Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 10/1 kur. 25-28
  • Linda Hisi Yako ya Uharaka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Linda Hisi Yako ya Uharaka
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nyakati Hususa za Uharaka
  • Uharaka Katika Nyakati za Ukristo
  • Je, Huo Ulikuwa Uharaka Usiofaa?
  • Kitia-Moyo Zaidi cha Uharaka
  • Tokeo Lifaalo la Uharaka
  • Dumisha Hisi Yako ya Uharaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Jinsi ya Kusitawisha Hisi ya Uharaka Katika Kazi ya Kuhubiri
    Huduma Yetu ya Ufalme—2014
  • “Siku Kuu ya Yehova Iko Karibu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Uwe Mwenye Bidii kwa Ajili ya Ibada ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 10/1 kur. 25-28

Linda Hisi Yako ya Uharaka

NI NJIA gani iliyo ya hakika inayokubaliwa na Mungu ya kuendelea kumtumikia Yehova kwa nafsi yote? Ni kuwa na hisi ya kweli ya uharaka yenye kina sana mioyoni mwetu. Kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kunamaanisha kumtumikia kabisa, nako kwahitaji kutii kabisa, kwa kila jambo atuambialo tufanye.

Nabii Musa alikazia uhitaji huo alipoagiza taifa la Israeli hivi: “Mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako [“nafsi yako,” NW] yote, na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Karne nyingi baadaye amri iyo hiyo ilirudiwa na Kristo Yesu: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako [“nafsi yako,” NW] yote, na kwa akili zako zote.” (Mathayo 22:37) Mtume Paulo alitaja takwa ilo hilo alipowaambia Waefeso wafanye “yampendezayo Mungu kwa moyo [“nafsi yote,” NW],” na aliwahimiza Wakolosai akisema: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo [“nafsi yote,” NW], kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu.”—Waefeso 6:6; Wakolosai 3:23.

Hata hivyo, ni vigumu kuweka moyo wetu na nafsi yetu kwenye utumishi wetu kwa Mungu ikiwa hatuna hisi ya uharaka ndani yetu au ikiwa hisi ya uharaka tuliyokuwa nayo wakati fulani sasa imepoa—au labda imekwisha. Leo, tunaishi wakati wa uharaka usiofanana na kipindi kingine chochote katika historia ya mwanadamu.

Nyakati Hususa za Uharaka

Katika nyakati za kabla ya Ukristo kulikuwa na nyakati kadhaa za uharaka. Siku za Noa na kipindi kilichoongoza hadi kwenye uharibifu wa Sodoma na Gomora kwa hakika zilikuwa nyakati za uharaka kwelikweli. (2 Petro 2:5, 6; Yuda 7) Ile miaka iliyotangulia Furiko bila shaka ilijawa na utendaji wa haraka. Ingawa Noa na familia yake hawakujua wakati hususa ambao Gharika ingeanza, ‘hofu yao ya kimungu’ ingaliwafanya wasiiahirishe siku hiyo.—Waebrania 11:7, NW.

Vilevile, kabla ya uharibifu wa Sodoma na Gomora, malaika ‘walimharakisha Loti’ na kumwambia “Okoa nafsi yako!” (Mwanzo 19:15, 17, NW) Ndiyo, katika tukio hilo pia, uharaka uliokoa uhai mwadilifu. Karne nyingi baadaye Wayahudi waliokuwa mateka katika Babiloni walihimizwa hivi: “Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu; tokeni kati yake.” (Isaya 52:11) Katika 537 K.W.K., watu wapatao 200,000 waliokuwa uhamishoni walifanya haraka kutoka Babiloni kwa utii wa amri hiyo ya kiunabii ya uharaka.

Hisi ya uharaka katika kila mojapo pindi hizo ilitokeza utumishi wa nafsi yote wa wale waliohisi na kudumisha usadikisho wa kwamba walikuwa wakiishi wakati wa uharaka.

Uharaka Katika Nyakati za Ukristo

Uhitaji wa uharaka unatajwa mara kwa mara katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. “Fulizeni kutazama,” “fulizeni kuwa macho,” “fulizeni kulinda,” “jithibitisheni wenyewe kuwa tayari,”—hizo zote ni semi alizotumia Kristo Yesu kuweka hisi ifaayo ya uharaka ndani ya wafuasi wake. (Mathayo 24:42-44; Marko 13:32-37, NW) Kuongezea hayo, vielezi vyake kuhusu wanawali kumi, mtumwa mwovu, talanta, na kutenganisha kondoo na mbuzi vyote huchochea matazamio fulani na hutokeza hisi ya uharaka.—Mathayo 25:1, 14, 15, 32, 33.

