Walikusanyika Wakiwa Wasifaji Wenye Shangwe
WATU wa kale wa Yehova Mungu walipokusanyika kwa ajili ya ibada, waliamuriwa ‘wawe tu wenye shangwe’ walipokusanyika kwa ajili ya ibada. (Kumbukumbu la Torati 16:15, New World Translation) “Wasifaji Wenye Shangwe” Mikusanyiko ya Wilaya ya 1995/96 kwa hakika imewapa Mashahidi wa Yehova sababu nzuri za kuwa na shangwe.
Tangu mfululizo huu wa mikusanyiko ulipoanza, wao wamejenga imani. Wameonyesha pia jinsi ya kupata shangwe katika ulimwengu usio na shangwe. Ebu tuangalie siku moja-moja ya mkusanyiko huo.
‘Msifuni Yehova, Enyi Watu . . . Iweni Wenye Shangwe!’
Kichwa kilicho juu cha siku ya kwanza ya mkusanyiko kilitegemea Zaburi 149:1, 2, NW. Hotuba “Tuna Sababu ya Kulia kwa Shangwe” ilichunguza utumizi wa unabii katika Isaya 35. Huo ulikuwa na utimizo katika Israeli la kale na hasa katika siku yetu kwa kurudishwa kwa waabudu wa Yehova kwenye ufanisi na afya katika paradiso ya kiroho. Hivyo, wakusanyikaji walikuwa na sababu ya kulia kwa shangwe juu ya kile ambacho Mungu amekusudia watu wake katika paradiso ya kiroho na katika Paradiso ya kimwili inayokuja karibuni sana.
Hotuba ya msingi, “Waliowekwa Kando Kuwa Wasifaji Wenye Shangwe Ulimwenguni Pote,” ilijibu swali: Ni nini kinachotuweka kando na ulimwengu huu? Ni ibada yetu ya Yehova yenye muungamano. Haidhuru ni wapi Mashahidi wa Yehova wanakoishi kwenye dunia hii, wao husema na hufundisha kwa upatano. Wao hushangilia pia, katika ahadi tukufu za Yehova za kulitakasa jina lake takatifu na kutetea enzi kuu yake kupitia Ufalme wake. Lakini, Yehova hutusaidiaje tuwe na sehemu katika kusudi lake? Yeye ametukabidhi kweli ya Neno lake takatifu. Mungu ametupa sisi roho takatifu yake. Ametubariki kwa kutupa udugu wa ulimwenguni pote na mpango kwa ajili ya ibada safi. Familia yetu ya kimataifa hutusaidia tumtumikie Yehova kwa shangwe kubwa ya moyo.
“Kuendelea Kujitenga na Ulimwengu Pasipo Mawaa” ilikazia uhitaji wa kuepuka mawaa ya ubaguzi na kufanya tofauti za vikundi-vikundi vya watu. (Yakobo 2:5-9) Huenda wengine wakashirikiana kijamii na wale tu wenye malezi yaleyale au wenye hali ileile ya kifedha, wakipuuza Wakristo wenzao walio maskini au wenye upungufu. Huenda wengine wakaelekea kupendelea wale walio na vyeo vyenye madaraka kutanikoni. Wanasahau kwamba pendeleo lililo kubwa zaidi ambalo mtu yeyote aweza kuwa nalo ni lile la kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa hiyo, lazima tusiruhusu mielekeo ya kilimwengu itutie waa na kuvunja amani ya kutaniko.—2 Petro 3:14.
Hotuba “Je, Niko Tayari Kufunga Ndoa?” ilionyesha kwamba wengi hufunga ndoa upesi-upesi. Wengine hufunga ndoa ili kuponyoka hali ngumu nyumbani au kwa sababu marika wao wanafunga ndoa. Hata hivyo, sababu halali za kufunga ndoa zatia ndani tamaa ya wote wawili ya kufuatia miradi ya kitheokrasi, upendo wa kweli, uhitaji wa urafiki na usalama, na tamaa ya kulea watoto. Mazoezi ya kiroho ni muhimu katika kutayarisha kwa ajili ya ndoa. Miongoni mwa mambo mengine, kuna uhitaji wa kujenga sifa zenye kutamanika kwa kujivika utu mpya. Ni jambo la hekima pia kuhakikisha kama mtu atakayekuwa mwenzi wa ndoa hutoa uthibitisho wa kuwa na uhusiano halisi na Yehova na hushughulika na wengine kwa staha. Kutafuta shauri kutoka kwa Wakristo wakomavu ni jambo la hekima pia.—Mithali 11:14.
