Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
“Fanya Kazi ya Mweneza-Evanjeli”
INAMAANISHA nini kuwa mweneza-evanjeli? Hilo neno ni tafsiri ya neno la Kigiriki eu·ag·ge·li·stesʹ, linalohusika kwa ukaribu na neno eu·ag·geʹli·on, limaanishalo “habari njema.” Hivyo, mweneza-evanjeli ni mhubiri, au mjumbe, wa habari njema.
Wakristo wote wa kweli ni waeneza-evanjeli kwa sababu wanatangaza habari njema juu ya Ufalme wa Mungu. Kwa kufaa, mtume Paulo alimpa Timotheo shauri la upole kwamba ‘afanye kazi ya mweneza-evanjeli.’ Timotheo alipaswa kuchukua kazi hiyo kwa uzito. Paulo alimsihi ‘atunze akili zake katika mambo yote’ na ‘kutimiza kikamili huduma yake.’—2 Timotheo 4:5, New World Translation.
Tukiwa waeneza-evanjeli sisi pia huchukua huduma yetu kwa uzito na ‘kutunza akili zetu’ au kuwa macho ili kushiriki habari njema kwa kila fursa. Hivyo wengi wamepata kumjua Yehova na ahadi zake baada ya kukutana na Mashahidi wa Yehova kivivi-hivi. Hivi ndivyo ilivyotokea kwa Seymore, mwanamume fulani katika Barbados.
Seymore alikuwa mwalimu wa shule ya serikali. Charles, mwalimu wa nusu wakati katika shule ileile na aliye mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alikuwa mweneza-evanjeli aliyekuwa macho. Yeye alikuwa mhudumu wa wakati wote, au painia, naye alitumia kila fursa kueleza wengine habari njema. Ni kupitia ushahidi wa kivivi-hivi wa Charles kwamba Seymore alisikia ujumbe wa Ufalme kwa mara ya kwanza.
Upesi Seymore pia aliazimia kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengi iwezekanavyo. Hivyo akaanzisha mazungumzo ya kivivi-hivi pamoja na watu mahali pake pa kazi, hasa pamoja na wanafunzi wake. Ingawa katika nchi fulani dini haipaswi kufundishwa katika shule za serikali, mwanamume huyu alipewa mgawo wa kufundisha mambo ya dini na kanuni za adili. Lakini sasa maoni ya zamani ya Seymore kuhusu mambo hayo yalikuwa yamebadilishwa na ujuzi mpya wa Biblia aliokuwa amejipatia. Nyakati za kupumzika, alizungumza na wanafunzi wake juu ya ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya na taraja la uhai udumuo milele.
Watoto hao waliitikiaje? Wengi walionyesha kupendezwa kikweli na habari njema ya Ufalme wa Yehova. Muda si muda, Seymore akaanza kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na 13 kati ya wanafunzi wake. Walipendezwa sana hivi kwamba walipanga kujifunza Biblia mara mbili kwa juma. Mwishowe wengi wao wakaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwao. Kufikia sasa tisa kati yao wamekuwa Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. Kwa habari ya Seymore, sasa anatimiza huduma yake kikamili kwa kutumikia akiwa painia wa kawaida na mzee katika mojapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika Barbados.
Hiki ni kielelezo kimoja tu cha jinsi Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote ‘hufanya kazi ya waeneza-evanjeli,’ kwa sehemu kwa kushiriki katika ushahidi wa kivivi-hivi. Wao hufuata shauri la upole la Biblia lipatikanalo kwenye Wakolosai 4:5, 6, ambalo husema: “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati. Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.”y