe Yerusalemu na kumwagwa kwa damu nyingi. Lakini Sedekia alikataa. Kwa nini? Yeye alikiri kwa Yeremia hivi: “Mimi nimo katika woga wa Wayahudi ambao wamewakimbilia Wakaldayo, kwa hofu ya kwamba huenda wao wakanitia mikononi mwao nao huenda kwa kweli wakanitenda vibaya.”—Yeremia 38:19, NW.
Hatimaye, hata mtume aweza kuogopa. Katika siku ambayo Yesu angekufa, yeye aliwaonya wafuasi wake kwamba wote wangemwacha. Hata hivyo, Petro alijulisha wazi kwa ujasiri hivi: “Bwana, niwapo pamoja nawe, mimi ni tayari kwenda gerezani au hata kifoni.” (Luka 22:33; Mathayo 26:31, 33) Maneno hayo yalithibitika kuwa yenye makosa kama nini! Saa chache tu baadaye, kwa hofu Petro alikana kuwa alikuwa pamoja na Yesu au hata kuwa amjua. Hofu kwa mwanadamu ilimshinda nguvu! Ndiyo, hofu kwa mwanadamu ni sumu ya kiakili kweli kweli.
Yatupasa Kuhofu Nani?
Sisi twaweza kushindaje hofu kwa mwanadamu? Kwa kuweka mahali payo hofu inayofaa zaidi. Mtume yule yule, Petro, ndiye aliyetia moyo kuwa na aina hii ya hofu, aliposema: “Hofuni Mungu.” (1 Petro 2:17, NW) Yule malaika aliyeonwa na Yohana katika Ufunuo aliita kwa sauti kubwa kwa aina ya binadamu hivi: “Hofuni Mungu na kumpa yeye utukufu.” (Ufunuo 14:7, NW) Mfalme Sulemani mwenye hekima alitia moyo pia kuwa na hofu kama hiyo, aliposema: “Umalizio wa shauri hilo, kila jambo likiwa limekwisha kusikiwa, ni: Mhofu Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu mzima wa mwanadamu.” (Mhubiri 12: 13, NW) Ndiyo, hofu kwa Mungu ni wajibu.
Hofu kwa Mungu huleta manufaa. Mtunga zaburi wa kale aliimba hivi: “Hakika wokovu [wa Yehova] u karibu na wale wanaohofu yeye.” (Zaburi 85:9, NW) Pia mithali ya Biblia hukazia hivi: “Hofu yenyewe ya Yehova itaongeza siku.” (Mithali 10:27, NW) Ndiyo, hofu kwa Yehova ni jambo linalofaa, lenye kunufaisha. ‘Lakini hakika,’ huenda ukasema, ‘Yehova ni Mungu mwenye upendo. Kwa nini tuhofu Mungu wa upendo?’
Je! Uhofu Mungu wa Upendo?
Kwa sababu hofu kwa Mungu si ile hofu duni, yenye kulemaza kabisa ambayo hushika watu katika hali fulani. Ni hofu ya aina ile ambayo huenda mtoto akahisi kwa baba yake, hata ingawa yeye apenda baba yake na ajua kwamba baba yake ampenda.
Kwa kweli hofu kwa Mungu ni heshima nyingi sana kwa Muumba inayotokana na ung’amuaji wa kwamba yeye ndiye kielelezo halisi cha uadilifu, haki, hekima, na upendo. Inahusu woga unaofaa wa kutochukiza Mungu kwa sababu yeye ndiye Hakimu Mkuu Zaidi aliye na mamlaka ya kuthawabisha na kuadhibu. “Ni jambo la kutisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai,” akaandika mtume Paulo. (Waebrania 10:31) Upendo wa Mungu si jambo la kuchukuliwa vivi hivi, wala hukumu yake si jambo la kuchezewa. Ndiyo sababu Biblia hutukumbusha hivi: “Hofu kwa Yehova ndio mwanzo wa hekima.”—Mithali 9:10, NW.
Hata hivyo, inatupasa kukumbuka kwamba ingawa Yehova ana mamlaka ya kuadhibu wale wanaokosa kumtii—naye amefanya hivyo mara nyingi—kwa vyovyote yeye hataki kuona damu ikimwagika wala si mkatili. Kwa kweli yeye ni Mungu wa upendo, hata ingawa yeye, kama vile mzazi mwenye upendo, nyakati nyingine hupatwa na kasirani yenye uadilifu. (1 Yohana 4:8) Ndiyo sababu kumhofu ni jambo lenye kufaa. Linatuongoza tutii sheria zake, ambazo zimekusudiwa zituletee mema. Kutii sheria za Mungu huleta furaha, hali sikuzote kutozitii huleta matokeo mabaya. (Wagalatia 6:7, 8) Mtunga zaburi alivuviwa ajulishe wazi hivi: “Hofuni Yehova, nyinyi watakatifu wake, kwa maana hakuna ukosefu kwa wale wanaohofu yeye.”—Zaburi 34:9, NW.
Wewe Wahofu Nani?