Mazungumzo hayo yenye kutia nuru yalifuatwa na mengine yenye kichwa “Wazazi Wanaofurahia Watoto Wao.” Kwa kawaida kuzaliwa kwa mtoto ni wakati wa kushangilia sana. Hata hivyo, kuzaa watoto huleta daraka kubwa pia. (Zaburi 127:3) Hivyo, ni jambo la maana kwamba watoto wafundishwe kumpenda Yehova. Wazazi waweza kufanya hivyo kwa kuwaambia watoto wao kwa ukawaida kumhusu Yehova na kwa kutumia kanuni za Neno lake katika familia.
Siku ya kwanza ya mkusanyiko iliisha kwa jambo lisilotazamiwa—kutolewa kwa broshua mpya Mashahidi wa Yehova na Elimu. Hiyo yaeleza waziwazi kwamba Mashahidi “hutia moyo vijana wao wasome kwa bidii na kuchukua kwa uzito kazi wanazogawiwa shuleni.” Kichapo hiki pia hueleza juu ya matokeo ya ajabu ya madarasa ya kufunza watu kusoma na kuandika ambayo Mashahidi wa Yehova wameongoza kwa miaka mingi katika Nigeria, Mexico, na nchi nyinginezo. Hii broshua yatumainiwa kusaidia waelimishaji waone kwamba sisi huona elimu kuwa ya maana sana.
“Sikuzote na Tumtolee Mungu Dhabihu ya Sifa”
Kichwa kilichotangulia cha siku ya pili kilitegemea Waebrania 13:15, NW. Programu ya asubuhi ilitoa mfululizo juu ya “Kuitikia Wito wa Kumsifu Yehova.” Umri si kizuizi kwa kuitikia wito huo. Zaburi 148:12, 13 huwahimiza wanaume vijana, mabikira, wanaume wazee, na wavulana wamsifu Yehova. Wengi kati ya watumishi wa Yehova wenye shangwe wameweza kuongeza sifa yao. Ulimwenguni pote, watu zaidi ya 600,000 hushiriki katika utendaji wa kuhubiri wa wakati wote, au utumishi wa painia. Watu zaidi ya 15,000 hushiriki katika kazi ya upainia wa pekee, na watu zaidi ya 15,000 wamo katika utumishi wa Betheli.
“Kutumikia kwa Uaminifu-Mshikamanifu Pamoja na Tengenezo la Yehova” ilikuwa hotuba iliyoonyesha kwamba uaminifu-mshikamanifu ni muhimu kwa watumishi wa Mungu. Kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova kwamaanisha kushikamana naye kwa ujitoaji wenye nguvu sana hivi kwamba unatenda kama gundi yenye nguvu. Uaminifu-mshikamanifu hutaka kwamba tuepuke kukiuka amri za Biblia kimakusudi, iwe wengine watuona au la. Hutaka pia kwamba tuunge mkono kwa uaminifu-mshikamanifu mafundisho ya Biblia yanayopatikana katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na pia chakula chote kinginecho cha kiroho kinachoandaliwa na Watch Tower Society. Hotuba hii ilifuatwa na hotuba ya ubatizo. Kulikuwa na shangwe kama nini wakati wataka-kubatizwa walipotoa uthibitisho wa wakfu wao kwa Yehova!
Maneno ya Hosea 4:1-3 yaliwekea kigezo hotuba ya alasiri “Wema Wenye Adili au Ubaya—Ni Upi Wewe Hufuatia?” Ingawa maoni ya ulimwengu juu ya wema wenye adili umezorota, ni lazima Wakristo ‘wajitahidi sana’ kufuatia ubora wa kiadili. (2 Petro 1:5) Hilo huanza kwa jinsi mtu afikirivyo. Ikiwa mawazo yake ni yenye wema wenye adili, yeye atasema maneno yaliyo safi, yafaayo, na yenye kujenga naye atajitahidi kuwa mwenye kufuatia haki katika kushughulika kwake na wengine. Kufuatia wema wenye adili hutia ndani pia kujitahidi kuwa mwenye kuelewa na mwenye huruma kuelekea Mkristo mwenzako anayepatwa na hali yenye taabu au ya kushuka moyo.—1 Wathesalonike 5:14.
