Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kutoa Ushahidi Huzaa Tunda Nyumbani na Shuleni
MAISHA ya Mkristo hutia ndani kufanyia wengine mema, hasa kwa kushiriki nao habari njema ya Ufalme wa Mungu. Mithali 3:27 husema: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Katika Argentina Shahidi mchanga katika mwaka wake wa tatu katika shule ya sekondari alitaka kushiriki habari njema ya Ufalme na rafiki yake shuleni. Kufanya kwake hivyo kukawa na matokeo makubwa.
Siku moja Shahidi huyo mchanga alimtajia rafiki yake kwamba si dini zote zilizo nzuri. Mwanamume huyo mchanga alipojibu kwamba hakufanya jambo lolote baya, Shahidi huyo akasema: “Wala humfanyii Mungu lolote.” Hilo lilimfanya kijana huyo afikiri. Baadaye Shahidi huyo alieleza kwamba hizi ni siku za mwisho na kwamba ili kupata kibali cha Mungu, ni lazima kupata ujuzi sahihi wa Biblia na kuishi kulingana nao. Rafiki yake wa shuleni akakubali. Lakini je, familia yake ingemruhusu kuwa na funzo la Biblia? Ili kumpa rafikiye jambo la kufikiria, Shahidi huyo akamwambia asome kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.
Wakati ukapita, na rafiki huyo akaacha shule. Hakupata habari zake kwa zaidi ya mwaka mmoja. Kisha siku moja Shahidi yule mchanga alishangaa kupokea simu kutoka kwa rafikiye aliyesema kwamba angeweza kuona kwamba unabii mbalimbali wa Biblia kwa kweli ulikuwa ukitimizwa. Shahidi huyo akapanga kujifunza Biblia pamoja naye mara moja.
Alipoenda nyumbani mwa rafikiye aliyekuwa mwanashule mwenzake, aliona kwamba wazazi wa rafikiye walikuwa na wasiwasi sana kuhusu kile ambacho mwana wao alikuwa akihusika nacho. Hata ndugu mdogo wa rafikiye alifikiri kwamba ndugu yake mkubwa alikuwa anashikwa na kichaa. Hivyo wazazi walimwambia ndugu huyo mdogo awepo kwenye funzo lililofuata. Baadaye, akiwa na machozi machoni mwake, kijana huyo mdogo akaripoti kwa wazazi kwamba ndugu yake mkubwa hakuwa na kichaa, aliposikia hivyo huyo mama akapaaza sauti akisema, “Badala ya kuwa na tatizo moja, sasa nina mawili!”
Hivyo, kwenye funzo lililofuata yeye mwenyewe akawepo naye alilazimika kukubali kwamba vijana hao hawakuwa na kichaa. Baadaye funzo la Biblia lake na mumeye lilipangwa. Mara familia nzima ikaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwenye Jumba la Ufalme. Mwishowe, babu na nyanya pia wakaanza kujifunza Biblia na kuanza kwenda mikutanoni. Tangu wakati huo, yule kijana wa kwanza amebatizwa. Alioa, na yeye na mkeye ni wahubiri wenye bidii.
Zaidi ya hayo, kupitia ushahidi wa vivi hivi shuleni, yule Shahidi mchanga amesaidia wanashule wenzake wengine wawili na vilevile mama na dada ya mmoja wao kuanza kujifunza Biblia. Kwa ujumla, watu 11 walijifunza kweli ya Biblia kwa sababu yule Shahidi kijana hakuacha kufanyia wanashule wenzake yaliyo mema. Ni tokeo lenye furaha kama nini! Kwa kweli, “Heri watu wenye BWANA kuwa Mungu wao!”—Zaburi 144:15.y