Hofu kwa Mungu hutusaidiaje kushinda hofu kwa mwanadamu? Basi, huenda binadamu wakatudhihaki au hata wakatunyanyasa kwa kufanya yaliyo sawa, jambo ambalo hutubana sisi. Lakini hofu yenye staha kwa Mungu itatubana tushikamane na mwendo ulio sawa, kwa kuwa hatutaki kumchukiza. Zaidi ya hilo, upendo kwa Mungu utatuhimiza tufanye mambo yanayoleta furaha kwa moyo wake. Kuongezea, sisi twakumbuka kwamba Mungu anatuthawabisha sana kwa kufanya yaliyo sawa, jambo ambalo hutufanya tumpende hata zaidi na hutufanya tutake kufanya mapenzi yake. Kwa sababu hiyo, maoni yaliyosawazika juu ya Mungu hutusaidia tushinde hofu yoyote ambayo huenda tukawa nayo kwa wanadamu.
Kama kielelezo, watu wengi hukazwa wafanye kosa kwa sababu ya kuhofu yale ambayo marika yao watafikiri. Huenda vijana shuleni wakavuta sigareti, wakatumia maneno mabaya, wakajisifu juu ya ngono walizofanya (za kweli au za kuwazia tu), na hata wakajaribu kutumia kileo au dawa za kulevya. Kwa nini? Si kwa sababu sikuzote wanataka kufanya hivyo, bali kwa sababu wanaogopa marika yao wangesema nini wakitenda tofauti. Kwa tineja, huenda kuvumilia kuchekwa na dhihaka likawa jambo gumu kama vile kuvumilia mnyanyaso wa kimwili.
Mtu mzima anaweza pia kuhisi mbano wa kufanya kosa. Pengine mwajiri-kazi atamwambia mwajiriwa-kazi aongeze gharama za malipo ya mteja au ajaze bila unyofu fomu ya malipo ya kodi ya kampuni ili kupunguza kodi inayopasa kulipwa. Huenda Mkristo akahisi kwamba asipotii, atapoteza kazi yake. Hivyo, kuhofu mwanadamu huenda kukambana afanye kosa.
Katika visa vyote viwili, hofu inayomfaa Mungu na staha kwa amri zake ingemzuia Mkristo asilemazwe kabisa na hofu kwa mwanadamu. Na upendo kwa Mungu ungemzuia asijitie katika vitendo ambavyo Mungu hukataza. (Mithali 8:13) Zaidi ya hilo, imani yake katika Mungu ingemhakikishia kwamba akitenda kulingana na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, Mungu angemtegemeza hata tokeo liweje. Mtume Paulo alionyesha imani yake kwa maneno haya: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.
Biblia huandaa vielelezo vingi sana vya wanaume na wanawake waliokuwa waaminifu kwa Yehova hata chini ya mitihani iliyo mikali kupita yote. “Walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, . . . kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga.” (Waebrania 11:36, 37) Lakini wao hawakuruhusu hofu ya mwanadamu idhibiti akili zao. Badala ya hivyo, walifuata mwendo ule ule wenye hekima ambao baadaye Yesu aliwapa wanafunzi wake: “Msiwe wenye kuhofu wale ambao huua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; afadhali mwe wenye kuhofu yeye [Mungu] ambaye aweza kuharibu nafsi na mwili pia katika Gehenna.”—Mathayo 10:28, NW.
Kufuata shauri hili la Yesu la kuhofu Mungu badala ya wanadamu kuliwawezesha Wakristo wa mapema kuvumilia pia namna zote za magumu, majaribu, na minyanyaso “kwa ajili ya habari njema.” (Filemoni 13, NW) Mtume Paulo ni kielelezo kinachostahili kuangaliwa cha jambo hili. Katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, yeye huonyesha jinsi hofu kwa Mungu ilivyompa ujasiri wa kuvumilia vifungo, mapigo, kupigwa mawe, kuvunjikiwa merikebu, hatari mbalimbali njiani, kukosa usingizi mausiku, njaa, kiu, baridi, na uchi.—2 Wakorintho 11:23-27.
Pia hofu kwa Mungu iliimarisha Wakristo hao wa mapema wavumilie mnyanyaso mkali chini ya Milki ya Roma, wakati baadhi yao hata walitupwa kwa hayawani-mwitu katika uwanja. Katika zile Enzi za Katikati, waamini wajasiri walichomwa peupe mpaka kufa kwa sababu wao hawangeacha imani yao. Wakati wa ile vita ya ulimwengu iliyopita, Wakristo walipendelea kuteseka na kufa katika kambi za mateso badala ya kufanya mambo yaliyomchukiza Mungu. Lo! hofu ya kimungu ni kani yenye nguvu nyingi kama nini! Hakika, ikiwa iliwaimarisha Wakristo washinde hofu kwa mwanadamu chini ya hali hizo zenye kupita kiasi, inaweza kutuimarisha sisi katika hali yoyote tunamojikuta.
Leo, Shetani Ibilisi anafanya yote awezayo kutubana tufanye yanayochukiza Mungu. Kwa hiyo yawapasa Wakristo wa kweli wawe na azimio lile lile kama aliloonyesha mtume Paulo alipoandika: “Sisi hatumo miongoni mwa hao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho [nafsi, NW] zetu.” (Waebrania 10:39) Hofu kwa Yehova ni chanzo halisi cha nguvu. Kwa msaada wayo, acheni sisi ‘tuwe na ushujaa na kusema: “Yehova ndiye msaidiaji wangu; mimi sitaogopa. Mwanadamu aweza kunitenda nini?”’—Waebrania 13:6, NW.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Hofu kwa Mungu ilimpa Paulo ushujaa wa kuvumilia mambo yote, kutia na mapigo, vifungo, na hata kuvunjikiwa merikebu.—2 Wakorintho 11:23-27