Hotuba nyingine, “Jilindeni na Mitego ya Ibilisi,” iliwaonya Wakristo dhidi ya kujiweka wazi kupatwa na uvutano mbalimbali wa roho waovu. Katika uwanja wa utibabu wa magonjwa, Wakristo wahitaji kuwa waangalifu kuhusu njia mbalimbali, kama vile uzugaji, zinazoonyesha dalili za mafumbo. Kwa vyovyote, kile ambacho watu mmoja-mmoja hufanya kutunza afya yao ya kimwili ni jambo la kibinafsi.
Siku ya pili iliisha kwa jambo lisilotazamiwa lenye shangwe—kutolewa kwa kichapo kipya chenye ukubwa wa kutoshea mfukoni ambacho kimekusudiwa kusaidia watu wenye moyo wa kufuatia haki wafanye maendeleo upesi hadi kwenye wakfu na ubatizo. Kitabu hiki kipya cha kurasa 192 kina kichwa Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kitabu Ujuzi chatokeza kweli kwa njia chanya. Hakikazii kukanusha mafundisho bandia. Uwazi wa maneno na ukuzi wa mambo kwa njia ya akili watazamiwa kufanya iwe rahisi kukitumia kitabu hiki kuongoza mafunzo ya Biblia na kusaidia watu waelewe ujuzi wenye kuchangamsha moyo juu ya Mungu.
“Furahini, Mkashangilie Daima”
Maneno hayo kutoka katika Isaya 65:18 yalikuwa kichwa cha siku ya tatu ya mkusanyiko. Utimizo wa unabii wa Biblia huelekeza kwenye 1914 kuwa ndio mwaka ambao mfumo huu mwovu uliingia siku zao za mwisho. Kwa hiyo, mfululizo wa hotuba wenye kichwa “Wasifaji Wenye Shangwe Katika Umalizio wa Mfumo Huu” ulivuta usikivu wote wa wasikilizaji. Wasemaji walionyesha jinsi maelfu ya mamilioni wanavutwa na roho ya ulimwengu yenye pupa na iliyo na jeuri. Hatimaye, watahukumiwa kuwa sehemu ya ulimwengu ambao Shetani ndiye mtawala wao. Hivyo, sasa ndio wakati wa kufanya chaguo. Sisi twataka kuwa upande gani? Je, twataka kumwabudu Yehova na kuunga mkono enzi kuu yake, au tutamruhusu Shetani awe mtawala wetu kwa kufanya mambo yanayompendeza? Sisi sote twapaswa kuchukua msimamo wetu waziwazi upande wa Yehova.
Hotuba ya watu wote ya mkusanyiko, “Msifuni Mfalme wa Umilele!” iliwapa wahudhuriaji wote chakula kigumu cha kufikiria. Ingawa wazo la umilele laonekana kupita uelewevu wa wanadamu walio dhaifu, Yehova hulielewa kikamili. “BWANA ndiye Mfalme milele na milele,” akaimba mtunga-zaburi. (Zaburi 10:16) Mfalme huyu wa umilele amefungulia wanadamu njia ya kufurahia uhai wa milele kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. (Yohana 17:3) “Ndiyo, sisi wanadamu wenye dhambi twaweza kupata uhai udumuo milele kupitia elimu ya kimungu na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu,” akasema msemaji.
Mkusanyiko ulipokaribia kwisha, wahudhuriaji wote walijengwa na hotuba ya mwisho, yenye kichwa “Kumsifu Yehova kwa Shangwe Siku kwa Siku.” Ilichangamsha moyo kupokea ripoti za maendeleo ya kazi ya kufanya wanafunzi kotekote duniani. Na wakusanyikaji walisukumwa ‘kumbariki Yehova kila siku na kulisifu jina lake milele.’—Zaburi 145:2, NW.
Matendo ya ukatili yenye kuchukiza huunyang’anya ulimwengu shangwe. Hata hivyo, watu mmoja-mmoja wenye imani kamili katika Yehova waweza kuwa na shangwe ya kimungu. Wakiwa udugu wa ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova waweza basi kurudia maneno yafuatayo ya Zaburi 35:27, 28: “Washangilie na kufurahi, wapendezwao na haki yangu, naam, waseme daima, Atukuzwe BWANA, apendezwaye na amani ya mtumishi wake. Na ulimi wangu utanena haki yako, na sifa zako mchana kutwa.”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Familia zitanufaika na broshua “Mashahidi wa Yehova na Elimu”
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Kitabu kipya, “Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele,” chatokeza kweli za Biblia kwa njia yenye kujenga
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wengi walibatizwa kwa ufananisho wa wakfu wao kwa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wakusanyikaji walichochewa sana na drama “Kuheshimu Wastahiki Katika Miaka Yao ya Uzee”