Yesu alizungumza juu ya uharaka na pia alitegemeza uhalisi wa maneno yake kwa kufanya kazi kwa uharaka. Katika pindi moja aliuambia hivi umati wa watu walipojaribu kumzuia asiende: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:42, 43) Zaidi ya hayo, aliwatia moyo wanafunzi wake wamwombe Bwana wa mavuno atume wafanyakazi wengi zaidi katika mavuno Yake kwa sababu “mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.” (Mathayo 9:37, 38) Ombi kama hilo la sala kwa Mungu kwa kweli laonyesha roho ya uharaka.

Je, Huo Ulikuwa Uharaka Usiofaa?

Huenda wengine wakazusha swali hili la maana, Kwa nini hisi ya uharaka ilihitajiwa wakati huo ikiwa “dhiki kubwa” iliyotabiriwa ilikuwa bado kwa karne nyingi?—Mathayo 24:21.

Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu hakutumia ujanja ili kuharakisha wafuasi wake katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. La, ulikuwa upendo wa Kristo kwa wanafunzi wake, vilevile ufahamu wake mkamilifu wa maoni ya Yehova juu ya wakati, ndio uliokuwa msingi wa shauri lake juu ya uharaka. Ndiyo, Kristo Yesu alijua kwamba roho ya uharaka ilihitajiwa ili kutimiza mapenzi ya Yehova kulingana na kusudi la Mungu. Zaidi ya hayo, alijua kwamba wanafunzi wake wangejifaidi kiroho kwa kudumisha hisi ya uharaka hadi arudipo.

Yesu Kristo alikuwa ameonyesha waziwazi kwamba kulikuwa na kazi ya kutoa ushahidi ulimwenguni pote iliyopaswa kutimizwa kwa muda mfupi. (Mathayo 24:14; Marko 13:10) Hatua zenye kufuatana za mgawo huu zilifunuliwa wakati tu kazi ilipoendelea. Lakini uharaka ulihitajiwa ili kutimiza kila hatua. Yesu alionyesha uendelevu wa mgawo huo aliposema: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” (Matendo 1:8) Na hivyo ndivyo mgawo huo umefunuliwa hadi leo hii. Umetokeza mshangao kwa watumishi wa Mungu kwa muda ambao umepita, ukilazimu marekebisho yafanywe katika ufahamu nyakati nyingine.

Hisi ya Kikristo ya uharaka imetumikia kusudi la Yehova. Imesaidia wanafunzi wa Kristo kuendelea na mgawo wao kulingana na ratiba ya Yehova isiyokosea. Na hivyo leo, tukitazama nyuma kwa zaidi ya miaka 2,000, twafahamu zaidi ratiba hiyo ya kimungu.

Uharaka wa Kikristo ulisaidia wanafunzi kutoa ushahidi kikamili katika Yerusalemu, Yudea, Samaria, na kwa Wayahudi waliotawanyika kabla ya 36 W.K. wakati pendeleo la pekee kuelekea Israeli lilipokoma. (Danieli 9:27; Matendo 2:46, 47) Vilevile, uharaka wa Kikristo ulisaidia kutaniko la mapema kutoa onyo la wazi kwa Wayahudi wote kwamba mfumo wao ungekwisha karibuni. (Luka 19:43, 44; Wakolosai 1:5, 6, 23) Na ulipokwisha kwa ghafula katika 70 W.K., uharaka ulisaidia mashahidi wa Kristo wa karne ya kwanza kutangaza tumaini la kimbingu kwa wengi kabla ya uasi-imani uliotabiriwa kueneza giza la kiroho lenye kuleta kifo. (2 Wathesalonike 2:3; 2 Timotheo 4:2) Kisha, kupitia karne za Enzi za Giza, Wakristo wachache wenye mfano wa ngano walidumisha tumaini la Ufalme, kama Kristo Yesu alivyokuwa ametabiri. (Mathayo 13:28-30) Mwishowe, katika wakati wake uliowekwa, Yehova alianzisha kutaniko la kisasa lenye nguvu, lenye kuchochewa na ujumbe wake wa hukumu wa haraka kwa wale waishio katika kizazi hiki cha mwisho.—Mathayo 24:34.

Kama Danieli wa kale, Mashahidi wa Mungu waaminifu wa kisasa hawawezi kamwe kujaribu kumuuliza Yehova, wakisema: “Unafanya nini wewe?” (Danieli 4:35) Wana uhakika kwamba Yehova anajua vizuri kabisa ni nini kinachohitajiwa kumaliza kazi yake kulingana na ratiba. Hivyo badala ya kutilia shaka njia ya Yehova ya kupanga mambo, wanafurahi kwamba Mungu amewapa fursa ya kufanya kazi pamoja naye katika nyakati hizi za maana.—1 Wakorintho 3:9.

Kitia-Moyo Zaidi cha Uharaka

Sababu nyingine ya uharaka ni kutojua kwetu siku na saa yenyewe ya kutokea kwa ghafula ile dhiki kubwa. Kristo Yesu alijua kwa hakika kwamba hakuna yeyote duniani ajuae siku na saa iliyowekwa ya kuanza kwa tukio hilo kuu. (Mathayo 24:36) Katika pindi nyingine aliwaambia hivi mitume wake waliokuwa na hamu ya kujua: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Matendo 1:7) Ndiyo, yatakayotokea ni wazi, lakini mambo yote hususa si juu yetu kujua.

Mtume Paulo alikuwa na mtazamo ufaao wa uharaka. Labda alikuwa akifikiria maneno ya Yesu alipowaandikia Wathesalonike kuhusu kuwapo kwa Kristo: “Kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.” (1 Wathesalonike 5:1) Aliandika barua hiyo miaka 17 hivi baada ya Yesu kusema: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hata mwisho wa nchi.” (Matendo 1:8) Wakati huo hakuna mengi zaidi yangeweza kuandikwa kwa sababu hakuna mengi zaidi yaliyokuwa yamefunuliwa. Hata hivyo wangekuwa na uhakika kwamba siku ya Yehova ingekuja kwa hakika “kama mwivi ajavyo usiku” wakati Wakristo wangekuwa bado wakihubiri kwa uharaka.—1 Wathesalonike 5:2.

Haingewezekana kwamba kwa maneno hayo, Wakristo wa karne ya kwanza wangefikiri kwamba siku ya Yehova ilikuwa bado mbali kwa karne nyingi. Kwa kweli, walijua mifano ya Yesu juu ya mfalme aliyeenda nchi ya mbali na juu ya mtu aliyesafiri ng’ambo. Pia walijua kwamba mifano hiyo ilionyesha kwamba mfalme angerudi “mwishowe” na yule msafiri “baada ya siku nyingi.” Lakini bila shaka walijiuliza maswali kama vile, “Mwishowe” ni lini? Na ni nini kinachomaanishwa na “baada ya siku nyingi”? Je, ni miaka kumi? Ni miaka ishirini? Miaka hamsini? Au muda mrefu zaidi? (Luka 19:12, 15, NW; Mathayo 25:14, 19) Wangeendelea kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.”—Luka 12:40.

Tokeo Lifaalo la Uharaka

Ndiyo, hisi ya uharaka yenye kuchochewa na Mungu ilikuwa na tokeo la kitia-moyo cha ajabu juu ya Wakristo wa karne ya kwanza, ikiwasaidia kufanya kazi iliyo ya maana sana ya kuhubiri na kufundisha. Hiyo yaendelea kututia moyo kwa njia nyingi leo. Inatusaidia tusilegee au ‘kuchoka katika kutenda mema.’ (Wagalatia 6:9) Inatulinda kutojiingiza kupita kiasi katika ulimwengu na ufuatiaji wao wa vitu vya kimwili. Inaweka akili zetu kwenye “uzima ulio kweli kweli.” (1 Timotheo 6:19) Bwana Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangekuwa kama “kondoo kati ya mbwa-mwitu,” naye alijua uhitaji wetu wa kuwa na mtazamo imara ili kukabili ulimwengu. Ndiyo, tumelindwa salama, kwa ulinzi wa hisi yetu ya Kikristo ya uharaka.—Mathayo 10:16.

Yehova Mungu kwa hekima yake isiyo na kikomo sikuzote amewapa watumishi wake habari ya kutosha ili wadumishe hisi yao ya uharaka. Kwa fadhili ametuhakikishia kwamba tumo katika “siku za mwisho” wa mfumo huu wa mambo uliopotoka. (2 Timotheo 3:1) Tunakumbushwa kwa kuendelea kwamba ni lazima tung’ae kama vimulikaji hadi kizazi tunachoishi kipite katika dhiki kubwa, upeo wayo ukiwa kwenye Har–Magedoni.—Wafilipi 2:15; Ufunuo 7:14; 16:14, 16.

Ndiyo, hisi ya kimungu ya uharaka ni sehemu ya maana sana ya utumishi wa nafsi yote kwa Yehova. Huondoa na kusaidia kukabili majaribu ya Ibilisi ya kuwafanya watumishi wa Mungu ‘wachoke na kuzimia katika nafsi zao.’ (Waebrania 12:3) Kwa umilele wote, ujitoaji wa nafsi yote utafanya watumishi wa Yehova kumtii, lakini sasa, katika hizi siku za kabla ya Har–Magedoni, hisi ya kweli yenye kina ya uharaka, iliyo halisi ni sehemu muhimu ya ujitoaji wa nafsi yote.

Yehova Mungu wetu na atusaidie sisi sote tulinde hisi yetu ya uharaka huku tukiendelea kusema maneno haya ya mtume Yohana: “Amina; na uje, Bwana Yesu.”—Ufunuo 22:20.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki